Agano Jipya 2023
Septemba 11–17. 2 Wakorintho 1–7: “Na Mpatanishwe na Mungu”


“Septemba 11–17. 2 Wakorintho 1–7: ‘Na Mpatanishwe kwa Mungu’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya (2023)

“Septemba 11–17. 2 Wakorintho 1–7,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2023

Picha
Yesu Kristo

Septemba 11–17

2 Wakorintho 1–7

“Na Mpatanishwe kwa Mungu”

Unapojifunza barua za Paulo kwa Wakorintho, andika baadhi ya kanuni za injili unazogundua na tafakari jinsi utakavyozitumia katika maisha yako.

Andika Misukumo Yako

Wakati mwingine, kuwa kiongozi wa Kanisa humaanisha kuweza kusema mambo mengine magumu. Hii ilikuwa kweli katika siku ya Paulo kama ilivyo leo. Inavyoonekana barua ya awali kutoka kwa Paulo kwa Watakatifu wa Korintho ilijumuisha kukemewa na kulisababisha hisia za kuumiza. Katika barua iliyokuja kuwa 2 Wakorintho, yeye alijaribu kuelezea kile kilichokuwa kimechochea maneno yake kuwa makali: “Maana katika dhiki nyingi na taabu ya moyo niliwaandikia na machozi mengi; si kwamba mhuzunishwe, bali mpate kujua upendo wangu nilionao kwenu jinsi ulivyo mwingi” (2 Wakorintho 2:4). Wakati unapokuwa katika upande wa kupokea baadhi ya masahihisho kutoka kwa kiongozi, kwa hakika inasaidia kujua kwamba yanachochewa na upendo kama wa Kristo. Na hata katika hali zile ambazo sivyo, kama tuko tayari kuwaona wengine kwa aina ya upendo Paulo aliouhisi, ni rahisi kuitikia kwa njia ifaayo kwa maudhi yoyote. Kama Mzee Jeffrey R. Holland alivyoshauri, “Kuwa mkarimu kuhusiana na udhaifu wa kibinadamu—wa kwako mwenyewe na vilevile wa wale wanaotumikia pamoja nawe katika Kanisa linaloongozwa na wanaojitolea, wanaume na wanawake wenye mwili wenye kufa. Isipokuwa katika suala la Mwanawe wa Pekee aliye mkamilifu, watu wasio wakamilifu ndio ambao Mungu amekuwa akishughulika nao” (“Bwana Naamini,” Liahona, Mei 2013, 94).

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa Ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

2 Wakorintho 1:3–7; 4:6–10, 17–18; 7:4–7

Majaribu yangu yanaweza kuwa baraka.

Ukichukulia kila kitu ambacho Paulo alikabiliana nacho katika maisha yake, siyo kitu cha kushangaza kwamba aliandika mengi kuhusu madhumuni na baraka za dhiki. Unaposoma 2 Wakorintho 1:3–7; 4:6–10, 17–18; 7:4–7, fikiria kuhusu njia ambazo majaribu yako yanaweza kuwa baraka. Kwa mfano, ungeweza kutafakari jinsi gani Mungu “amekufariji [wewe] katika dhiki [zako] zote” na jinsi gani wewe unaweza, kama malipo, “kuwafariji wale walio katika dhiki za namna yoyote” (2 Wakorintho 1:4). Au ungeweza kufokasi juu ya jinsi ambavyo nuru ya Yesu Kristo “iling’ara moyoni mwako,” hata wakati “umedhikika” na “kuona shaka” (2 Wakorintho 4:68).

Ona pia Mosia 24:13–17; Henry B. Eyring, “Kujaribiwa, Kuthibitishwa, na Kung’arishwa,” Liahona, Nov. 2020, 96–99; Mada za Injili, “Dhiki,” topics.ChurchofJesusChrist.org.

2 Wakorintho 2:5–11

Msamaha ni baraka ninayoweza kutoa na kupokea.

Hatujui mengi kuhusu mtu ambaye Paulo alimtaja katika 2 Wakorintho 2:5–11—ni kwamba tu alivunja sheria (ona mstari wa 5–6) na kwamba Paulo aliwataka Watakatifu wamsamehe (ona mstari wa 7–8). Je, ni kwa nini wakati mwingine tunashindwa “kuthibitisha upendo wetu kwa” mpendwa wetu aliyetukosea? (mstari wa 8). Ni kwa jinsi gani kuzuia msamaha kunawadhuru wengine na sisi wenyewe? (ona mstari wa 7, 10–11). Ni kwa jinsi gani kuzuia msamaha kunampatia “Shetani … faida ya kutushinda”? (mstari wa 11).

Ona pia Mafundisho na Maagano 64:9–11.

2 Wakorintho 5:14–21

Kupitia Upatanisho wa Yesu Kristo, ninaweza kupatanishwa na Mungu.

