Njoo, Unifuate
Juni 15–21. Alma 13–16: “Ingia Katika Pumziko la Bwana”


“Juni 15–21. Alma 13–16: ‘Ingia Katika Pumziko la Bwana,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Kitabu cha Mormoni 2020 (2020)

“Juni 15–21. Alma 13–16,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia 2020

Picha
Alma na Amuleki wakitoka gerezani

Kielelezo cha Alma na Amuleki wakikombolewa kutoka gerezani, na Andrew Bosley

Juni 15–21

Alma 13–16

“Ingia Katika Pumziko la Bwana”

Msukumo unaopokea wakati unapotafakari kuhusu maandiko ni wa thamani kubwa. Unaweza kuonyesha kwamba unauthamini kwa kuuandika na kutenda kulingana nao.

Andika Misukumo Yako

Katika njia nyingi, maisha katika Amoniha yalikuwa yamekuwa mazuri kwa wote Amuleki na Zeezromu. Amuleki alikuwa “sio mtu aliye na heshima ndogo,” mwenye “jamaa na marafiki wengi” na “utajiri mwingi” (Alma 10:4). Zeezromu alikuwa “mwenye ujuzi mwingi” miongoni mwa mawakili na alifurahia “shughuli nyingi” (Alma 10:31). Kisha Alma akawasili katika Amoniha akiwa na mwaliko mtukufu wa kutubu na “kuingia katika pumziko la Bwana” (Alma 13:16). Kwa Amuleki, Zeezromu, na wengine, kukubali mwaliko huu kulihitaji dhabihu na hata kulisababisha shida zilizokaribia kutowezekana kuvumiliwa.

Lakini bila shaka hadithi hii haikomei hapo. Katika Alma 13–16, tunajifunza kile ambacho hatimaye hutokea kwa wale wanaoamini “katika nguvu za wokovu za Kristo” (Alma 15:6). Wakati mwingine kuna ukombozi, wakati mwingine uponyaji—na wakati mwingine hali huenda isibadilike na kuwa rahisi katika maisha haya. Lakini daima, “Bwana mwenyewe anawapokea [watu Wake] kwa utukufu” (Alma 14:11). Daima, Bwana hutupatia “uwezo, kulingana na imani [yetu] katika Kristo” (Alma 14:28). Na daima, hiyo “imani katika Bwana” inatupatia “tumaini kwamba [sisi] tutapokea uzima wa milele” (Alma 13:29). Unaposoma sura hizi, unaweza kupata faraja katika ahadi hizi, na unaweza kuja kuelewa vizuri zaidi kile ambacho Alma alimanisha wakati alipozungumza kuhusu “pumziko la Bwana.”

Picha
ikoni ya kujifunza kibinafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kibinafsi

Alma 13:1–19

Ibada za ukuhani zinanisaidia kupokea ukombozi kupitia Yesu Kristo.

Unaweza kukumbuka ya kwamba katika Alma 12, Alma alifundisha kuhusu mpango wa Mungu wa wokovu (ona Alma 12:24–27). Katika sura ya 13, alizungumza kuhusu makuhani ambao Mungu aliwatawaza “kufunza watu vitu hivi” (Alma 13:1). Maneno ya Alma yanafunua kweli nyingi zenye nguvu kuhusu ukuhani. Pengine unaweza ukajaribu kutambua angalau ukweli mmoja kutoka kwenye kila mstari katika Alma 13:1–9. Haya ni baadhi ya mawazo kukuwezesha kuanza:

Mstari wa 1:Ukuhani pia unaitwa “kwa mfano wa Mwana wa [Mungu]” (ona pia M&M 107:1–4).

Mstari wa 2:Mungu huwatawaza makuhani ili kuwasaidia watu kumtazama Mwana Wake kwa ajili ya ukombozi.

Mstari wa 3:Wenye ukuhani walitayarishwa kwa ajili ya majukumu yao “tangu kuwekwa misingi ya ulimwengu.”

Je, ni nini kingine unapata? Unahisi vipi kuhusu ukuhani unapotafakari kweli hizi? Ni jinsi gani ibada za ukuhani zimekusaidia kumtazama Kristo kwa ajili ya ukombozi?

Ni muhimu kujua ya kwamba wengi wa watu katika Amoniha walikuwa wafuasi wa Nehori (ona Alma 14:18; 15:15). Ni kwa namna gani makuhani wa mfano wa Nehori (ona Alma 1:3–6) walitofautiana na makuhani waliotawazwa “kwa Mfano wa Mwana wa Mungu” (M&M 107:3), ambao Alma aliwaelezea? (ona Alma 13:1–19).

Ona pia Dale G. Renlund, “Ukuhani na Nguvu ya Upatanisho ya Mwokozi,” Ensign au Liahona, Nov. 2017, 64–67.

Picha
wavulana kwenye meza ya sakramenti

Ibada za ukuhani hutusaidia kumtazama Yesu Kristo kwa ajili ya ukombozi.

