Agano Jipya 2023
Septemba 4–10. 1 Wakorintho 14–16: “Mungu si Mungu wa Machafuko, bali wa Amani”


“Septemba 4–10. 1 Wakorintho 14–16: ‘Mungu si Mungu wa Machafuko, bali wa Amani’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Shule ya Jumapili: Agano Jipya 2023 (2022)

“Septemba 4–10. 1 Wakorintho 14–16,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Shule ya Jumapili: 2023

Picha
kisima cha maji ya ubatizo hekaluni

Septemba 4–10

1 Wakorintho 14–16

“Mungu si Mungu wa Machafuko, bali wa Amani”

Kabla ya kurejea muhtasari huu, soma 1 Wakorintho 14–16. Andika misukumo yako ya awali kuhusu kweli zipi zitawasaidia washiriki wa darasa lako, na endelea kutafuta mwongozo wa ziada kutoka kwa Roho Mtakatifu wakati unapojiandaa kufundisha.

Picha
ikoni ya kushiriki

Alika Kushiriki

Toa dakika chache kwa ajili ya washiriki wa darasa kurejea 1 Wakorintho 14–16 na kutafuta mstari wanaohisi una maana maalumu kwao. Waalike kumtafuta mtu fulani katika darasa ambaye wanaweza kushiriki naye mstari huo na kuelezea kwa nini waliuchagua.

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho

1 Wakorintho 14

Wakati Watakatifu wanapokusanyika pamoja, wanapaswa kutafuta kujengana.

  • Fikiria kutumia mafundisho ya Paulo katika 1 Wakorintho 14 kuwakumbusha washiriki wa darasa kwamba tunaweza kujengana—au kusaidiana na kuinuana—katika kanisa. Njia rahisi ya kufanya marejeo ya sura hii ingeweza kuwa kwa kuandika swali kwenye ubao, kama vile Ni lipi linapaswa kuwa lengo letu pale tunapokusanyika pamoja? Alika washiriki wa darasa kutafuta yanayowezekana kuwa majibu katika 1 Wakorintho 14. Mawazo mengine yanaweza kupatikana katika Moroni 6:4–5 na Mafundisho na Maagano 50:17–23. Wakati washiriki wa darasa wakishiriki kile walichopata, fikiria kuwauliza ni jinsi gani wanahisi darasa lenu linaendelea katika kutimiza malengo haya. Wangeweza pia kuelezea uzoefu wao pale walipohisi kujengwa na kitu ambacho mshiriki wa darasa alishiriki nao.

1 Wakorintho 15

Kwa sababu Yesu Kristo alifufuka, sisi sote tutafufuka.

  • Je, unawezaje kutumia ushauri wa Paulo katika 1 Wakorintho 15 ili kuimarisha shuhuda za washiriki wa darasa lako juu ya Ufufuko? Njia mojawapo ingeweza kuwa kwa kugawanya darasa katika makundi mawili na kuliomba kundi moja kutafuta kutoka 1 Wakorintho 15 matokeo ambayo tungeyapata kama Yesu Kristo asingefufuka. Kundi lingine lingeweza kutafuta baraka ambazo tunapokea kutokana na Ufufuko Wake. Kisha kila kundi lingeweza kuandika kwenye ubao kile walichojifunza. Je, ni kitu gani wangeweza kuongeza kwenye orodha yao ya awali baada ya kusoma maelezo kutoka kwa Mzee D. Todd Christofferson katika “Nyenzo za Ziada”? Ili kuwasaidia washiriki wa darasa kuhisi Roho wakati wa mjadala huu, fikiria kuonyesha picha ya Mwokozi aliyefufuka (ona Muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Nifuate—Kwa ajili ya Watu Binafsi na Familia) au kupiga au kuimba wimbo wa dini kuhusu Ufufuko.

