Njoo, Unifuate
Februari 24–Machi 1. 2 Nefi 26–30: “Kazi ya Kushangaza na ya Maajabu”


“Februari 24–March 1. 2 Nefi 26–30: ‘Kazi ya Kushangaza na ya Maajabu,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: Kitabu cha Mormoni 2020 (2020)

“Februari 24–Machi 1. 2 Nefi 26–30,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: 2020

Picha
Yesu akimsaidia mwanamke

Atakuongoza kwa Mkono Wake, na Sandra Rast

Februari 24–Machi 1

2 Nefi 26–30

“Kazi ya kushangaza na ya maajabu”

Kabla ya kuanza kuandaa shughuli za kujifunza kwa ajili ya watoto darasani kwako, soma 2 Nefi 26–30. Hii itamwalika Roho kuongoza maandalizi yako.

Andika Misukumo Yako

Picha
ikoni ya kushiriki

Alika Kushiriki

Nyanyua juu Kitabu cha Mormoni, na uelezee kwamba Nefi aliona kabla kwamba Kitabu cha Mormoni kingekuwa muhimu katika siku yetu. Waalike watoto kushiriki kitu chochote walichojifunza kuhusu Kitabu cha Mormoni mwaka huu.

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wadogo

2 Nefi 26:33

Yesu Kristo anamtaka kila mmoja kuja Kwake.

Nefi alishuhudia kwamba Mwokozi anampenda kila mtu, bila kujali wao ni kina nani, na anawaalika wote “kupokea wema wake.”

Shughuli za Yakini

  • Onyesha picha za watu kutoka makabila na machimbuko mbalimbali (unaweza kupata baadhi katika magazeti ya Kanisa). Waombe watoto waelezee baadhi ya vitu wanavyoona katika picha. Fungua maandiko katika 2 Nefi 26:33 na usome, “[Yesu Kristo] anawakaribisha wote kuja kwake.” Rudia kifungu hiki cha maneno pamoja na watoto unapoonyesha kila picha kwa kidole. Kisha mwonyeshe kila mtoto kwa kidole na sema, “Yesu Kristo anakukaribisha wewe kuja Kwake.” Ni nini tunaweza kufanya kuja kwa Mwokozi?

  • Imba wimbo pamoja na watoto kuhusu kuwapenda watu wote, kama vile “I’ll Walk with You” au “We Are Different” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 140–41, 263). Onyesha maneno au vifungu vya maneno katika wimbo ambavyo unahisi vinaupa nguvu ujumbe wa 2 Nefi 26:33.

2 Nefi 28:2; 30:6

Kitabu cha Mormoni ni baraka.

Fikiria jinsi utakavyowasaidia watoto darasani kwako kuhisi kwamba Kitabu cha Mormoni ni “baraka kwao kutoka mkono wa Mungu” (2 Nefi 30:6).

Shughuli za Yakini

  • Waonyeshe watoto Kitabu cha Mormoni kikiwa kimefungwa kama zawadi, na waambie kwamba kitu fulani cha thamani kimo ndani. Waache washikilie zawadi, na wape dokezo kuwasaidia kubashiri zawadi hiyo ni nini; kwa mfano, ni kitu ambacho Bwana ametupatia, kinatusaidia kuamini katika Yesu Kristo, na kadhalika. Soma kutoka 2 Nefi 30:6: “Ni baraka kwao kutoka mkono wa Mungu.” Acha watoto wafungue zawadi, na elezea kwamba lazima tufungue Kitabu cha Mormoni na kukisoma ili kupokea baraka zilizomo.

  • Soma 2 Nefi 28:2 kwa watoto. Elezea kwamba Nefi aliona kwamba Kitabu cha Mormoni kingekuwa “cha thamani kuu” kwetu, ambayo humaanisha kwamba kitatusaidia na kutubariki. Waambie watoto kwa nini Kitabu cha Mormoni ni cha thamani kuu kwako. Shiriki mstari unaoupenda au hadithi kutoka kwenye Kitabu cha Mormoni, na waalike watoto kushiriki zao. Onyesha picha kutoka kwenye Kitabu cha Sanaa za Injili kuwapa mawazo.

2 Nefi 28:30

Baba wa Mbinguni hunifundisha kidogo kidogo.

Pengine unaweza kufikiria somo la vitendo au shughuli ambayo itawasaidia watoto kuona kile inachomaanisha kujifunza “mstari juu ya mstari.” Mapendekezo hapa chini yanaweza kuanzisha baadhi ya mawazo.

Shughuli za Yakini

  • Wasaidie watoto kuweka pamoja fumbo rahisi au kujenga kitu kwa vitofali. Wape kipande kimoja cha fumbo au kitofali kimoja kimoja, na wakati wakijenga, elezea kwamba hivi ndivyo jinsi Baba wa Mbinguni hutufundisha—ukweli mmoja baada ya mwingine. Ni nini kingetokea kama tungejaribu kuweka vipande vyote pamoja mara moja?

