Agano Jipya 2023
Julai 31–Agosti 6. Matendo ya Mitume 22–28: “Mtumishi na Shahidi”


“Julai 31–Agosti 6. Matendo ya Mitume 22–28: ‘Mtumishi na Shahidi’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya 2023 (2022)

“Julai 31–Agosti 6. Matendo ya Mitume 22–28,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2023

Picha
Paulo akiwa gerezani

Julai 31–Agosti 6

Matendo ya Mitume 22–28

“Mtumishi na Shahidi”

Misukumo kutoka kwa Roho Mtakatifu mara nyingi ni tulivu na mara nyingine ni ya muda mfupi tu. Kuandika misukumo yako hukuruhusu kuitafakari kwa kina zaidi. Unaposoma Matendo ya Mitume 22–28, andika mawazo na hisia zinazokujia na jipe muda wa kuzitafakari.

Andika Misukumo Yako

“Tunapokuwa katika kazi ya Bwana,” Rais Thomas S. Monson aliahidi, “tunakuwa wenye kustahili msaada wa Bwana” (“Kujifunza, Kutenda, Kuwa,” Liahona, Nov. 2008, 62). Hatuna haki, hata hivyo, kwenye barabara nzuri na kijito kinachobubujika cha mafanikio yasiyo na mwisho. Kwa ushahidi wa hili, hatuhitaji kuangalia mbali zaidi ya Paulo Mtume. Kazi yake kutoka kwa Mwokozi ilikuwa “kulichukua jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli” (Matendo ya Mitume 9:15). Katika sura 22–28 za Matendo ya Mitume, tunaona Paulo akitimiza kazi hii na kupata upinzani mkubwa—minyororo, kufungwa jela, mateso ya kimwili, kuvunjika kwa merikebu, na hata kuvamiwa na nyoka. Lakini pia tunaona kwamba Yesu “alisimama karibu naye, na kusema, Uwe na moyo mkuu, Paulo” (Matendo ya Mitume 23:11). Uzoefu wa Paulo ni ukumbusho wa wenye kushawishi kwamba wito wa Bwana wa “kuihubiri injili [Yake] kwa sauti ya shangwe” huja na ahadi: “Inueni mioyo yenu na furahini, kwani Mimi niko katikati yenu” (Mafundisho na Maagano 29:4–5); ona pia Mathayo 28:19–20).

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa Ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

Matendo ya Mitume 22:1–21; 26:1–29

Wafuasi wa Yesu Kristo hutoa shuhuda zao kwa ujasiri.

Wakati Paulo alipotoa shuhuda zake zenye nguvu zilizoandikwa katika Matendo ya Mitume 22 na 26, alikuwa akishikiliwa kama mfungwa na askari wa Kirumi. Watu aliozungumza nao walikuwa na uwezo wa kumpa hukumu ya kifo. Lakini bado yeye alichagua kwa ujasiri kutoa ushahidi juu ya Yesu Kristo na “lile ono la mbinguni” (Matendo ya Mitume 26:19) alilokuwa amepokea. Je, ni kitu gani kinakuvutia kuhusu maneno yake? Fikiria fursa ulizonazo za kushiriki ushuhuda wako. Kwa mfano, marafiki zako wanajua jinsi unavyohisi kuhusu Yesu Kristo? Au ni lini ilikuwa mara yako ya mwisho kuwaambia familia yako au wengine jinsi ulivyopata ushuhuda wako juu ya injili?

Wakati kijana Joseph Smith alipokejeliwa kwa kusema kuhusu Ono lake la Kwanza, alihamasishwa na njia ambayo Paulo alishuhudia juu ya ono lake (ona Joseph Smith—Historia 1:24–25). Ni kwa jinsi gani unaweza kufanya muhtasari wa kitu ambacho Joseph Smith alijifunza kutoka kwa Paulo? Unajifunza nini kutoka kwa hawa mashahidi wawili wa Yesu Kristo?

Ona pia Neil L. Andersen, “Tunazungumza Kuhusu Kristo,” Liahona, Nov. 2020, 88–91.

Matendo ya Mitume 23:10–11; 27:13–25, 40–44

Bwana husimama karibu na wale wanaojitahidi kumtumikia.

Kama huduma ya Paulo inavyoonyesha wazi, magumu katika maisha yetu siyo ishara kwamba Mungu hakubaliani nasi au na kazi tunayofanya. Kwa kweli, wakati mwingine ni katika wakati wa magumu ambapo tunauona msaada Wake kwa nguvu sana. Inaweza kuwa ya kuvutia kurudia kile ulichosoma hivi karibuni kuhusu huduma ya Paulo na kuorodhesha baadhi ya mambo aliyovumilia (ona, kwa mfano, Matendo ya Mitume 14:19–20; 16:19–27; 21:31–34; 23:10–11; 27:13–25, 40–44). Ni kwa jinsi gani Bwana alisimama naye? Ni kwa jinsi gani Yeye amesimama nawe?

