Mafundisho na Maagano 2021
Agosti 22. Kwa nini Bwana Anataka Mimi Niwe Mwenye Afya? Mafundisho na Maagano 89–92


“Agosti 22. Kwa nini Bwana Anataka Mimi Niwe Mwenye Afya? Mafundisho na Maagano 89–92,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Akidi za Ukuhani wa Haruni na Madarasa ya Wasichana: Mada za Mafundisho 2021 (2020)

“Agosti 22. Kwa nini Bwana Anataka Mimi Niwe Mwenye Afya?” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Akidi za Ukuhani wa Haruni na Madarasa ya Wasichana: Mada za Mafundisho 2021

Picha
wasichana wakipanda mlima msituni

Agosti 22

Kwa nini Bwana Anataka Mimi Niwe Mwenye Afya?

Mafundisho na Maagano 89–92

Picha
ikoni ya kushauriana kwa pamoja

Shaurianeni kwa Pamoja

Ikiongozwa na mshiriki wa urais wa akidi au wa darasa; takribani kwa dakika 10–20

Mwanzoni mwa mkutano, rudieni kwa pamoja Dhima ya Akidi ya Ukuhani wa Haruni au Dhima ya Wasichana. Kisha ongoza majadiliano kuhusu vitu kama vifuatavyo, na panga njia za kutenda juu ya kile mnachojadiliana (mnaweza kuamua katika mkutano wa urais ni vitu gani vya kujadili):

  • Akidi au darasa letu. Je, ni nani mgeni katika kata yetu, na ni kwa jinsi gani tunaweza kuwasaidia kuhisi wamekaribishwa? Ni nini tunafanya ili kufanya muda wetu katika mikutano ya akidi au madarasa kuwa wa maana?

  • Wajibu wetu au majukumu. Ni yapi baadhi ya majukumu na wajibu tulionao kama wavulana na wasichana? Tunawezaje kuyatimiza vyema?

  • Maisha yetu. Ni nini tunafanya ili kuwa zaidi kama Yesu Kristo na kupokea nguvu Yake katika maisha yetu? Je, tunafanya nini ili kuzisaidia familia zetu kuja Kwake?

Mwishoni mwa somo, kama inafaa, fanya yafuatayo:

  • Shuhudia juu ya kanuni zilizofundishwa.

  • Wakumbushe washiriki wa akidi au darasa kuhusu mipango na mialiko iliyotolewa wakati wa mkutano.

Picha
ikoni ya kufundisha mafundisho

Fundisha Mafundisho

Ikiongozwa na kiongozi mtu mzima au kijana; takribani kwa dakika 25–35

Jiandae Binafsi Kiroho

Ni rahisi kwa baadhi ya watu kulichukulia Neno la Hekima, linalopatikana katika Mafundisho na Maagano 89, kama orodha ya vitu vya kufanya na kutokufanya. Neno la Hekima lina baadhi ya hayo, lakini pia linazo kanuni za kuufanya mwili wetu kuwa wenye afya. Pia linafundisha kwamba jinsi tunavyoitendea miili yetu huchangia kwenye afya yetu ya kiakili, kihisia, na kiroho. Je, ni baraka gani umezipokea wakati unapojitahidi kuishi maisha yenye afya?

Washiriki wa akidi yako au darasa lako wanaweza kuwa walisoma Neno la Hekima walipokuwa wakisoma Mafundisho na Maagano 89–92 wiki hii. Unawezaje kuwasaidia kuelewa baraka za kimwili na za kiroho zinazotokana na utii kwa ufunuo huu? Unaweza kupata utambuzi wenye kusaidia kwa kurejea makala ya Mada za Injili “Neno la Hekima” (topics.ChurchofJesusChrist.org) au “Afya ya Kimwili na Kihisia” katika Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana ([2011], 25–27).

Picha
wavulana wakipanda mlima msituni

Kuijali miili yetu huchangia katika afya zetu za kiakilia, kihisia, na kiroho.

