Agano la Kale 2022
Mei 23–29. Yoshua 1–8; 23–24: “Uwe Hodari na Moyo wa Ushujaa”


“Mei 23–29. Yoshua 1–8; 23–24: ‘Uwe Hodari na Moyo wa Ushujaa’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: Agano la Kale 2022 (2021)

“Mei 23–29. Yoshua 1–8; 23–24,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: 2022

Picha
Musa akimtawaza Joshua

Kielelezo cha Musa akimtawaza Yoshua, na Darrell Thomas

Mei 23–29

Yoshua 1–8; 23–24

“Uwe Hodari na Moyo wa Ushujaa”

Unaposoma Yoshua 1–8 na 23–24, andika misukumo ya kiroho unayopokea. Unaweza kufanya nini kugundua kile watoto unaowafundisha wanahitaji kujifunza kutoka katika sura hizi?

Andika Misukumo Yako

Picha
ikoni ya kushiriki

Alika Kushiriki

Chora picha ubaoni ya kitu fulani kutoka kwa mojawapo wa hadithi katika Yoshua 1–8; 23–24, na uone kama watoto wanaweza kubahatisha hadithi inatoka wapi. Kwa mfano, unaweza kuchora mto au ukuta wa mji.

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wadogo

Yoshua 1:8

Ninaweza kufikiria kuhusu maandiko mchana na usiku.

Bwana alimwambia Yoshua kwamba kama angetakafari juu ya maandiko na kufuata ushauri uliomo ndani yake, atapata ufanisi katika kuwaongoza Waisraeli hadi nchi ya ahadi. Ni nini tunaweza kufanya kuwafundisha watoto juu ya baraka kuu ambazo huja kutoka kwenye maandiko?

Shughuli Yamkini

  • Mpe kila mtoto picha au mchoro wa jua na mwezi. Wasomee kutoka Yoshua 1:8: “Yatafakari [maandiko] mchana na usiku.” Elezea kwamba kutafakari kunamaanisha kufikiria kwa undani kuhusu jambo fulani. Rudia kifungu hiki mara kadhaa, na uwaalike watoto kuinua juu mchoro wa jua unaposema “mchana” na mwezi unaposema “usiku.” Waache watoto warudie kifungu cha maneno pamoja na wewe.

  • Waombe watoto wataje vitu wanavyofanya wakati wa mchana na vitu wanavyofanya usiku. Waambie kwamba Yoshua aliambiwa afikirie kuhusu maandiko mchana na usiku. Wasaidie kufikiria hadithi au mafundisho kutoka kwenye maandiko ambayo wanaweza kuyafikiria mchana na usiku. Waalike wachore picha zao wenyewe au familia zao zikijifunza maandiko. Kwa nini wanapenda kujifunza maandiko? Je, ni kwa jinsi gani wanabarikiwa wanapofanya hivyo?

Yoshua 3

Ni lazima nibatizwe ili kuingia ufalme wa mbinguni.

Hadithi ya Yoshua akiwaongoza Waisraeli kupita Mto Yordani hata nchi ya ahadi hutoa fursa ya kuwafundisha watoto kwamba ni lazima tubatizwe ili kuingia katika ufalme wa mbinguni.

Shughuli Yamkini

  • Pitia maelezo kadhaa ya hadithi ya wana wa Israeli wakivuka Mto Yordani kuingia nchi ya ahadi (ona “Yoshua Nabii” katika Hadithi za Agano la Kale). Kisha onyesha picha ya Yesu akibatizwa, na waambie watoto kwamba Yesu alibatizwa katika mto huo huo. Waalike watoto kushiriki vitu wanavyojua kuhusu ubatizo wa Yesu.

  • Imba wimbo kuhusu ubatizo pamoja na watoto, kama vile “Baptism” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 100–101). Wasaidie kutambua kile wimbo huu unatufundisha kuhusu kwa nini Yesu alibatizwa na kwa nini tunapaswa kufuata mfano Wake. Waache watoto washiriki hisia zao kuhusu kubatizwa. Zungumza kuhusu kile watoto wanaweza kufanya sasa ili kujiandaa kubatizwa wanapofika umri wa miaka minane.

    Picha
    msichana amesimama katika kisima cha ubatizo

    Hatuna budi kubatizwa ili kuingia katika ufalme wa mbinguni.

Yoshua 24:15.

Ninaweza kuchagua kumtumikia Yesu Kristo.

Ujumbe wa mwisho wa Yoshua kwa watu wake ulikuwa kwamba walikuwa na uchaguzi kuendelea kumtumikia Bwana au kumwacha Yeye. Kwa upendo huo huo ambao Yoshua alikuwa nao kwa watu wake, unaweza kuwahimiza watoto unaowafundisha kuchagua kumtumikia Bwana “siku hii.”

Shughuli Yamkini

  • Waombe watoto kuzungumza kuhusu baadhi ya chaguzi walizozifanya leo. Wasomee watoto kutoka katika Yoshua 24:15: “Chagueni hivi leo mtakayemtumikia; … lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia Bwana.” Ni kwa jinsi gani watoto wamechagua kumtumikia Bwana leo? Je, ni baadhi ya njia gani tunazoweza kuchagua kumtumikia Yeye kila siku?

