Agano Jipya 2023
Oktoba 2–8. Waefeso: “Kwa Kusudi la Kuwakamilisha Watakatifu”


“Oktoba 2–8. Waefeso: ‘Kwa Kusudi la Kuwakamilisha Watakatifu’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano Jipya 2023 (2022)

“Oktoba 2–8. Waefeso,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2023

Picha
familia ikitazama picha

Oktoba 2–8

Waefeso

“Kwa Kusudi la Kuwakamilisha Watakatifu”

Je, unaona uhusiano wowote kati ya ujumbe katika mkutano mkuu na Waraka wa Paulo kwa Waefeso?

Andika Misukumo Yako

Wakati injili ilipoanza kusambaa katika Efeso, ilisababisha “ghasia si haba” (Matendo 19:23) miongoni mwa Waefeso. Mafundi stadi wa mahali pale waliotengeneza madhabahu kwa mungu wa kike wa wapagani waliona Ukristo kama tishio kwa maisha yao, na punde “walijawa na ghadhabu, … na mji wote ukajaa ghasia” (ona Matendo 19:27–29). Fikiria kuwa muongofu mpya kwenye injili katika mazingira kama hayo. Waefeso wengi walipokea na kuishi injili katikati ya “hatari” hii (Matendo ya Mitume 19:40), na Paulo aliwahakikishia kwamba “Kristo … ndiye amani yetu” (Waefeso 2:13–14). Maneno haya, pamoja na mwaliko wake “acha uchungu wote, na ghadhabu, na hasira, na kelele, na matukano, yaondoke” (Waefeso 4:31), yanaonekana kuja kwa wakati na ya kutia faraja sasa kama ilivyokuwa wakati huo. Kwa Waefeso, kama ilivyo kwako, nguvu ya kukabiliana na majaribu huja “katika Bwana, na katika uweza wa nguvu zake” (ona Waefeso 6:10–13).

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa Ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

Waefeso 1:4–11, 17–19

Mungu alinichagua, au alinitawaza kabla sijazaliwa ili kutimiza majukumu fulani hapa duniani

Paulo aliongelea juu ya Watakatifu kuwa “walichaguliwa tangu awali” na Mungu na “kuteuliwa … kabla ya kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu” ili kuwa watu Wake. Hata hivyo, kama Rais Henry B. Eyring alinena, hii haimaanishi kwamba “Mungu ameshaamua mapema ni nani katika watoto Wake angewaokoa na kufanya injili ipatikane kwao, huku wale ambao hawakuisikia injili ‘hawakuchaguliwa.’ … Mpango wa Mungu ni wa upendo na wenye haki zaidi ya hilo. Baba yetu wa Mbinguni anatamani kukusanya na kubariki familia Yake yote” (“Kukusanya Familia ya Mungu,” Liahona, Mei 2017, 20–21). Watoto wote wa Mungu wanaweza kuikubali injili na ibada zake kwa sababu ya kazi inayofanyika kwa ajili ya wafu katika mahekalu matakatifu.

Japokuwa hakuna aliyechaguliwa tangu awali kuokolewa au kutookolewa, ufunuo wa siku hizi hufundisha kwamba baadhi ya watoto wa Mungu walichaguliwa au “walitawazwa tangu awali” katika maisha kabla ya kuzaliwa ili kutimiza majukumu fulani katika kukamilisha madhumuni ya Mungu hapa duniani. Unaposoma Waefeso 1 na Mada za Injili, “Kutawazwa kabla ya kuzaliwa” (topics.ChurchofJesusChrist.org), tafakari jinsi kweli hizi zinatumika kwako.

Waefeso 1:10

Mungu “atavijumlisha vitu vyote katika Kristo.”

Kwa nini tunadhani siku yetu inaitwa “kipindi cha utimilifu wa nyakati”? Je, ingemaanisha nini “kuvijumlisha vitu vyote katika Kristo”? Unapotafakari virai hivi, soma maandiko yafuatayo: Waefeso 4:13; 2 Nefi 30:7–8; Mafundisho na Maagano 110:11–16; 112:30–32; 128:18–21. Unaweza kushawishika kuandika maelezo yako mwenyewe ya virai hivi.

Mzee David A. Bednar, “Kukusanya Pamoja Vitu Vyote katika Kristo,” Liahona, Nov. 2018, 21–24.

Waefeso 2:19–22; 3:1–7; 4:11–16

Kanisa lilianzishwa juu ya mitume na manabii, na Yesu Kristo mwenyewe akiwa jiwe kuu la pembeni.

Kulingana na Waefeso 2:19–22; 3:1–7; 4:11–16, kwa nini tunao manabii na mitume? Fikiria kuhusu jumbe kutoka kwa manabii na mitume ulizosikia wakati wa mkutano mkuu. Ni kwa jinsi gani mafundisho yao yanatimiza madhumuni aliyoelezea Paulo? Kwa mfano, ni kwa jinsi gani mafundisho haya yalikusaidia wewe “kutotupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu”?

