Agano la Kale 2022
Aprili 4–10. Kutoka 14–17: “Simama Kimya, na Uone Wokovu wa Bwana”


“Aprili 4–10. Kutoka 14–17: ‘Simama Kimya, na Uone Wokovu wa Bwana,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano la Kale 2022 (2021)

“Aprili 4–10. Kutoka 14–17,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Watu Binafsi na Famila: 2022

Picha
Bahari ya Shamu

Bahari ya Shamu

Aprili 4–10

Kutoka 14–17

“Simama Kimya, na Uone Wokovu wa Bwana”

Mungu alimwamuru Musa kuandika kuhusu matukio yake “kwa ajili ya ukumbusho katika kitabu, na kuyasimulia” kwa Yoshua (Kutoka 17:14). Vivyo hivyo, kuandika matukio yako ya kiroho itakusaidia wewe na wapendwa wako kukumbuka wema wa Mungu.

Andika Misukumo Yako

Waisraeli walikuwa wako mtegoni. Bahari ya Shamu ilikuwa upande mmoja, na jeshi la Farao lilikuwa likiwasogelea upande mwingine. Kutoroka kwao kutoka Misri, ilionekana, kungekuwa kwa muda mfupi. Lakini Mungu alikuwa na ujumbe kwa ajili ya Waisraeli kwamba Yeye aliwataka kukumbuka kwa vizazi vingi: “Msiogope. … Bwana atapigana kwa ajili yenu” (Kutoka 14:13–14).

Tangu wakati huo, watu wa Mungu walipohitaji imani na ujasiri, wamekuwa daima wakigeukia kwenye hadithi hii ya ukombozi wa kimiujiza wa Israeli. Wakati Nefi alipotaka kuwashawishi kaka zake, alisema, “Tuwe hodari kama Musa; kwani aliyazungumzia maji ya Bahari ya Shamu na yakagawanyika sehemu mbili huku na huku, na mababu zetu wakapita , wakatoka utumwani, juu ya nchi kavu” (1 Nefi 4:2). Wakati mfalme Limhi alipowataka watu wake walio utumwani “kuinua vichwa [vyao], na kushangilia,” aliwakumbusha juu ya hadithi hii (Mosia 7:19). Wakati Alma alipotaka kushuhudia kwa mwanawe juu ya nguvu za Mungu, yeye pia aliitaja hadithi hii (ona Alma 36:28). Na wakati sisi tunapohitaji ukombozi—wakati tunapohitaji imani zaidi, wakati tunapohitaji “kusimama tu, na kuona wokovu wa Bwana”—tunaweza kukumbuka jinsi Bwana alivyoikomboa Israeli siku ile kutoka mikononi mwa Wamisri” (Kutoka 14:13, 30).

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

Kutoka 14

Mungu anao uwezo wa kunikomboa.

Unaposoma Kutoka 14:1–10, fikiria jinsi Waisraeli walivyojisikia walipoona jeshi la Farao linawakaribia. Pengine unajisikia kwamba unahitaji muujiza wa kupona changamoto ngumu unayokabiliana nayo. Je, unajifunza nini kutoka kitabu cha Kutoka 14:13–31 ambacho kinaweza kukusaidia kutafuta ukombozi wa Mungu katka maisha yako? Je, umejifunza nini kuhusu njia ambazo Mungu anatoa ukombozi kutoka kwenye shida? Tafakari umeoinaje nguvu ya ukombozi Wake katika maisha yako.

Ona pia Mafundisho na Maagano 8:2–3; L. Tom Perry, “Nguvu ya Ukombozi,” Liahona, Mei 2012, 94–97; Ramani za Biblia, na. 2, “Kutoka kwa Waisraeli Misri na Kuingia Kanaani.”

Kutoka 15:22–27

Bwana anaweza kufanya vitu vichachu kuwa vitamu.

Unaposoma katika Kutoka 15:22–27 kuhusu kusafiri kwa Israeli kuelekea nchi ya ahadi, fikiria kuhusu vitu katika maisha yako ambavyo vilionekana “vichungu” kama maji ya Mara. Fikiria maswali yafuatayo unapotafakari mistari hii: Je Bwana anawezaje kufanya vitu vichungu katika maisha yako kuwa vitamu? Je, uzoefu huu umekuwa na thamani gani katika maisha yako? Je, mistari ya 26 na 27 inapendekeza nini kuhusu jinsi Bwana anavyotubariki sisi wakati tunapoisikiliza sauti Yake?

Kutoka 15:23–27; 16:1–15; 17:1–7

Ninaweza kumwamini Bwana, hata wakati wa nyakati ngumu.

Inashawishi kuwa mkosoaji wa Israeli kwa sababu walinung’unika na kulalamika wakati hali zao zilipokuwa ngumu, hata baada ya kila kitu Mungu alichofanya kwa ajili yao. Lakini unaposoma Kutoka 15:23–27; 16:1–15; 17:1–7, fikiria kama nawe umefanya kitu hicho hicho. Je, unajifunza nini kutokana na matukio haya ya Waisraeli ambacho kinaweza kukusaidia kupunguza kunung’unika na kuamini kikamilifu zaidi kwa Mungu? Kwa mfano, ni tofauti gani unazoona kuhusu njia ambayo Waisraeli walijibu wakati wa magumu na njia ambayo Musa alitumia kujibu? Aya hizi zinakufundisha nini kuhusu Mungu?

