Njoo, Unifuate
Agosti 31–Septemba 6. Helamani 13–16: “Habari Njema ya Shangwe Kuu”


“Agosti 31–Septemba 6. Helamani 13–16: ‘Habari Njema ya Shangwe Kuu,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: Kitabu cha Mormoni 2020 (2020)

“Agosti 31–Septemba 6,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: 2020

Picha
Samweli Mlamani akifundisha juu ya ukuta

Samweli Mlamani juu ya Ukuta, na Arnold Friberg

Agosti 31–Septemba 6

Helamani 13–16

“Habari Njema ya Shangwe Kuu”

Jiandae kufundisha kwa kusoma Helaman 13–16 na kutafakari shughuli zipi zitawasaidia vizuri watoto kujifunza kweli katika sura hizi.

Andika Misukumo Yako

Picha
ikoni ya kushiriki

Alika Kushiriki

Onyesha picha ya Samweli Mlamani, na waalike watoto kushiriki jambo wanalolijua kumhusu. Kwa mfano, je, wangeweza kuzungumza kuhusu hadithi ya Samweli akifundisha juu ya ukuta au ishara alizosema zingetokea wakati wa kuzaliwa Yesu?

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wadogo

Helamani 13:2–5

Roho anaweza kuzungumza na mioyo yetu.

Samweli Mlamani alipoamriwa kuhubiri kwa Wanefi, Baba wa Mbinguni alimsaidia kujua katika moyo wake kile alichopaswa kusema.

Shughuli za Yakini

  • Wafundishe watoto kwamba wakati sisi tunazungumza kwa kutumia maneno, Roho Mtakatifu anaweza kuzungumza kupitia hisia katika mioyo yetu. Waalike kuweka mikono yao juu ya mioyo yao kila mara unaposoma neno “moyo” katika Helamani 13:2–5. Wasaidie kupamba vipande vya karatasi vyenye umbo la moyo vinavyosema, “Roho huzungumza nami katika moyo wangu.”

  • Waambie watoto kwamba wanapobatizwa na kuthibitishwa, watakuwa na kipawa cha Roho Mtakatifu kuwasaidia kujua kile Baba wa Mbinguni anawataka kufanya na kusema. Wasaidie kufikiria mambo ambayo Roho Mtakatifu angeweza kuwaambia, na waalike kushiriki kile ambacho wangeweza kufanya kufuata uvuvio Wake.

Helamani 14:2–7, 20–25

Manabii wanafundisha kuhusu Yesu Kristo.

Tukio la Samweli Mlamani ni fursa kubwa ya kuwafundisha watoto kwamba manabii wanafundisha kuhusu Yesu Kristo.

Shughuli za Yakini

  • Onyesha picha ya Samweli Mlamani kwenye muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia, na waambie watoto, kwa maneno rahisi, kuhusu uzoefu wake katika Helamani 13–16. Ungeweza pia kutumia “Mlango wa 40: Samweli Mlamani Anazungumza kuhusu Yesu Kristo” (Hadithi za Kitabu cha Mormoni, 111–13, au video inayohusiana katika ChurchofJesusChrist.org). Waache watoto kushiriki kile wanachojua kuhusu Samweli Mlamani.

  • Imbeni kwa pamoja “Samweli Anamzungumzia Mtoto Yesu” au aya ya saba ya “Hadithi za Kitabu cha Mormoni” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 36, 118–19). Shiriki jambo linalokuvutia kuhusu Samweli, na waruhusu watoto kushiriki kile wanachokipenda kuhusu hadithi yake.

  • Ficha picha kuzunguka chumba ambazo zinawakilisha ishara ambazo Samweli alizitolea unabii katika Helamani 14:2–7 na 20–25. Soma kifungu cha maneno ambacho kinaelezea moja ya ishara, na waombe watoto watafute picha ya ishara hiyo. Elezea kwamba ishara hizi ziliwasaidia Wanefi kujua kuhusu Yesu Kristo. Shuhudia kwamba, kama Samweli, manabii wote hushuhudia juu ya Yesu Kristo.

Picha
Rais Russell M. Nelson

Nabii hutuongoza kuelekea kwa Yesu Kristo.

Helamani 16:1–6

Ninabarikiwa pale ninapomfuata nabii.

Baba wa Mbinguni ametupatia Nabii ili kutusaidia kujua mapenzi Yake na kufuata mpango Wake. Tunabarikiwa tunaposikiliza maneno ya nabii na kuyatii.

Shughuli za Yakini

  • Wasaidie watoto kujenga ukuta mdogo kwa matofali au vitabu. Kwa kutumia mwanasesere mdogo kumwakilisha Samweli, waruhusu watoto kufanya zamu kumsaidia “Samweli” kupanda ukuta ili kuwafundisha watu kuhusu Yesu Kristo. (Ona pia ukurasa wa shughuli ya wiki hii.) Shiriki vifungu vya maneno kutoka Helamani 16:1 na 5 kuelezea kwamba baadhi ya watu walimwamini Samweli na walibatizwa. Tumia vifungu vya maneno kutoka Helamani 16:2 na 6 kuonyesha kwamba wengine hawakuamini na walimkasirikia Samweli. Shuhudia kwamba watu wanaomfuata nabii wanabarikiwa.