Je, ni kwa jinsi gani Yesu Kristo ni kama jiwe la pembeni la Kanisa? Ni jinsi gani Yeye amekuwa kama jiwe la pembeni katika maisha yako?

Ona pia Matendo ya Mitume 4:10–12.

Picha
jiwe la pembeni la jengo

Yesu Kristo ni jiwe la pembeni la Kanisa.

Waefeso 5:216:4

Kufuata mfano wa Kristo kunaweza kuimarisha uhusiano katika familia yangu.

Unaposoma Waefeso 5:216:4, fikiria kuhusu jinsi ushauri katika mistari hii unavyoweza kuimarisha uhusiano wa familia yako.

Ni muhimu kukumbuka kwamba maneno ya Paulo katika Waefeso 5:22–24 yaliandikwa katika mazingira ya mila za kijamii za enzi yake. Manabii na mitume leo hufundisha kwamba wanaume si bora zaidi ya wanawake na kwamba wanandoa wanatakiwa kuwa “wenza walio sawa” (ona “Familia: Tangazo kwa Ulimwengu,” ChurchofJesusChrist.org) Hata hivyo, bado unaweza kupata ushauri husika katika Waefeso 5:25–33. Kwa mfano, ni kwa jinsi gani Kristo huonyesha upendo Wake kwa Watakatifu? Hii hudokeza nini kuhusu jinsi wanandoa, kama wenzi sawa, wanavyopaswa kuchukuliana? Ni jumbe zipi unazipata kwa ajili yako katika mistari hii?

Waefeso 6:10–18

Silaha za Mungu zitasaidia kunilinda dhidi ya uovu.

Unaposoma Waefeso 6:10–18, fikiria kwa nini Paulo aliweza kutaja kila kipande cha silaha kwa jinsi alivyofanya. “Silaha zote za Mungu” zinakulinda dhidi ya nini? Je, unaweza kufanya nini ili kuvaa kikamilifu kila kipande cha silaha kila siku?

Ona pia 2 Nefi 1:23; Mafundisho na Maagano 27:15–18.

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

Waefeso 1:10.Ili kufundisha kuhusu mstari huu, David A. Bednar alitumia mfano wa kamba (ona “Atavijumlisha Vitu Vyote katika Kristo”). Fikiria kuwaonyesha wanafamilia kamba na waruhusu waishikilie na kuikagua huku ukishiriki sehemu za ujumbe wa Mzee Bednar. Ni kwa jinsi gani Mungu anavijumlisha vitu vyote katika Kristo? Ni kwa jinsi gani tumebarikiwa kwa sababu ya ujumuishaji huu?

Waefeso 2:4–10; 3:14–21.Waalike wanafamilia waelezee matukio ambapo wamehisi upendo na rehema ya Mungu na Yesu Kristo iliyoelezewa katika mistari hii.

Waefeso 2:12–19.Familia yako inaweza kufurahia kujenga kuta kwa kutumia mito au vitu vingine mlivyonavyo nyumbani na kisha kuvibomoa. Wakati Paulo alipotaja “kuta” katikati ya Wayunani na Wayahudi, ni aina gani za kuta zinatenganisha watu leo? Ni kwa jinsi gani Yesu Kristo “amebomoa” kuta hizi? Ni kwa jinsi gani Yeye “atatupatanisha [sisi] na Mungu”? (mstari wa 16).

Waefeso 6:10–18.Familia yako inaweza kujitengenezea wenyewe “silaha za Mungu” kwa kutumia vitu vya nyumbani. Video “The Armour of God” (ChurchofJesusChrist.org) inaweza kuwasaidia wanafamilia kupata taswira ya silaha hizi, na wanaweza kupata maelezo rahisi katika “Silaha Zote za Mungu” (Gazeti la Rafiki, Juni 2016, 24–25). Ni kwa jinsi gani kila kipande cha silaha hutulinda kiroho? Je, tunaweza kufanya nini ili kusaidiana sisi kwa sisi “kuvaa silaha zote za Mungu” (Waefeso 6:11) kila siku?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “Hope of Israeli,” Nyimbo za Kanisa, na. 259.

Kuboresha Kujifunza Binafsi

Mruhusu Roho aongoze kujifunza kwako. Kuwa mwepesi kuhisi Roho anapokuongoza kwenye mambo unayohitaji kujifunza kila siku, hata kama hii hukuongoza kujifunza mada ambayo hukuipanga.

Picha
mtu katika silaha za enzi za Agano Jipya

Kuvaa silaha za Mungu kunaweza kutulinda kiroho.

Chapisha