Njoo, Unifuate
Desemba 30–Januari 5. Kurasa za Utangulizi za Kitabu cha Mormoni: “Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo”


“Desemba 30–Januari 5. Kurasa za Utangulizi za Kitabu cha Mormoni: ‘Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Kitabu cha Mormoni 2020 (2020)

“Desemba 30–Januari 5. Kurasa za Utangulizi za Kitabu cha Mormoni,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2020

Picha
bamba za dhahabu

Desemba 30–Januari 5

Kurasa za Utangulizi za Kitabu cha Mormoni

“Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo”

Kujifunza kwako Kitabu cha Mormoni kunaweza kusitawishwa ikiwa utaanza kwa kusoma kurasa zinazopatikana kabla ya 1 Nefi. Unapata nini kinachoimarisha ushuhuda wako?

Andika Misukumo Yako

Kabla hata haujafikia 1 Nefi sura ya 1, ni wazi kwamba Kitabu cha Mormoni si kitabu cha kawaida. Kurasa zake za utangulizi zinaelezea historia isiyoweza kulinganishwa na nyingine—ikijumuisha huduma ya malaika, maandishi ya kale yaliyozikwa kwa karne nyingi pembeni mwa kilima, na mkulima asiyejulikana kutafsiri kumbukumbu hiyo kwa uwezo wa Mungu. Kitabu cha Mormoni siyo tu historia kuhusu tamaduni zenye ustaarabu za Amerika. Kinao “utimilifu wa injili isiyo na mwisho” (dibaji ya Kitabu cha Mormoni), na Mungu Mwenyewe aliongoza kuja kwake—jinsi kilivyoandikwa, jinsi kilivyohifadhiwa, na jinsi kilivyopatikana katika siku zetu. Mwaka huu, unaposoma Kitabu cha Mormoni, kusali kwa ajili yake, na kutenda kulingana na mafunzo yake, utaalika nguvu zake maishani mwako, na unaweza ukahisi kusema, jinsi Mashahidi Watatu walivyofanya katika ushuhuda wao, “ni ajabu machoni [mwangu].”

Picha
ikoni ya kujifunza kibinafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kibinafsi

Ukurasa wa jina wa Kitabu cha Mormoni

Kitabu cha Mormoni kinaweza kuimarisha imani yangu kwa Yesu Kristo.

Ukurasa wa jina wa Kitabu cha Mormoni unatoa zaidi ya jina tu. Pamoja na mambo mengine, unaorodhesha malengo kadhaa ya kumbukumbu hii takatifu. Tafuta malengo haya, kisha unapojifunza Kitabu cha Mormoni mwaka huu, andika vifungu ambavyo unahisi kwamba vinatimiza malengo haya. Kwa mfano, vifungu gani vinasaidia kukushawishi “kwamba Yesu ndiye Kristo, Mungu wa Milele”?

Utangulizi wa Kitabu cha Mormoni

Kitabu cha Mormoni “kinadokeza juu ya mpango wa wokovu.”

Mpango wa wokovu ni mpango wa Baba wa Mbinguni wa kuwasaidia watoto wake ili waweze kuinuliwa, jinsi Yeye alivyo, na kuwa na furaha Yeye aliyonayo (ona 2 Nefi 2:25–26). Upatanisho wa Yesu Kristo unawezesha mpango huu, na kila fundisho, ibada, agano, na amri ambazo Mungu ametoa ni kwa ajili ya kufanikisha mpango huu.

Ikiwa unataka kuelewa mpango wa wokovu, hakuna kitabu kizuri zaidi cha kusoma kushinda Kitabu cha Mormoni. Kinarejelea mpango wa Mungu—kwa kutumia aina kadhaa za majina—zaidi ya mara 20 . Wakati wa kujifunza kwako mwaka huu, tambua wakati mpango wa Mungu unapotajwa au kudokezwa na kile ambacho Kitabu cha Mormoni kinasema kuuhusu.

Hii ni shughuli ya kukuwezesha kuanza. Soma vifungu vifuatavyo, na uorodheshe majina tofauti yaliyopewa mpango wa Mungu: 2 Nefi 9:13; 11:5; na Alma 12:32–34; 24:14; 41:2; 42:15–16. Je, kila moja ya majina haya yanapendekeza nini kwako kuhusu mpango wa Baba?

Ushuhuda wa Mashahidi Watatu”; “Ushuhuda wa Mashahidi Wanane

Naweza kuwa shahidi wa Kitabu cha Mormoni.

Roho Mtakatifu anaweza kukushuhudia kwamba Kitabu cha Mormoni ni cha kweli, hata kama haujaziona bamba za dhahabu jinsi walivyofanya Mashahidi Watatu na Mashahidi Wanane. Ni kwa jinsi gani ushuhuda wao unaimarisha wako? Ni kwa jinsi gani unaweza “kutoa [jina lako] ulimwengu, ili kushuhudia ulimwengu” yale unayojua kuhusu Kitabu cha Mormoni? (“Ushuhuda wa Mashahidi Wanane”).