Kama ilivyo kwa mtu yeyote, Paulo alijua jinsi inavyokuwa kwa mtu kuwa “kiumbe kipya” (2 Wakorintho 5:17). Alitoka kwenye kuwa mtesaji wa Wakristo mpaka kuwa mtetezi jasiri wa Kristo. Unaposoma 2 Wakorintho 5:14–21, fikiria kuhusu maswali kama haya: Inamaanisha nini kupatanisha? Inamaanisha nini kupatanishwa na Mungu? Tafakari nini kinaweza kuwa kinakutenganisha wewe na Mungu? Je, unahitaji kufanya nini ili kupatanishwa Naye kikamilifu? Ni kwa jinsi gani Mwokozi anafanya hiyo iwezekane?

Ungeweza pia kutafakari kile inachomaanisha kuwa “mabalozi wa Kristo” katika “huduma ya kupatanisha” (mstari wa 18, 20). Ni umaizi gani unaupata kutoka kwenye ujumbe wa Mzee Jeffrey R. Holland “Huduma ya Kupatanisha”? (Liahona, Nov. 2018, 77–79).

Ona pia 2 Nefi 10:23–25.

2 Wakorintho 7:8–11

Huzuni ya kiungu hutuongoza kwenye toba.

Kwa kawaida hatufikirii huzuni kama kitu kizuri, lakini Paulo aliongelea juu ya “huzuni ipitayo kiasi” (2 Wakorintho 7:10) kama sehemu muhimu ya toba. Fikiria kile unajifunza kuhusu huzuni ya kiungu kutoka katika yafuatayo: 2 Wakorintho 7:8–11; Alma 36:16–21; Mormoni 2:11–15; na ujumbe wa Dada Michelle D. Craig “Kutoridhika Kiungu” (Liahona, Nov. 2018, 52–55). Ni lini ulihisi huzuni ya kiungu, na imekuwa na matokeo gani katika maisha yako?

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

2 Wakorintho 3:1–3.Je, watu wa familia yako wamewahi kumuomba mtu kuwaandikia barua ya mapendekezo, kama vile kwa ajili ya maombi ya kazi au shule? Waalike wazungumze kuhusu uzoefu huu. Paulo alifundisha kwamba maisha ya Watakatifu yalikuwa kama barua za mapendekezo kwa ajili ya injili ya Yesu Kristo, “zilizoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye hai.” Mnaposoma 2 Wakorintho 3:1–3 pamoja, jadilini jinsi mifano yetu ni kama barua ambazo zinaweza “kujulikana na kusomwa na watu wote,” kuonyesha ukweli na ustahili wa injili. Pengine kila mwanafamilia anaweza kuandika barua au “waraka” akielezea jinsi ambavyo mwanafamilia mwingine amekuwa mfano mzuri wa mfuasi wa Yesu Kristo. Wanaweza kusoma barua zao kwa familia na kumpa mwanafamilia waliyeandika juu yake. Kwa nini ni muhimu kuelewa kwamba maisha yetu ni “waraka wa Kristo”?

2 Wakorintho 5:6–7.Inamaanisha nini “kuenenda kwa imani, si kwa kuona”? Je, sisi tunafanya nini ili kuonyesha kwamba tunaamini katika Mwokozi hata ingawa hatuwezi kumuona Yeye?

2 Wakorintho 5:17.Je, familia yako inaweza kufikiria au kutafuta mifano katika uhalisia wa vitu ambavyo hupitia mabadiliko yasiyo kifani na kuwa viumbe vipya? (Ona picha mwisho wa muhtasari huu). Ni kwa jinsi gani injili ya Yesu Kristo inaweza kutubadilisha?

2 Wakorintho 6:1–10.Kulingana na 2 Wakorintho 6:1–10, inamaanishas nini kuwa “watumishi wa Mungu”? (mstari wa 4). Ni sifa gani mtumishi wa Mungu anazo?

2 Wakorintho 6:14–18.Je, ni kwa jinsi gani tunaweza kufuata ushauri wa Paulo, “Tokeni kati ya [wasioamini], na mkatengwe nao,” huku pia tukiwapenda wale wanaotuzunguka?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa “Help Me, Dear Father,” Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 99.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Fundisha masomo ya vitendo. Baadhi ya dhana za injili, kama vile Upatanisho, zinaweza kuwa ngumu kuelewa. Fikiria kutumia picha au vitu ambavyo vitaisaidia familia yako kuelewa kanuni unazogundua katika maandiko.

Picha
kiwavi, kifukofuko, na kipepeo

Tunapoongoka kwenye injili ya Kristo, badiliko letu ni kubwa sana kwamba Paulo alilielezea kama kuwa “kiumbe kipya” (2 Wakorintho 5:17).

Chapisha