Agano la Kale 2022
Oktoba 3–9. Isaya 58–66: “Mkombozi Atakuja Sayuni”


“Oktoba 3–9. Isaya 58–66: ‘Mkombozi atakuja Sayuni,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: Agano la Kale 2022 (2021)

“Oktoba 3–9. Kutoka 58–66,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: 2022

Picha
Yesu akifundisha ndani ya sinagogi

Yesu katika Sinagogi huko Nazareti, na Greg K. Olsen

Oktoba 3–9

Isaya 58–66

“Mkombozi Atakuja Sayuni”

Mawazo ya shughuli katika muhtasari huu yamekusudia kutoa msukumo kwenye ubunifu wako. Usihisi ulazima kuyafuata kama yalivyo; fuata ushawishi wa Roho kabla na wakati wa somo.

Andika Misukumo Yako

Picha
ikoni ya kushiriki

Alika Kushiriki

Mengi ya maneno ya Isaya yanashuhudia na kufundisha kuhusu Mwokozi. Onesha picha ya Yesu Kristo, na uwaalike watoto kushiriki jambo walilojifunza kuhusu Yeye wiki hii.

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wadogo

Isaya 58:13–14

Sabato inaweza kuwa ya furaha kwangu.

Siku ya Sabato ni muda kwetu kumkumbuka Bwana na kupumzika kutokana na shughuli zetu za kila siku. Ni kwa jinsi gani unaweza kuwasaidia watoto unaowafundisha kuifanya Sabato kuwa yenye furaha?

Shughuli Yamkini

  • Waombe watoto warudie kirai “Ukiita sabato siku ya furaha, siku takatifu ya Bwana” (Isaya 58:13) mara kadhaa. Eleza kwamba “furaha” humaanisha kitu kinacholeta shangwe. Waalike watoto kushiriki baadhi ya vitu vinavyowaletea shangwe. Shuhudia kwamba Bwana alitupatia siku ya Sabato kwa sababu Yeye anataka sisi tuwe na shangwe. Waambie watoto kwa nini Sabato ni ya furaha kwako.

  • Wasomee watoto kutoka Isaya 58:14: “Ndipo utakapojifurahisha katika Bwana.” Wafafanulie watoto kwamba Sabato ni siku maalum—muda tunaoweza kufikiria kuhusu mambo ambayo Baba wa Mbinguni na Yesu walifanya ili kutusaidia sisi tuwe na furaha. Wasaidie watoto wafikirie mambo wanayoweza kufanya katika siku ya Sabato ili kumkumbuka Baba wa Mbinguni na Yesu. Waalike wachore mawazo yao na kushiriki picha zao wao kwa wao na familia zao.

Picha
mwanamke akiwasha taa ya kandili ya udongo kutoka kwenye taa iliyoshikiliwa na mikono ya mwanamume

“Bwana atakuwa nuru ya milele kwako” (Isaya 60:19). Zawadi ya Nuru, na Eva Timothy

Isaya 60:1–3

Ninaweza kuangaza nuru ya Mwokozi kwa wengine.

Isaya alitabiri kwamba katika siku za mwisho, watu wa Bwana watakuwa kama nuru kwa wale walio gizani. Zingatia jinsi utakavyowasaidia watoto “kuinuka” na “kuangaza.”

Shughuli Yamkini

  • Waalike watoto wafumbe macho yao wakati ukisoma Isaya 60:1–3. Waombe wafumbue macho yao pale wanaposikia neno “nuru” na kuyafumba pale wanaposikia neno “giza.” Eleza kwamba Yesu Kristo na injili Yake ni kama nuru inayotusaidia kuona njia yetu ya kurudi kwa Baba wa Mbinguni.

  • Mpe kila mtoto picha ya nuru (kama vile jua, mshumaa au balbu ya umeme). Wasaidie wafikirie njia wanazoweza kushiriki nuru ya Mwokozi pamoja na wengine. Kadiri kila wazo linapotolewa, waalike “wainuke” na “waangaze” nuru yao kwa kunyanyua juu picha zao. Waambie watoto kuhusu njia ambazo umewaona wao wakishiriki nuru ya Mwokozi.

  • Imbeni pamoja wimbo kuhusu kushiriki nuru, kama vile “Shine On” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto,144). Wasaidie watoto watambue maneno katika wimbo ambayo yanaimarisha kile wanachojifunza kutoka Isaya 60:1–3.

Isaya 61:1–3

Yesu Kristo ni Mwokozi na Mkombozi wangu.

Isaya 61:1–3 inatoa ufafanuzi wenye nguvu wa huduma ya Mwokozi ya kufundisha na kuponya. Tafuta njia za kuwasaidia watoto kuona jinsi Yesu Kristo anavyoweza kuwafundisha na kuwaponya wao binafsi.

Shughuli Yamkini

  • Waruhusu watoto wanyanyue picha za Yesu akifundisha, akiponya na akiwasaidia wengine wakati unaposoma Isaya 61:1 (ona Kitabu cha Sanaa ya Injili). Eleza kwamba Mungu alimtuma Yesu Kristo kufanya mambo haya kwa ajili yetu sote. Waombe watoto kushiriki hisia zao kuhusu Yesu Kristo. Shuhudia juu ya upendo wa Mwokozi kwa kila mmoja wa watoto.

