2017
Kulenga Kitovu
Januari 2017


Ujumbe wa Urais wa Kwanza, Januari 2017

Kulenga Kitovu

Hivi karibuni, niliona kundi la watu wakifanya zoezi la fani ya upigaji mishale. Kwa kutazama tu, ikawa wazi kwangu kwamba ikiwa unataka kuwa mweledi wa pinde na mshale, hiyo huchukua muda na mazoezi.

Mimi sidhani kuwa unaweza kukuza sifa za kuwa mpiga mishale mahiri kwa kupiga mishale kwenye ukuta mtupu na kisha kuchora dango kuzunguka ile mishale. Unahitaji kujifunza fani ya kulenga dango na kupiga katikati kabisa.

Kuchora Shabaha

Kupiga mishale kwanza na kisha kuchora dango baadaye inaweza kuonekana kama upuuzi, lakini wakati mwingine sisi wenyewe tunaakisi tabia hiyo sana katika hali nyingine za maisha.

Kama waumini wa Kanisa, tunapendelea kujiunganisha na mipango ya injili, mambo, na hata mafundisho ambayo yanaonekana kupendeza, muhimu, ama yenye kutuburudisha sisi. Tunajaribiwa kuchora madango kuyazunguka hayo, na kutufanya tuamini kuwa tunalenga kitovu cha injili.

Hili ni rahisi kufanya.

Kwa muda mrefu tumepokea ushauri bora sana na maongozi kutoka kwa manabii wa Mungu. Pia tunapokea maelekezo na ufafanuzi kutoka kwenye machapisho mbali mbali, vitabu vya maelekezo na vitabu vya kiada vya Kanisa. Sisi kwa urahisi zaidi tungeweza kuchagua mada tuipendayo ya injili, na kuchora dango katikati yake, na kudai kwamba tumekipata kitovu cha injili.

Mwokozi anafafanua:

Hii sio shida ya kipekee katika siku zetu. Hapo kale, viongozi wa kidini walitumia muda mwingi sana wakiorodhesha, wakiweka tabaka, na kujadili ni ipi katika mamia ya amri iliyo muhimu sana.

Siku moja kundi la wasomi wa kidini walijaribu kumwingiza Mwokozi katika mabishano hayo. Walimuomba Yeye atoe hoja yenye nguvu ambayo wachache wangeweza kukubaliana.

“Mwalimu,” walimuuliza Yeye, “katika torati ni amri ipi iliyo kuu?”

Sote tunajua jinsi Yesu alivyojibu: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote.

“Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza.

“Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako.

“Katika amri hizi mbili hutegemea torati yote na manabii.”1

Tafadhali tazama sentensi ya mwisho: “Katika amri hizi mbili hutegemea yote torati na manabii.”

Mwokozi sio tu alituonyesha sisi ile shabaha, bali Yeye pia ilionyesha katikati yake kabisa.

Kupiga Dango

Kama waumini wa Kanisa, tunafanya agano la kujichukulia juu yetu jina la Yesu Kristo. Kinachojitokeza katika hili agano ni uelewa wa kwamba tutajitahidi kujifunza juu ya Mungu, kumpenda Yeye, kuongeza imani yetu katika Yeye, kumheshimu Yeye, kutembea katika njia Yake, na kusimama imara kama mashahidi Wake.

Kadiri tunavyojifunza juu ya Mungu na kuona upendo Wake kwetu, ndivyo tunavyogundua zaidi kwamba dhabibu isiyo na mwisho ya Yesu Kristo ni zawadi takatifu kutoka kwa Mungu. Upendo wa Mungu hutupatia msukumo wa kutumia mapito ya toba ya kweli, ambayo yatatuongoza hadi kwenye muujiza wa msamaha. Huu mchakato hutuwezesha kuwa na upendo mwingi na huruma kwa wale wanaotuzunguka. Tutajifunza kuona zaidi ya kitambulisho chenye maelezo. Tutashinda majaribu ya kutuhumu au kuhukumu wengine kwa ajili ya dhambi zao, mapungufu yao, dosari zao, mwelekeo wao wa kisiasa, imani zao kidini, uraia, au rangi ya ngozi yao.

Tutamuona kila mmoja tunayekutana naye kama mtoto wa Baba yetu wa Mbinguni—kaka yetu ama dada yetu.

Tutawafikia wengine kwa uelewa na upendo—hata wale ambao yawezekana hatuwezi kuwapenda kwa urahisi. Tutaomboleza na wale wanaoomboleza na kuwafariji wale ambao wanahitaji kufarijiwa.2

Na tutagundua kwamba hakuna haja kwetu sisi kuhangaika kuhusu shabaha sahihi ya injili.

Zile amri kuu mbili ndiyo shabaha. Katika amri hizi mbili hutegemea torati yote na manabii.3 Tunapokubali haya, mambo yote mengine mazuri yataingia katika sehemu yake.

Kama lengo letu la msingi, mawazo, na jitihada zitazingatia ongezeko la upendo wetu kwa Mwenyezi Mungu na kufungua mioyo yetu kwa wengine, tunaweza kujua kwamba tumepata shabaha sahihi na tunalenga katikati kabisa—kuwa wafuasi wakweli wa Yesu Kristo.

Kufundisha kutokana na Ujumbe Huu

Kabla ya kufundisha ujumbe huu, mnaweza kuimba wimbo “Our Savior’s Love” (Hymns. no. 113). Kisha fikiria kuwahimiza wale unaowatembelea kutafakari juu ya “shabaha” katika maisha yao. Unaweza kujadili njia za kuhakikisha kwamba amri hizi kuu mbili—”kumpenda Bwana Mungu wako” na “kumpenda jirani yako kama unavyojipenda” (ona Mathayo 22:37, 39)—daima ndizo zinazoongoza matendo yako. Unaweza pia kuelezea njia mahsusi ambazo kwazo wewe mwenyewe umeyalenga maisha yako katika Kristo na utoe ushuhuda wa jinsi haya yalivyokubariki wewe.

Chapisha