Njoo, Unifuate
Julai 27–Agosti 2. Alma 39–42: “Mpango Mkuu wa Furaha”


“Julai 27–Agosti 2. Alma 39–42: ‘Mpango Mkuu wa Furaha,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Kitabu cha Mormoni 2020 (2020)

“Julai 27–Agosti 2. Alma 39–42,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2020

Picha
Yesu na Mariamu

Mwanamke, Kwa nini Unalia? na Mark R. Pugh

Julai 27–Agosti 2

Alma 39–42

“Mpango Mkuu wa Furaha”

Unapojifunza Alma 39–42, Roho Mtakatifu anaweza kukupa misukumo kuhusu mambo ambayo yanafanyika maishani mwako.

Andika Misukumo Yako

Wakati mtu tunayempenda anapokuwa ametenda kosa kubwa, inaweza kuwa vigumu kujua jinsi ya kujibu. Sehemu ya kile kinachofanya Alma 39–42 kuwa yenye thamani kubwa ni kwamba inafunua jinsi Alma—mwanafunzi wa Kristo ambaye kwa wakati mmoja alikuwa na dhambi zake mwenyewe za kutubu—alishughulikia hali kama hiyo. Mwana wa Alma Koriantoni alikuwa ametenda dhambi ya uasherati, na Alma, kama ilivyokuwa mazoe yake, aliamini uwezo wa mafundisho ya kweli katika kuchochea toba (ona Alma 4:19; 31:5). Katika sura hizi, tunaona ujasiri wa Alma katika kulaani dhambi na huruma na upendo wake kwa Koriantoni. Na hatimaye, tunahisi imani ya Alma kwamba Mwokozi “atakuja kuondoa [dhambi na] kutangaza habari njema ya wokovu” kwa wale wanaotubu (Alma 39:15). Ukweli kwamba Koriantoni hatimaye alirudi katika kazi ya huduma (ona Alma 49:30) unaweza kutupa tumaini la msamaha na ukombozi wakati [tuna]sumbuliwa” (Alma 42:29) kuhusu dhambi zetu wenyewe au dhambi za mtu tunayempenda.

Picha
ikoni ya kujifunza kibinafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kibinafsi

Alma 39

Dhambi ya uasherati ni chukizo machoni pa Bwana.

Ili kumuonyesha mwanaye uzito wa dhambi ya uasherati, Alma alifundisha, “kwamba vitu hivi ni machukizo machoni mwa Bwana” (Alma 39:5). Kwa nini usafi wa kimwili ni muhimu kwako? Kwa nini ni muhimu kwa Mungu? Maelezo yafuatayo kutoka kwa Mzee Jeffrey R. Holland yanaweza kuwa yenye msaada :

“Ni dhahiri kuwa kati ya shughuli Zake kuu kuhusu maisha ya duniani ni jinsi mtu huingia katika dunia hii na jinsi mtu anavyoondoka . Yeye ameweka mashariti ya kikomo katika mambo haya.

“… Uhusiano wa kimapenzi umehifadhiwa kwa ajili ya wanandoa kwa sababu ni ishara kuu ya muungano kamili, muungano uliotawazwa na kufafanuliwa na Mungu.… Ndoa ilidhamiriwa kumaanisha kuungana kamili kwa mwanaume na mwanamke. … Huu ni muungano wa ukamilifu kiasi kwamba tunatumia neno kuunganisha kuelezea ahadi yake ya milele” (“Utakatifu wa Kibinafsi,” Ensign, Nov. 1998, 76).

Fikiria ushauri Alma aliompa Koriantoni katika Alma 39:8–15. Inakusaidiaje kuelewa zaidi umuhimu wa sheria ya usafi wa kimwili na jinsi ya kushinda majaribu? Mafunzo ya Alma yanaonyesha jinsi ambavyo Bwana yuko tayari kutusamehe wakati tunapotubu na kwamba kuna tumaini kwetu sote. Unaposoma Alma 39–42 wiki hii, tafuta ushahidi wa rehema ya Mungu. Ni jinsi gani rehema ya Mungu imekubariki wewe?

Ona pia “Usafi wa Kimwili,” Kwa Nguvu ya Vijana, 35–37.

Alma 40–41

Nitafufuliwa na kusimama mbele ya Mungu kuhukumiwa.

Wakati Alma alipogundua kwamba Koriantoni alikuwa na maswali kuhusu Ufufuo, alimfundisha kuhusu kile kinachofanyika baada ya sisi kufa . Ni kweli zipi Alma alifundisha katika sura za 40–41 ambazo zingekuwa msaada kwa Koriantoni—na yeyote ambaye ametenda dhambi—kuelewa? Unaweza kupanga unachojifunza kwa kutambua mada ambazo Alma anazungumzia (kama vile ulimwengu wa roho, ufufuo, na urejesho) na kisha kuandika kile Alma anachofundisha kuhusu kila moja. Jinsi gani kukumbuka kweli hizi kunakusaidia wewe wakati unapohisi kujaribiwa au unapotafuta msamaha?