Ushuhuda wa Nabii Joseph Smith

Ujio wa Kitabu cha Mormoni ulikuwa ni muujiza.

Kama mtu angekuuliza Kitabu cha Mormoni kilitoka wapi, ungesema nini? Ungelezea namna gani mkono wa Bwana katika kukileta Kitabu cha Mormoni? Ni jinsi gani Joseph Smith alielezea ujio wa Kitabu cha Mormoni?

Ushuhuda wa Nabii Joseph Smith

Kitabu cha Mormoni kilitafsiriwa kwa njia gani?

Kitabu cha Mormoni kilitafsiriwa “kwa karama na uwezo wa Mungu.” Hatujui maelezo mengi kuhusu mchakato wa kimiujiza wa kutafsiri, lakini tunajua ya kwamba Joseph Smith alikuwa mwonaji, akipata usaidizi kutokana na vifaa ambavyo Mungu alikuwa amevitayarisha: mawe mawili angavu yaliyoitwa Urimu na Thumimu na jiwe lingine lililoitwa jiwe la mwonaji. Joseph aliona katika mawe haya ufafanuzi wa Kiingereza wa herufi zilizokuwa kwenye bamba, na alisoma tafsiri hiyo kwa sauti kubwa huku mwandishi akiiandika. Kila mmoja wa waandishi wa Joseph alishuhudia ya kwamba uwezo wa Mungu ulidhihirishwa katika tafsiri ya kazi hii takatifu.

Ona “Tafsiri ya Kitabu cha Mormoni” (Mada za Injili, topics.ChurchofJesusChrist.org).

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani.

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zisisitizwe na kujadiliwa ili kukidhi mahitaji ya familia yako. Haya ni baadhi ya mawazo.

Ukurasa wa jina wa Kitabu cha Mormoni

Pengine familia yako yaweza kuanzisha orodha ya mistari kutoka Kitabu cha Mormoni ambayo imeimarisha imani yenu “kwamba Yesu ndiye Kristo” na kuongeza kwenye orodha hiyo kwa mwaka mzima. Huu pia waweza kuwa wakati mzuri wa kutengeneza mpango wa familia kwa ajili ya kusoma Kitabu cha Mormoni: Lini na wapi mtakutanika ili kusoma? Ni kwa jinsi gani kila mwanafamilia atashiriki? Kwa usaidizi wa ziada , ona “Mawazo ya Kuboresha Kujifunza Maandiko kwa Familia Yako” mwanzoni mwa nyenzo hii.

Utangulizi wa Kitabu cha Mormoni

Jiwe la katikati la tao ni jiwe lililo na umbo la kabari lililoko juu ya tao ambalo linashikilia mawe mengine pamoja. Ili kuwasaidia wanafamilia wako kuelewa jinsi Kitabu cha Mormoni ni “jiwe la katikati la tao la dini yetu,” unaweza kujenga au kuchora tao ikiwa na jiwe la katikati kileleni. Ni nini kitafanyika kama jiwe la katikati la tao litatolewa? Nini kingetendeka kama hatungekuwa na Kitabu cha Mormoni? Tunawezaje kufanya Kitabu cha Mormoni kuwa jiwe la katikati la tao la imani yetu kwa Yesu Kristo?

Picha
Tao iliyojengwa kwa mawe ikishikiliwa na jiwe la katikati

Kitabu cha Mormoni ni jiwe la katikati la tao la dini yetu.

Ushuhuda wa Mashahidi Watatu”; “Ushuhuda wa Mashahidi Wanane

Wanafamilia wako wanaweza kuandika shuhuda zao kuhusu Kitabu cha Mormoni, kuweka sahihi ya majina yao kwenye vitabu, na kufikiria kuhusu njia wanazoweza kutumia kushiriki shuhuda zao na wengine.

Ushuhuda wa Nabii Joseph Smith

Katika historia ya Joseph Smith, ni ushahidi gani tunapata kwamba Mungu alihusika katika kuleta Kitabu cha Moroni?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kufundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Kuboresha Kujifunza Kibinafsi

Ahadi ya kinabii. Rais Russell M. Nelson alisema, “Ninaahidi kwamba unapotafakari kile unachojifunza [kutoka katika Kitabu cha Mormoni], madirisha ya mbinguni yatafunguka, na utapokea majibu ya maswali yako na mwongozo katika maisha yako” (“Kitabu cha Mormoni: Maisha Yako Yangekuwaje Usingalikuwa Nacho?Ensign au Liahona, Nov. 2017, 62–63).

Picha
Joseph akipokea bamba za dhahabu kutoka kwa Moroni

Moroni Akiwasilisha Bamba za Dhahabu, na Gary L. Kapp

Chapisha