Historia ya Kanisa
Utangulizi


“Utangulizi,” Historia za Ulimwengu (2018)

Utangulizi

Wokovu wa watoto wote wa Mungu ni kiini cha injili Yake. Yeye aliahidi kwamba “mataifa yote ya ulimwengu [yatabarikiwa],” kupitia uzao wa Ibrahimu (Mwanzo 22:18), na kwa wachunga kondoo wa Yudea, ilitangazwa kwamba “habari njema” ya injili ilikuwa “kwa watu wote” (Luka 2:10). Katika kurasa za mwanzo za Kitabu cha Mormoni Nefi alitangaza kwamba Bwana “hafanyi chochote ila tu kwa manufaa ya ulimwengu; kwani anapenda ulimwengu, hata kwamba anatoa maisha yake ili awavute wanaume wote [na wanawake] kwake” (2 Nefi 26:24; italiki imeongezwa).

Punde tu baada ya Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho kuanzishwa, Bwana aliwaelekeza Watakatifu kuihubiri injili kote ulimwenguni: “Kwani atauweka wazi mkono wake mtakatifu machoni pa mataifa yote,” Bwana alisema mnamo 1831. “Jitengenezeeni, jitengenezeeni, Enyi watu wangu. … Ndiyo, acheni kilio kiendelee miongoni mwa watu wote” (Mafundisho na Maagano 133:3–4, 10). Vivyo hivyo, Watakatifu waaminifu wameitikia miito ya kuhubiri kote ulimwenguni, Kitabu cha Mormoni kimetafsiriwa (chote au kwa sehemu) katika lugha zaidi ya 110 na mikusanyiko imeanzishwa na kustawi ulimwenguni kote.

Wakati Watakatifu wengi wa Siku za Mwisho wakielewa kwamba Kanisa ni imani ya ulimwenguni kote, historia ya Kanisa katika sehemu nyingi za ulimwengu haijulikani. Historia hizi za ulimwengu zinatafuta kushiriki hadithi zenye misukumo ya jinsi ujumbe wa Urejesho ulivyopokelewa na kushirikiwa kote ulimwenguni.

Kila historia ina maelezo mafupi ya jumla, uchaguzi wa hadithi za imani, mpangilio wa matukio, taarifa za takwimu na vyanzo vya ziada ambavyo msomaji anaweza kurejelea. Hadithi zimefokasi kwenye waumini wa eneo husika ambao wamesikia na kuitikia wito wa “kulitangaza neno katika maeneo yanayowazunguka” (Mafundisho na Maagano 52:39) na ambao wametumia imani kushinda changamoto maalum za kuwa Mtakatifu wa Siku za Mwisho kwenye nchi zao.

Chapisha