2017
Thawabu ya Kustahimili Vyema
July 2017


Ujumbe wa Urais wa Kwanza, Julai 2017

Thawabu ya Kustahimili Vyema

Nilipokuwa kijana, nilihudumu katika Kanisa kama mshauri kwa rais wa wilaya mwenye busara. Alikuwa mara kwa mara akijaribu kunifundisha. Nakumbuka ushauri alionipa hapo nyuma: “Unapokutana na watu, wewe watendee kana kwamba watu hao wako katika tatizo kubwa, na mara nyingi zaidi utakuwa sahihi kuliko kinyume chake.” Nilifikiri wakati huo kwamba alikuwa bila rajua. Sasa, zaidi ya miaka 50 baadae, Naweza kuona jinsi gani aliuelewa vyema ulimwengu na maisha.

Sisi wote tuna majaribu ya kukabiliana nayo—wakati mwingine, majaribu magumu sana. Tunajua kwamba Bwana anaturuhusu kupitia majaribu ili tuweze kukwatulia na kukamilishwa ili tuweze kuwa pamoja na Yeye milele.

Bwana alimfundisha Nabii Joseph Smith katika Jela ya Liberty kwamba thawabu ya kustahimili majaribu yake vyema itamsaidia yeye kufuzu kupata uzima wa milele:

“Mwanangu, amani iwe katika nafsi yako; taabu yako na mateso yako yatakuwa kwa muda mfupi tu;

“Na halafu, kama utastahimili vyema, Mungu atakuinua juu; nawe utawashinda maadui zako wote” (M&M 121:7–8).

Mambo mengi yanatuzonga katika maisha yetu kiasi kwamba inaweza kuonekana ni vigumu kustahmili vyema. Inawezekana kuonekana hivyo kwa familia inayoishi kwa kutegemea mazao wakati hakuna mvua. Wanaweza kujiuliza, “Ni kwa muda gani tunaweza kustahimili?” Inawezekana kuwa hivyo kwa kijana anayekabiliwa na kupingana na mafuriko ya uchafu na ya majaribu. Inawezekana kuonekana hivyo kwa kijana anayejitahidi sana kupata elimu au mafunzo anayohitaji kwa ajili ya kazi ili kumtunza mke na familia. Inawezekana kuonekana kwa njia hiyo kwa mtu ambaye hawezi kupata kazi au kwa yule ambaye amepoteza kazi moja baada ya nyingine na huku biashara zikifilisika. Inaweza kuonekana kwa njia hiyo kwa wale wanaokabiliwa na kudhoofika kwa afya na nguvu za kimwili, ambavyo vinaweza kuja mapema au baadaye maishani mwao au kwa wapendwa wao.

Lakini Mungu mwenye upendo hajayaweka majaribu kama hayo mbele yetu ili tu aone kama tunaweza kustahimili matatizo bali aone kama tunaweza kustahimili vyema na hivyo kukwatuliwa.

Urais wa Kwanza ulimfundisha Mzee Parley P. Pratt (1807–57) wakati alipokuwa ameitwa tu kuwa mshiriki wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili: “Umejiandikisha katika kazi ambayo inahitaji usikivu wako wote; … ili kuwa mwale iliokwatuliwa. …. Lazima uvumilie kazi za sulubu kali, kazi nyingi, na ufukara mkubwa ili kukwatuliwa kikamilifu. … Baba yako wa Mbinguni anataka hilo; shamba ni Lake; kazi ni Yake; na ata … kushangilia … na atakuchangamsha.”1

Katika kitabu cha Waebrania, Paulo anazungumzia juu ya tunda la kustahimili vyema: “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani” (Waebrania 12:11).

Majaribu yetu na matatizo yetu yanatupa fursa ya kujifunza na kukua, na yanaweza hata kubadili asili yetu. Kama tunaweza kumgeukia Mwokozi katika upeo wa dhiki yetu, roho zetu zinaweza kukwatuliwa tunapovumilia.

Kwa hiyo, kitu cha kwanza kukumbuka ni kuomba wakati wote (ona M&M 10:5; Alma 34:19–29).

Kitu cha pili ni kuendelea kujitahidi kushika amri—licha ya upinzani wowote ule, majaribu, au ghasia zinazotuzunguka (ona Mosia 4:30).

Kitu cha tatu muhimu sana kufanya ni kumtumikia Bwana (ona M&M 4:2; 20:31).

Katika huduma ya Bwana, tunakuja kumjua na kumpenda Yeye. Tutaweza, kama tutashikilia maombi na huduma ya uaminifu, kuanza kuutambua mkono wa Mwokozi na ushawishi wa Roho Mtakatifu katika maisha yetu. Wengi wetu kwa muda fulani tuliokuwa tumetoa huduma kama hiyo na tulipata kuuhisi uenzi huo. Kama ukifikiri nyuma wakati ule, utakumbuka kwamba kulikuwa na mabadiliko ndani yako. Majaribu ya kufanya uovu yalionekana kupungua. Hamu ya kufanya mema iliongezeka. Wale waliokujua vizuri sana na kukupenda waliweza kusema: “Umekua mkarimu zaidi na mvumilivu zaidi. Huonekani kuwa mtu yule yule.”

Hukuwa mtu yule yule. Ulibadilishwa kupitia Upatanisho wa Yesu Kristo kwa sababu ulimtegemea Yeye katika wakati wa majaribu yako.

Ninakuahidini ninyi kwamba Bwana atakuja kukusaidieni katika majaribu yenu kama mtamtafuta na kumtumikia Yeye na kwamba nafsi zenu zitakwatuliwa katika mchakato huo. Ninakupeni changamoto ya kuweka imani yenu Kwake katika dhiki yenu yote.

Ninajua ya kuwa Mungu Baba yu hai na kwamba husikiliza na anajibu kila ombi letu. Ninajua kwamba Mwanae, Yesu Kristo, alilipa deni la dhambi zetu zote na kwamba anatutaka sisi twende Kwake. Ninajua ya kwamba Baba na Mwana wanatulinda na wametayarisha njia kwa ajili yetu sisi ili tustahimili vyema na ili turudi nyumbani tena.

Muhtasari

  1. Autobiography of Parley P. Pratt, ed. Parley P. Pratt Jr. (1979), 120.

Chapisha