Njoo, Unifuate
Februari 4–10. Mathayo 4; Luka 4–5: ‘Roho wa Bwana Yu juu Yangu’


“Februari 4–10. Mathayo 4; Luka 4–5: ‘Roho wa Bwana Yu juu Yangu’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya 2019 (2019)

“Februari 4–10. Mathayo 4; Luka 4–5,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2019

Picha
Kristo anamshinda Shetani

Kristo Anamshinda Shetani, na Robert T. Barrett

Februari 4–10

Mathayo 4; Luka 4–5

“Roho wa Bwana Yu juu Yangu”

Anza kwa kusoma Mathayo 4 na Luke 4–5, na zingatia umaizi wowote unaopokea. Mawazo ya kujifunza katika muhtasari huu yanaweza kukusaidia kutambua kanuni muhimu katika sura hizi.

Andika Misukumo Yako

Toka ujana Wake, Yesu alionekana kujua kwamba Alikuwa na huduma ya kipekee, takatifu. Lakini Yesu alipokuwa akijiandaa kwa huduma Yake ya duniani, adui alitafuta kupanda shaka katika akili ya Mwokozi. Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu,” Shetani alisema (Luka 4:3, mlazo yameongezwa). Lakini Mwokozi alikuwa na ushirika na Baba Yake wa Mbinguni. Alijua maandiko, na alijua Yeye alikuwa nani. Kwake Yeye, toleo la Shetani—“Nitakupa wewe enzi hii yote” (Luka 4:6)—ilikuwa ya uongo, kwani matayarisho ya maisha yote ya Mwokozi yalimruhusu Yeye kupokea “nguvu za Roho” (Luka 4:14). Hivyo licha ya majaribu, taabu, na kukataliwa, Yesu Kristo kamwe hakutetereka kutoka kwenye kazi yake teule: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu … maana kwa sababu hiyo Nalitumwa” (Luka 4:43).

Picha
Ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo ya Kujifunza Maandiko Binafsi

Mathayo 4:1–2

Kuwa na ushirika na Mungu huniandaa mimi kumtumikia Yeye.

Kujiandaa kwa ajili ya huduma Yake, Yesu alienda nyikani ili “awe na Mungu” (Tafsiri ya Joseph Smith, Mathayo 4:1 [katika Mathayo 4:1, tanbihi b]). Fikiria juu ya kile unachofanya ili ujisikie kuwa karibu na Mungu. Je, ni kwa jinsi gani hii hukuandaa wewe kwa kazi ambayo Yeye anataka ufanye?

Mathayo 4:1–11; Luka 4:1–13

Yesu Kristo aliweka mfano kwa ajili yangu kwa kushinda majaribu.

Wakati mwingine watu hujiona kuwa wenye hatia wakati wanapojaribiwa kufanya dhambi. Lakini hata Mwokozi, aliyeishi “bila kufanya dhambi” (Waebrania 4:15), alijaribiwa. Inaweza kuleta faraja kujua kwamba kwa sababu Kristo pia alipata na kushinda majaribu, Yeye anajua majaribu tunayoyapata na anaweza kutusaidia kuyashinda (ona Waebrania 2:18; Alma 7:11–12).

Unaposoma Mathayo 4:1–11 na Luka 4:1–13, unajifunza nini kinachoweza kukusaidia unapokabiliwa na majaribu? Unaweza kupangilia mawazo yako katika jedwali kama hili hapa:

Yesu Kristo

Mimi

Yesu Kristo

Je, Shetani alimjaribu Kristo afanye nini?

Kutumia nguvu Zake kukidhi njaa Yake.

Mimi

Je, Shetani ananijaribu ili nifanye nini?

Yesu Kristo

Je, ni kwa nini Kristo aliandaliwa ili ashinde majaribu?

Alifunga; Alikwenda kuwa na Mungu; Alijua maandiko.

Mimi

Je, ni kwa jinsi gani mimi ninaweza kujiandaa ili kushinda majaribu?

Yesu Kristo

Mimi

Je, ni umaizi gani wa ziada unapata kutoka katika Tafsiri ya Joseph Smith ya Mathayo 4? Ona marejeo yote katika Mathayo 4).

Ona pia 1 Wakorintho 10:13; Alma 13:28; Musa 1:10–22; “Jaribu,” Mada za Injili, topics.lds.org.

Luka 4:16–32

Yesu Kristo ndiye Masiya aliyetolewa unabii.

Kama ungeulizwa kuelezea Yesu Kristo alitumwa duniani kufanya nini, je wewe ungesema nini? Katika Luka 4:18–19, Mwokozi alielezea vipengele vya huduma Yake mwenyewe kwa kunukuu mojawapo ya unabii wa Isaya kuhusu Masiya (ona Isaya 61:1–2). Unajifunza nini kuhusu misheni Yake unaposoma mistari hii?

Picha
Yesu Anafundisha ndani ya sinagogi

Yesu Kristo alishuhudia kwamba Yeye ni Masiya.

