Mafundisho na Maagano 2021
Agosti 8. Ninawezaje Kushiriki Katika Kukusanya Israeli? Mafundisho na Maagano 85–87


“Agosti 8. Ninawezaje Kushiriki Katika Kukusanya Israeli? Mafundisho na Maagano 85–87,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Akidi za Ukuhani wa Haruni na Madarasa ya Wasichana: Mada za Mafundisho 2021 (2020)

“Agosti 8. Ninawezaje Kushiriki Katika Kukusanya Israeli?” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Akidi za Ukuhani wa Haruni na Madarasa ya Wasichana: Mada za Mafundisho 2021

Picha
wavulana wakiwa mbele ya hekalu

Agosti 8

Ninawezaje Kushiriki Katika Kukusanya Israeli?

Mafundisho na Maagano 85–87

Picha
ikoni ya kushauriana kwa pamoja

Shaurianeni kwa Pamoja

Ikiongozwa na mshiriki wa urais wa akidi au wa darasa; takribani kwa dakika 10–20

Mwanzoni mwa mkutano, rudieni kwa pamoja Dhima ya Akidi ya Ukuhani wa Haruni au Dhima ya Wasichana. Kisha ongoza majadiliano kuhusu vitu kama vifuatavyo, na panga njia za kutenda juu ya kile mnachojadiliana (mnaweza kuamua katika mkutano wa urais ni vitu gani vya kujadili):

  • Akidi au darasa letu. Je, ni shughuli gani tumezifanya hivi karibuni? Je, zilifanikiwa? Ni nini kilifanyika vizuri, na ni jinsi gani tunaweza kuziboresha?

  • Wajibu wetu au majukumu. Ni nani anahitaji huduma yetu? Tunawezaje kuwasaidia?

  • Maisha yetu. Ni malengo gani tunayashughulikia kibinafsi? Ni uzoefu gani tunaweza kuushiriki? Ni baraka zipi tumepokea?

Mwishoni mwa somo, kama inafaa, fanya yafuatayo:

  • Shuhudia juu ya kanuni zilizofundishwa.

  • Wakumbushe washiriki wa akidi au darasa kuhusu mipango na mialiko iliyotolewa wakati wa mkutano.

Picha
ikoni ya kufundisha mafundisho

Fundisha Mafundisho

Ikiongozwa na kiongozi mtu mzima au kijana; takribani kwa dakika 25–35

Jiandae Binafsi Kiroho

Wale walioko kwenye akidi yako au darasa lako huenda wanajua kitu kuhusu majukumu yao ya kufanya kazi ya umisionari na hekalu na kazi ya historia ya familia. Lakini ukiongea nao kuhusu kukusanya Israeli, wanaweza wasijue unachoongelea. Unawezaje kuwasaidia waelewe kwamba kushiriki injili, kutafiti historia ya familia yao, na kufanya ibada hekaluni ni sehemu ya kazi kubwa sana ya kukusanya Israeli katika kujiandaa kwa Ujio wa Pili wa Mwokozi?

Wale unaowafundisha wanaweza kuwa wamesoma mfano wa ngano na magugu katika Mafundisho na Maagano 86, ambao hufundisha kuhusu kukusanya Israeli katika siku za mwisho. Unaposoma sehemu hii, jaribu kupiga taswira ya watu katika akidi yako au darasa lako wakiwa kama wafanyakazi katika shamba la Bwana. Je, utawezaje kuwasaidia kupata shangwe inayotokana na kushiriki katika kazi hii kuu? Kujifunza zaidi kuhusu mada hii, soma ujumbe wa Rais Russell M. Nelson na Dada Wendy W. Nelson “Tumaini la Israeli” ([ibada ya vijana duniani kote, Juni 3, 2018], Nyongeza kwenye New Era na Ensign, ChurchofJesusChrist.org).

Picha
msichana na mwanamke mtu mzima wakiangalia kompyuta

Wavulana na wasichana wanaweza kusaidia kukusanya Israeli kwa kufanya kazi ya hekaluni na historia ya familia.

Jifunzeni Pamoja

Unaweza kuanza kwa kuwauliza washiriki wa darasa maswali kama haya: Ni nini kilikuvutia ulipokuwa ukisoma Mafundisho na Maagano 86 nyumbani? Ulijifunza nini kuhusu kazi ya kukusanya watoto wa Mungu katika siku za mwisho? Tunafanya nini ili kushiriki katika kazi hii? Hapa chini ni mawazo ya ziada ya kuhamasisha akidi yako au darasa lako ili washiriki katika kukusanya Israeli.

