Mafundisho na Maagano 2021
Januari 4–10. Joseph Smith—Historia ya 1:1–26: “Niliona Nguzo ya Mwanga”


“Januari 4–10. Joseph Smith—Historia ya 1:1–26: ‘Niliona Nguzo ya Mwanga,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Mafundisho na Maagano 2021 (2020)

“Januari 4–10. Joseph Smith—Historia ya 1:1–26” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2021

Picha
Kijisitu Kitakatifu

Kijisitu Kitakatifu, na Greg K. Olsen

Januari 4–10

Joseph Smith—Historia ya 1:1–26

“Niliona Nguzo ya Mwanga”

Unaposoma Joseph Smith—Historia ya 1:1–26, ni jumbe zipi unazopata kwa ajili ya maisha yako? Je, vifungu gani ni vya thamani kubwa zaidi kwako na kwa familia yako?

Andika Misukumo Yako

Mafundisho na Maagano ni kitabu cha majibu kwa sala: mengi ya maono matakatifu katika kitabu hiki yalikuja kama majibu ya maswali. Kwa hiyo yafaa kuanza kujifunza Mafundisho na Maagano kwa kufikiria swali ambalo lilianzisha mbubujiko wa ufunuo wa siku za mwisho—lile Joseph Smith alilouliza katika kijisitu cha miti mnamo mwaka 1820. “Vita vya maneno na makelele ya maoni” (Joseph Smith—Historia ya 1:10) vilimwacha Joseph akiwa amekanganyikiwa kuhusu dini na hali ya nafsi yake; pengine unaweza kujifananisha na hilo. Kuna mawazo mengi yanayopingana na sauti zinazoshawishi katika siku hizi, na tunapotaka kuchambua jumbe hizi na kupata ukweli, tunaweza kufanya kile Joseph alichofanya. Tunaweza kuuliza maswali, kujifunza maandiko, kutafakari, na hatimaye kumuuliza Mungu. Katika kujibu sala ya Joseph, nguzo ya mwanga ilishuka kutoka mbinguni; Mungu Baba na Yesu Kristo walitokea na walijibu maswali yake. Ushuhuda wa Joseph wa uzoefu ule wa kimiujiza kwa ujasiri unatangaza kwamba yeyote “ambaye [amepungukiwa] na hekima aombe dua kwa Mungu, naye atapata” (Joseph Smith—Historia ya 1:26). Tunaweza wote kupokea, kama sio ono la kimbingu, angalau ono la wazi zaidi, lililoangazwa na nuru ya mbinguni.

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

Joseph Smith—Historia ya 1:1–26

Joseph Smith ni Nabii wa Urejesho.

Azma ya historia ya Joseph Smith ilikuwa kutuweka sisi “katika kuupata ukweli” kwa sababu ukweli kuhusu Joseph mara nyingi umepotoshwa (Joseph Smith—Historia ya 1:1). Unaposoma Joseph Smith—Historia ya 1:1–26, ni kipi kinaimarisha ushuhuda wako wa wito wake mtakatifu? Andika ushahidi unaoupata kwamba Bwana alimtayarisha Joseph Smith kwa ajili ya utumishi wake wa kinabii. Unaposoma, unaweza pia kurekodi mawazo yako na hisia kuhusu Joseph Smith na ushuhuda wake.

Ona pia Watakatifu, 1:3–19.

Joseph Smith—Historia ya 1:5–20

Kama nitaomba kwa imani, Mungu atajibu.

Je, Umewahi “kupungukiwa na hekima” au kuhisi kukanganyikiwa kuhusu uamuzi uliohitaji kufanya? (Joseph Smith—Historia ya 1:13). Unajifunza nini kutokana na uzoefu wa Joseph Smith katika mistari 5–20? Fikiria juu ya hitaji lako mwenyewe la hekima na uelewa mkubwa, na fikiria jinsi utakavyotafuta ukweli.

Ona pia 1 Nefi 10:17–19; 15:6–11; Russell M. Nelson, “Ufunuo kwa ajili ya Kanisa, Ufunuo kwa ajili ya Maisha Yetu,” Ensign au Liahona, Mei 2018, 93–96.

Picha
msichana akiomba

Tunaweza kumuuliza Mungu maswali yetu kupitia sala.

Joseph Smith—Historia ya 1:15–20

Kwa nini kuna simulizi tofauti za Ono la Kwanza?

