Njoo, Unifuate
Septemba 30–Oktoba 13. Waefeso: ‘Kwa kusudi la Kuwakamilisha Watakatifu’


“Septemba 30–Oktoba 13. Waefeso: ‘Kwa kusudi la Kuwakamilisha Watakatifu’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya 2019 (2019)

“Septemba 30–Oktoba 13. Waefeso,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2019

Picha
familia ikitazama picha

Septemba 30–Oktoba 13

Waefeso

“Kwa Kusudi la Kuwakamilisha Watakatifu”

Je, unaona uhusiano wowote kati ya ujumbe katika mkutano mkuu na waraka wa Paulo kwa Waefeso?

Andika Misukumo Yako

Wakati injili ilipoanza kusambaa katika Efeso, ilisababisha “ghasia si haba” (Matendo ya Mitume 19:23) miongoni mwa Waefeso. Mafundi stadi wa mahali pale waliotengeneza madhabahu kwa mungu wa kike wa wapagani waliona Ukristo kama tishio kwa maisha yao, na punde “walijawa na ghadhabu, … na mji wote ukajaa ghasia” (ona Matendo ya Mitume 19:27–29). Fikiria kuwa muongofu mpya kwenye injili katika mazingira kama hayo. Waefeso wengi walipokea na kuishi injili katikati ya “hatari” hii (Matendo ya Mitume 19:40), na Paulo aliwahakikishia kwamba “Kristo … ndiye amani yetu” (Waefeso 2:13–14). Maneno haya, pamoja na mwaliko wake “acha uchungu wote, na ghadhabu, na hasira, na kelele, na matukano, yaondoke” (Waefeso 4:31) yanaonekana kuja kwa wakati na vya kutia faraja sasa kama ilivyokuwa wakati huo. Kwa Waefeso, kama ilivyo kwako, nguvu ya kukabiliana na majaribu huja “katika Bwana, na katika uweza wa nguvu zake” (Waefeso 6:10–13).

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo ya Kujifunza Maandiko Binafsi

Waefeso 1:4–11, 17–19

Je, Mungu “ameteua” au “ameamua mapema” baadhi ya watoto Wake kuokolewa?

Paulo aliongelea juu ya Watakatifu “kuamuliwa mapema” na Mungu na “kuchaguliwa … kabla ya kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu” ili kuwa watu wake. Kama Rais Henry B. Eyring alivyoona, ukweli kwamba watu wengi sana wanaishi na kufa bila nafasi ya kupokea injili husababisha baadhi “kuhitimisha kwamba Mungu lazima atakuwa ameamua mapema yupi kati ya watoto Wake angemwokoa na kufanya injili ipatikane kwao, wakati wale ambao hawakuwahi kuisikia injili ni kwamba tu ‘hawakuchaguliwa.’ Lakini … mpango wa Mungu ni wa upendo zaidi na zaidi hata ya hilo. Baba yetu wa Mbinguni anatamani kukusanya na kubariki familia Yake yote” (“Kukusanya Familia ya Mungu,” Ensign au Liahona, Mei 2017, 20–21). Watoto wote wa Mungu wanaweza kuikubali injili na ibada zake kwa sababu ya kazi inayofanyika kwa ajili ya wafu katika mahekalu matakatifu.

Japokuwa hakuna aliyeamuliwa mapema kuokolewa au kutookolewa, ufunuo wa siku hizi hufundisha kwamba baadhi walichaguliwa au “kutawazwa kabla” katika maisha kabla ya kuja ulimwenguni kutimiza majukumu fulani hapa duniani. Hii hujumuisha jukumu ambalo Watakatifu wa Siku za Mwisho wote wanalo kuhubiri injili na kuwasaidia watoto wote wa Mungu katika pande zote za pazia kuja kwa Kristo. (Ona pia “Kutawazwa Kabla,” Mada za Injili, topics.lds.org.)

Waefeso 1:10

Mungu “atavijumlisha vitu vyote katika Kristo.”

Je, umewahi kujiuliza “kipindi cha maongozi ya Mungu cha utimilifu wa nyakati” ni nini au inamaanisha nini kuvijumlisha vitu vyote katika Kristo”? Unapotafakari virai hivi, soma maandiko yafuatayo: Waefeso 4:13; 15:9–17; 2 Nefi 30:7–8; Mafundisho na Maagano 110:11–16; 112:30–32; 128:18–21. Unaweza kushawishika kuandika maelezo yako mwenyewe ya virai hivi.

Waefeso 2:19–22; 4:11–16

Kanisa lilianzishwa juu ya mitume na manabii, na Yesu Kristo mwenyewe akiwa jiwe kuu la pembeni.

