Liahona
Lisha Nafsi Yako kwa Sala ya Mara kwa Mara
Aprili 2024


“Lisha Nafsi Yako kwa Sala ya Mara kwa Mara,” Liahona, Apr. 2024

Ujumbe wa Kila Mwezi wa Liahona, Aprili 2024

Lisha Nafsi Yako kwa Sala ya Mara kwa Mara

Tunahitaji lishe ya kiroho ya kuwasiliana na Baba yetu wa Mbinguni, baraka inayopatikana kwetu kila mahali na daima.

Picha
Enoshi akisali

Picha ya mwigizaji akijichukulia kama Enoshi na Matt Reier

Sisi sote tumewahi kuhisi njaa kabla. Maumivu ya njaa ni njia ya mwili ya kutuambia tunahitaji lishe. Na tunapokuwa na njaa, tunajua tunahitajika kufanya nini—kula.

Roho zetu pia zinazo njia za kutufanya sisi tujue tunapohitaji lishe ya kiroho. Lakini inaonekana kwamba ni rahisi kwetu kupuuza njaa ya kiroho kuliko njaa ya kimwili.

Kama vile tu kulivyo na vyakula vya aina nyingi tunavyoweza kula tunapokuwa na njaa, kuna aina tofauti za vitu tunavyoweza kufanya kushibisha njaa yetu ya kiroho. Kwa mfano, tunaweza “kusherehekea kwa kula maneno ya Kristo” (2 Nefii 32:3) katika maandiko na kupitia manabii. Tunaweza kuhudhuria kanisani mara kwa mara na kupokea sakramenti (ona Mafundisho na Maagano 59:9). Tunaweza kumtumikia Mungu na watoto Wake (ona Mosia 2:17).

Lakini kuna chanzo kingine cha lishe ya kiroho kinachopatikana kwa ajili yetu nyakati zote, kila wakati, wa maisha yetu, bila kujali hali zetu. Tunanaweza daima kuwasiliana na Baba wa Mbinguni kupitia sala.

“Na Nafsi Yangu Ikapata Njaa”

Nabii Enoshi alipokuwa akiwinda wanyama msituni, alitafakari “maneno ambayo [yeye] mara nyingi amemsikia baba [yake] akizungumza kuhusu uzima wa milele, na shangwe ya watakatifu.” Maneno haya “yalizama kwa kina ndani ya moyo [wake]” (Enoshi 1:3).

Kwa sababu Enoshi alikuwa katika hali hii ya mawazo kiroho, alihisi hitaji lenye nguvu: “Nafsi yangu ikapata njaa,” yeye alisema (Enoshi 1:4; msisitizo umeongezwa).

Enoshi alifanya nini alipohisi njaa hii ya kiroho, hitaji hili la lishe ya kiroho? “Nilipiga magoti mbele ya Muumba wangu,” alisema, “na nikamlilia kwa sala kuu na nikamsihi kwa ajili ya nafsi yangu” (Enoshi 1:4).

Njaa ya kiroho ya Enoshi ilikuwa kuu sana kiasi kwamba alisali “mchana wote … na usiku ulipofika [yeye] bado alipaza sauti [yake] juu kwamba ilifika mbinguni” (Enoshi 1:4). Mwishowe, Mungu akajibu sala yake na kumsamehe dhambi zake. Enoshi alihisi hatia yake imeondoshwa mbali. Lakini lishe yake ya kiroho haikuishia hapo.

Yeye alikuwa amejifunza kuhusu nguvu ya imani katika Yesu Kristo, na hivyo akaimimina roho yake yote kwa niaba ya watu wake—hata wale maadui zake. Alifanya maagano na Bwana na akajipatia ahadi kutoka Kwake. Na baada ya sala ile kuu Enoshi, alienda miongoni mwa watu wake akitoa unabii, na kushuhudia kuhusu mambo ambayo alikuwa ameyasikia na kuyaona. (Ona Enoshi 1:5–19.)

Siyo kila sala itajibiwa katika njia kama hii ya kushangaza, lakini uzoefu wetu wa sala bado unaweza kuwa wenye maana na wenye kubadilisha maisha. Tunaweza kujifunza masomo fulani muhimu kutokana na uzoefu wa Enoshi juu ya sala. Kwa mfano:

  • Kujitahidi kiukamilifu kuishi injili kunaweza kutusaidia kutambua njaa yetu ya kiroho.