  • Imbeni wimbo kuhusu kufanya maamuzi mazuri, kama vile “Choose the Right Way” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 160–61). Tunajihisi vipi tunapochagua kumtumikia Yesu Kristo? Waalike watoto wachore picha zao wenyewe wakifanya kitu fulani kumtumikia Bwana. Shiriki hadithi kutoka katika maisha yako au kutoka kwenye jarida la Kanisa kuhusu kuchagua kumtumikia Bwana.

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wakubwa

Yoshua 1–4; 6

“Uwe Hodari na Moyo wa Ushujaa”

Baada ya Yoshua kuwa kiongozi wa Waisraeli, Bwana alimtia moyo kwa kusema “Uwe Hodari na Moyo wa Ushujaa” (Yoshua 1:6). Watoto wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yoshua kuhusu jinsi ya kuwa hodari na shujaa kwa ajili ya Kristo?

Shughuli Yamkini

  • Waalike watoto watafute kifungu cha maneno ambacho kimerudiwa katika Yoshua 1:6, 9, na 18, na ukiandike ubaoni (ona pia mstari wa 7). Wasaidie watoto wafikirie sababu ambazo tunaweza kuhitaji ujumbe huu, kama vile Yoshua alivyofanya. Rejeleeni kama darasa baadhi ya hadithi katika Yoshua 1–4; 6 (ona pia “Yoshua Nabii” na “Rahabu na Wapelelezi” katika Hadithi za Agano la Kale), na uwaombe watoto watambue jinsi watu katika hadithi hizi walionyesha ushujaa na uthabiti.

  • Waalike watoto wazungumze kuhusu mtu wanayemjua ambaye ni hodari na shujaa kwa ajili ya Yesu Kristo. Wahimize wao waandike kitu ambacho wangependa kufanya ili wawe hodari na mashujaa zaidi kwa ajili ya Kristo.

Yoshua 1:8

Ninaweza kuyatafakari maandiko mchana na usiku.

Njia moja Bwana aliyomsaidia Yoshua kujiandaa kwa ajili ya changamoto alizokumbana nazo ilikuwa ni kwa kumhimiza yeye “kutafakari” maandiko “mchana na usiku.” Ni kwa jinsi gani ushauri huu ungeweza kuwabariki watoto unaowafundisha?

Shughuli Yamkini

  • Waalike watoto waandike ni muda gani wanatumia katika siku ya kawaida kwa shughuli tofauti. Kisha waalike wasome Yoshua 1:8, wakitafuta kitu ambacho sisi sote tunahitaji kufanya kila siku mchana na usiku. Waombe watafute maneno na vifungu vya maneno katika mstari huu ambavyo hutufundisha kuhusu baraka za kujifunza maandiko. Ni kwa jinsi gani kutafakari maandiko kunatusaidia kuwa na ufanisi katika vitu vingine tunavyofanya kila siku?

  • Waalike watoto wasome pamoja maandiko yafuatayo: Yoshua 1:8; 1 Nefi 15:23–24; 2 Nefi 31:20; 32:3; Yakobo 4:6; Helamani 3:29–30. Waombe watoto watafute neno au kirai katika kila kifungu cha maneno ambacho kinawafundisha kuhusu uwezo wa kujifunza maandiko. Je, ni malengo gani wanaweza kuweka kwa ajili ya kujifunza maandiko kibinafsi?

Yoshua 24:15

Ninaweza kuchagua kumtumikia Yesu Kristo.

Miongoni wa maneno ya mwisho ya Yoshua kwa Waisraeli ilikuwa ni ombi la “chagueni … hivi leo mtakayemtumikia.” Tafakari jinsi ushauri huu ungeweza pia kuwabariki watoto unaowafundisha.

Shughuli Yamkini

  • Waalike watoto watengeneze bango wakitumia maneno muhimu na vifungu vya maneno katika Yoshua 24:15. Waache wao washiriki mabango yao na kuelezea kwa nini wao wamechagua maneno hayo. Ni kwa jinsi gani tunaweza kumwonyesha Mungu kwamba tumechagua kumtumikia Yeye?

  • Waalike watoto kupendekeza hali ambazo kwazo wangeweza kuamua kuchagua Mungu juu ya vitu vingine. Waombe wafikirie kile ambacho wangeweza kufanya. Kwa nini ni muhimu “kuchagua … siku hii” badala ya kungojea hali zijitokeze? Tutabarikiwa vipi tunapofanya uamuzi sahihi?

Picha
ikoni ya kujifunza

Himiza Kujifunza Nyumbani

Waalike watoto wachague kitu fulani ulichoongea ambacho wangependa kushiriki pamoja na familia zao. Wahimize wafikirie njia wanayoweza kushiriki wiki hii inayofuata.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Wasaidie watoto kuwa wanafunzi wazuri. Madhumuni yako katika kuwafundisha watoto sio tu kuwapa wao ukweli. Unatakiwa pia kuwasaidia kukua na kuwa watafutaji wa ukweli wa kujitegemea.

Chapisha