Mafundisho na Maagano 2021
Kukidhi Mahitaji ya Watoto wenye Ulemavu


“Kukidhi Mahitaji ya Watoto wenye Ulemavu,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: Mafundisho na Maagano 2021 (2020)

“Kukidhi Mahitaji ya Watoto wenye Ulemavu,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: 2021

Picha
watoto wakiimba

Kukidhi Mahitaji ya Watoto wenye Ulemavu

Viongozi wa msingi wanawajibika kufundisha injili ya Yesu Kristo kwa watoto wote, ikijumuisha wale wenye ulemavu. Katika msingi, kila mtoto anapaswa kukaribishwa, kupendwa, kulelewa, na kujumuishwa. Katika mazingira haya ni rahisi kwa watoto wote kuelewa upendo wa Baba yetu wa Mbinguni na Yesu Kristo na kuhisi na kutambua ushawishi wa Roho Mtakatifu. Mawazo yafuatayo yanaweza kukusaidia kukidhi mahitaji ya watoto wenye ulemavu.

  • Jifunze kuhusu mahitaji maalumu ya mtoto. Njia nzuri ya kufanya hili ni kuzungumza na wazazi wa mtoto au watoa huduma. Tafuta ni kwa jinsi gani mtoto anajifunza vizuri zaidi na mbinu zipi zina msaada zaidi. Ungeweza pia kushauriana na viongozi wengine na walimu wa Msingi ambao wana uzoefu na utambuzi wa kukueleza.

  • Tengeneza mazingira chanya ambapo kila mtoto anahisi yuko salama na anapendwa. Yajue majina ya watoto wote katika darasa lako, na wasaidie wahisi kukubaliwa, kupendwa, na kujumuishwa. Watoto wenye ulemavu mara nyingi wanakosolewa, hivyo tafuta fursa za kuwasifu kwa tabia chanya. Wasaidie watoto wengine kuwa wenye kupenda na wenye kuwakubali wengine.

  • Fanya marekebisho ili kwamba kila mmoja aweze kushiriki. Mabadiliko madogo madogo yanaweza kufanywa kwenye shughuli ili kuhakikisha kwamba watoto wote wanaweza kujifunza, ikijumuisha wale wenye mapungufu ya kimaumbile au wenye shida ya kujifunza. Kwa mfano, kama shughuli inapendekeza kuonesha picha, mnaweza kuimba wimbo unaohusiana kama mbadala ili kujumuisha watoto wenye mapungufu ya kuona.

  • Imarisha utaratibu na muundo endelevu wa darasa. Njia moja ya kufanya hili ni kutengeneza bango lenye ratiba ya darasa likionesha jinsi darasa litakavyoenda. Ratiba yako ingeweza kujumuisha sala, muda wa kufundisha, na muda wa shughuli. Hii inaweza kusaidia kupunguza hisia za mashaka ambazo zinaweza kuongeza wasiwasi kwa baadhi ya watoto.

  • Tumia ishara za kuonekana kwa macho. Watoto wenye ulemavu wa kuona au changamoto za tabia wanaweza kunufaika kutokana na ishara za kuonekana kwa macho, kama vile picha zinazoonesha mtindo wa tabia zinazofaa kama kuinua mkono juu kabla ya kujibu swali.

  • Elewa kwa nini tabia zenye kuleta changamoto hutokea. Jifunze kuhusu ulemavu au hali ambazo zinaweza kushawishi mtoto kutenda isivyofaa. Kuwa makini sana kwenye kile kinachofanyika wakati tabia zenye kuleta changamoto zinapojitokeza. Kwa sala fikiria jinsi ya kurekebisha hali ili kumsaidia mtoto vizuri zaidi.

  • Msaidie kila mtoto akue na aendelee. Joseph Smith alifundisha “Viumbe vyote na roho ambao Mungu amewahi kuwaleta ulimwenguni wanao uwezo wa kuongezeka” (Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith [2007], 210). Usidhani mtoto mwenye ulemavu hawezi kujifunza au kuchangia. Mwombe Bwana akusaidie kujua jinsi ya kuwasaidia watoto kufikia uwezekano wao wa kiroho.

Chapisha