  • Isaya 61:3 inawaelezea wale wanaosikia na kumtii Bwana kama “miti ya haki.” Chora mti ubaoni na waalike watoto wafikirie mambo ya haki wanayoweza kufanya. Kwa kila wazo, waruhusu watoto wachore jani juu ya mti.

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wakubwa

Isaya 58:6–11

Kufunga kunanibariki mimi na wengine wenye mahitaji.

Baadhi ya watoto unaowafundisha wanaweza kuwa wakubwa kuweza kufunga. Lakini hata wale wasioweza wanaweza kunufaika kutokana na kujifunza kuhusu sheria ya Bwana ya kufunga na kujitayarisha kufunga wakati wawapo tayari.

Shughuli Yamkini

  • Andika ubaoni Kwa nini tunafunga? na Ni jinsi gani tunafunga? Waalike watoto waandike majibu yanayopatikana ubaoni. Waalike warejelee “Funga, Kufunga” katika Mwongozo wa Maandiko (scriptures.ChurchofJesusChrist.org) na Isaya 58:6–11 ili kupata majibu ya ziada. Ni jinsi gani Isaya 58:6–11 inatusaidia wakati kufunga inapokuwa vigumu?

  • Shiriki na watoto uzoefu binafsi kwenye kufunga, au shiriki hadithi kutoka magazeti ya Kanisa kuhusu kufunga. Sisitiza baraka ambazo huja kutokana na kufunga kunakoambatana na lengo la kiroho. Ikiwa yeyote kati ya watoto amewahi kufunga, waalike kushiriki uzoefu wao. Wahimize watoto wazungumze na wazazi wao Jumapili ya mfungo inayofuata kuhusu kile inachomaanisha kufunga. Wasaidie waelewe ina maana gani kufunga kwa lengo la dhati na kwa moyo wa sala.

  • Someni pamoja Isaya 58:6–7, na eleza kwamba njia moja ya “kuwagawia wenye njaa chakula [chetu]” pale tunapofunga ni kwa kuchangia pesa ambayo tungeitumia kwenye chakula kama matoleo ya mfungo. Waoneshe watoto katarasi ya matoleo kwa ajili ya zaka na matoleo ya mfungo na fafanua jinsi ya kuijaza. Waalike watoto wasome Isaya 58:8–10, wakitafuta baraka tulizoahidiwa wakati tunapofunga. Ni jinsi gani kufunga kunaweza kutubariki sisi na wale wenye mahitaji?

Isaya 61:1–3

Yesu Kristo ni Mwokozi na Mkombozi wangu.

Tafakari ni jinsi gani unaweza kutumia vyema zaidi maneno ya Isaya ili kuimarisha shuhuda za watoto juu ya Yesu Kristo kama Mwokozi na Mkombozi wao.

Shughuli Yamkini

  • Wape watoto dakika chache za kusoma Isaya 61:1–3 peke yao. Kisha waalike waandike kwenye kipande cha karatasi au kwenye shajara ya kujifunzia kitu ambacho mistari hii inawafundisha kuhusu Yesu Kristo. Waalike watoto wachache kushiriki mawazo yao.

  • Waalike watoto kushiriki kirai kutoka kwenye mistari hii ambacho hasa kina maana kwao na waeleze ni kwa nini. Je, mistari hii inatusaidiaje kuelewa kitu ambacho Yesu Kristo alitumwa kufanya duniani?

Isaya 65:17–25

Milenia itakuwa ni wakati wa amani na furaha.

Isaya aliona wakati ambapo watu wa Mungu watakuwa na amani na furaha. Unabii huu utatimizwa wakati Yesu Kristo atakaporudi duniani na kutawala kwa miaka elfu moja—kipindi kinachoitwa Milenia.

Shughuli Yamkini

  • Isaya 65:17–25 inafafanua vile dunia itakavyokua wakati Mwokozi atakapokuja tena. Wagawe watoto katika makundi madogo madogo, ukiwapa kila kundi baadhi ya mistari hii kusoma. Baada ya dakika chache, tengeneza orodha ya pamoja ubaoni ya jinsi maisha yatakavyokuwa tofauti katika “nchi mpya” iliyoelezewa katika mistari hii (mstari wa 17). Kwa nini huu utakuwa wakati wa “kufurahi na kushangilia daima”? (mstari wa18).

  • Kabla ya darasa, tayarisha vipande vya maneno vyenye maneno na virai kutoka kwenye makala ya kumi ya imani. Mwalike mmoja wa watoto akariri makala ya imani na waombe watoto waweke vipande vya maneno kwenye mpangilio sahihi. Wasaidie watoto waelewe kile makala hii ya imani inachotufundisha sisi kuhusu milenia.

Picha
ikoni ya kujifunza

Himiza Kujifunza Nyumbani

Waalike watoto kushiriki kitu walichojifunza leo kuhusu Mwokozi pamoja na familia zao. Wahimize wasome maandiko pamoja na familia zao wiki hii.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Uliza maswali yenye kuvutia. Uliza maswali yanayoalika watoto kufikiria kwa undani kuliko kutoa tu ukweli wa mambo. Kwa mfano, fikiria maswali yanayowahimiza kushiriki shuhuda na uzoefu wao.

Chapisha