Agano Jipya 2023
Julai 24–30. Matendo ya Mitume 16–21: “Bwana Alituita Kuihubiri Injili”


“Julai 24–30. Matendo ya Mitume 16–21: ‘Bwana Alituita Kuihubiri Injili’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya 2023 (2022)

“Julai 24–30. Matendo ya Mitume 16–21,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2023

Picha
Paulo akifundisha juu ya kilima

Julai 24–30

Matendo ya Mitume 16–21

“Bwana Alituita Kuihubiri Injili”

Unaposoma kuhusu juhudi za Paulo kuihubiri injili, Roho anaweza kukushawishi kwa mawazo au hisia. Andika ushawishi huo, na weka mipango ya kuifanyia kazi.

Andika Misukumo Yako

Miongoni mwa maneno ya mwisho ya Bwana kwa Mitume Wake ilikuwa ni amri, “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu: na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi” (Mathayo 28:19–20). Hali Mitume hawakuweza kufika katika mataifa yote, Matendo ya Mitume 16–21 huonyesha kwamba Paulo na wenzake walifanya maendeleo yasiyo na kifani katika kulikuza Kanisa. Walifundisha, walibatiza, na kutunuku kipawa cha Roho Mtakatifu. Walifanya miujiza, hata kumfufua mtu kutoka wafu, na kutabiri Ukengeufu Mkuu (Matendo ya Mitume 20:7–12; 28–31). Na kazi waliyoanzisha inaendelezwa na Mitume walio hai leo, sambamba na wafuasi wanaojitolea kama wewe, ambao husaidia kutimiza jukumu la Mwokozi katika njia ambazo Paulo hakuweza kuzifikiria. Pengine unawajua watu ambao hawamjui Baba yao wa Mbinguni au injili Yake. Pengine umehisi kwamba “roho yako ilichochewa sana ndani [yako]” kushiriki na wengine kile unachojua kumhusu Yeye (Matendo ya Mitume 17:16). Kama ukifuata mfano wa Paulo wa unyenyekevu na ujasiri katika kushiriki injili, unaweza kumpata mtu “ambaye moyo wake [umefunguliwa] na Bwana” (Matendo ya Mitume 16:14).

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa Ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

Matendo ya Mitume 16–21

Roho ataniongoza katika jitihada zangu za kushiriki injili kwa wengine.

Nabii Joseph Smith alitangaza, “Hakuna mtu anayeweza kuihubiri Injili bila kuwa na Roho Mtakatifu” (Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith [2007], 332). Unaposoma Matendo ya Mitume 16–21, fikiria kwa nini maelezo ya Nabii ni ya kweli. Tazama nyakati ambapo Roho aliwaongoza Paulo na wenzake. Ni baraka zipi zilikuja kwa sababu walimfuata Roho? Je, ni lini wewe umehisi Roho akikushawishi katika jitihada zako za kushiriki injili kwa wengine?

Matendo ya Mitume 16–21

Ninaweza kutangaza injili katika hali zozote.

Kuwekwa gerezani kwa sababu ya kuihubiri injili yaweza kuonekana kama sababu isiyoeleweka ya kuacha kuhubiri. Lakini kwa Paulo na Sila, ilikuwa ni fursa ya kumuongoa mlinzi wa gereza (ona Matendo ya Mitume 16:16–34). Kote katika Matendo ya Mitume 16–21, tafuta mifano mingine ya utayari wa Paulo kushiriki ushahidi wake kwa kila mtu. Kwa nini unadhani alikuwa mkakamavu na jasiri? Je, unajifunza nini kutoka katika mfano wa Paulo?

Kuna jumbe nyingi zaidi kuhusu kushiriki injili katika Matendo ya Mitume 16–21. Unapojifunza sura hizi, tafuta baadhi ambazo ni maalumu kwako.

Ona pia Dieter F. Uchtdorf, “Kazi ya Umisionari: Kushiriki Yaliyo Moyoni Mwako,” Liahona, Mei 2019, 15–18.

Picha
mtoto amebebwa

Kila mmoja wetu ni mtoto wa Mungu.

Matendo ya Mitume 17:16–34

“Sisi ni wazao wa Mungu.”

