2021
Kupenda, Kutumikia na kuwahudumia Wengine
Februari 2021


UJUMBE WA URAIS WA ENEO

Kupenda, Kutumikia na kuwahudumia Wengine

“Wakati tunapohudumu, tunawasaidia wengine kutengeneza mpango wa kupata imani kubwa katika Kristo, kufanya maagano na Mungu, na kuponywa kwa rehema ya Kristo.”

Injili ya Marko inasimulia hadithi nzuri ya jinsi Yesu Kristo anavyowajali na kuwasaidia watoto wa Baba yetu wa Mbinguni ambao wanatenda kwa imani katika kusikiliza mafundisho ya Kristo na kufuata amri Zake. Yesu yuko katika mji wa Kapernaumu. Wakati watu wanaposikia Yuko hapo, wanapata shauku ya kumuona Yeye, na wanajaza nyumba ambapo Yesu Kristo anaishi. Inajaa watu kiasi kwamba maandiko yanafundisha, “Wakakusanyika watu wengi, isibaki nafasi hata mlangoni; akawa akisema nao neno lake.”1 Kulikuwa na mtu ambaye alitaka kumsikia Yesu akifundisha, lakini alikuwa mgonjwa sana ilibidi achukuliwe na rafiki zake kitandani. Alikuwa akiteseka kwa kupooza, au aina fulani ya kupooza miguuni. Lakini alitaka kwa dhati kusikia maneno ya Kristo. Rafiki zake walimsaidia kwa kumchukua mpaka kwenye nyumba ambapo angeweza kusikia na kujifunza kutoka kwa Yesu Kristo. Wakiona kwamba hawangeweza kuingia mahali ambapo Kristo alikuwa akifundisha, marafiki walimchukua juu ya jengo na “waliitoboa dari . . . na . . . wakalitelemsha godoro alilolilalia yule mwenye kupooza.”2

Kristo alivutiwa na imani yao. Kama unavyoweza kukumbuka hadithi, Kristo kwanza alisamehe dhambi za mtu aliyeteseka kwa kupooza, na kisha alimponya kimwili ili kuonyesha kwamba alikuwa na nguvu za kuponya kiroho na kimwili. Maandiko yanafundisha, “mara akaondoka, akajitwika godoro lake, akatoka mbele yao wote.”3

Kuna kweli nyingi tunazoweza kujifunza kutoka kwenye tukio hili katika huduma ya Kristo. Moja ninalotaka kuliangazia ni jinsi wanaume wanne walivyompeleka mtu aliyepooza kwa Mwokozi ili aponywe kiroho na kimwili.

Mtu aliyepooza alihitaji usaidizi wa kuja kwa Mwokozi. Asingeweza kumwona Kristo wala kumsikia akiwa peke yake. Rafiki zake walimchukua na kufungua njia kwa ajili yake kuponywa kwa rehema na nguvu ya Kristo. Ni mfano wa kupendeza ulioje wa kuhudumu. Mimi na wewe, kama akina kaka na dada wahudumiaji, kwa sala tunatafuta kutumikia kama ambavyo Kristo angetumikia.4 Tunapaswa “kutembelea nyumba ya kila muumini, kuwahimiza kusali kwa sauti na sirini na kushiriki kazi zote za familia.”5 Tunawaangalia, kuwa nao na kuwaimarisha.6

Kwa ufupi, wakati tunapohudumu, tunawasaidia wengine kutengeneza mpango wa kupata imani kubwa katika Kristo, kufanya maagano na Mungu, na kuponywa kwa rehema ya Kristo. Nimemsikia Mzee Ulisses Soares, wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili, akifundisha kwamba tofauti kati ya mhudumiaji na rafiki ni mwaliko wa kutenda. Acha tuwaalike wale ambao tunawahudumia kutenda wakati wanapoendelea kwenye njia ya agano.

Lucy Mack Smith, mama wa Nabii Joseph Smith, alieleza: “Tunapaswa kuthaminiana, kutunzana, kufarijiana, na kupata maelekezo kwamba sote tuweze kukaa pamoja mbinguni.”7

Ili kutusaidia kuelewa jinsi ya kuwa wahudumiaji wenye ufanisi na kuwa kama Yeye, Baba yetu wa Mbinguni alitutumia Mwana Wake mkamilifu, Yesu Kristo, kuwa mfano wetu. Kristo anatupenda, anatufahamu, na anatusaidia kukua na kutubu na kubadilika, hivyo hutusaidia kupona kiroho na kimwili.

Baba wa Mbinguni pia ametuma malaika kutupatia mfano wa jinsi ya kuwahudumia watoto wa watu.8 Yeye pia ametupatia Mitume wa kutuhudumia sisi. Fikiria jinsi Rais Russell M. Nelson na Mitume wengine wa siku yetu wanavyotuhudumia kwa mafundisho yao ambayo hutuongoza kuongeza imani yetu katika Yesu Kristo na kusonga Kwake.

Wakati tunapojitayarisha kwa Ujio wa Pili wa Yesu Kristo, tunajifunza kutoka kwenye Sura ya 61 ya Isaya, “Katika siku za mwisho Bwana atawaita watumishi wake na kufanya agano la milele na watu.”9 Isaya pia alifundisha kwamba kama watumishi “Wakasaidiana, kila mtu na mwenzake; na kila mtu akamwambia ndugu yake, Uwe na moyo mkuu.”10

Tunapolinganisha maandiko na maisha yetu wenyewe, sisi ambao tumefanya maagano ya ubatizo ndani ya Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, tunaitwa wahudumiaji, tukiwasaidia kila mtu na mwenzake.

Kama vile marafiki wanne waliompeleka mtu aliyepooza kwa Kristo, walioitoboa dari na kumtelemsha chini yule mwenye kupooza ili kwamba Kristo aweze kumponya, tunaombwa kuwainua na kuwaongoza akina kaka na dada wenzetu kwenye njia ya agano iendayo kwa Kristo.

Kwa sala na tutafute mwongozo wa mbingu pale tunapotafuta kuhudumu kwa wale ambao juu yao tumepewa jukumu. Tunapowaalika kwa ujasiri kuchukua hatua inayofuata kwenye njia yao ya agano, tunajitayarisha kwa ajili ya siku moja kukaa nao pamoja mbinguni.

Matthew L. Carpenter aliitwa kama Sabini Mkuu mwenye Mamlaka mnamo Machi 2018. Amemuona Michelle (Shelly) Kay Brown; wao ni wazazi wa watoto watano.

MUHTASARI

  1. Marko 2:2.

  2. Marko 2:4.

  3. Marko 2:12.

  4. Ona General Handbook: Serving in The Church of Jesus Christ of Latter-day Saints [2020], 21.0.

  5. Mafundisho na Maagano 20:51.

  6. Ona Mafundisho na Maagano 20:53.

  7. Lucy Mack Smith, katika Relief Society Minute Book, Mar. 24, 1842, 18-19, Church History Library, Salt Lake City.

  8. Ona 1 Nefi 11:30; 3 Nefi 19:14; Moroni 7:29–31.

  9. Isaya 61 kichwa cha habari.

  10. Isaya 41:6.

Chapisha