Alma 40

Ninaweza kutafuta majibu ya maswali yangu ya injili kwa imani.

Wakati mwingine tunaweza kudhania kwamba manabii wanajua majibu kwa kila swali la injili. Lakini tambua kwamba kote katika sura ya 40, Alma alikuwa na maswali kadhaa bila majibu kuhusu maisha baada ya kifo. Ni nini alifanya kutafuta majibu? Alifanya nini wakati alipokuwa hana majibu? Fikiria jinsi mfano wa Alma unavyoweza kukusaidia kwa maswali ya injili ambayo unayo.

Picha
mwanamke akisali

Sala ni njia moja tunayoweza kupata majibu ya maswali yetu ya injili.

Alma 42

Upatanisho wa Yesu Kristo unafanya mpango wa wokovu uwezekane.

Koriantoni aliamini kwamba adhabu kwa ajili ya dhambi haikuwa haki (ona Alma 42:1). Lakini Alma alifundisha ya kwamba kulikuwa na njia ya kuepuka “hali ya taabu” ambapo dhambi inatuweka ndani yake: toba na imani katika Upatanisho wa Yesu Kristo, ambao ni wa rehema na haki (ona Alma 42:15). Unaposoma Alma 42, tafuta jinsi ambavyo Upatanisho wa Mwokozi unafanya uweze kupokea rehema bila ya “kuibia haki” (mstari wa 25). Ni kweli gani unazozipata katika sura hii ambazo zinakusaidia wewe kuhisi rehema Yake?

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zisisitizwe na kujadiliwa ili kukidhi mahitaji ya familia yako. Haya ni baadhi ya mawazo.

Alma 39:1–9

Je, familia yako ingenufaika kutokana na majadiliano kuhusu sheria ya usafi wa kimwili? Kama ni hivyo, fikiria kutumia nyenzo zifuatazo kulingana na mahitaji ya familia yako: Alma 39:1–9; “Usafi wa Kimwili,” Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana, 35–37; “Usafi wa Kimwili,” Mada za Injili, topics.ChurchofJesusChrist.org; overcomingpornography.org; na video “Nifanye Nini Wakati Ninapoona Pornografia?” na “Nachagua Kuwa Msafi” (ChurchofJesusChrist.org). Tafakari jinsi unavyoweza kusaidia familia yako kuelewa baraka za usafi wa kimwili na ngono katika ndoa (kwa mfano, tazama video “Jinsi ya Kuzungumza na Watoto Wako Kuhusu Ngono” kwenye ChurchofJesusChrist.org).

Alma 39:9–15

Je, tunajifunza nini kutoka kwenye aya hizi kuhusu jinsi tunavyoweza kuepuka dhambi?

Alma 42:4

Mnaweza kucheza mchezo ambapo vijikaratasi vilivyoandikwa sifa za Kristo au kanuni za injili vimetawanywa katika chumba. Unaweza kuona ni vipande vingapi vya karatasi wanafamilia wanaweza kukusanya katika muda fulani, kisha mjadiliane jinsi vitu vilivyoandikwa kwenye karatasi vinaweza kutusaidia zaidi kuwa kama Mungu. Ni kwa jinsi gani “muda tuliopewa” hapa duniani ni kama muda uliopangwa katika mchezo huu? Ni kwa jinsi gani twaweza kutumia “wakati wa majaribio” duniani ili tuweze kufanana zaidi na Mwokozi?

Alma 42:12–15, 22–24

Pengine unaweza kuonyesha uhusiano baina ya haki na rehema kwa kutumia mchoro rahisi wa mizani ili kujadiliana maswali kama haya: Ni nini kinachofanyika kwenye mizani wakati tunapotenda dhambi? Haki inahitaji nini ili mizani iwe sawa? Ni jinsi gani Mwokozi anatosheleza mahitaji ya haki na kufanya rehema kuwezekana?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kufundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Zingatia kanuni ambazo zitabariki familia yako. Unapojifunza neno la Mungu kwa kusali jiulize, “Ni nini ninachopata hapa ambacho kitakuwa cha muhimu hasa kwa familia yangu?” Tafuta maelekezo ya Roho unapotafakari jinsi ya kuisaidia familia yako kugundua kweli hizi.

Picha
Alma na Koriantoni

Huyu Mwanangu, na Elspeth Caitlin Young

Chapisha