Mafundisho na Maagano 2021
Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi


“Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Kwako Maandiko Kibinafsi,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Mafundisho na Maagano 2021 (2020)

“Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2021

Picha
mwanaume akisoma maandiko

Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko Kwako Binafsi

Hizi ni baadhi ya njia rahisi za kuboresha kujifunza kwako neno la Mungu katika maandiko.

Sali kwa Ajili ya Mwongozo

Maandiko ni neno la Mungu, kwa hiyo muombe Yeye kwa ajili ya msaada ili kuyaelewa.

Tafuta Kweli zihusianazo na Yesu Kristo

Maandiko hutufundisha kwamba vitu vyote humshuhudia Kristo (ona 2 Nefi 11:4; Musa 6:63), kwa hivyo weka kumbukumbu au alama mistari ambayo inashuhudia juu ya Mwokozi, inayoongeza upendo wako kwa ajili Yake na inafundisha jinsi ya kumfuata Yeye.

Tafuta Maneno na Vifungu vya Kutia Moyo

Unaweza kukuta kwamba maneno na vifungu fulani katika maandiko vinakugusa wewe, kana kwamba viliandikwa mahususi kwa ajili yako. Vinaweza kuwa na maana kwako binafsi na kukutia moyo na kukuhamasisha. Unaweza kuviwekea alama katika maandiko yako au kuviandika katika shajara ya kujifunzia.

Tafuta Kweli za Injili

Wakati mwingine kweli za injili (mara nyingi zikiitwa mafundisho au kanuni) zinasemwa wazi, na wakati mwingine zinatolewa kupitia mfano au hadithi. Jiulize, “Ni kweli zipi za milele zinafundishwa katika mistari hii?”

Msikilize Roho

Kuwa makini na mawazo na hisia zako, hata kama havihusiani na kile unachokisoma. Misukumo hiyo inaweza kuwa ni mambo hasa ambayo Baba wa Mbinguni anakutaka ujifunze.

Yafananishe Maandiko na Maisha Yako

Fikiria jinsi hadithi na mafundisho unayoyasoma yanavyohusiana na maisha yako. Kwa mfano, ungeweza kujiuliza, “Je ni uzoefu gani nilioupata ambao unafanana na hiki ninachokisoma?” au “Ni kwa jinsi gani ninaweza kufuata mfano wa mtu huyu katika maandiko?”

Uliza Maswali Unapojifunza

Unapojifunza maandiko, maswali yanaweza kuja akilini. Maswali haya yanaweza kuhusiana na kile unachokisoma au maisha yako kwa ujumla. Tafakari maswali haya na tafuta majibu kadiri unavyoendelea kujifunza maandiko.

Tumia Misaada ya Kujifunza Maandiko

Ili kupata umaizi wa ziada katika mistari unayoisoma, tumia tanbihi, Mwongozo wa Mada, Kamusi ya Biblia, Mwongozo kwenye Maandiko (scriptures.ChurchofJesusChrist.org), na misaada mingine ya kujifunza.

Zingatia Muktadha wa Maandiko

Unaweza kupata umaizi wa maana kuhusu kifungu cha maandiko unapozingatia muktadha wake, pamoja na hali au muktadha wa kilipotokea. Kwa mfano, kufahamu chimbuko na imani za watu ambao Mungu alizungumza nao kunaweza kukusaidia kuelewa vyema dhamira ya maneno yake.

Andika Mawazo na Hisia zako

Kuna njia nyingi za kuandika misukumo ambayo hukujia unapojifunza. Kwa mfano, ungeweza kuwekea alama neno lenye maana au kifungu na kuandika mawazo yako kama neno la kukumbuka katika maandiko yako. Unaweza pia kutunza shajara ya umaizi, hisia, na misukumo unayoipata.

Jifunze Maneno ya Manabii na Mitume wa Siku za Mwisho

Soma kile ambacho manabii na mitume wa siku za mwisho wamefundisha kuhusu kanuni unazozipata ndani ya maandiko (kwa mfano, ona conference.ChurchofJesusChrist.org na majarida ya Kanisa).

Shiriki Umaizi

Kujadili umaizi kutokana na kujifunza kwako kibinafsi sio tu ni njia nzuri ya kuwafundisha wengine, bali pia husaidia kuimarisha uelewa wako katika kile ambacho umesoma.

Ishi kwa Kile Unachojifunza

Kujifunza maandiko hakupaswi tu kututia moyo lakini pia kunapaswa kutuongoza kwenye kubadilisha jinsi tunavyoishi. Sikiliza kile ambacho Roho anakushawishi kufanya unaposoma, na kisha diriki kuitendea kazi misukumo hiyo.

Picha
mwanamke akisoma maandiko

Mzee David A. Bednar alisema: “Hatupaswi kutegemea Kanisa kama taasisi ya kutufundisha au kutuambia kila kitu tunachohitaji kujua na kufanya ili kuwa wafuasi waaminifu na kuvumilia kwa ujasiri mpaka mwisho. Badala yake, wajibu wetu binafsi ni kujifunza kile tunachopaswa kujifunza, kuishi kama tunavyojua tunapaswa kuishi, na kuwa yule ambaye Bwana angetaka tuwe. Na nyumba zetu ni mpangilio wa juu zaidi kwa ajili ya kujifunza, kuishi, na kuwa” (“Kujiandaa Kupata Kila kitu Kinachohitajika,” Ensign au Liahona, Mei 2019, 102).

Chapisha