Njoo, Unifuate 2024
Septemba 23–29: “Inukeni na Mje Kwangu.” 3 Nefi 8–11


“Septemba 23–29: ‘Inukeni na Mje Kwangu.’ 3 Nefi 8–11,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Nyumbani na Kanisani: Kitabu cha Mormoni 2024 (2023)

“Septemba 23–29. 3 Nefi 8–11,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Nyumbani na Kanisani: 2024 (2023)

Picha
Yesu akiwatokea Wanefi

Mimi Ndimi Nuru ya Ulimwengu, na James Fullmer

Septemba 23–29: “Inukeni na Mje Kwangu”

3 Nefi 8–11

“Tazama, Mimi ni Yesu Kristo ambaye manabii walishuhudia atakuja ndani ya ulimwengu” (3 Nefi 11:10). Kwa maneno haya, Mwokozi aliyefufuka alijitambulisha Mwenyewe, akitimiza unabii wa zaidi ya miaka 600 wa Kitabu cha Mormoni. “Kutokea kule na tamko lile,” Mzee Jeffrey R. Holland aliandika, “vilijumuisha lengo kuu, wakati muhimu, katika historia yote ya Kitabu cha Mormoni. Lilikuwa ni onyesho na tangazo ambalo lilikuwa limetoa taarifa na kumtia msukumo kila nabii Mnefi. … Kila mtu alikuwa amezungumza juu yake, kuimba juu yake, kuota juu yake na kusali kwa ajili ya ujio wake—lakini hapa alikuwepo kiuhalisia. Siku kuu zaidi ya siku zote! Mungu ambaye anabadilisha kila usiku wa giza kuwa mwangaza wa asubuhi alikuwa amefika” (Christ and the New Covenant [1997], 250–51).

Ona pia “Jesus Christ Appears in the Ancient Americas” (video), Maktaba ya Injili.

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Nyumbani na Kanisani

3 Nefi 8–11

Yesu Kristo ni Nuru ya Ulimwengu.

Unaweza kugundua kwamba dhima zinazohusiana na giza na nuru zimerudiwa kote katika 3 Nefi 8–11. Unajifunza nini kutoka kwenye sura hizi kuhusu giza la kiroho na nuru ya kiroho? (ona kwa mfano, 3 Nefi 8:19–23; 9:18; 10:9–13). Nini huleta giza maishani mwako? Je, ni kitu gani huleta nuru? Kwa nini unadhani Mwokozi alichagua kujitambulisha Mwenyewe kama “nuru na uzima wa ulimwengu”? (3 Nefi 9:18; 11:11).

Matukio yaliyoelezwa katika 3 Nefi 9–11 ni miongoni mwa matukio matakatifu zaidi katika Kitabu cha Mormoni. Yasome pole pole, na uyatafakari kwa makini. Hapa kuna baadhi ya maswali ya kukusaidia. Fikiria kuandika misukumo ambayo inakujia kwako.

  • Ni kwa jinsi gani ningehisi kama ningekuwa miongoni mwa watu hawa?

  • Ni nini kinanivutia kuhusu Mwokozi kutoka katika sura hizi?

  • Ni kwa jinsi gani ninajua kwamba Yesu Kristo ni Mwokozi wangu.

  • Ni kwa jinsi gani Yeye amekuwa nuru katika maisha yangu?

Ona pia Sharon Eubank, “Kristo: Nuru Ing’aayo Gizani,” Liahona, Mei 2019, 73–76.

Andika Misukumo. Unapoandika msisukumo ya kiroho unayopokea, una uwezekano wa kuIpokea zaidi.

3 Nefi 9–10

Yesu Kristo anatamani kusamehe.

Mzee Neil L. Andersen alisema, “Ninashuhudia kwamba Mwokozi anaweza na ana hamu ya kusamehe dhambi zetu” (“Tubu … Ili Niweze Kukuponya,” Liahona, Nov. 2009, 40). Chunguza 3 Nefi 9–10 kwa ajili ya ushahidi wa hamu ya Kristo ya kusamehe. Ni kipi unakipata katika 3 Nefi 9:13–22; na 10:1–6 ambacho kinakusaidia uhisi upendo na rehema Yake? Ni lini ulihisi Yeye “akikukusanya” na “akikulisha” wewe? (ona 3 Nefi 10:4).

3 Nefi 9:19–22

Bwana anahitaji “moyo uliovunjika na roho iliyopondeka.”

Kabla ya ujio wa Mwokozi, dhabibu za wanyama zilikuwa ishara ya dhabihu ya Yesu Kristo (ona Musa 5:5–8). Ni amri gani mpya Mwokozi aliitoa katika 3 Nefi 9:20–22? Ni kwa jinsi gani inatuelekeza Kwake na kwenye dhabihu Yake?

Je, inamaanisha nini kwako kutoa dhabihu ya moyo uliovunjika na roho iliyopondeka? Kwa nini unahisi Mwokozi anataka dhabihu hii kutoka kwako?

3 Nefi 11:1–8

Picha
seminary icon
Ninaweza kujifunza kuisikia na kuielewa sauti ya Mungu.

Ni kwa jinsi gani unaweza kujua wakati Mungu anapozungumza nawe? Pengine uzoefu wa watu katika 3 Nefi 11:1–8 unaweza kukusaidia uelewe baadhi ya kanuni za kuisikia na kuielewa sauti ya Mungu. Unaweza kugundua sifa za sauti ya Mungu ambayo watu waliisikia na kile walichofanya ili kuielewa vyema zaidi.

