Njoo, Unifuate
Juni 8–14. Alma 8–12: Yesu Kristo Atakuja Kukomboa Watu Wake


Juni 8–14. Alma 8–12: Yesu Kristo Atakuja Kukomboa Watu Wake,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Kitabu cha Mormoni 2020 (2020)

“Juni 8–14. Alma 8–12,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2020

Picha
Alma akihubiri

Kufundisha Mafundisho ya Kweli, na Michael T. Malm

Juni 8–14

Alma 8–12

Yesu Kristo Atakuja Kukomboa Watu Wake

Kusoma maandiko kunaalika ufunuo. Kwa hiyo, unaposoma Alma 8–12, andika misukumo ya Roho anapokufundisha kutokana na jumbe za Alma na Amuleki.

Andika Misukumo Yako

Kazi ya Mungu haitakosa kufaulu. Lakini juhudi zetu kutoa usaidizi kwenye kazi Yake mara nyingine huonekana kutofaulu—angalau, tunaweza kukosa kuona kwa haraka matokeo tunayotumainia. Mara nyingine tunaweza kuhisi kidogo kama Alma wakati alipohubiri injili kule Amoniha—kukataliwa, kutemewa mate, na kufukuzwa. Lakini wakati malaika alipomuamuru arudi na ajaribu tena, Alma kwa ujasiri “alirudi kwa haraka” (Alma 8:18), na Mungu alitayarisha njia mbele yake. Hakumpa tu Alma chakula na mahali pa kuishi, bali pia alimtayarisha Amuleki, ambaye alikuja kuwa mtumishi mwenza, mtetezi mwenye nguvu wa injili, na rafiki mwaminifu. Tunapokabiliana na changamoto na masikitiko pale tunapotumikia katika ufalme wa Bwana, tunaweza kukumbuka jinsi Mungu alivyomtegemeza na kumuongoza Alma, nasi tunaweza tukaamini kwamba Mungu atatutegemeza na kutuongoza pia, hata katika hali ngumu.

Picha
ikoni ya kujifunza kibinafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kibinafsi

Alma 8

Juhudi zangu za kushiriki injili zinaweza kuhitaji bidii na subira.

Ingawaje mtu anaweza kupuuza ushuhuda wako kuhusu injili, hiyo haimaanishi kwamba unapaswa kupoteza tumaini—baada ya yote, Bwana hatakata tamaa juu ya mtu huyo, na atakuongoza jinsi utakavyofanya. Katika kisa cha Alma, Malaika alimuamuru arudi kule Amoniha kuhubiri injili hata ingawa watu waliokuwa kule walikuwa tayari wamemfukuza kwa vurugu (ona Alma 8:14–16). Unajifunza nini kutokana na mfano wa Alma wa kushiriki injili licha ya changamoto na upinzani? Ni mistari gani katika Alma 8 inazidisha hamu yako ya kutaka kushiriki injili?

Ona pia 3 Nefi 18:30–32; Jeffrey R. Holland, “Gharama—na Baraka—za Ufuasi,” Ensign au Liahona, Mei 2014, 6–9.

Alma 9:18–25; 10:16–23

Mungu huwahukumu watoto Wake kulingana na nuru na ufahamu waliopokea.

Unaposoma kuhusu jinsi ambavyo Wanefi katika Amoniha walivyowafanyia watumishi wa Bwana, ni rahisi kusahau kwamba wakati fulani walikuwa “watu waliopendwa sana na Bwana” walioishi injili (Alma 9:20). Kwa kweli, sehemu ya ujumbe wa Alma kwa watu wa Amoniha ilikuwa kwamba kwa sababu walikuwa wameshupaza mioyo yao licha ya kubarikiwa sana, hali yao ilikuwa mbaya zaidi kuliko ile ya Walamani, ambao walitenda dhambi mara nyingi kwa sababu ya ujinga. Je, tofauti hii inatufundisha nini kuhusu jinsi Mungu anavyowahukumu watoto Wake?

Unaposoma kuhusu baraka kuu ambazo Mungu aliwapa watu wa Nefi (ona hasa Alma 9:19–23), tafakari kuhusu baraka kuu ambazo Amekupa wewe. Unafanya nini ili kusalia mkweli kwenye baraka hizi? Ni mabadiliko gani unahisi unahitaji kufanya?

Ona pia Mafundisho na Maagano 82:3.

Alma 11–12

Mpango wa Mungu ni mpango wa ukombozi.

Manabii wa Kitabu cha Mormoni walitumia aina nyingi ya majina kuelezea kuhusu mpango wa Mungu kwa ajili ya watoto Wake, kama vile mpango wa wokovu au mpango wa furaha. Katika Alma 11–12, Alma na Amuleki waliuita mpango wa ukombozi. Unaposoma sura hizi, tafakari ni kwa nini neno “ukombozi” linatumika kuelezea mpango huu. Ungeweza pia kuandika muhtasari mfupi kuhusu kile ambacho Alma na Amuleki walifundisha kuhusu vipengele vifuatavyo vya mpango huu.

