Agano Jipya 2023
Agosti 13. Ni kwa Jinsi Gani Yesu Kristo Anaweza Kunisaidia Kubadilika? Warumi 1–6


Agosti 13. Ni kwa Jinsi Gani Yesu Kristo Anaweza Kunisaidia Kubadilika? Warumi 1–6,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Akidi za Ukuhani wa Haruni na Madarasa ya Wasichana: Mada za Mafundisho 2023 (2022)

“Agosti 13. Ni kwa Jinsi Gani Yesu Kristo Anaweza Kunisaidia Kubadilika?,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Akidi za Ukuhani wa Haruni na Madarasa ya Wasichana: Mada za Mafundisho 2023

Picha
ubatizo

Agosti 13

Ni kwa Jinsi Gani Yesu Kristo Anaweza Kunisaidia Kubadilika?

Warumi 1–6

Picha
ikoni ya kushauriana kwa pamoja

Shaurianeni kwa Pamoja

Ikiongozwa na mshiriki wa urais wa darasa au akidi; takribani kwa dakika 10–20

Mwanzoni mwa mkutano, rudieni kwa pamoja Dhima ya Wasichana au Dhima ya Akidi ya Ukuhani wa Haruni. Kisha ongoza mjadala kuhusu kazi ya wokovu na kuinuliwa ukitumia swali moja ua mengi ya yale yaliyopo hapo chini au yako mwenyewe (ona Kitabu cha Maelezo ya Jumla, 10.2, 11.2). Panga njia za kutenda juu ya kile mnachojadili.

  • Ishi injili. Ni kwa jinsi gani ninaweza kupata furaha kwa kumfuata Yesu Kristo?

  • Kuwajali wenye mahitaji. Nani katika kata yetu au jamii yetu anahitaji msaada wetu? Tunawezaje kuwasaidia?

  • Waalike wote kuipokea injili. Je, ni kwa jinsi gani tunaweza kusaidiana kujiandaa kwa ajili ya huduma ya ummisionari?

  • Unganisha familia milele. Je, Tunaweza kuchangia vipi katika juhudi za kata za kazi ya historia ya familia na kazi ya hekaluni?

Mwishoni mwa somo, kama inafaa, fanya yafuatayo:

  • Shuhudia juu ya kanuni zilizofundishwa.

  • Wakumbushe washiriki wa darasa au akidi kuhusu mipango na mialiko iliyotolewa wakati wa mkutano.

Picha
ikoni ya kufundisha mafundisho

Fundisha Mafundisho

Mkiongozwa na kiongozi mtu mzima au kijana; takribani kwa dakika 25–35

Jiandae Binafsi Kiroho

“Injili ya Yesu Kristo ni injili ya mabadiliko!” Rais Russell M. Nelson alisema, (“Maamuzi ya Milele,” Liahona, Nov. 2013, 108). Vivyo hivyo, Mtume Paulo alielezea kwamba wakati tunapobatizwa, sisi “tunaenenda katika upya wa uzima” (Warumi 6:4). Kwa sababu ya Yesu Kristo, kila siku—sio tu siku tunayobatizwa—inaweza kuleta “upya wa uzima” au fursa ya kuenenda mbali na dhambi na karibu na Mungu. Kuishi Injili ya Yesu Kristo humaanisha kutubu na kusogea karibu na Mungu—kila mara, wakati mwingine polepole—tukijua kwamba juhudi zetu zituelekeza kwenye ujalivu wa shangwe.

Tafakari jinsi Mwokozi anakubadilisha wewe na watu unaowafundisha. Je, ni kwa jinsi gani tunaweza kupokea kikamilifu nguvu ya Mwokozi ya kutubadilisha? Fikiria kuhusu hili unaposoma Warumi 1–6 na unapojiandaa kufundisha. Ungeweza pia kupitia tena ujumbe wa Rais Russell M. Nelson “Tunaweza Kufanya Vizuri Zaidi na Kuwa Wazuri Zaidi” (Liahona, Mei 2019, 67–69) au ujumbe wa Dada Becky Craven “Hifadhi Mabadiliko” (Liahona, Nov. 2020, 58–60).

Jifunzeni Pamoja

Kwa baadhi yetu, “upya wa uzima” ambao Kristo anatoa (Warumi 6:4) ni vigumu kuutambua kwa sababu hutokea pole pole, hali kwa wengine, mabadiliko haya hutokea kwa upesi zaidi. Ungeweza kuwaalika washiriki wa darasa au akidi kushiriki kile “kuenenda katika upya wa uzima” humaanisha kwao. Ni baadhi ya maneno na virai gani kutoka katika Warumi 6 ambavyo vinaelezea maisha yetu tukiwa na au bila ushawishi wa Mwokozi? (Kama vijana wanahitaji msaada, wangeweza kuangalia katika mstari wa 6, 11, 22–23.) Ni maneno na virai gani tunaweza kufikiria? Ni kwa jinsi gani Mwokozi anatoa msaada kutusaidia kubadilika? Shughuli kama hii ifuatayo inaweza kuongoza hadi kwenye mjadala wa kina katika mada hii.