Ingeweza pia kuwa yenye msaada kuyachunguza maandiko mengine ambayo yanaelezea sauti ya Mungu au ushawishi wa Roho Wake. Hapa kuna machache: Pengine, baada ya kuyasoma haya, ungeweza kuandika baadhi ya miongozo kwa ajili ya kutambua ufunuo: 1 Wafalme 19:11–12; Wagalatia 5:22–23; Alma 32:27–28, 35; Helamani 10:2–4; Etheri 4:11–12; Mafundisho na Maagano 9:7–9; 11:11–14.

Ungeweza pia kufaidika kwa kusikia kutoka kwa manabii wa siku hizi, mitume, na viongozi wengine wa Kanisa ambao wana uzoefu wa kuisikia na kuifuata sauti ya Mungu. Baadhi yao wameshiriki uzoefu wao katika “Hear Him!” mkusanyiko wa video katika Maktaba ya Injili. Fikiria kuangalia moja au zaidi ya video hizo.

Ni kwa jinsi gani unaweza kutumia kile ulichojifunza kuisikia na kuitambua sauti ya Mungu kwa uwazi zaidi?

Ona pia Russell M. Nelson, “Msikilize Yeye,” Liahona, Mei 2020, 88–92; “This Is My Beloved Son,” Kitabu cha Nyimbo cha Watoto, 76; Mada za Injili, “Ufunuo Binafsi,” Maktaba ya Injili.

Picha
Yesu akiwaonesha Wanefi makovu katika mikono Yake

Mmoja Mmoja, na Walter Rane

3 Nefi 11:8–17

Yesu Kristo ananialika nitafute ushahidi binafsi juu Yake.

Takriban watu 2,500 walikusanyika katika hekalu huko Neema wakati Yesu Kristo alipotokea (ona 3 Nefi 17:25). Licha ya idadi hii kubwa, Mwokozi aliwaalika kila mtu “mmoja mmoja” waguse alama za misumari katika mikono na miguu Yake (3 Nefi 11:14–15). Unaposoma, fikiria vile ambavyo ingeweza kuwa kama ungekuwa pale. Ni katika njia zipi Mwokozi anakualika “uinuka na uje” Kwake? (3 Nefi 11:14).

Kwa mawazo zaidi, ona toleo la mwezi huu la Liahona na magazeti ya Kwa ajili ya Nguvu kwa Vijana.

Mawazo kwa ajili ya Kuwafundisha Watoto

3 Nefi 8–9

Wakati ninapokuwa gizani, Yesu Kristo anaweza kuwa nuru yangu.

  • Ili kuwasaidia watoto wako wajihusishe na uzoefu ulioelezwa katika 3 Nefi 8–9, mngeweza kusimulia tena au kusikiliza sehemu zilizorekodiwa za sura hizi ndani ya chumba chenye giza. Jadilianeni vile ambavyo ingeweza kuwa kuwa katika giza kwa muda wa siku tatu. Kisha mngeweza kuzungumza kuhusu kwa nini Yesu Kristo alijiita Nuru ya Ulimwengu (ona 3 Nefi 9:18). Yesu aliwaalika watu, pamoja nasi, kufanya kitu gani ili Yeye aweze kuwa nuru yetu? (ona 3 Nefi 9:20–22).

3 Nefi 10:4–6

Yesu huwalinda watu Wake kama vile kuku anavyowalinda vifaranga wake.

  • Tafakuri ya kufikirika ya kuku akikusanya vifaranga vyake inaweza kuwa zana yenye nguvu ya kufundishia ili kuwasaidia watoto waelewe tabia na misheni ya Mwokozi. Ungeweza kusoma 3 Nefi 10:4–6 wakati familia yako inatazama picha ya kuku na vifaranga. Kwa nini kuku anahitaji kukusanya vifaranga vyake? Kwa nini Mwokozi anataka kutukusanya tuwe karibu Naye? Ni kwa jinsi gani tunaweza kuja Kwake kwa ajili ya usalama?

3 Nefi 11:1–15

Yesu Kristo ananialika nije Kwake.

  • Ni kwa jinsi gani unawasaidia watoto wako wamhisi Roho mnaposoma 3 Nephi 11:1–15 pamoja? Pengine ungeweza kuwaomba wakuambie wakati wanapopata kitu katika mistari hii ambacho kinawasaidia wahisi upendo wa Mungu. Ungeweza kufanya vivyo hivyo na picha zilizo katika muhtasari huu au video “Jesus Christ Appears at the Temple” (Maktaba ya Injili). Waambie watoto wako kuhusu jinsi unavyohisi wakati unaposoma na kutafakari matukio haya. Waruhusu washiriki hisia zao pia.

3 Nefi 11:1–8

Mungu huzungumza nami kwa sauti ndogo, ya utulivu.

  • Pengine ungeweza kusoma baadhi ya mistari hii kwa “sauti ndogo” tulivu (3 Nefi 11:3). Au ungeweza kupiga wimbo uliorekodiwa kama vile “This Is My Beloved Son” (Kitabu cha Nyimbo cha Watoto, 76) kwa utulivu ili kwamba iwe vigumu kusikia. Je, watu walifanya nini ili waweze kuielewa sauti kutoka mbinguni? (ona mistari 5–7). Je, tunajifunza nini kutokana na uzoefu wao?

3 Nefi 11:21–26

Yesu Kristo ananitaka nibatizwe.

  • Unaposoma 3 Nefi 11:21–26, ungeweza kuwaalika watoto wako wasimame kila mara wanaposikia neno batiza. Ni kipi Yesu alifundisha kuhusu ubatizo? Kama watoto wamewahi kuona ubatizo kabla, waombe waelezee kile walichoona. Kwa nini Yesu anatutaka sisi tubatizwe?

Kwa ajili ya mawazo zaidi, ona toleo la mwezi huu la gazeti la Rafiki.

Picha
Yesu akiwatokea Wanefi

Mchungaji Mmoja, na Howard Lyon

Chapisha