Alma 13:3

Je, wenye ukuhani ndiyo watu peke “walioitwa na kutayarishwa tangu msingi wa ulimwengu”?

Mafundisho ya Alma katika Alma 13:3 yanarejelea hasa kwa wenye ukuhani. Hata hivyo, kanuni ambayo alifundisha—kwamba watu binafsi walipokea majukumu na walijitayarisha kuyatimiza “tangu msingi wa ulimwengu”—inatuhusu sisi sote. Rais Spencer  W. Kimball alisema: “Katika ulimwengu kabla hatujaja hapa, wanawake waaminifu walipangiwa majukumu fulani maalumu wakati wanaume waaminifu walitawazwa kabla kwa kazi fulani za ukuhani. Ingawa kwa sasa hatukumbuki vipengele hasa, hii haibadilishi ukweli mtukufu wa kile ambacho sisi mwanzo tulikubaliana nacho” (Mafundisho ya Marais wa Kanisa: Spencer W. Kimball [2006], 215–16; ona pia M&M 138:55–56).

Alma 14

Wakati mwingine Mungu huruhusu wenye haki kuteseka.

Alma 14 inazungumzia kuhusu watu wenye haki ambao waliteseka na hata kufariki kwa sababu ya imani yao. Unaweza kushangaa, jinsi wengi wafanyavyo, kwa nini mambo mabaya hutendeka kwa watu wanaojaribu kuishi kwa uadilifu. Huenda usipate majibu yote kwa swali hili gumu katika Alma 14, lakini kuna mengi ya kujifunza kutokana na jinsi ambavyo Alma na Amuleki walijibu hali ambazo walikabiliana nazo. Ni nini maneno na vitendo vyao vinakufundisha kuhusu sababu ya Bwana wakati mwingine kukubali watu wenye haki kuteseka? Je, unajifunza nini kutoka kwao kuhusu kukabiliana na mateso?

Ona pia Mathayo 5:43–44; Marko 14:55–65; Warumi 8:35–39; 1 Petro 4:12–14; Mafundisho na Maagano 122:5–9.

Alma 15:16, 18

Ufuasi unahitaji dhabihu.

Inaweza kuwa muhimu kuorodhesha vitu ambavyo Amuleki aliviacha ili kuikumbatia injili (ona Alma 10:4–5; 15:16) na ulinganishe na orodha ya kile alichopata (ona Alma 15:18; 16:13–15; 34:8). Je, wewe uko radhi kutoa nini dhabihu ili uweze kuwa mfuasi mwaminifu zaidi?

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zisisitizwe na kujadiliwa ili kukidhi mahitaji ya familia yako. Haya ni baadhi ya mawazo.

Alma 13

Familia yako inaweza kufaidika kutokana na kutilia maanani kila wakati neno “pumziko” linapotokea katika Alma 13. Ni maneno na dhana gani zingine huonekana pamoja nalo? Ni jinsi gani hili linatusaidia kuelewa kile “pumziko la Bwana” yaweza kuwa inamaanisha? Ni kwa jinsi gani hii ni tofauti na pumziko la kimwili?

Alma 13:10–12

Kuisaidia familia yako ipate taswira ya kile ambacho mistari hii hufundisha, pengine mnaweza kuosha kitu fulani pamoja—kama vile nguo nyeupe. Tunajisikiaje tunapokuwa wachafu? Tunajisikiaje tunapokuwa wasafi tena? Je, ni jinsi gani hisia hizi zinafanana na kile tunachohisi wakati tunatenda dhambi na kisha kutubu na kuwa wasafi kupitiia Upatanisho wa Mwokozi?

Alma 15:1–12

Tunajifunza nini kutokana na uzoefu wa Zeezromu kuhusu uwezo wa Bwana kutuimarisha na kutuponya, hata wakati tunapofanya makosa? Ni wajibu gani ukuhani unaweza kuwa nao katika kupokea kwetu uwezo na uponyaji Wake?

Alma 16:1–10

Baada ya kusoma mistari hii, unaweza kusoma Alma 9:4. Tunajifunza nini kwa kutofautisha jinsi Zoramu alivyohisi kuhusu maneno ya nabii na jinsi ambavyo watu wa Amoniha walivyohisi? Tunafanya nini ili kuwa waaminifu kwa maneno ya nabii wetu aliye hai?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kufundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Kuwa tayari daima. Nafasi za kufundisha hupita haraka, kwa hiyo zitumie vyema wakati zinapotokea. Jambo liletalo huzuni ulimwenguni, kwa mfano, laweza kuwa nafasi ya kushiriki kanuni kutoka Alma 14 kuhusu ni kwa nini Bwana wakati mwingine anaruhusu wasio na hatia kuteseka. (Ona Kufundisha katika Njia ya Mwokozi, 16.)

Picha
Alma na Amuleki gerezani

Alma na Amuleki Gerezani, na Gary L. Kapp

Chapisha