Njoo, Unifuate
Oktoba 21–27. 1 na 2 Wathesalonike: ‘Msifadhaishwe Upesi hata Kuiacha Nia Yenu, wala Msisitushwe’


“Oktoba 21–27. 1 na 2 Wathesalonike: ‘Msifadhaishwe Upesi hata Kuiacha Nia Yenu, wala Msisitushwe’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya 2019 (2019)

“Oktoba 21–27. 1 na 2 Wathesalonike,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2019

Picha
wamisionari wasichana wakiongea na kijana wa kiume

Oktoba 21–27

1 na 2 Wathesalonike

“Msifadhaishwe Upesi hata Kuiacha Nia Yenu, wala Msisitushwe”

Kama hatuandiki misukumo tunayopokea kutoka kwa Roho Mtakatifu, tunaweza kusahau. Je, Roho anakushawishi kuandika nini unaposoma 1 na 2 Wathesalonike?

Andika Misukumo Yako

Katika Thesalonike, Paulo na Sila walishitakiwa kwa “kuupindua ulimwengu” (Matendo17:6). Mahubiri yao yaliwakasirisha viongozi fulani miongoni mwa Wayahudi, na viongozi hawa walichochea watu kufanya ghasia (ona Matendo ya Mitume 17:1–10). Matokeo yake, Paulo na Sila walishauriwa kuondoka Thesalonike. Paulo alihofia kuhusu waongofu wapya wa Thesalonike na mateso waliyokuwa wakipata, lakini hakuweza kurudi kuwatembelea. “Nilipokuwa siwezi kuvumilia tena,” aliandika, “Nalituma mtu ili kujua imani yenu.” Katika kujibu, Timotheo msaidizi wa Paulo, aliyekuwa akitumikia katika Thesalonike, “alituletea habari njema za imani yenu na upendo wenu” (1 Wathesalonike 3:5–6). Hata hivyo, Watakatifu wa Thesalonike walijulikana kama vielelezo “kwa watu wote waaminio” (1 Wathesalonike 1:7), na habari kuhusu imani yao ilisambaa katika miji ya mbali. Fikiria shangwe na faraja ya Paulo kusikia kwamba kazi yake miongoni mwao “haikuwa bure” (1 Wathesalonike 2:1). Lakini Paulo alijua kwamba uaminifu katika kipindi cha nyuma hautoshi kuendelea kuishi katika siku za baadaye, na alikuwa mwangalifu juu ya ushawishi wa walimu wa uongo kati ya Watakatifu (ona 2 Wathesalonike 2:2–3). Ujumbe wake kwao, na kwetu, ni kuendelea “kuyatengeneza mapungufu ya imani [yetu]” na “kuzidi sana” katika upendo (ona 1 Wathesalonike 3:10; 4:10).

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo ya Kujifunza Maandiko Binafsi

1 Wathesalonike 1–2

Wahudumu wa injili huhubiri kwa uaminifu na upendo.

Katika 1 Wathesalonike, maneno ya Paulo huonyesha vyote kujali na shangwe ya mtu ambaye amejitoa mwenyewe kikamilifu kuwatumikia watoto wa Mungu. Hasa katika sura mbili za mwanzo za 1 Wathesalonike, utakuta maneno na virai ambavyo huelezea jinsi mhubiri wa kweli anavyofundisha injili. Je, unashawishika kufanya nini ili kuboresha ufundishaji wako wa injili?

1 Wathesalonike 3:9–4:12

Ninapomfuata Yesu Kristo, Ninaweza kuwa mtakatifu.

Sote tunatumaini kwamba katika “ujio wa Bwana wetu,” tutaweza kusimama mbele Zake kwa “mioyo isiyo na lawama katika utakatifu mbele za Mungu” (1 Wathesalonike 3:13). Je, Paulo alifundisha nini kuhusu kuwa watakatifu zaidi katika 1 Wathesalonike 3:9–13; 4:1–12?

Ona pia Moroni 10:32–33; Kamusi ya Biblia, “Utakatifu”; Carol F. McConkie, “Uzuri wa Utakatifu,” Ensign au Liahona, Mei 2017, 9–12.

1 Wathesalonike 4:16–18; 5:1–10; 2 Wathesalonike 1:4–10

Kama mimi ni mwaminifu na mwangalifu, nitatayarishwa kwa Ujio wa Pili wa Mwokozi.

Katika 1 Wathesalonike 5:1–10, Paulo alitumia sitiari kadhaa kufundisha kweli za muhimu kuhusu wakati Yesu atakaporudi duniani. Unapojifunza sitiari hizi, fikiria kuandika misukumo inayokujia kuhusu Ujio wa Pili wa Yesu Kristo:

“Mwivi ajavyo usiku”:

“Utungu umjiavyo mwenye mimba”:

Sitiari zingine unazopata:

Ni kweli zipi za ziada unajifunza kuhusu Ujio wa Pili wa Yesu Kristo kutoka 1 Wathesalonike 4:16–18; 5:1–10; 2 Wathesalonike 1:4–10? Wewe unashawishika kufanya nini ili kujihadhari na kujiandaa kwa ajili ya ujio Wake?