Japokuwa Wayahudi walikuwa wakisubiri kwa karne nyingi kwa unabii wa Isaya kutimizwa, wengi hawakukubali kwamba Yesu alikuwa ndiye Masiya wakati alipotangaza, “Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu” (Luka 4:21). Unaposoma Luka 4:20–30 (ona pia Marko 6:1–6), jaribu kujiweka katika nafasi ya watu wa Nazareti. Je, kuna kitu cho chote ambacho kinaweza kukuzuia kumkubali kikamilifu Kristo kama Mwokozi wako binafsi?

Ona pia Mosia 3:5–12; “Yesu Anatangaza kuwa Yeye ndiye Masiya” (video, LDS.org).

Mathayo 4:18–22; Luka 5:1–11

Ninapoamini katika Bwana, Yeye anaweza kunisaidia kufikia fursa zangu takatifu.

Rais Ezra Taft Benson alifundisha, “Wanaume na wanawake wanaompa Mungu maisha yao watagundua kwamba Yeye anaweza kufanya mengi zaidi kutoka katika maisha yao kuliko wao wanavyoweza” (Teachings of the Presidents of the Church: Ezra Taft Benson [2014], 42). Hiki ndicho kilichotokea kwa Petro na wavuvi wenzake. Yesu aliwasaidia kutambua kwamba wangeweza kufanya zaidi ya kuvua samaki—wangeweza kuwa “wavuvi wa watu” (Mathayo 4:19; ona pia Luka 5:10). Kuwasaidia kuona hili, Yesu alitumia matukio ambayo yalijulikana kwao.

Je, ni lini umehisi Mwokozi akikuita umfuate? Je, ni kwa jinsi gani unaweza kumwonyesha Bwana kwamba uko tayari ku “[acha] vyote” (Luka 5:11) ili kumfuata Yeye? Tafakari maswali haya unaposoma Mathayo 4:18–22 na Luka 5:1–11.

Ona pia “Njoo, Unifuate,” Wimbo, no. 116.

Picha
Ikoni ya kujifunza kwa familia.

Mawazo ya Kujifunza Maandiko Kwa Familia na Jioni ya Familia Nyumbani.

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zisisitizwe na kujadiliwa ili kukidhi mahitaji ya familia yako. Haya ni baadhi ya mapendekezo:

Mathayo 4:1–2; Luka 4:1–2

Yesu alikuwa amefunga kabla ya kujaribiwa na adui. Je, ni umaizi gani tunaweza kupata kutoka kwenye maelezo haya kuhusu nguvu ya kufunga? Maelezo katika “Mfungo na Matoleo ya Mfungo,” Mada za Injili, topics.lds.org yanaweza kukusaidia kuongoza mjadala wa familia kuhusu kufunga. Unaweza kuwaalika wanafamilia kuelezea uzoefu waliowahi kuwa nao katika kufunga. Pengine, familia yako inaweza kwa sala kupanga mipango ya kufunga pamoja kwa lengo mahususi.

Mathayo 4:3–4; Luka 4:3–4

Wakati Shetani alipomjaribu Kristo ili kubadili jiwe kuwa mkate, aliupa changamoto utambulisho mtakatifu wa Kristo kwa kusema “Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu” (Mathayo 4:3, mlazo yameongezwa). Kwa nini Shetani hujaribu kutufanya tuwe na shaka kuhusu utambulisho wetu mtakatifu? Je, ni kwa namna gani yeye anajaribu kufanya hili? (Ona pia Musa 1:10–23.)

Tafsiri ya Joseph Smith, Mathayo 4:11

Baada ya Yesu kujaribiwa kimwili na kiroho, mawazo Yake yaligeukia mahitaji ya Yohana Mbatizaji, ambaye alikuwa gerezani: “Na sasa Yesu alijua kwamba Yohana alikuwa amefungwa gerezani, na alituma malaika, na, tazama, walikuja na kumhudumia [Yohana]” (Tafsiri ya Joseph Smith, Mathayo 4:11 [katika Mathayo 4:11, tanbihi a). Ni kwa jinsi gani tunabarikiwa tunapofuata mfano wa Kristo wa kuwafikiria wengine kabla ya kujifikiria sisi wenyewe? Je, ni kwa jinsi gani sisi tunaweza kufuata mfano Wake?

Luka 4:16–21

Je, tunamjua mtu ye yote ambaye amevunjika moyo au anahitaji “kuwekwa huru”? (Luka 4:18). Je, ni kwa jinsi gani tunaweza kuwasaidia wengine kupokea uponyaji na ukombozi wa Mwokozi? Unaweza kujadili pia jinsi ilivyo kwa kufanya ibada za hekaluni husaidia kuleta “uhuru kwa waliosetwa” (Luke 4:18).

Kwa mawazo zaidi juu ya kufundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii ndani ya Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Ishi Injili ya Yesu Kristo. “Pengine kitu cha muhimu zaidi unachoweza kufanya [kama mzazi au mwalimu] ni … kuishi injili kwa moyo wako wote . … Hii ni njia kuu ya kustahili kuambatana na Roho Mtakatifu. Hauhitaji kuwa mkamilifu, uwe unajaribu tu kwa bidii—ukitafuta msamaha kupitia Upatanisho wa Mwokozi wakati unapokosea” (Kufundisha katika Njia ya Mwokozi, 13).

Picha
Yesu anawaita Mitume kuwa wavuvi wa watu

Wito, na Jorge Cocco

Chapisha