Wakati wa uhai wake, Joseph Smith alirekodi uzoefu wake katika Kijisitu Kitakatifu takribani mara nne, mara kwa mara akitumia mwandishi. Kwa kuongezea, baadhi ya simulizi tofauti na ile ya kwanza ziliandikwa na watu waliomsikia Joseph akizungumza kuhusu ono lake. Ingawa simulizi hizi zinatofautiana katika baadhi ya taarifa, kutegemeana na wasikilizaji na mpangilio, vinginevyo ziko sawa. Na kila simulizi inaongeza taarifa ambayo inatusaidia kuelewa vyema uzoefu wa Joseph Smith, sawa sawa na kila moja ya Injili nne zinavyotusaidia kuelewa vyema huduma ya Mwokozi.

Kusoma maelezo mengine ya Joseph, ona “First Vision Accounts” (Gospel Topics, topics.ChurchofJesusChrist.org). Je, unajifunza nini kutokana na kusoma simulizi hizi zote?

Joseph Smith—Historia ya 1:15–20

Ono la Kwanza lilianzisha Urejesho wa injili ya Yesu Kristo.

Joseph Smith aliamini kwamba Mungu angejibu sala yake, lakini hakuweza kutarajia jinsi ambavyo jibu lile lingebadili maisha yake—na ulimwengu. Unaposoma kuhusu uzoefu wa Joseph, tafakari jinsi Ono la Kwanza lilivyobadili maisha yako. Kwa mfano, unaweza kukamilisha sentensi hii katika njia tofauti: “Kwa sababu Ono la Kwanza lilitokea, Ninajua kwamba …” Ni kwa jinsi gani umebarikiwa kwa sababu ya Ono la Kwanza?

Ona pia “Ask of God: Joseph Smith’s First Vision,” video, ChurchofJesusChrist.org; Saints, 1:14–19; Russell M. Nelson, “Msikilize Yeye,” Ensign au Liahona, Mei 2020, 88–92.

Joseph Smith—Historia ya 1:21–26

Ninaweza kubaki mkweli kwa kile ninachokijua, hata kama wengine watanikataa.

Mojawapo ya baraka za maandiko ni kwamba yana mifano ya kutia moyo ya mashujaa wanaume na wanawake ambao walikabiliana na changamoto kwa imani katika Yesu Kristo. Wakati Joseph Smith alipokabiliana na upinzani kwa sababu ya ono lake, alijifananisha na Mtume Paulo, ambaye pia aliteswa kwa kusema ameona ono. Unaposoma simulizi ya Joseph, nini kinakusukuma kubaki mkweli kwenye ushuhuda wako? Ni mifano gani mingine—kutoka kwenye maandiko au watu unaowajua—inakupa ujasiri kubaki mkweli kwenye uzoefu wa kiroho uliokuwa nao?

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

Joseph Smith—Historia ya 1:6.Ni kwa jinsi gani tunaweza kushughulikia kutokukubaliana bila kuwa wagomvi kama watu walioelezwa katika mstari huu?

Joseph Smith—Historia ya 1:11–13.Kusoma mistari hii kunaweza kuwatia moyo wanafamilia kushiriki uzoefu wa wakati kifungu cha maandiko kilipogusa mioyo yao na kuwatia moyo kutenda.

Joseph Smith—Historia ya 1:16–20.Familia yako inaposoma mistari hii, fikiria kuonesha mchoro ambao unaambatana na muhtasari huu au picha nyingine ya Ono la Kwanza (labda familia yako ingefurahia kuchora picha zao wenyewe). Mngeweza pia kuangalia video “Ask of God: Joseph Smith’s First Vision” (ChurchofJesusChrist.org). Mngeweza kila mmoja wenu kutengeneza orodha ya kweli tunazojifunza kutoka ono hili, kisha shiriki orodha yako na mwingine. Huu ungekuwa wakati mzuri kwa ajili ya wanafamilia kushiriki jinsi walivyopata shuhuda zao za Ono la Kwanza la Joseph Smith.

Joseph Smith—Historia ya 1:17.Wakati Mungu alipomtokea Joseph Smith, Alimwita Joseph kwa jina lake. Ni lini wanafamilia yako wamehisi kwamba Baba wa Mbinguni anawajua kibinafsi?

Joseph Smith—Historia ya 1:21–26.Ni kwa jinsi gani tunaweza kujibu wakati watu wanapotilia shaka ushuhuda wetu?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “Sala ya Kwanza ya Joseph Smith,” Nyimbo za Kanisa, na. 26.

