Agano la Kale 2022
Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko kwa Familia Yako


“Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko kwa Familia Yako,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano la Kale 2022 (2021)

“Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko kwa Familia Yako,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu binafsi na Familia: 2022

Picha
mtoto na mama wakijifunza maandiko nyumbani

Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko kwa Familia Yako

Kujifunza maandiko kwa familia kila mara ni njia yenye nguvu zaidi katika kuisaidia familia yako kujifunza injili. Ni kiasi gani na kwa muda gani mnasoma kama familia siyo muhimu kama vile kuwa thabiti katika jitihada zenu. Unapofanya kujifunza kwako maandiko kuwa sehemu muhimu ya maisha ya familia yako, utawasaidia wanafamilia yako kuja karibu na Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo na kujenga shuhuda zao juu ya msingi wa neno Lake.

Fikiria maswali yafuatayo:

  • Je, ni kwa jinsi gani unaweza kuwatia moyo wanafamilia kusoma maandiko peke yao?

  • Je, unaweza kufanya nini cha kuwatia moyo wanafamilia kushiriki kile wanachojifunza?

  • Je, ni kwa jinsi gani unaweza kusisitiza kanuni unazojifunza katika Agano la Kale katika nyakati za kila siku za kujifunza.

Kumbuka kwamba nyumbani ni mahali bora pa kujifunza injili. Unaweza kujifunza na kufundisha injili nyumbani katika njia ambazo haziwezekani katika darasa la Kanisani. Kuwa mbunifu unapofikiria njia za kuisaidia familia yako kujifunza kutoka kwenye maandiko. Fikiria baadhi ya mawazo yafuatayo ili kuboresha kujifunza maandiko kwa familia yako.

Tumia Muziki.

Imbeni nyimbo zinazoimarisha kanuni zinazofundishwa katika maandiko. Wimbo uliopendekezwa au wimbo wa watoto umeorodheshwa katika kila muhtasari wa wiki. Unaweza kuwauliza mwana familia maswali kuhusu maneno au virai katika maneno ya nyimbo. Kwa kuongezea kwenye kuimba, familia yako inaweza kutenda vitendo vinavyoendana na nyimbo au kusikiliza nyimbo zikiimbwa taratibu wakati wakifanya shughuli zingine. Kwa mawazo zaidi, ona “Kujumuisha Muziki Mtakatifu katika Kujifunza Injili Kwako” katika nyenzo hii.

Shiriki Maandiko Yenye Maana Zaidi

Wape wanafamilia muda wa kuelezea vifungu vya maandiko ambavyo wameona vina maana zaidi wakati wa kujifunza kwao binafsi.

Tumia Maneno Yako Mwenyewe.

Waalike wanafamilia kufanya muhtasari kwa maneno yao wenyewe kile wanachojifunza kutoka kwenye maandiko mnayojifunza.

Picha
kijana akimsaidia mtoto mdogo kusoma maandiko

Tumia Maandiko katika Maisha Yako

Baada ya kusoma kifungu cha maandiko, waalike wanafamilia kuelezea jinsi kifungu hicho kinavyohusiana na maisha yao.

Uliza Swali

Waalike wanafamilia kuuliza swali la injili, na kisha kutumia muda kutafuta mistari inayoweza kusaidia kujibu swali hilo.

Onyesha picha.

Chagua mstari unaouona una maana, na ubandike mahali ambapo wanafamilia watauona mara kwa mara. Waalike wanafamilia wengine kufanya zamu ya kuchagua andiko la kubandika.

Tengeneza Orodha ya Maandiko

Kama familia, chagueni mistari kadhaa ambayo mngependa kujadili wiki inayofuata.

Kariri Maandiko

Chagua kifungu cha maandiko ambacho kina maana kwa familia yako, na waalike wanafamilia kukikariri kwa kukirudia kila siku au kucheza mchezo wa kukariri.

Picha
watu wakiimba pamoja nyumbani

Shiriki Masomo ya Vitendo

Tafuta vitu ambavyo vinahusiana na kanuni za injili katika mistari ambayo mnasoma kama familia. Waalike wanafamilia kuongelea jinsi kila kitu kinavyohusiana na mafundisho katika maandiko.

Chagua Mada

Waalike wanafamilia kufanya zamu za kuchagua mada ambayo familia itajifunza pamoja. Tumia Mwongozo wa Mada, Kamusi ya Biblia, au Mwongozo wa Maandiko (scriptures.lds.org) ili kutafuta vifungu vya maandiko kuhusu mada.

Chora picha

Someni mistari michache kama familia, na kisha toa muda kwa wanafamilia kuchora kitu kinachohusiana na kile mnachokisoma. Tumieni muda kujadili mchoro wa kila mmoja.

Igiza Hadithi

Baada ya kusoma hadithi, waalike wanafamilia kuiigiza. Baadaye, zungumzieni kuhusu jinsi hadithi inavyohusiana na mambo mnayopitia kibinafsi na kama familia.

Rais Russell M. Nelson alisema: “Ninakuahidi ya kwamba utakapofanya bidii kupanga upya nyumba yako kuwa kituo cha kujifunza injili, baada ya muda Siku zako za Sabato zitakuwa takatifu sana. Watoto wako watafurahia kujifunza na kuishi mafunzo ya Mwokozi, na ushawishi wa adui katika maisha yako na katika nyumba yako utapungua. Mabadiliko katika familia yako yatakuwa ya kuvutia na endelevu” (“Kuwa Mtakatifu wa Siku za Mwisho wa Mfano,” Ensign au Liahona, Nov. 2018,113).

Chapisha