Njoo, Unifuate 2024
Septemba 2–8: “Mkumbuke Bwana.” Helamani 7–12


Septemba 2–8: ‘Mkumbuke Bwana.’ Helamani 7–12,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Nyumbani na Kanisani: Kitabu cha Mormoni 2024 (2023)

“Septemba 2–8. Helamani 7–12,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Nyumbani na Kanisani: 2024 (2023)

Picha
Nefi akisali kwenye mnara wa bustani

Kielelezo cha Nefi kwenye mnara wa bustani, na Jerry Thompson

Septemba 2–8: “Mkumbuke Bwana”

Helamani 7–12

Baba wa Nefi, Helamani, aliwasihi wanawe “kumbukeni, kumbukeni.” Aliwataka wawakumbuke mababu zao, wakumbuke maneno ya manabii na zaidi ya yote wamkumbuke “Mkombozi wetu, ambaye ni Kristo” (ona Helamani 5:5–14). Ni wazi kwamba Nefi alikumbuka kwa sababu huu ujumbe ni sawa na ule alioutangaza kwa watu miaka mingi baadaye “bila kusita” (Helamani 10:4). “Mmewezaje kumsahau Mungu wenu?” aliuliza (Helmani 7:20). Juhudi zote za Nefi—kuhubiri, kusali, kufanya miujiza na kumuomba Mungu alete baa la njaa—zilikuwa majaribio ya kuwasaidia watu wamgeukie Mungu na wamkumbuke Yeye. Katika njia nyingi, kumsahau Mungu ni tatizo kubwa zaidi hata kuliko kutokumjua Yeye. Na ni rahisi kumsahau Yeye wakati akili zetu zinapokuwa zimevutiwa na “vitu vya ulimwengu visivyo vya maana” na kufunikwa na wingu la dhambi (Helamani 7:21; ona pia Helamani 12:2). Lakini, kama huduma ya Nefi inavyoonesha, kamwe haujachelewa sana kumkumbuka na “kumgeukia … Bwana Mungu [wako]” (Helamani 7:17).

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Nyumbani na Kanisani

Helamani 7–11

Picha
seminary icon
Manabii hufunua mapenzi ya Mungu kwa watu.

Helamani 7–11 ni mahali pazuri maalum pa kujifunza kuhusu kile ambacho manabi wanafanya. Unaposoma sura hizi, angalia kwa makini matendo, mawazo na mahusiano ya Nefi na Bwana. Ni kwa jinsi gani huduma ya Nefi inakusaidia uelewe vyema jukumu la manabii? Hapa kuna mifano michache. Je, ni kipi kingine unakipata?

Kulingana na kile unachokisoma, ni kwa jinsi gani ungeweza kueleza nabii ni nani na kile ambacho yeye hufanya? Fikiria kuandika maelezo mafupi. Kisha ona kile ambacho ungeongeza kwenye maelezo yako baada ya kusoma ingizo la “Nabii”katika Mwongozo wa Maandiko (Maktaba ya Injili) au “Follow the Living Prophet,” (Teachings of Presidents of the Church: Ezra Taft Benson [2014], 147–55).

Je, uliona jinsi Nefi alivyokuwa jasiri katika Helamani 7:11–29? Je, ni kwa nini unahisi manabii wakati mwingine wanahitajika kuzungumza kwa ujasiri kama Nefi alivyofanya? Fikiria kutafuta majibu katika sehemu yenye kichwa cha habari “Usishangae” ya ujumbe wa Mzee Neil L. Andersen “Nabii wa Mungu” (Liahona, Mei 2018, 38).

Ukiwa na kweli hizi zote akilini, tafakari jinsi Bwana alivyokubariki kupitia huduma ya manabii Wake. Ni kipi Yeye amekufundisha hivi karibuni kupitia nabii wetu aliye hai? Ni kipi unafanya ili kusikiliza na kufuata mwongozo wa Bwana?

Ona pia Mada za Injili, “Manabii,” Maktaba ya Injili.

Helamani 9; 10:1, 12–15

Imani yangu katika Yesu Kristo lazima ijengwe si tu juu ya ishara na miujiza.

Kama ishara au miujiza ingekuwa inatosha kubadili moyo wa mtu, Wanefi wote wangeongolewa kwa ishara za ajabu walizopewa na Nefi katika Helamani 9. Lakini hilo halikutokea. Tazama njia mbalimbali ambazo kupitia hizo watu waliitikia muujiza katika Helamani 9 2–10. Kwa mfano, ungeweza kulinganisha majibu ya wanaume watano na waamuzi wakuu katika Helamani 9:1–20 (ona pia Helamani 9:39–41; 10:12–15). Unajifunza nini kutoka kwenye uzoefu huu kuhusu jinsi ya kujenga imani yako katika Kristo?

Ona pia 3 Nefi 1:22; 2:1–2.

Helamani 10:1–12

Bwana huwapa nguvu watu ambao wanatafuta mapenzi Yake na kujitahidi kushika amri Zake.

Unaposoma Helamani 10:1–12, gundua kile ambacho Wanefi walifanya ili kuaminiwa na Bwana. Je, ni kwa jinsi gani yeye alionesha kwamba alitafuta mapenzi ya Bwana badala ya mapenzi yake mwenyewe? Je, uzoefu wa Nefi unakushawishi ufanye kipi?

Helamani 10:2–4

Kutafakari neno la Mungu hualika ufunuo.

Unapohisi kunyanyaswa, wasiwasi, au mkanganyiko, ungeweza kujifunza somo muhimu kutokana na mfano wa Nefi katika Helamani 10:2–4. Je, yeye alifanya kipi wakati alipohisi “kuhuzunishwa”? (mstari wa 3).