  • Kwa sababu Paulo alikuwa akiwajibu watu ambao walikuwa hawaamini katika ufufuko, washiriki wa darasa lako wanaweza kunufaika kupitia kuigiza hali kama hii. Kwa mfano, ni kwa namna gani wangeweza kuimarisha imani ya mpendwa wao katika Ufufuko? Tunagundua nini katika 1 Wakorintho 15 ambacho kingewasaidia kuelezea umuhimu na ushahidi wa Ufufuko wa Yesu Kristo? Ni maandiko gani mengine tungeweza kuyatumia? (Ona, kwa mfano, Luka 24:1–12, 36–46; Alma 11:42–45.)

    Picha
    mawio

    Paulo alifundisha kuhusu Ufufuko kwa kurejelea “miili ya kiselestia” kama jua (1 Wakorintho 15:40).

  • 1 Wakorintho 15 ni moja kati ya sehemu chache kwenye maandiko ambapo ubatizo kwa niaba ya wafu umetajwa (ona mstari 29; ona pia Mafundisho na Maagano 128:18). Labda washiriki wa darasa wangeweza kushiriki uzoefu ambao waliupata wakati walipofanya ubatizo au ibada zingine kwa niaba ya mababu zao. Kwa nini Paulo alitumia ubatizo kwa niaba ya wafu kama ushahidi wa Ufufuko? Kama itasaidia kujadili kwa nini ubatizo kwa niaba ya wafu ni muhimu, ona makala ya Mada za Injili “Ubatizo kwa niaba ya wafu” (topics.ChurchofJesusChrist.org. Video ya “Glad Tidings: The History of Baptisms for the Dead” (ChurchofJesusChrist.org) inaelezea jinsi kanuni hii ilivyorejeshwa katika siku yetu.

Picha
ikoni ya nyenzo

Nyenzo za Ziada

Upekee wa Ufufuko

Mzee D. Todd Christofferson alifundisha:

Fikiria kwa muda upekee wa Ufufuko katika kuamua mara moja na milele utambulisho wa kweli juu ya Yesu wa Nazareti na mashindano makubwa ya kifalsafa na maswali ya maisha. Kama kweli Yesu alifufuka kiuhalisia, basi ni muhimu ikafuata kuwa Yeye ni kiumbe wa kiungu. Hakuna kiumbe chenye mwili wenye kufa kilicho na nguvu ndani yake ya kurudia uhai tena baada ya kufa. Kwa sababu Yeye alifufuka, Yesu hawezi kuwa alikuwa tu fundi seremala, mwalimu, rabi au nabii. Kwa sababu Yeye alifufuka, Yesu lazima alikuwa Mungu, hata Mwana wa Pekee wa Baba.

“Kwa hivyo, kile Alichofundisha ni kweli; Mungu hawezi kudanganya.

“Kwa hivyo, Yeye alikuwa Muumbaji wa dunia, kama Yeye alivyosema.

“Kwa hivyo, mbingu na jehanamu ni halisi, kama alivyofundisha.

“Kwa hivyo, kuna ulimwengu wa roho, ambao Yeye aliutembelea baada ya kifo Chake.

“Kwa hivyo, Atakuja tena, kama malaika walivyosema, na ‘kutawala mwenyewe juu ya dunia.’

“Kwa hivyo, kuna ufufuko na hukumu ya mwisho kwa wote” (“Ufufuko wa Yesu Kristo,” Liahona, Mei 2014, 113).

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Pata kuwajua wale unaowafundisha. Hakuna watu wawili walio sawa kikamilifu; kila mtu unayemfundisha ana chimbuko la kipekee, mtazamo, na vipaji vyake. Sali kujua jinsi gani unaweza kuvitumia hivi ili kuwashirikisha wanafunzi wako. Unapowaelewa vyema wale unaowafundisha, unaweza kutengeneza nyakati zenye maana na za kukumbukwa kwa ajili yao (ona Kufundisha katika Njia ya Mwokozi7).

Chapisha