Katika Athene, Paulo alikuta watu wa mawazo na mitazamo tofauti ya kidini. Wao daima walitafuta “kusikia elimu mpya,” na kile Paulo alichotaka kuwapa kilikuwa hasa kipya kwao (ona Matendo ya Mitume 17:19–21). Waliabudu miungu mingi, ikijumuisha mmoja waliyemuita “mungu asiyejulikana” (Matendo ya Mitume 17:23), lakini waliamini kwamba miungu ilikuwa ni uwezo au nguvu, siyo viumbe, walio hai, na kwa uhakika siyo Baba yetu. Tafakari kile Paulo alichosema ili kuwasaidia wao kumjua Mungu. Inamaanisha nini kwako kuwa “wazao wa Mungu”? (Matendo ya Mitume 17:29). Kwa maoni yako, ni kwa jinsi gani kuwa mwana wa Mungu kunatofautiana na kuwa mmoja tu wa viumbe Wake? Ni kwa jinsi gani kuelewa ukweli huu kunashawishi jinsi unavyojiona na kuwaona wengine?

Kama ulikuwa umesimama kando ya Paulo wakati alipokuwa akishuhudia, ni nini ungewaambia Wagiriki wa kale kuhusu Baba yetu wa Mbinguni? Je, unamjua mtu anayeweza kunufaika kutokana na kusikiliza ushuhuda wako?

Ona pia Warumi 8:16; 1 Yohana 5:2; “We Are the Offspring of God” (video), ChurchofJesusChrist.org.

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

Matendo ya Mitume 16–21.Ili kuongeza kina cha uelewa wa familia yako juu ya Matendo ya Mitume 16:21, mgeweza kujifunza ramani mwisho wa muhtasari huu, mkitafuta miji ambayo Paulo alihubiri injili katika sura hizi. Ni nyenzo gani tulizonazo leo za kutusaidia kuipeleka injili kwa mataifa yote?

Ili kuhamasisha familia yako kushiriki injili, ungeweza kuonyesha video moja au zaidi katika “Sharing the Gospel” sehemu ya Maktaba ya Injili.

Matendo ya Mitume 17:10–12; 18:24–28.Ni kwa jinsi gani tunaweza kuwa zaidi kama Watakatifu katika mistari hii? Ingeweza kumaanisha nini “[kupokea] neno kwa uelekevu wote wa moyo”? (Matendo ya Mitume 17:11). Je, tunaweza kufanya nini ili kuwa “hodari katika maandiko”? (Matendo ya Mitume 18:24).

Matendo ya Mitume 19:1–7.Mistari hii inaweza kuisaidia familia yako kuwa na mjadala kuhusu umuhimu wa kubatizwa na kuthibitishwa. Ili kuelewa vyema kweli katika Matendo ya Mitume 19:1–7, mngeweza kujadili baadhi ya vitu ambavyo ni bure bila kitu kingine, kama vile simu ya mkononi bila betri. Au ungeweza kushiriki fundisho hili kutoka kwa Nabii Joseph Smith: “Ubatizo wa maji ni nusu ya ubatizo, na hauna faida yoyote bila ile nusu nyingine—ambayo ni ubatizo kwa Roho Mtakatifu” (Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith,95). Kwa nini ubatizo ni “bure” bila kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu? (ona 3 Nefi 27:19–20; Musa 6:59–61).

Matendo ya Mitume 19:18–20.Unaposoma Matendo ya Mitume 19:18–20, tazama thamani za mali ambayo watu walikuwa radhi kuacha kwa minajili ya kuikumbatia injili (ona mstari wa 19). Je, kuna mali au shughuli za ulimwengu ambazo tunahitaji kuziacha ili kupokea baraka za mbinguni?

Matendo ya Mitume 20:32–35.Je, ni wakati gani familia yako ilipata uzoefu wa fundisho la Kristo kwamba “ni heri kutoa kuliko kupokea”? (Matendo ya Mitume 20:35). Je, kuna mtu anayeweza kunufaika kutokana na huduma, muda, au karama ambayo familia yako inaweza kutoa? Kama familia, jadilini baadhi ya mawazo na mfanye mipango ya kumtumikia mtu fulani. Tunajisikiaje tunapowatumikia watu wengine? Kwa nini ni heri kutoa kuliko kupokea?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “I Am a Child of God,” Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 2–3.

Kuboresha Kujifunza Binafsi.

Andika Misukumo. “Wakati unapoandika misukumo ya kiroho, unamuonyesha Bwana kwamba unathamini kuongozwa Naye, na atakubariki zaidi kwa ufunuo wa kila mara” (Kufundisha katika Njia ya Mwokozi, 12; ona pia ukurasa wa 30).

Picha
ramani ya safari za kimisionari za Paulo

Safari za umisionari za Mtume Paulo.

Chapisha