Njoo, Unifuate
Julai 13–19. Alma 32–35: “Mtapanda Hili Neno Kwenye Mioyo Yenu”


“Julai 13–19. Alma 32–35: ‘Mtapanda Hili Neno Kwenye Mioyo Yenu,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Kitabu cha Mormoni 2020 (2020)

“Julai 13–19. Alma 32–35,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2020

Picha
Mbegu kwenye mkono wa mtoto

Julai 13–19

Alma 32–35

“Mtapanda Hili Neno Kwenye Mioyo Yenu”

Andika misukumo ya kiroho unayopata wakati unapojifunza. Alma 32–35. Unahisi umetiwa msukumo kufanya nini kwa sababu ya kile unachojifunza ?

Andika Misukumo Yako

Kwa Wazoramu, sala ilikuwa mazoea ya desturi ya kujifikiria, ambayo ilifanyika mara moja kwa wiki. Ilijumuisha kusimama mahali ambapo kila mtu aliweza kuona na kurudia maneno ovyo, ya kujifikiria. Pengine baya zaidi, Wazoramu walikosa imani katika Yesu Kristo—hata wakakana kuwepo Kwake—na kuwatesa masikini (ona Alma 31:9–25). Kinyume chake, Alma na Amuleki walifundisha kwa ujasiri kwamba sala inahusika zaidi na kile kinachofanyika ndani ya mioyo yetu badala ya kwenyejukwaa la umma. Na kama haitasababisha huruma kwa masikini, ni “bure, na hayatakupatia … chochote” (Alma 34:28). Muhimu zaidi, ni onyesho la imani katika Yesu Kristo, ambaye anatoa ukombozi kupitia “dhabihu [Yake] isiyo na mwisho na ya milele” (Alma 34:10). Imani kama hii, Alma alieleza, inatokana na unyenyekevu na “kutamani kuamini” (Alma 32:27). Inamea polepole, kama mti, na inahitaji kulishwa mara kwa mara. Unaposoma Alma 32–35, unaweza fikiria kuhusu imani na sala zako; je, umewahi kuhisi mitazamo ya Kizoramu ikinyemelea ndani? Ni kwa jinsi gani utalisha imani yako katika Yesu Kristo ili iweze kuwa “mti unaochipua kwenye maisha ya milele”? (Alma 32:41).

Picha
ikoni ya kujifunza kibinafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kibinafsi

Alma 32:1–16

Naweza kuchagua kuwa mnyenyekevu.

Alma alitambua kwamba Wazoramu masikini walikuwa wanyenyekevu na “walikuwa wamejiandaa kusikiliza neno” (Alma 32:6). Unaposoma Alma 32:1–16, fikiria kuhusu jinsi unavyojitayarisha kusikiliza neno la Mungu.

Ni uzoefu gani umekunyenyekeza? Umefanya nini ili kuwa mnyenyekevu zaidi? Mistari hii inaweza kukufundisha jinsi ya kuchagua unyenyekevu badala ya kulazimishwa kuwa mnyenyekevu. Kwa mfano, ni nini tofauti baina ya kuwa “masikini kulingana na vitu vya ulimwengu” na kuwa “masikini katika mioyo”? (mstari wa 3). Ina maanisha nini “kujinyenyekeza [wewe mwenyewe] kwa sababu ya neno”? (mstari wa 14).

Ona Pia “Unyenyekevu,” Mada za Injili, topics.ChurchofJesusChrist.org.

Alma 32:17–43; 33–34

Ninaonyesha imani katika Yesu Kristo kwa kupanda na kulisha neno Lake moyoni mwangu.

Unafikiria ni kwa nini Alma alizungumza kuhusu kupanda mbegu kama jibu kwa swali la Wazoramu kuhusu kuabudu? Ni nini mbegu aliyoizungumzia Alma? (ona Alma 32:28; 33:22–23). Unaposoma Alma 32:17–43, na 24:17-43, tilia maanani maneno na virai ambavyo vinakusaidia kuelewa jinsi ya kuwa na imani katika Yesu Kristo na neno Lake. Je, unajifunza nini kuhusu imani ni nini na nini ambacho imani sio? Kisha, unaposoma sura za 33–34, tafuta majibu kwa swali la Wazoramu “Ni kwa jinsi gani [tuna] panda mbegu?” (Alma 33:1).

Hii ni njia nyingine ya kujifunza Alma 32–34: Chora picha zinazowakilisha awamu tofauti za ukuaji wa mbegu. Kisha kwa kila picha weka kitambulisho chenye maelezo ukitumia maneno kutoka Alma 32:28–43 ambayo yanakusaidia kuelewa jinsi ya kupanda na kulisha neno la Mungu katika moyo wako.