  • Onyesha picha ya Mwokozi, na muombe mtoto kumwakilisha nabii na kuongoza watoto wengine kuzunguka chumba wakati wakiimba mistari kadhaa ya “Follow the Prophet” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 110–11) au wimbo mwingine kuhusu manabii. Kisha muombe mtoto anayemwakilisha nabii kuwaongoza watoto kwenye picha ya Mwokozi. Shuhudia kwamba tukimfuata nabii, atatuongoza kwa Yesu Kristo. Shiriki baadhi ya mambo ambayo nabii wetu amefundisha kuhusu Yesu hivi karibuni. Ni kwa jinsi gani tunaweza kufuata ushauri wake?

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wakubwa

Helamani 13:2–4

Roho anaweza kuzungumza na mioyo yetu.

Siku moja, watoto unaowafundisha watahitaji kujua jinsi ya kufanya kile Samweli alichofanya: kushiriki ujumbe ambao Bwana anaweka katika mioyo yao.

Shughuli za Yakini

  • Onyesha picha ya Samweli Mlamani (kama ile iliyoko katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia), na waulize watoto ni kwa jinsi gani Samweli alijua nini cha kusema wakati alipokuwa akihubiri kutoka kwenye ukuta wa mji. Waalike watafute Helamani 13:2–4 kwa ajili ya majibu. Simulia kuhusu wakati ambapo Roho Mtakatifu alikusaidia kujua katika moyo wako kile ambacho Mungu alitaka ufanye au useme. Waombe watoto kushiriki uzoefu sawa na huo waliowahi kuwa nao.

  • Onyesha picha ya nabii aliye hai akizungumza kwenye mkutano mkuu. Waambie watoto kwamba Mungu humwambia nabii nini cha kusema kwetu, kama vile Alivyomwambia Samweli nini cha kusema kwa Wanefi. Zungumzeni pamoja kuhusu mambo nabii aliyosema ambayo yamekuwa yenye ushawishi kwako au kwa watoto.

Helamani 14:2–28

Manabii wanafundisha kuhusu Yesu Kristo.

Lengo la ujumbe wa Samweli lilikuwa ni kushuhudia juu ya Yesu Kristo na kuwaalika watu kutubu na kuja Kwake. Manabii wetu leo wana jukumu sawa na hilo.

Shughuli za Yakini

  • Alika nusu ya watoto wasome Helamani 14:2–6 na kuchora picha za ishara za kuzaliwa kwa Yesu. Alika nusu nyingine ya darasa wasome Helamani 14:20–28 na kuchora picha za ishara za kifo cha Yesu. Kisha liombe kila kundi kushiriki kile walichochora. Someni pamoja Helamani 14:11–12, na waombe watoto wasikilize kwa nini Samweli alitoa unabii kuhusu ishara hizi. Ni kwa jinsi gani tunajifunza kuhusu Yesu Kristo leo?

  • Elezea kwamba kama vile Samweli Mlamani alivyofundisha kuhusu Yesu Kristo, manabii walio hai wanafanya vivyo hivyo leo. Shiriki maelezo kutoka kwenye ujumbe wa mkutano wa hivi karibuni ambapo nabii aliye hai alishuhudia juu ya Kristo. Waombe watoto kushiriki kile nabii alichowafundisha kuhusu Yesu Kristo.

Helamani 16:1–6

Ninabarikiwa pale ninapomfuata nabii.

Baba wa Mbinguni ametupatia Nabii ili kutusaidia kujua mapenzi Yake na kufuata mpango Wake. Tunabarikiwa pale tunaposikiliza na kutii maneno ya nabii.

Shughuli za Yakini

  • Soma kwa sauti Helamani 16:1 na 5, na waombe watoto wasimame wakati wanaposikia jambo watu walilofanya wakati walipoamini maneno ya Samweli. Kisha soma mstari wa 2 na wa 6, na waombe watoto waketi wakati wanaposikia jambo watu walilofanya wakati hawakuamini. Ni kwa jinsi gani tunaweza kuonyesha kwamba tunaamini maneno ya nabii aliye hai?

  • Onyesha picha ya nabii aliye hai, na waombe watoto kushiriki kile wanachokijua kuhusu yeye. Shiriki jinsi unavyojaribu kufuata mafundisho yake na jinsi gani kufanya hivyo kumekubariki.

Picha
ikoni ya kujifunza

Himiza Kujifunza Nyumbani

Waalike watoto kujifunza kuhusu jambo nabii alilosema na kushiriki na darasa wiki inayofuata.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Wahimize watoto kuuliza maswali “Jitahidi kuona maswali ya [watoto] kama fursa, sio kama usumbufu au vizuizi kwa somo lako. … Maswali kama hayo yanakupa utambuzi muhimu wa kujua kile watoto wanachofikiria, wasiwasi walio nao, na jinsi wanavyoitikia mambo wanayojifunza” (ona pia Kufundisha katika Njia ya Mwokozi, 25–26).

Chapisha