Anguko:

Mkombozi:

Toba:

Kifo:

Ufufuo:

Hukumu:

Tazama athari ambayo maneno ya Amuleki yalikuwa nayo kwa watu (ona Alma 11:46). Kwa nini unafikiri kanuni hizi zilikuwa na ushawishi mkubwa namna hii? Je, ni namna gani zimeathiri maisha yako?

Ona pia D. Todd Christofferson, “Ufufuo wa Yesu Kristo,” Ensign au Liahona, Mei 2014, 111–14.

Alma 12:8-18

Ikiwa sitashupaza moyo wangu, naweza kupokea zaidi ya neno la Mungu.

Watu wengine wanaweza kuwaza ni kwa nini Baba wa Mbiguni hasababishi kila kitu kujulikana kwetu. Katika Alma 12:9–14, Alma alieleza sababu moja inayoweza kusababisha siri za Mungu wakati mwingine zisijulikane kwetu. Maswali haya yanaweza kukusaidia kutafakari kile ambacho alifundisha:

  • Je, inamaanisha nini kushupaza mioyo yetu? Je, kuna wakati unagundua tabia hii ndani yako?

  • Je, kwa nini Bwana angeweza kuacha kuwapa neno Lake wale ambao wameshupaza mioyo yao?

  • Ni kwa jinsi gani umepata uzoefu wa ahadi ya kupokea “sehemu kubwa ya neno”? (Alma 12:10). Uzoefu huo ulikuwaje?

  • Unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba neno la Mungu “lipo ndani [yako]”? (Alma 12:13). Kama una neno la Mungu ndani yako, ni athari gani linaweza kuwa nayo juu ya “maneno,” “matendo,” na “mawazo” yako? (Alma 12:14).

Kwa mfano wa kanuni hizi, mfananishe Amuleki na watu wengine wa Amoniha. Ni kwa jinsi gani uzoefu wa Amuleki (ona hasa Alma 10:1–11) unaonyesha kile ambacho Alma anafundisha katika mistari hii?

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zisisitizwe na kujadiliwa ili kukidhi mahitaji ya familia yako. Haya ni baadhi ya mawazo.

Alma 8:10–18

Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Alma kuhusu kumtii Bwana “kwa haraka” (mstari wa 18) hata wakati inapoweza kuwa vigumu? Kuimarisha kanuni hii kwa watoto wadogo, ungeweza kucheza mchezo ambapo unatoa maagizo kwa ajili ya jukumu na uone ni upesi kiasi gani washiriki wa familia wanalikamilisha. Kwa mfano, ungeweza kuona nani angeweza kukunja nguo kwa haraka zaidi.

Alma 10:1–12

Je, tunaweza kujifunza nini kutokana na uzoefu wa Amuleki katika mistari hii? Ni athari gani ushuhuda wake ulikuwa nao kwa watu waliokuwa wakisikiliza? Waalike wanafamilia wako kuweka mpango wa kutenda jambo moja wiki hii kutokana na kile walichojifunza kutoka kwenye mfano wa Amuleki.

Alma 10:22–23

Tunajifunza nini kutoka kwenye mistari hii kuhusu athari za ushawishi ambao kundi moja la watu wenye haki linaweza kuwa nao katika mji wenye uovu?

Alma 11:34–37

Kuna tofauti gani kati ya Yesu Kristo kutuokoa katika dhambi zetu na kutoka kwa dhambi zetu? (ona Helamani 5:10; ona pia 1 Yohana 1:9–10). Kuonyesha kile ambacho Amuleki alifundisha, ungeweza kushiriki hadithi iliyoko mwanzoni mwa ujumbe wa Mzee Allen D. Haynie “Kukumbuka ni Nani Tumemwamini” (Ensign au Liahona, Nov. 2015, 121–23). Ni kwa jinsi gani Yesu Kristo anatuokoa kutoka kwa dhambi zetu?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Kuboresha Kujifunza Kibinafsi

Jifunze maneno ya manabii na mitume wa siku za mwisho. Soma kile ambacho manabii na mitume wa siku za mwisho wamefundisha kuhusu kweli unazopata ndani ya maandiko. Kwa mfano, ungeweza kutambua mada katika Alma 8–12 na uitafute mada hiyo katika mkutano mkuu wa hivi karibuni (ona Kufundisha Katika Njia ya Mwokozi, 21).

Picha
Alma akila na Amuleki

Kielelezo cha Alma akila na Amuleki na Dan Burr

Chapisha