Agano Jipya 2023
Machi 27–Aprili 2. Mathayo 14; Marko 6; Yohana 5–6: “Msiogope”


Machi 27–Aprili 2. Mathayo 14; Marko 6; Yohana 5–6: ‘Msiogope’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya 2023 (2022)

Machi 27–Aprili 2. Mathayo 14; Marko 6; Yohana 5–6,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2023

Picha
Yesu akitembea na wanafunzi wamebeba vikapu vya mkate

Machi 27–Aprili 2

Mathayo 14; Marko 6; Yohana 5–6

“Msiogope”

Unaposoma Mathayo 14; Marko 6; na Yohana 5–6, tafuta kweli ambazo zina maana kwako. Unaweza kujiuliza mwenyewe maswali kama vile “Je, ni kwa jinsi gani matukio katika sura hizi yananihusu mimi?” “Je, ni ujumbe gani ninapata kwa ajili ya maisha yangu?” au “Je, ni kitu gani ningependa kushiriki na familia yangu au na wengine?

Andika Misukumo Yako

Je, ni kitu gani kiliweza kumshawishi Petro atoke kwenye usalama wa mashua yake katikati ya Bahari ya Galilaya wakati wa dhoruba kali? Je, ni kitu gani kilimfanya aamini kwamba kama Yesu aliweza kutembea juu ya maji, naye angeweza pia? Hatuwezi kujua kwa hakika, lakini pengine Petro alielewa kwamba Mwana wa Mungu alikuja sio tu kufanya mambo ya ajabu kwa watu lakini kuwawezesha watu kama Petro kufanya mambo ya ajabu pia. Mwaliko wa Yesu, hata hivyo, ulikuwa “Njoo, unifuate” (Luka 18:22). Petro alikuwa amekubali mwaliko huu mara moja, na alikuwa tayari kuukubali tena, hata kama ilimaanisha kukabiliana na woga wake na kufanya jambo ambalo lilionekana kutowezekana. Pengine Bwana hatatuambia tutoke nje ya mashua katikati ya dhoruba au kuchangia akiba yetu ndogo ya mkate wakati maelfu wanapohitaji kula, lakini anaweza kututaka tuikubali miongozo hata wakati ambapo hatuielewi kikamilifu. Vyovyote mialiko Yake yoyote kwetu itakavyokuwa, yawezekana wakati mwingine ikaonekana ya kushangaza au hata ya kuogopesha. Lakini miujiza inaweza kutokea ikiwa sisi, kama Petro, tutaweka kando woga wetu, shaka yetu, na kikomo cha uelewa wetu na kumfuata Yeye kwa imani.

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa Ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

Yohana 5:16–47

Yesu Kristo anamheshimu Baba Yake.

Uhusiano kati ya Baba wa Mbinguni na kila mmoja wa watoto Wake unapaswa kuwa mtakatifu. Katika mistari hii, Yesu Kristo alitupatia mfano wa kuvutia wa kufuata katika uhusiano wetu na Baba wa Mbinguni. Soma Yohana 5:16–47, na uwekee alama au kuandika kila linapotamkwa neno Baba. Je, ni kwa jinsi gani Mwana anaonyesha heshima kwa Baba, na jinsi gani wewe unaweza kufuata mfano Wake? Je, ni kitu gani unajifunza kuhusu jinsi Baba anavyohisi juu ya Mwana? Je! Unapata mwongozo wa kufanya nini ili kuimarisha uhusiano wako na Baba yako wa Mbinguni?

Ona pia Yohana 17; Jeffrey R. Holland, “Ukuu wa Mungu,” Liahona, Nov. 2003, 70–73.

Picha
mikate na samaki

Yesu aliwalisha watu 5000 kimiujiza kwa mikate mitano na samaki wawili.

Mathayo 14:15–21; Marko 6:33–44; Yohana 6:5–14

Mwokozi anaweza kukuza matoleo yangu haya madogo ili kufikia malengo Yake.

Je, umewahi kuhisi usiyefaa kutimiza mahitaji yote unayoona yanakuzunguka—nyumbani kwako, katika uhusiano wako, au katika jamii? Wanafunzi wa Yesu lazima walihisi wasiofaa alipowataka kuwalisha watu elfu tano wenye njaa wakati ilipokuwepo mikate mitano na samaki wawili tu. Unaposoma kuhusu muujiza uliofuata, tafakari jinsi gani Mungu angeweza kutumia matoleo yako madogo ya huduma kuwabariki wale wanaokuzunguka. Je, ni kwa jinsi gani Yeye ameweza kukuza jitihada zako wakati ulipohudumu? Fikiria maelezo haya kutoka kwa Dada Michelle D. Graig: “Wewe na mimi tunaweza kutoa tulichonacho kwa Kristo, naye atazidisha juhudi zetu. Kile unachoweza kutoa ni zaidi ya cha kutosha—hata pamoja na kasoro na mapungufu yako ya kibinadamu—kama ukitegemea neema ya Mungu” (“Kutoridhika kwa Kiungu,” Liahona, Nov 2018, 54).