Rais Henry B. Eyring alieleza, “Tunapotafakari, tunaalika ufunuo kwa Roho” (“Serve with the Spirit,” Liahona, Nov. 2010, 60). Je, unawezaje kujenga tabia ya kutafakari?

Helamani 12

Bwana ananitaka nimkumbuke Yeye.

Ni kwa jinsi gani kukumbuka ni muhimu—kama vile siku ya kuzaliwa ya mwanafamilia au taarifa juu ya mtihani? Je, ni kwa jinsi gani hii ni sawa na juhudi ambayo inahitajika “kumkumbuka Bwana”? (Helamani 12:5). Ni kwa jinsi gani hii ni tofauti?

Helamani 12 inaelezea vitu kadhaa ambavyo vinawasababisha watu kumsahau Bwana. Pengine ungeweza kuviorodhesha na kutafakari kama vingeweza kuvuruga mawazo yako kwake. Je, Ni kitu gani hukusaidia umkumbuke Yesu Kristo? Je, Ni kitu gani umevutiwa kufanya kulingana na kile ulichojifunza?

Ona pia Mafundisho na Maagano 20:77, 79; “Sasa kwa Ustahifu,” Nyimbo za Dini, na. 100.

Tumia masomo ya vitendo. Mwokozi kila mara alihusisha kanuni za Injili na mambo ya kila siku ambayo walikuwa wanayafahamu. Wakati unapojifunza au kufundisha kuhusu Helamani 12:1–6, ungeweza kulinganisha “kutokuwa imara … kwa wanadamu” na jinsi tunavyohisi tunapojaribu kusimama kwa mguu mmoja. Ni kwa jinsi gani tunaweza kubaki imara kiroho?

Kwa mawazo zaidi, ona toleo la mwezi huu la Liahona na magazeti ya Kwa ajili ya Nguvu kwa Vijana.

Mawazo kwa ajili ya Kuwafundisha Watoto

Helamani 7:20–21

Bwana ananitaka nimkumbuke Yeye.

  • Ili kuanza mazungumzo kuhusu kumkumbuka Bwana, ungeweza kuwaambia watoto wako kuhusu wakati uliposahau kitu fulani. Waruhusu washiriki uzoefu sawa na huo wao wenyewe. Kisha mngesoma pamoja Helamani 7:20–21 na uwaulize watoto wako kile wanachofikiri inamaanisha kumsahau Mungu. Pengine watoto wako wangeweza kuchora picha za vitu ambavyo vingetusababisha tumsahau Bwana na kutumia michoro yao kufunika picha ya Yesu. Kisha wangeweza kufikiria juu ya mambo wanayoweza kufanya ili kumkumbuka Yeye. Wanaposhiriki mawazo yao, wangeweza kuondoa michoro mmoja mmoja mpaka picha ya Mwokozi ionekane vyema.

Helamani 8:13–23

Manabii wanashuhudia juu ya Yesu Kristo.

  • Wasaidie watoto wapekue Helamani 8:13–23 ili kupata majina ya manabii ambao walifundisha kuhusu Yesu Kristo. Pengine wanaweza kupitisha picha ya Yesu kila wakati wanapoipata. Je, nabii wetu aliye hai amefundisha nini kuhusu Mwokozi?

  • Mngeweza pia kuimba pamoja wimbo kuhusu manabii, kama vile “Follow the Prophet” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 110–11). Pengine wewe na watoto wako mngechagua kifungu cha maneno muhimu kutoka kwenye wimbo na kuandika neno moja kutoka kwenye kifungu hicho kwenye kila moja ya karatasi zenye alama za nyayo. Kisha ungeweza kutandaza nyayo sakafuni zikielekea kwenye picha ya Mwokozi, na watoto wako wangefuata nyayo kuelekea kwenye picha hiyo. Ni kwa jinsi gani kumfuata nabii kulituongoza kwa Yesu Kristo?

Helamani 10:1–4

Kutafakari maneno ya Mungu hualika ufunuo.

  • Ili kuwasaidia watoto wako waelewe kutafakari kumaanisha nini, mngeweza kusoma pamoja “Tafakari” katika Mwongozo wa Maandiko (Maktaba ya Injili). Je, ni maneno yapi mengine ambayo ni sawa na tafakari? Pengine mngeweza kusoma Helamani 10:1–3 pamoja na kubadilisha neno tafakari kwa maneno hayo mengine. Zungumza na watoto wako kuhusu njia za kufanya kutafakari kuwe sehemu ya kujifunza kwao maandiko.

Helamani 10:11–12

Nitamtii Baba wa Mbinguni.

  • Nefi alimtii Baba wa Mbinguni hata wakati ilipombidi kufanya jambo gumu. Kwa mfano wa hili, wewe na watoto wako mngeweza kusoma Helamani 10: 2, 11–12. Pengine watoto wako wangeigiza kile Nefi alichofanya—watembee kuelekea upande mmoja wa chumba (kama vile wanaenda nyumbani), wasimame, wageuke na watembee kuelekea upande mwingine wa chumba (kama vile wanarudi kuwafundisha watu). Ni nini baadhi ya vitu ambavyo Baba wa Mbinguni anatutaka tufanye?

Kwa ajili ya mawazo zaidi, ona toleo la mwezi huu la gazeti la Rafiki.

Picha
Seantumu alitambuliwa kuwa ndiye muuaji

Kupitia kipawa cha utambuzi, Nefi alitatua mauaji ya mwamuzi mkuu.

© Kitabu cha Mormoni kwa ajili ya Wasomaji Wadogo, Seantumu—Muuaji Anatambuliwa, na Briana Shawcroft; isinakiliwe

Chapisha