  • Njaa zetu za kiroho zinaweza na zinapaswa zitupelekee kupiga magoti ili kutafuta usaidizi wa Baba wa Mbinguni.

  • Kusali kwa Baba wa Mbinguni kunaweza kutusaidia sisi kutuliza njaa yetu ya kiroho—na vinginevyo.

  • Tunaweza kusali popote, wakati wowote.

  • Sala inaweza kutusaidia sisi kutubu.

  • Sala inaweza kuimarisha imani yetu katika Yesu Kristo.

  • Tunaweza kupokea ushuhuda binafsi kwamba Baba yetu wa Mbinguni anatusikia na anatujua.

  • Ushuhuda na nguvu tunazopokea kupitia sala zinaweza kutusaidia kuwahudumia na kuwaimarisha wengine.

Picha
Mzee Soares alipokuwa mvulana

Uzoefu Wangu wa Nguvu ya Sala

Kama Enoshi, nilijifunza baadhi ya masomo haya haya kupitia uzoefu binafsi. Wazazi wangu walijiunga na Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho wakati nilipokuwa mvulana mdogo, na nilibatizwa nilipofikisha umri wa miaka minane. Daima nilikuwa na hisia nzuri, moyoni mwangu kuhusu Baba wa Mbinguni na kuhusu Yesu Kristo, injili Yake iliyorejeshwa, na Kanisa Lake. Lakini haikuwa hadi pale nilipokuwa takribani na miaka 16 ndipo nilipokuja kusali kuhusu ukweli wa mambo haya.

Askofu wangu kupitia mwongozo aliniomba kufundisha darasa la Shule ya Jumapili la vijana. Nilipaswa kufundisha somo kuhusu jinsi gani tunaweza kupata ushuhuda wa injili kupitia sala. Jukumu hili kutoka kwa askofu wangu lilinisababisha mimi kufikiria kwa kina kuhusu ushuhuda wangu mwenyewe. Nilipata muda wa kujifunza Kitabu cha Mormoni na daima nilihisi kuwa Kanisa ni la kweli. Daima nimekuwa nikiamini katika Mwokozi Yesu Kristo, lakini kamwe sikuwa nimeweka moyoni ahadi ya Moroni inayopatikana katika Moroni 10:4–5. Sikuwa nimewahi kusali kuhusu ukweli wa injili.

Nakumbuka kuhisi moyoni mwangu kwamba kama ninaenda kuwafundisha vijana hawa jinsi gani ya kupata ushuhuda kupitia sala, ninapaswa kusali kwa ajili ya ushuhuda wangu mwenyewe. Nafsi yangu ikahisi njaa—pengine katika njia tofauti na ya Enoshi, lakini hata hivyo nilihisi hitaji la kiroho.

Nilipokuwa nikiandaa somo lile, nilipiga magoti na kutoa hamu ya moyo wangu kwa Baba wa Mbinguni ili kuthibitisha ukweli niliouhisi ndani yangu. Sikuwa nikitarajia dhihirisho lolote kubwa. Lakini nilipomuuliza Bwana kama injili ni ya kweli, hapo ilikuja moyoni mwangu hisia tamu—ambayo ni tulivu, sauti ndogo ikithibitisha kwangu mimi kwamba ilikuwa ya kweli na kwamba niendelee kufanya kile nilichokuwa nikikifanya.

Hisia ilikuwa yenye nguvu sana kiasi kwamba sikuweza kupuuza jibu lile na kusema kwamba sikujua. Niliitumia siku ile nzima nikijisikia mwenye furaha sana. Akili yangu ilikuwa mbinguni nikitafakari ule uzuri wa hisia zilizo moyoni mwangu.

Jumapili iliyofuata, nilisimama mbele ya wana darasa wenzangu watatu au wanne, ambao wote walikuwa wadogo kuliko nilivyokuwa mimi. Niliwashuhudia kwamba Baba wa Mbinguni angejibu sala zao kama wana imani.

Picha
Mzee Soares

Sala iliyojibiwa iiliyopokelewa na Mzee Soares akiwa kijana ilimruhusu yeye kushuhudia—kama mmisionari (hapo juu), kama baba na mume, na Mtume—kwamba Baba wa Mbinguni anajibu sala zinazotolewa kwa imani.