Mathayo 14:22–33; Marko 6:45–52; Yohana 6:15–21

Yesu Kristo ananialika kuweka kando woga na shaka yangu na kuonyesha imani yangu Kwake.

Weka taswira akilini mwako ya maelezo ya kina ya tukio lililoelezwa katika Mathayo 14:22–33; Marko 6:45–52; na Yohana 6:15–21. Fikiria jinsi gani Petro na wale wanafunzi wengine walivyohisi. Je, unajifunza nini kuhusu ufuasi kutokana na maneno na matendo ya Mwokozi katika mistari hii? Je, unajifunza nini kutokana na maneno na matendo ya Petro? (Ona pia 1 Nefi 3:7.) Je, Bwana anakualika kufanya nini ambacho kinaweza kuwa sawa na kushuka chomboni? Je, unapata nini katika mistari hii ambacho kinakupa ujasiri wa kuonyesha imani yako kwa Yesu Kristo?

Yohana 6:22–71

Kama mfuasi wa Yesu Kristo, ni lazima niwe radhi kuamini na kukubali ukweli, hata kama ni vigumu kufanya hivyo.

Wakati Yesu alipojielezea Yeye Mwenyewe kama ndiye “mkate wa uzima” (Yohana 6:48), wengi waliona hili kuwa ni “neno gumu” (Yohana 6:60). Je, inawezekanaje maneno ya Petro katika Yohana 6:68–69 yakakusaidia wewe katika nyakati ambazo mafundisho ya Mwokozi yanaonekana kuwa magumu kuyakubali au kuyaishi? Kitu gani kinakuvutia kuhusu ushuhuda wa Petro? Je, ni “maneno gani ya uzima wa milele” katika (Yohana 6:68) ambayo hukusaidia kubaki kwenye ahadi uliyojiwekea ya kumfuata Mwokozi?

Ona pia M. Russell Ballard, “Twende kwa Nani?,” Liahona, Nov. 2016, 90–92.

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

Mathayo 14:15–21.Fikiria jinsi ambavyo ungeweza kuisaidia familia yako kufikiria ni kiasi gani ingechukua kulisha watu elfu tano. Je, muujiza katika Mathayo 14:15–21 hutufundisha nini kuhusu Mwokozi? Fikiria kushiriki uzoefu wa wakati ulipohisi haukuwa na vya kutosha kutoa na Mwokozi alizidisha juhudi zako.

Mathayo 14:22–33.Familia yako inaweza kufurahia kuigiza tena hadithi iliyo katika mistari hii. Je, kwa nini wanafunzi walikuwa wameogopa? Je, kwa nini Petro aliweza kushinda woga wake na kuondoka chomboni? Je, ni kwa jinsi gani alionyesha imani hata wakati alipoanza kuzama? Je, ni kwa jinsi gani sisi wakati mwingine tuko kama Petro?

Yohana 5:1–16.Waalike wanafamilia kuandika mifano ya kirai “ponya” katika mistari hii. Ni katika njia zipi Yesu Kristo huwaponya watu? Lini na jinsi gani Yeye ametuponya sisi?

Yohana 6:28–58.Mpe kila mwanafamilia kipande cha mkate ale, na kujadili faida tunayopata kutoka kwenye mkate na vyakula vingine vyenye kutupa afya. Kisha pekueni mistari hii pamoja, mkitafuta kwa nini Yesu Kristo alijiita “mkate wa uzima” (Yohana 6:35). Ingeweza kumaanisha nini “kula” mkate wa uzima? (ona D. Todd Christofferson, “Mkate Ulio Hai Ambao Ulishuka Kutoka Mbinguni,” Liahona, Nov. 2017, 36–39).

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “How Great the Wisdom and the Love,” Nyimbo za Kanisa, na. 195.

Kuboresha Kujifunza Binafsi.

Tafuta umaizi wako mwenyewe wa kiroho. Katika kujifunza kwako binafsi na kama familia, usijiwekee ukomo kwenye vifungu vya maandiko vilivyoonyeshwa katika miuhtasari hii. Bwana pengine ana jumbe kwa ajili yako katika sura hizi ambazo hazijaelezewa hapa. Kwa maombi zitafute.

Picha
Yesu akimwinua Petro kutoka majini

Dhidi ya Upepo, na Liz Lemon Swindle

Chapisha