Jifunzeni Pamoja

Kwa kuanza mjadala kuhusu Neno la Hekima, andika maneno haya ubaoni: Kimwili, Kiakili, Kiroho, na Kijamii. Waalike washiriki wa akidi au darasa kusoma Mafundisho na Maagano 89:18–21 na kujadili ni kwa jinsi gani ahadi zilizoko katika mistari zinaweza kutumika katika maeneo haya. Ni baraka zipi zinaweza kuja kwa kutii Neno la Hekima? Ni kwa jinsi gani tumepata uzoefu wa baraka hizi katika maisha yetu?

  • Washiriki wa akidi yako au darasa lako wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa wenzao kwa kuandaa orodha ya pamoja ya vitu wanavyofanya ili wawe wenye afya. Igawe akidi au darasa katika makundi, na lipangie kila kundi kutafuta kifungu kimoja au zaidi cha maandiko katika doti ya kwanza kwenye “Nyenzo Saidizi,” kutafuta kweli zinazohusu afya ya kimwili. Litake kila kundi lishiriki kile walichojifunza na orodhesha mawazo yao ubaoni. Ni majibu gani tutatoa kwa maswali kama yafuatayo: Kwa nini Mungu hutupatia sheria zihusianazo na afya ya kimwili? Kwa nini tunazitii?

  • Washiriki wa akidi yako au darasa lako wanaweza kuulizwa maswali kuhusu kwa nini hawanywi pombe, hawavuti sigara, au hawajihusishi na madawa ya kulevya. Ni kwa jinsi gani wanajibu maswali haya? Wanaweza kutafuta “Afya ya Mwili na Akili” katika Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana (25–27) na kupata ushauri na baraka zilizoahidiwa ambazo wanaweza kuzishiriki kwa wengine. Ni kwa jinsi gani tunavyoijali miili yetu huathiri mahusiano yetu na Mungu? Ni kwa jinsi gani washiriki wa akidi au darasa wamepokea shuhuda zao kwamba kutii Neno la Hekima kunabariki maisha yao?

  • Uzoefu ambao unaonyesha baraka za kutii Neno la Hekima unaweza kuwapa mwongozo wa kiungu washiriki wa akidi au darasa kuwa na msimamo zaidi wa kuishi sheria hii. Unaweza kushiriki uzoefu kutoka katika maisha yako au uzoefu alioushiriki Rais Thomas S. Monson katika ujumbe wake “Kanuni na Ahadi” (Liahona, Nov. 2016, 78–79). Video ya “Leave the Party” (ChurchofJesusChrist.org) inao mfano mwingine. Unaweza kuwahimiza washiriki wa akidi au darasa kushiriki uzoefu wao.

  • Kwa kuanza mjadala kuhusu jinsi ya kukabiliana na vishawishi vya kuvunja Neno la Hekima, unaweza kuwaonyesha akidi yako au darasa lako chambo wa kutegea samaki (au picha yake). Ni kwa jinsi gani chambo ya samaki huwadanganya samaki? Jibu kwa swali hili linaweza kupatikana katika video ya “You Will Be Freed” (ChurchofJesusChrist.org; ona pia M. Russell Ballard, “O That Cunning Plan of the Evil One,” Liahona, Nov. 2010, 108–10). Ni kwa jinsi gani chambo wa samaki wanafanana na kile ambacho Shetani hukifanya ili kutudanganya au kutufanyia hila? Ni ujumbe gani ambao Rais Ballard anao kwa wale walionaswa katika uraibu? Ni kwa jinsi gani tunaweza kumsaidia mtu anayetaabika na vishawishi kumgeukia Mwokozi? (ona maandiko katika doti ya pili kwenye “Nyenzo Saidizi”).

Tenda kwa Imani

Wahimize washiriki wa akidi au darasa kutafakari na kuandika kile watakachokifanya ili kutenda juu ya hisia ambazo wamezipokea leo. Ni kwa jinsi gani somo la leo linahusiana na malengo binafsi ambayo wameyaweka? Kama watapenda, washiriki wa akidi au darasa wanaweza kushiriki mawazo yao.

Nyenzo Saidizi

Kufundisha katika Njia ya Mwokozi

Katika hali zote, Mwokozi alikuwa mfano wetu na mnasihi. Unapojiandaa kufundisha, fikiria jinsi Bwana alivyowasiliana na wengine na jinsi unavyoweza kuwasiliana katika njia ambayo itainua na kuhimiza wale unaowafundisha.

Chapisha