Ona pia Mathayo 13:3–8, 18–23; Waebrania 11; Neil L. Andersen, “Imani Haiji kwa Bahati, lakini Kupitia Uchaguzi,” Ensign au Liahona, Nov. 2015, 65–68; “Imani katika Yesu Kristo,” Mada za Injili, topics.ChurchofJesusChrist.org.

Alma 33:2–11; 34:17–29

Naweza kumwabudu Mungu katika sala, wakati wowote na mahali popote.

Ushauri wa Alma na Amuleki kuhusu kuabudu na sala ulidhamiria kurekebisha sintofahamu maalumu Wazoramu waliyokuwa nayo (ona Alma 31:13–23). Lakini kweli ambazo walifundisha zinaweza kusaidia yeyote kati yetu kuelewa sala na kuabudu vizuri zaidi. Pengine unaweza kutengeneza orodha ya kweli kuhusu sala ambazo unapata katika Alma 33:2–11 na 34:17–29. Pembeni ya orodha hiyo, andika orodha ya mambo yanayoweza kuwa yanaeleweka vibaya kuhusu sala ambayo kweli hizi zinarekebisha (ona Alma 31:12–23). Je, ni jinsi gani vitu ambavyo unajifunza kutoka kwenye mistari hii vitaathiri jinsi unavyosali na kuabudu?

Alma 33:3–17

Zeno na Zenoki walikuwa akina nani?

Zeno na Zenoki walikuwa manabii ambao walitoa ushuhuda juu ya Yesu Kristo katika nyakati za Agano la Kale, lakini mafundisho yao hayapatikani katika Agano la Kale. Wanefi walikuwa na mafundisho ya manabii hawa, pengine kwa sababu yalijumuishwa katika bamba za shaba ambazo Nefi alichukua kutoka kwa Labani. Wametajwa katika 1 Nefi 19:10–12; Yakobo 5:1; na Helamani 8:19–20.

Alma 34:30–41

Maisha haya ni wakati … kujitayarisha kukutana na Mungu.”

Unaposoma Alma 34:30–41, fikiria jinsi ambavyo unaweza “kutenda mema wakati [uko] kwenye maisha haya” (mstari wa 33). Ni jinsi gani toba na subira vyaweza kukusaidia kujitayarisha kukutana na Mungu? Je, kuna mabadiliko ambayo unahitaji kufanya ambayo umekuwa ukiahirisha? Hakikisha unatenda kulingana na misukumo yoyote ya kiroho unayopokea.

Ona pia Alma 12:24; Larry R. Lawrence, “Nimepungukiwa Na Nini Tena?Ensign au Liahona, Nov. 2015, 33–35.

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zisisitizwe na kujadiliwa ili kukidhi mahitaji ya familia yako. Haya ni baadhi ya mawazo.

Alma 32:9–11; 33:2–11; 34:38–39

Je, ingekuwaje kama tungekubaliwa tu kuabudu na kusali Jumapili pekee? Mnaposoma aya hizi kwa pamoja, wanafamilia wanaweza kujadiliana jinsi ambavyo wanaweza kuabudu kila siku na kwa nini wana shukrani kwamba wanaweza kufanya hivyo.

Alma 32:28–43

Picha ya mti inaandamana na mwongozo huu; unaweza kuitumia kuonyesha maneno ya Alma katika mistari hii. Au familia yako inaweza kwenda kwenye matembezi kutafuta mimea ikiwa kwenye awamu tofauti za ukuaji na kusoma mistari kutoka Alma 32 ambayo inalinganisha mmea unaokua na imani yetu. Pengine kila mwanafamilia anaweza kupanda mbegu na kujadiliana kile ambacho tunahitaji kufanya kuisaidia kukua. Katika wiki zinazofuata mnaweza kukagua mbegu zenu na kukumbushana juu ya haja ya kuendelea kulisha ushuhuda wetu wa Yesu Kristo.

Alma 33:2–11; 34:17–29

Ni nini aya hizi zinapendekeza kuhusu jinsi tunavyoweza kuboresha sala zetu za binafsi na za familia?

Alma 34:31

Ni uzoefu gani umetuonyesha kwamba wakati tunapotubu, “mara moja” tunaanza kupata baraka za mpango wa ukombozi?

Alma 34:33–35

Je, familia yako inajua maana ya kuahirisha? Pengine mtu anaweza kushiriki mifano ya kuahirisha na matokeo yake hasi. Inamaanisha nini “kuahirisha siku [yetu] ya toba”?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kufundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Chora picha. Unaweza kuwaruhusu wanafamilia wachore wakati wanajifunza kutoka kwenye maandiko. Kwa mfano, wanaweza kufurahia kuchora mbegu ikikua na kuwa mti wanapojifunza Alma 32.

Picha
Tunda katika mti

“Na kwa sababu ya bidii yenu na imani yenu na uvumilivu wenu kwa neno kwa kulilisha, … tazama, baadaye mtavuna matunda yake , ambayo ni ya thamani sana” (Alma 32:42).

Chapisha