Matendo ya Mitume 24:24–27; 26:1–3, 24–29;27

Kuna usalama na amani katika kushika maneno ya watumishi wa Mungu.

Katika huduma yake yote, Paulo alitoa ushuhuda wenye nguvu juu ya Yesu Kristo na injili Yake. Watu wengi walikubali ushahidi wake, lakini si kila mtu aliukubali. Unaposoma Matendo ya Mitume 24:24–27 na Matendo ya Mitume 26:1–3, 24–29, tafuta maneno na virai ambavyo huonyesha jinsi watawala wafuatao wa Kirumi katika Yudea walivyopokea mafundisho ya Paulo:

  • Feliki

  • Festo

  • Mfalme Agripa

Wakati wakisafiri kwa merikebu kwenda Rumi kuhukumiwa na Kaisari, Paulo alitoa unabii kwamba “madhara na hasara nyingi” zingeipata merikebu na abiria wake (Matendo ya Mitume 27:10). Soma sura ya 27 kujua jinsi abiria wenzake na Paulo walivyopokea maonyo yake. Je, unapata funzo lolote kwa ajili yako katika tukio lao hili?

Je, umewahi kutoa jibu kama yeyote kati ya watu hawa wakati uliposikiliza mafundisho ya viongozi wa Kanisa? Je, ni nini baadhi ya matokeo ya kutoa jibu katika njia hizi? Je, unajifunza nini kutoka katika matukio haya kuhusu kusikiliza ushauri wa Bwana kupitia watumishi Wake?

Ona pia 2 Nefi 33:1–2; D. Todd Christofferson, “Sauti ya Onyo,” Liahona, Mei 2017, 108–11; “Follow the Living Prophet,” Teachings of Presidents of the Church: Ezra Taft Benson (2014), 147–55.

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

Matendo ya Mitume 24:16.Kabla ya uongofu wake, Paulo alikuwa na historia ndefu ya hatia dhidi ya Mungu. Lakini kwa sababu alikuwa radhi kutubu, aliweza kusema, “Nami ninajizoeza katika neno hili, niwe na dhamiri isiyo na hatia mbele za Mungu na mbele ya watu” (ona pia Mafundisho na Maagano 135:4–5). Ni kwa jinsi gani tunaweza kuondoa dhamiri zetu za hatia mbele za Mungu na mbele ya wengine?

Matendo ya Mitume 26:16–18.Katika mistari hii, Bwana alimuita Paulo kufanya nini? Ni fursa zipi ambazo tunazo za kufanya mambo kama hayo?

Matendo ya Mitume 28:1–9.Je, kuna mtu katika familia yako anayewapenda nyoka? Unaweza kumuomba mtu huyo au mwanafamilia mwingine kusimulia hadithi zinazopatikana katika Matendo ya Mitume 28:1–9. Watoto wako wanaweza kufurahia kuchora picha ya hadithi hizi au kuziigiza. Ni mafunzo gani tunaweza kupata kutokana na matukio haya? Moja laweza kuwa kwamba Bwana hutimiza ahadi Zake kwa watumishi Wake. Kwa mfano, unaweza kulinganisha ahadi zilizofanywa katika Marko 16:18 na utimizwaji wake katika matukio ya Paulo. Unaweza pia kutafuta katika hotuba ya mkutano mkuu wa hivi karibuni ahadi iliyofanywa na mmoja wa watumishi wa Bwana—pengine moja ambayo ina maana kwa familia yako—na kuibandika nyumbani kwako. Ni kwa jinsi gani tunaweza kuonyesha imani yetu kwamba ahadi hii itatimizwa?

Picha
nyoka mwenye sumu

Mungu alimlinda Paulo wakati nyoka mwenye sumu alipomuuma.

Matendo ya Mitume 28:22–24.Kama Kanisa katika siku za Paulo (lilivyoitwa “dhehebu” katika mstari wa 22), Kanisa leo mara kwa mara “limenenwa vibaya.” Watu walipompinga Mwokozi na Kanisa Lake, ni kwa jinsi gani Paulo alijibu? Je, tunaweza kujifunza nini kutokana na uzoefu wa Paulo?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “My Redeemer Lives,” Nyimbo za Kanisa, na. 135.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Zingatia kanuni ambazo zitaibariki familia yako. Unapojifunza maandiko, jiulize mwenyewe, “Ni nini ninachopata hapa ambacho kitakuwa na umuhimu wa kipekee kwa familia yangu?” (Ona Kufundisha katika Njia ya Mwokozi, 17.)

Picha
Paulo mbele ya Mfalme Agripa

Paulo mbele ya Mfalme Agripa. Jasiri katika Ushuhuda wa Kristo, na Daniel A. Lewis.

Chapisha