  • Ili kusaidia darasa au akidi kufikiria kuhusu mabadiliko Mwokozi angeweza kuwasaidia kufanya, waalike wao kusoma maelezo chini ya “Tubu, Toba” katika Mwongozo wa Maandiko (scriptures.ChurchofJesusChrist.org). Wangeweza pia kujadili maelezo ya toba ya Rais Russell M. Nelson katika aya saba za kwanza katika ujumbe wake “Tunaweza Kufanya Vizuri Zaidi na Kuwa Wazuri Zaidi.” Ni kweli gani muhimu tunajifunza kuhusu toba kutoka katika maelezo haya? Ungeweza pia kuwapa muda darasa au akidi kutafakari orodha ya Rais Nelson ya vitu ambavyo Yesu ametuomba kubadilisha (katika aya ya tano ya ujumbe wake. Wahimize waandike kitu mahsusi wanachopata ushawishi kukibadilisha. Toa ushuhuda wako wa nguvu ya Mungu ya kutusaidia kutubu na kubadilika.

  • Dada Becky Craven alisema kwamba marafiki wake wa zamani wakati mwingine walisema, “Haujabadilika hata kidogo! Ungeweza kushiriki maneno ya Dada Craven kuhusu hili (ona “Hifadhi Mabadiliko,” 59–60). Waombe washiriki wa darasa au akidi kufikiria kwamba katika miaka mitano au kumi, watakutana na rafiki wa zamani. Je, ni mabadiliko gani yangekuwa wazi kwa marafiki zao? Ni katika njia gani tutatarajia tuwe tumebadilika? Ni kwa jinsi gani imani katika Yesu Kristo hutusadia kubadilika? (Ona Mosia 5:2–5, 7; Alma 5:11–13; Etheri 12:27, au “mpangilio endelevu wa mabadiliko” Dada Craven alioelezea katika aya nne za ujumbe wake kuanzia “Nilipokuwa mdogo”). Ungeweza kuwaomba wao kushiriki uzoefu wowote wakati Yesu Kristo alipowasaidia kubadilika.

  • Wakati mwingine tunaweza kufikiria kwamba tunatarajiwa kufanya mabadiliko au kuboreka katika maisha yetu sisi wenyewe peke yetu. Ni kwa jinsi gani hii ni tofauti na toba ya kweli? Ili kusaidia darasa lako au akidi yako kujadili swali hili, mngeweza kupitia tena maandiko katika “Nyenzo Saidizi.” Nini tunaweza kufanya sasa kutafuta msaada na nguvu ya Mwokozi ili kwamba mabadiliko yetu yawe ya kudumu na shangwe? Hii ingeweza kuwa fursa nzuri ya vijana kufikiria malengo yao binafsi ya ukuaji. Je, ni kwa jinsi gani tunaweza kumjumuisha Mwokozi katika malengo yetu?

Picha
wasichana wakitembea

Imani katika Yesu Kristo hutusaidia kutubu na kuwa zaidi kama Yeye kila siku.

Tenda kwa Imani

Watie moyo washiriki wa darasa au akidi kutafakari na kuandika kile watakachofanya juu misukumo waliyoipokea leo. Kama wangependa, wangeweza kushiriki mawazo yao. Waalike wafikirie kuhusu jinsi kutenda juu ya misukumo yao kutaimarisha mahusiano yao na Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo.

Nyenzo Saidizi

  • Rais Russell M. Nelson alielezea: “Tunaweza kubadili tabia zetu. Tamaa zetu zinaweza kubadilika. Kivipi? Kuna njia moja tu. Mabadiliko ya kweli—mabadiliko ya kudumu—yanaweza kuja tu kupitia uponyaji, usafishaji, na uwezo wa nguvu za Upatanisho wa Yesu Kristo. Yeye anawapenda—kila mmoja wenu! Yeye hukuruhusu wewe kufikia nguvu Yake unapozishika amri Zake, kwa moyo, kwa dhati, na kwa kutii” (“Maamuzi ya Milele,” 108).

  • Mzee Dale G. Renlund alifundisha: “Nguvu inayowezesha toba, dhabihu ya upatanisho ya Mwokozi wetu. Toba halisi lazima ihusishe imani katika Bwana Yesu Kristo, imani kwamba Yeye anaweza kutubadilisha, imani kwamba Yeye anaweza kutusamehe, na imani kwamba Yeye atatusaidia kuepuka makosa zaidi. Aina hii ya imani hufanya Upatanisho Wake kuwa hai katika maisha yetu. Tunapojua … ‘kugeuka kutoka’ [tubu] kwa usaidizi wa Mwokozi, tunaweza kuhisi matumaini katika ahadi Zake na furaha ya msamaha. Bila Mkombozi, matumaini haya ya asili na furaha huyeyuka, na toba huwa tu mabadilisho duni ya tabia. Lakini kwa kudhihirisha imani Kwake, tunaongoka kwa uwezo Wake na utayari Wake wa kusamehe dhambi (Dale G. Renlund, “Toba: Chaguo la Furaha,” Liahona, Nov. 2016, 122).

Kufundisha katika Njia ya Mwokozi

Shughuli katika muhtasari huu hupendekeza njia yamkini za kusaidia darasa ua akidi kujifunza pamoja kuhusu Mwokozi na nguvu Yake ya kutusaidia kubadilika. Kunaweza kuwa na mbinu zingine ambazo zitaweza kufanya kazi hata vizuri zaidi kwa wale unaowafundisha. Kwa maombi tafuta uongozi wa Roho unapopanga njia za kujenga imani katika Yesu Kristo.

Chapisha