  • Wafundishe watoto ujuzi hatua kwa hatua, kama vile kufunga upinde au kuchora picha. Soma kutoka 2 Nefi 28:30: “Nitawapatia watoto wa watu mstari juu ya mstari, … hapa kidogo na pale kidogo.” Je, ni kwa nini Mungu hutufundisha kidogo kidogo?

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wakubwa

2 Nefi 26:23–28, 33

Yesu Kristo anamtaka kila mmoja kuja Kwake.

Wasaidie watoto kuhisi kwamba mwaliko wa kuja kwa Kristo umeelekezwa kwao na kwa watu wote.

Shughuli za Yakini

  • Zungumza na watoto kuhusu nyakati ambapo waliwaalika marafiki au familia kuja kwenye tukio maalumu, kama sherehe za siku ya kuzaliwa. Ni nini walifanya kuwahimiza watu kuja? Soma pamoja na watoto 2 Nefi 26:23–28, 33, na wasaidie kutafuta kile Bwana anachotualika kufanya. Waalike watoto kubuni kadi au barua ikimualika mtu kuja kwa Yesu Kristo. Wahimize kutumia kifungu cha maneno kutoka kwenye mistari hii katika mwaliko wao (kama itahitajika, andika baadhi ya vifungu vya maneno ubaoni ili kusaidia).

  • Soma 2 Nefi 26:33 pamoja na watoto, na wasaidie kutengeneza orodha ya nani, kulingana na mstari huu, amealikwa “kupokea wema wa [Bwana].” (Unaweza kuhitaji kuelezea kwamba “kafiri” ni wale wasioamini katika Mungu.) Waalike kuongeza majina yao wenyewe kwenye orodha. Ni kwa jinsi gani tunapokea wema wa Bwana?

  • Zungumza na watoto kwa kifupi kuhusu jinsi watoto kote ulimwenguni ni tofauti, na shuhudia kwamba Bwana anawapenda wote (ona 2 Nefi 26:24, 33). Waalike watoto kuchora picha ya Yesu akiwa na watoto wengi tofauti.

2 Nefi 28:27–30.

Baba wa Mbinguni hufunua ukweli “mstari juu ya mstari.”

Nefi alionya dhidi ya mtazamo kwamba hatuhitaji ukweli zaidi kutoka kwa Mungu. Wasaidie watoto kuona kujifunza injili kama kitu cha taratibu na cha maisha yote.

Shughuli za Yakini

  • Chagua kifungu cha maneno kutoka 2 Nefi 28:30, na muombe mtoto kuandika neno la kwanza ubaoni. Kisha muombe mtoto mwingine kuandika neno linalofuata, na wengine pia mpaka kifungu chote cha maneno kiwe kimeandikwa. Ni kwa jinsi gani shughuli hii inafanana na jinsi Mungu anavyotupatia ukweli?

  • Wasaidie watoto kusoma na kuelewa 2 Nefi 28:27–30, wakitafuta majibu ya swali kama hili: ni nini mistari hii hufundisha kuhusu watu wanaoamini wana ukweli wa kutosha na hawahitaji zaidi? Waombe kupendekeza jinsi tunavyoweza kumwonyesha Bwana kwamba tunataka kupokea ukweli zaidi kutoka Kwake.

2 Nefi 29:7–11

Kitabu cha Mormoni na Biblia hufanya kazi pamoja.

Kwa sababu tunayo Biblia, baadhi ya watu huamini kwamba Kitabu cha Mormoni hakina umuhimu. Mistari hii inaweza kuwasaidia watoto kuelewa, na kuwaelezea wengine, kwa nini tuna shukrani kwa ajili ya vitabu vyote viwili vya maandiko.

Shughuli za Yakini

  • Mpe mtoto mmoja nakala ya Kitabu cha Mormoni na mwingine nakala ya Biblia. Waulize ni kwa jinsi gani vitabu hivi vinafanana na jinsi gani vinatofautiana. Waonyeshe watoto ramani ya ulimwengu, na wasaidie kuoanisha kila kitabu na sehemu ya ulimwengu kilipotoka. Soma na kujadili 2 Nefi 29:8. Ni kwa nini Mungu alitupatia “mashahidi” au vitabu vya maandiko vinavyotufundisha kuhusu Yeye?

  • Waombe watoto wafikirie kwamba rafiki aliwaambia, “Sihitaji kusoma Kitabu cha Mormoni. Nimekwisha kusoma Biblia.” Someni kwa pamoja 2 Nefi 29:7–11, ukielezea vifungu vya maneno au dhana kama inavyohitajika. Kisha waombe washiriki mawazo kuhusu kile ambacho wangeweza kusema kwa rafiki yao.

Picha
ikoni ya kujifunza

Himiza Kujifunza Nyumbani

Waalike watoto kuelezea familia zao jinsi Biblia na Kitabu cha Mormoni vinavyofanya kazi kwa pamoja kumshuhudia Yesu Kristo.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Fokasi kwa Watu, Sio Masomo. Mawazo yaliyoko katika muhtasari huu ni mapendekezo tu. Jisikie huru kuyatohoa kukidhi mahitaji na uwezo wa watoto unaowafundisha.

Chapisha