Ona pia Dallin H. Oaks, “Maandalizi kwa Ujio wa Pili,” Ensign au Liahona, Mei 2004, 7–10.

2 Wathesalonike 2

Ukengeufu, au kuanguka kutoka kwenye ukweli, kulitabiriwa kutangulia Ujio wa Pili.

Katikati ya ongezeko la mateso, wengi wa Watakatifu wa Thesalonike waliamini Ujio wa Pili wa Mwokozi lazima ulikaribia. Lakini Paulo alijua kwamba kabla ya Yesu kurudi duniani kungekuwepo na ukengeufu—uasi au “kuanguka” kutoka kwenye ukweli (ona 2 Wathesalonike 2:1–4). Unaweza kupanua uelewa wako juu ya Ukengeufu Mkuu—na shukrani zako kwa ajili ya Urejesho—kwa kutafiti baadhi ya nyenzo zifuatazo:

  • Maandiko yaliyotabiri Ukengeufu: Isaya 24:5; Amos 8:11–12; Mathayo 24:4–14; 2 Timothy 4:3–4

  • Maandiko yanayoonyesha ukengeufu ulikuwa tayari umeanza katika wakati wa Paulo: Matendo ya Mitume 20:28–30; Wagalatia 1:6–7; 1 Timotheo 1:5–7

  • Uchunguzi kuhusu Ukengeufu Mkuu uliofanywa na waleta mabadiliko wa Kikristo:

    Martin Luther: “Sikutafuta kingine zaidi ya kuleta mabadiliko kwa Kanisa katika kuendana na Maandiko Matakatifu. … Kwa urahisi ninasema kwamba Ukristo umetoweka kati ya wale ambao walipaswa kuutunza” (katika E. G. Schweibert, Luther and His Times: The Reformation from a New Perspective [1950], 590).

    Roger Williams: “Ukengeufu … mpaka sasa umeharibu kila kitu kwamba hakuwezi kuwepo na kupona kutokana na huo ukengeufu mpaka Kristo atume mitume wapya kupanda upya makanisa” (katika Philip Schaff, The Creeds of Christendom [1877], 851).

    Erasmus: “Kila kitu sasa ni cha kutatanisha kwa maswali haya [ya mafundisho] na maagizo kiasi kwamba hatudiriki hata kutumaini kuuita ulimwengu urudi kwenye Ukristo wa kweli” (The Praise of Folly, trans. Clarence H. Miller, toleo la 2. [2003], 155–56).

Ona pia 2 Nefi 28; “Ukengeufu,” Mada za Injili, topics.lds.org.

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia.

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani.

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zijadiliwe kulingana na mahitaji ya familia yako. Hapa kuna baadhi ya mapendekezo:

1 Wathesalonike 3:9–13

Je, ni nini kinachokupendeza kuhusu hisia alizokuwa nazo Paulo kwa rafiki zake? Je, ni kwa jinsi gani tunaweza kulea hisia kama hizo kwa familia zetu, marafiki, na Watakatifu wenzetu?

1 Wathesalonike 4:13–18

Je, ni kwa jinsi gani tunaweza kutumia mistari hii kujipa faraja wenyewe au mtu mwingine wakati mpendwa anapofariki?

1 Wathesalonike 5:14–25

Pitia tena ushauri wa Paulo katika 1 Wathesalonike 5:14–25, na tafuta kirai ambacho watu wa familia yako wangependa kuzingatia. Fikiria kukiandika kwenye bango la kuweka nyumbani kwako. Wanafamilia wanaweza kuongeza maandishi kwenye bango wanapoona kila mmoja akiishi kwa ushauri ulioko kwenyse bango.

2 Wathesalonike 3:13

Je, tumewahi kuhisi “kuchoka katika kutenda mema”—kuzidiwa, pengine, na mahitaji ya ufuasi? Je, ni kitu gani hutusaidia tunapojisikia hivyo” (Ona Wagalatia 6:9; M&M 64:33.) Ni kwa jinsi gani tunaweza kusaidiana wakati hili linapotokea?

Kwa mawazo zaidi juu ya kufundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii ndani ya Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Kuboresha Kujifunza Binafsi

Tafuta Ufunuo Kila Siku. “Ufunuo mara nyingi huja ‘mstari juu ya mstari’ (2 Nefi 28:30), wala sio wote kwa wakati mmoja. … Usifikirie [kujifunza injili] kama shughuli ambayo unaitengea muda bali kama vile tu shughuli ambayo unaifanya kila wakati” (Kufundisha katika Njia ya Mwokozi, 12).

Picha
Yesu akiwa mawinguni

Kristo Mfufuka, na Robert T. Barrett

Chapisha