  • Waulize washiriki wa akidi yako au darasa lako kile wanachofikiria wakati wanaposikia neno “kukusanya Israeli.” Kama wanahitaji msaada, pendekeza kwamba wasome ufafanuzi ufuatao wa Rais Russell M. Nelson: “Kukusanya Israeli hatimaye humaanisha kutoa injili ya Yesu Kristo kwa watoto wa Mungu katika pande zote mbili za pazia kwa wale ambao hawajafanya maagano muhimu na Mungu wala kupokea ibada zao za msingi. Kila mtoto wa Baba yetu wa Mbinguni anastahili kupata fursa ya kuchagua kumfuata Yesu Kristo, kuikubali na kuipokea injili Yake pamoja na baraka zake zote” (“Tumaini la Israeli,” 11–12). Ni kwa jinsi gani ufafanuzi huu huathiri jinsi tunavyofikiria kuhusu jukumu hili muhimu?

  • Ili kuwasaidia washiriki wa akidi au darasa kuona jinsi mfano wa ngano na magugu unavyotumika kwao, unaweza kuandika vifungu vya maneno kutoka Mafundisho na Maagano 86 ubaoni. Vifungu hivi vya maneno vinaweza kuelezea ishara katika mfano—kama vile “wapanda mbegu,” “magugu huikaba ngano,” “jani linapoanza kumea,” na “kukusanya ngano” (Mistari 2–4, 7). Vifungu vya maneno vinaweza pia kuelezea tafsiri za ishara hizi—kama vile “Mitume,” “Ukengeufu,” “Urejesho,” na “kazi ya umisionari.” Kisha washiriki wa akidi au darasa wanaweza kushirikiana kurejea sehemu ya 86 na kuoanisha ishara na maana zake. (Wanaweza pia kusoma Mathayo 13:36–43.) Je, tunajifunza nini kutoka kwenye mfano huu kuhusu kazi ya kukusanya Israeli? Tunaweza kufanya nini ili kufuata kuwa “nuru” na “mwokozi” kwa watoto wa Mungu? (Mafundisho na Maagano 86:11).

  • Washiriki wa akidi au darasa wanaweza kukumbuka kwamba katika ujumbe wake wa “Tumaini la Israeli,” Rais Russell M. Nelson aliwaalika kufanya vitu maalumu ili kujiandaa kusaidia katika kuikusanya Israeli (ona kurasa 14–17). Waulize ni mialiko gani wanaikumbuka, na pitieni mialiko kwa pamoja kama inavyohitajika. Ni kwa jinsi gani kufanya vitu hivi hutufanya tuwe wenye kufanya kazi vizuri zaidi katika kukusanya Israeli? Tunaweza kufanya nini ili kujikumbusha mialiko hii na kumsaidia kila mmoja wetu kuitimiza? Wahimize washiriki wa akidi au darasa kufikiri kwa ubunifu na kushiriki mawazo yao.

  • Washiriki wa akidi au darasa wanaweza kusoma utangulizi na sehemu mbili za mwanzo za ujumbe wa Mzee Quentin L. Cook “Upendo Mkuu kwa Watoto wa Baba Yetu” (Liahona, Mei 2019, 76–79), wakitafuta kwa nini upendo ni wa muhimu katika jitihada zetu za umisionari na hekalu na historia ya familia. Waombe washiriki kile walichojifunza kuhusu jinsi upendo unavyoweza kuleta tofauti kadiri tunavyojitahidi kushiriki injili pamoja na wale walioko pande zote mbili za pazia. Wape washiriki wa akidi au darasa muda wa kuandika kitu watakachopenda kufanya kwa sababu ya mjadala wa leo. Ili kuwasaidia kufikiria mawazo, unaweza kupendekeza kwamba wafikirie kuhusu watu wanaowajua. Je, ni kwa namna gani Mungu amekuwa akiwafikia watu hawa? Tunawezaje kusaidia?

Nyenzo Saidizi

  • Russell M. Nelson, “Kusanyiko la Israeli Iliyotawanyika,” Liahona, Nov. 2006, 79–82

  • Mada za Historia ya Kanisa, “The Gathering of Israel,” ChurchofJesusChrist.org/study/history/topics

Kufundisha katika Njia ya Mwokozi

Bwana aliwaamini wale waliomfuata Yeye. Aliwandaa na kuwapa majukumu muhimu ya kufundisha, kubariki na kuwatumikia wengine (ona Kufundisha katika Njia ya Mwokozi [2016], 28). Je, ni fursa gani ambazo unaweza kuzitoa kwa vijana ili wafundishane wao kwa wao?

Chapisha