Kusoma mafundisho ya Paulo kuhusu mitume na manabii kunaweza kukusaidia kujiandaa kusikia ujumbe wa mitume na manabii wa siku hizi wakati wa mkutano mkuu. Kulingana na Waefeso 2:19–22; 4:11–16, kwa nini tuna manabii na mitume? Je, ni kwa jinsi gani mafundisho yao yalikusaidia wewe “kutotupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu”?

Ona pia Matendo ya Mitume 4:10–12.

Picha
washiriki wa Urais wa Kwanza na Akidi ya Mitume Kumi na Wawili

Bwana huwaita manabii na mitume ili kuongoza Kanisa Lake.

Waefeso 5:21–6:4

Ninaweza kuimarisha uhusiano katika familia yangu.

Unaposoma Waefeso 5:21–6:4, ni mawazo gani hukujia kuhusu jinsi ya kuimarisha uhusiano wa familia yako?

Ni muhimu kukumbuka kwamba maneno ya Paulo katika Waefeso 5:22 yaliandikwa katika mazingira ya mila za kijamii za enzi yake. Manabii na mitume leo hufundisha kwamba wanaume si bora zaidi ya wanawake na kwamba wanandoa wanapaswa kuwa “wenza walio sawa” (ona “Familia: Tangazo kwa Ulimwengu,” Ensign au Liahona, Mei 2017, 145). Hata hivyo, bado unaweza kupata ushauri husika katika Waefeso 5:23–33, hasa kama uko katika ndoa au unajiandaa kwa ndoa. Kwa mfano, ni kwa jinsi gani Kristo huonyesha upendo Wake kwa Watakatifu? Hii hudokeza nini kuhusu jinsi wanaume wanavyopaswa kuwatendea wake zao? Ni ujumbe gani unaupata kwa ajili yako katika mistari hii?

Waefeso 6:10–18

Kuvaa “silaha zote za Mungu” kutasaidia kunilinda dhidi ya uovu.

Unaposoma Waefeso 6:10–18, fikiria kwa nini Paulo aliweza kutaja kila kipande cha silaha kwa jinsi alivyofanya. “Silaha zote za Mungu” zitatulinda dhidi ya nini? Je, unaweza kufanya nini ili kuvaa kikamilifu kila kipande cha silaha kila siku?

Ona pia 2 Nefi 1:23; Mafundisho na Maagano 27:15–18.

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia.

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani.

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zisisitizwe na kujadiliwa ili kukidhi mahitaji ya familia yako. Hapa kuna baadhi ya mapendekezo:

Waefeso 1:10

Kupitia Urejesho wa siku za mwisho, Mungu huvijumlisha vitu vyote pamoja, ikiwemo kanuni na ibada zote za injili. Kudhihirisha wazo hili, unaweza kuficha vitu au virai vilivyoandikwa kuzunguka nyumba yako ambavyo huwakilisha vitu ambavyo vimerejeshwa katika siku yetu (kama funguo za ukuhani, ibada za hekaluni, maandiko, na vipawa vya kiroho). Wana familia wanaweza kuvitafuta na “kuvikusanya” pamoja. Kwa nini sisi tunashukuru kuishi katika “kipindi hiki cha maongozi ya Mungu cha utimilifu wa nyakati”?

Waefeso 2:4–10; 3:14–21

Waalike wanafamilia waelezee uzoefu ambapo wamehisi upendo na rehema ya Mungu na Yesu Kristo iliyoelezewa katika mistari hii.

Waefeso 2:12–19

Familia yako inaweza kufurahia kujenga kuta kwa kutumia mito au vitu vingine mlivyonavyo nyumbani na kisha kuvibomoa. Ni aina zipi za kuta huwatenganisha watu leo? Ni kwa jinsi gani Yesu Kristo “amebomoa … ukuta uliyotutenga sisi” na Mungu?

Waefeso 6:10–18

Familia yako inaweza kujitengenezea wenyewe “silaha za Mungu” kwa kutumia vitu vya nyumbani. Filamu “Silaha za Mungu” (LDS.org) inaweza kuwasaidia wanafamilia kupata taswira ya silaha hizi, na wanaweza kupata maelezo rahisi katika “Silaha Zote za Mungu” (Friend, Juni 2016, 24–25). Ni kwa jinsi gani kila kipande cha silaha hutulinda kiroho? Je, tunaweza kufanya nini ili kusaidiana sisi kwa sisi “kuvaa silaha zote za Mungu” (Waefeso 6:11) kila siku?

Kwa mawazo zaidi juu ya kufundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii ndani ya Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Kuboresha Kujifunza Binafsi

Mwache Roho aongoze kujifunza kwako. Kuwa mwepesi kuhisi Roho anapokuongoza kwenye mambo unayohitaji kujifunza kila siku, hata kama hii hukuongoza kujifunza mada ambayo hukuipanga.

Picha
mtu katika silaha za enzi za Agano Jipya

Kuvaa silaha za Mungu kunaweza kutulinda kiroho.

Chapisha