2014
Maombi Ya Imani
Oktoba 2014


Ujumbe wa Urais wa Kwanza, Oktoba 2014

Maombi ya Imani

Picha
Rais Henry B. Eyring

Maombi ni zaidi ya maneno tunayozungumza na Mungu. Ni mawasiliano ya pande mbili kati ya Mungu na watoto Wake.

Wakati maombi yanapofanya kazi kama ipasavyo, tunatoa hisia za mioyo yetu kwa maneno rahisi. Baba wa Mbinguni kwa kawaida hujibu kwa kuweka mawazo katika fikra zetu yakiandamana na hisia. Yeye daima husikia maombi ya kweli tunayotoa tunapoomba kwa sharti la kumtii, kwa jibu Lake lolote na wakati wowote linapokuja.

Bwana anatoa ahadi hii kwa wale wote wanaosoma na kuomba juu ya Kitabu cha Mormoni:

“Na mtakapopokea vitu hivi, ningewashauri kwamba mngemwuliza Mungu, Baba wa Milele, katika jina la Kristo, ikiwa vitu hivi si vya kweli; na ikiwa mtauliza kwa moyo wa kweli, na kusudi halisi, mkiwa na imani katika Kristo, atawaonyesha ukweli wake kwenu, kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.

“Na kwa uwezo wa Roho Mtakatifu mtajua ukweli wa vitu vyote.” (Moroni 10:4–5).

Ahadi hiyo ni ya uhakika. Mamilioni ya watu wameonja na kuthibitisha ahadi hiyo ya ajabu juu ya sala kwa kupokea baraka ambayo imejaza maisha yao na shangwe na furaha ya kudumu. Ahadi hiyo inatumika kwa maombi yetu yote ili kujua nia na mapenzi ya Mungu kwa ajili yetu. Tunaweza kuitumia wakati wowote tunapopokea ushauri kutoka kwa mtumishi wa Mungu ambaye anamamlaka ya kutupa mwongozo. Kwa mfano, tunaweza kuitegemea wakati tunaposikiliza mahubiri katika mkutano mkuu. Tunaweza kuitumia wakati tunafundishwa na wamisionari wanyenyekevu walioitwa na Mungu kupitia nabii aliye hai. Inatumika vile vile kama ushauri tunaopokea kutoka kwa askofu wetu au rais wa tawi.

Ili maombi yaweze kufanya kazi katika maisha yetu, kanuni ni rahisi tu. Lazima tuulize ili tujue kile kilicho kweli kwa kuomba kwa Baba katika jina la Yesu Kristo. Lazima tuombe kwa moyo wa dhati, inayomaanisha kwamba ni lazima tuwe na nia thabiti ya kuweza kufanya chochote ambacho jibu la Mungu linahitaji kutoka kwetu. Na nia yetu halisi lazima itokane na imani yetu katika Yesu Kristo.

Mchunguzi anayesoma Kitabu cha Mormoni kabla ya kubatizwa na kuthibitishwa anaweza kupokea uhakika kwamba kitabu hicho ni cha kweli na ushuhuda kwamba Joseph Smith alikitafsiri kwa uwezo wa Mungu. Baada ya kuthibitishwa kuwa mshiriki wa Kanisa, tunaweza kuwa na Roho Mtakatifu kama rafiki yetu ili kuthibitisha kweli zingine. Kisha, wakati tunapoomba kwa imani, tunaweza kutarajia kwamba Roho Mtakatifu atatushuhudia kwamba Yesu ndiye Kristo, kwamba Mungu Baba anaishi, na kwamba Wao wanatupenda, na watoto wote wa Baba wa Mbinguni.

Hiyo ni sababu moja ya kuwa na ahadi katika Kitabu cha Mormoni kwamba tutakuwa na hisani katika mioyo yetu kadri Roho Mtakatifu anavyotushuhudia kwamba Yesu ndiye Kristo: “Na mtu akiwa mnyenyekevu na mpole katika moyo, na kukiri kwa uwezo wa Roho Mtakatifu kwamba Yesu ndiye Kristo, lazima awe na hisani” (Moroni 7:44).

Kuna fursa kubwa ya kukua kiroho kila Jumapili ya mfungo. Jumapili ya Mfungo inaweza kutusaidia kufikia uzoefu wa Alma na wana wa Mosia, ambao waliomba na kufunga ili kujua ukweli wa milele ili waweze kuwafundisha Walamani kwa nguvu, mamlaka, na upendo (ona Alma 17:3, 9).

Katika Jumapili ya mfungo sisi huunganisha maombi na kufunga. Kwa ajili ya kuwabariki maskini, sisi hutoa toleo karimu la mfungo kwa askofu au rais wa tawi ambalo linalingana karibu na thamani ya milo miwili tunayojinyima. Mawazo yetu na maombi yetu humgeukia Mwokozi na kwa wale ambao angetaka tuwatumikie kwa kushughulikia mahitaji yao ya kiroho na ya kimwili.

Hivyo Maombi yetu na shauku huja karibu na kuwa kama maombi na nia ya Mwokozi tunapofunga ili kuwa wanyenyekevu zaidi, wanaofundishika, na walio na upendo. Na kama alivyofanya Yeye, tunaomba ili kujua mapenzi ya Baba kwetu na kuyafanya.

Kufundisha kutoka katika Ujumbe huu

Rais Eyring anafundisha kwamba maombi na kufunga kunaweza kutusaidia “kujua ukweli wa milele.” Zingatia pale ushuhuda wa wale unaowatembelea unaweza kuhitaji uimarishaji na uandae somo juu ya mada hiyo. Kwa mfano, kama mtu unayemtembelea alipoteza rafiki wa karibu au mwana familia , zingatia kujadili familia za milele na maisha baada ya kifo. Unaweza kujitolea kufunga pamoja na wale unaowatembelea ili kuwasaidia kupata ushuhuda wa kanuni hiyo.

Chapisha