Picha
ikoni ya sauti za urejesho

Sauti za Urejesho

Familia ya Joseph Smith

Kila mmoja wetu ameathiriwa kwa kina na maisha yetu ya kifamilia, na Joseph Smith hakuwa tofauti. Msimamo wa kidini wa wazazi wake na desturi vilipanda mbegu za imani ambazo zilifanya Urejesho uwezekane. Shajara ya Joseph Smith inarekodi shukrani hii: “Maneno na lugha havitoshi kuelezea shukrani ambayo ninadaiwa na Mungu kwa ajili ya kuweza kunipa uzawa wa heshima.”1

Nukuu zifuatazo kutoka kwa mama yake, Lucy Mack Smith; kaka yake William Smith; na Nabii mwenyewe zinatupa mtazamo wa mara moja kwenye ushawishi wa kidini katika nyumba ya akina Smith.

Picha
Familia ya Smith

Familia ya Joseph Smith, na Dan Baxter

Lucy Mack Smith

Picha
Lucy Mack Smith

“[Yapata mwaka 1802], nilikuwa mgonjwa. … Nilijiambia mwenyewe, sijajitayarisha kufa kwani sijui njia za Kristo, na ilionekana kwangu kama vile kulikuwa na korongo la upweke na giza kati yangu na Kristo ambalo sithubutu kujaribu kulivuka. …

“Nilitazama kwa Bwana na niliomba na kumsihi Bwana kwamba angeyanusuru maisha yangu ili niweze kuwalea watoto wangu na kufariji moyo wa mume wangu; hivyo nilijilaza usiku kucha. … Nilifanya ahadi na Mungu [kwamba] kama angeniacha niishi ningefanya bidii kupata ile dini ambayo ingeniwezesha kumtumikia kwa usahihi, bila kujali ingekuwa katika Biblia au kama ingeweza kutafutwa, hata kama ingeweza kupatikana kutoka mbinguni kwa sala na imani. Hatimaye sauti ilizungumza nami na kusema, ‘Omba na utapata, bisha na utafunguliwa. Acha moyo wako ufarijiwe. Unamwamini Mungu, niamini na mimi pia.’ …

“Kutoka wakati huu na kuendelea nilipata nguvu endelevu. Nilisema japo kidogo juu ya mada ya dini ingawa ilichukua akili yangu yote, na nilifikiri kwamba ningefanya bidii yote mara nitakapoweza kumtafuta mtu fulani mwenye kumcha Mungu aliyejua njia za Mungu kunifundisha mambo ya Mbinguni.”2

William Smith

Picha
William Smith

“Mama yangu, ambaye alikuwa mwanamke mcha Mungu sana na mwenye kupenda ustawi wa watoto wake, kote hapa na baada ya hapa, alitumia kila uwezo ambao upendo wake wa mzazi ungeweza kupendekeza, kutufanya tujishughulishe katika kuomba kwa ajili ya wokovu wa nafsi zetu, au (kama neno lilivyokuwa wakati huo) ‘katika kupata dini.’ Alitushawishi kuhudhuria mikutano, na takribani familia yote ikapenda jambo hilo, na kuwa watafutaji wa ukweli.”3

“Siku zote tulikuwa na sala za familia kwa kadiri ninavyoweza kukumbuka. Ninakumbuka vizuri baba alikuwa na desturi ya kubeba miwani yake katika mfuko wa fulana yake, … na wakati sisi wavulana tulipomwona akipapasa miwani yake, tulijua ile ilikuwa ishara ya kuwa tayari kwa ajili ya sala, na kama hatukugundua mama angesema, ‘William,’ au yeyote yule aliyekuwa mzembe, ‘jitayarishe kwa ajili ya sala.’ Baada ya sala kulikuwa na wimbo ambao tungeimba.”4

Picha
miwani ikiwa juu ya maandiko

Joseph mkubwa na Lucy Smith walifundisha familia yao kusoma maandiko.

Joseph Smith

Picha
Joseph Smith

“Sasa ninasema, kwamba [baba yangu] kamwe hakufanya tendo la uchoyo ambalo lingesemekana si la ukarimu, katika maisha yake, kwa ufahamu wangu. Nilimpenda baba yangu na kumbukumbu yake; na kumbukumbu ya matendo yake ya wema, huja kwa uzito mkubwa juu ya akili zangu; na mengi ya maneno yake ya ukarimu na ya mzazi kwangu, yameandikwa juu ya kibao cha moyo wangu. Matakatifu kwangu, ni mawazo ambayo ninayahifadhi ya historia ya maisha yake, ambayo yamezunguka akili zangu na yamepandikizwa huko, kwa kufuatilia kwangu mwenyewe tangu nilipozaliwa. … Mama yangu pia ni mmoja wa waadilifu, na bora zaidi ya wanawake wote.”5

Picha
Ono la Kwanza

Ono la Kwanza la Urejesho, na Michael Bedard

Chapisha