Kuanzia hapo na kuendelea, ushuhuda huu umebaki nami. Umenisaidia kufanya maamuzi, hususani katika nyakati ninapokabiliwa na changamoto. Sala ile katika siku ile, pamoja na ushahidi wa ziada nilioupokea kwa miaka mingi, umeniruhusu kushuhudia kwa watu, kwa usadikisho, kwamba wanaweza kujibiwa na Baba wa Mbinguni kama watasali kwa imani. Hii imekuwa kweli niliposhuhudia kama mmisionari, kama kiongozi wa Kanisa, kama baba na mume, na hata leo kama Mtume.

Lini na Nini ya Sala

Bila shaka, hatusali tu tunapohisi hitaji maalum la nguvu la kiroho. Hivyo, tunapaswa kusali lini? Na tunapaswa kusali kwa ajili ya nini? Kwa jibu fupi ni wakati wowote na kwa ajili ya kitu chochote.

Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni. Kujua hili kunabadilisha jinsi ya kusali. Nabii Joseph Smith alifundisha: “Kuwa na maarifa juu ya Mungu, tunaanza kujua jinsi ya kumkaribia Yeye, na jinsi gani ya kuomba ili kupokea jibu. … Tunapokuwa tayari kuja Kwake, Yeye yuko tayari kuja kwetu sisi.”1

Baba yetu wa Mbinguni daima yuko tayari kutusikiliza na anatutaka tusali Kwake mara kwa mara na kila siku. Tunapaswa “kushauriana na Bwana katika matendo [yetu] yote” (Alma 37:37) na tusali asubuhi, mchana, na usiku. Tunapaswa kusali nyumbani, kazini, shuleni—po pote tunapokuwepo na juu ya kazi yetu yoyote (ona Alma 34:17–26).

Tunapaswa kusali katika familia zetu (ona 3 Nefi 18:21). Tunapaswa kusali “kwa sauti na katika mioyo [yetu], hadharani na sirini” (Mafundisho na Maagano 81:3). Ndiyo, “na wakati [sisi] hatumlilii Bwana, [tunapaswa] kuacha mioyo yetu ijae, ivutiwe katika sala kwake siku zote kwa ustawi [wetu], na pia kwa ustawi wa wale ambao wako karibu [nasi]” (Alma 34:27). Na lazima siku zote tusali kwa Baba katika jina la Yesu Kristo (ona 3 Nefi 18:19–20).

Picha
Joseph Smith akiwa mvulana mdogo

Kielelezo cha Joseph Smith na Walter Rane, kisinakiliwe

Kumkaribia Baba Yetu wa Mbinguni

Baba Yetu wa Mbinguni anataka kutubariki. Na Yeye atafanya hivyo—kama tutamwomba. Nabii Joseph Smith alifundisha, “Kumbukeni kwamba pasipo kuomba hatuwezi kupokea chochote; kwa hiyo, ombeni kwa imani, nanyi mtapokea baraka zile Mungu aonavyo vyema kuzitoa juu yenu ninyi.”2

Sala zetu za kila siku na za mara kwa mara ni sehemu muhimu ya mlo kamili wa lishe ya kiroho kwa nafsi zetu zenye kuhisi njaa. Mawasiliano na Baba wa Mbinguni kupitia sala yanapatikana na kukarisbishwa kila mahali na daima.

Moja ya maandiko yangu pendwa yanafundisha jinsi gani tunapaswa kumkaribia Baba yetu wa Mbinguni tunapopiga magoti ili kusali: “Jinyenyekeze na Bwana Mungu wako atakuongoza kwa mkono, na kukupa jibu la sala zako” (Mafundisho na Maagano 112:10). Tunapokuwa wanyenyekevu na watiifu, Baba wa Mbinguni atakuwa pamoja nasi. Yeye atatuongoza kwa kutushika mkono. Yeye atatutia msukumo wa wapi pa kwenda na nini cha kufanya. Yeye atatupa jibu la sala zetu kulingana na mapenzi Yake, njia, ratiba, na ufahamu kamili wa kile kilicho chema kwetu.

Tunapaswa kukumbuka hili na kuthamini fursa za kukikaribia kiti cha enzi cha Mungu na kupokea baraka mkononi Mwake.

Muhtasari

  1. Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith (2011), 4041.

  2. Teachings: Joseph Smith, 131.

Chapisha