Ona pia 1 Nefi 2:11–12; “Sin of Murmuring” (video), ChurchofJesusChrist.org.

Picha
mwanamke anaokota mana

Mana kutoka kwa Mungu iliwalisha Israeli kimwili; sisi pia tunahitaji kila siku lishe ya kiroho. Fresco na Leopold Bruckner

Kutoka 16

Ninapaswa kutafuta lishe ya kiroho kila siku.

Kuna masomo mengi ya kiroho tunayoweza kujifunza kutokana na muujiza wa mana, yanayopatikana katika Kutoka 16. Fahamu maelekezo ya kina waliyopewa Waisraeli kuhusu jinsi ya kuokota, kutumia, na kuhifadhi mana (ona Kutoka 16:16, 19, 22–26). Ni kipi unapata katika maelekezo haya ambacho kinatumika kwako wewe kila siku unapotafuta lishe ya kiroho?

Ona pia Yohana 6:31–35, 48–58 na video ya “Daily Bread: Pattern,” “Daily Bread: Experience,” na “Daily Bread: Change” (ChurchofJesusChrist.org).

Kutoka 17:1–7

Yesu Kristo ni mwamba wangu wa kiroho na ni maji ya uzima.

Fikiria kuhusu Mwokozi unaposoma Kutoka 17:1–7. Je, ni kwa jinsi gani Yesu Kristo ni mwamba kwako? (ona Zaburi 62:6–7; Helamani 5:12). Je, ni kwa jinsi gani Yeye ni kama maji? (ona Yohana 4:10–14; 1 Wakorintho 10:1–4; 1 Nefi 11:25).

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

Kutoka 14:13–22.Washiriki wa familia yako wanaweza kufurahia kujaribu “kuyagawanya” maji ndani ya bakuli au bafu, kama Musa alivyoigawanya Bahari ya Shamu. Wasaidie kuelewa kwamba Bahari ya Shamu isingeweza kugawanyika pasipo nguvu za Mungu. Je, tumeionaje nguvu ya Mungu katika maisha yetu na katika maisha ya mababu zetu?

Kutoka 15:1-21.Baada ya kuvuka Bahari ya Shamu kimiujiza, Waisraeli waliimba wimbo wa kusifu uliojulikana kama wimbo wa Musa, unaopatikana katika Kutoka 15:1–21. Kama familia pekueni mistari hii kwa ajili ya kupata vifungu vya maneno ambavyo vinashuhudia kile ambacho Mungu alifanya kwa ajili ya Waisraeli na vifungu vingine vyenye umuhimu. Kisha mnaweza kuimba wimbo ambao unaikumbusha familia yako kile ambacho Mungu amekifanya kwa ajili yenu.

Kutoka 16:1–5; 17:1–7.Kusoma Kutoka 16:1–5 na 17:1–7 kungeweza kuwaongoza kwenye mjadala kuhusu Mwokozi kama Mkate wa Uzima, kama Maji yaliyo Hai na kama Mwamba. Je, ni kwa jinsi gani hadithi hizi zinatukumbusha sisi juu ya kile ambacho Yesu Kristo anafanya kwa ajili yetu? Kama sehemu ya majadiliano yenu, pengine mngesoma Yohana 4:10–14; 6:29–35, 48–51; Helamani 5:12; Mafundisho na Maagano 20:77, 79.

Kutoka 17:8-16.Mngeweza kuigiza hadithi ya Haruni na Huri wakishikilia mikono ya Musa na jadilianeni jinsi hili linavyoweza kuwa alama ya jinsi tunavyowakubali wale ambao Mungu amewaita kutuongoza sisi. Mngeweza pia kuonyesha kinyume cha mfano wa Haruni na Huri na Waisraeli wakinungunika dhidi ya Musa (inayoelezewa kote katika mlango wa 15–17). Je, ni zipi baadhi ya njia tunazoweza kusaidia na kuwakubali viongozi wetu? Je, ni baraka gaani huja kwetu na kwa viongozi wetu tunapofanya hivyo?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “Redeemer of Israeli,” Nyimbo za Kanisa, na. 6.

Kuboresha Kujifunza Kibinafsi.

Tafuta utambuzi wako mwenyewe wa kiroho. Katika kujifunza kwako binafsi na familia, usijiwekee mpaka kwenye vifungu vya maandiko viliyoonyeshwa katika mihtasari hii. Bwana yaelekea anao ujumbe kwa ajili yako katika milango hii ambao haujasisitizwa hapa. Kwa maombi utafute mwongozo wa kiungu.

Picha
Musa akiigawanya Bahari ya Shamu

Kielelezo cha Musa akiigawa Bahari ya Shamu, na Robert T. Barrett

Chapisha