Njoo, Unifuate 2024
ApriIi 29–Mei 5: “Badiliko Kuu” Mosia 4–6


“ApriIi 29–Mei 5: ‘Badiliko Kuu.’ Mosia 4–6,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Nyumbani na Kanisani: Kitabu cha Mormoni 2024 (2024)

“Aprili 29–Mei 5. Mosia 4–6,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Nyumbani na Kanisani: 2024 (2024)

Picha
Mfalme Benjamini akiwafundisha watu wake

Katika Kumtumikia Mungu Wenu, na Walter Rane

ApriIi 29–Mei 5: “Badiliko Kuu”

Mosia 4–6

Je, umewahi kumsikiliza mtu akizungumza na ukahisi umeshawishika kubadilisha maisha yako? Pengine uliamua, kwa sababu ya kile ulichokisikia, kuishi tofauti kidogo—au hata tofauti kabisa. Mahubiri ya Mfalme Benjamini yalikuwa aina hiyo ya mahubiri, na kweli alizozifundisha zilikuwa zinawagusa wale watu ambao walizisikiliza. Mfalme Benjamini alishiriki na watu wake kile ambacho malaika alikuwa amemfundisha—kwamba baraka za kupendeza zinapatikana kupitia “damu ya upatanisho wa Kristo” (Mosia 4:2). Kwa sababu ya ujumbe Wake, walibadilisha mtazamo wao juu yao wenyewe (ona Mosia 4:2), Roho alibadilisha tamaa zao (ona Mosia 5:2), na waliagana na Mungu kwamba daima wangetenda mapenzi Yake (ona Mosia 5:5). Hivi ndivyo maneno ya Mfalme Benjamini yalivyoleta matokeo chanya kwa watu wake. Je, ni kwa namna gani yataleta matokeo chanya kwako wewe?

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Nyumbani na Kanisani

Mosia 4

Kupitia Yesu Kristo, ninaweza kupokea na kuhifadhi msamaha wa dhambi zangu.

Nyakati zingine, hata unapohisi kuwa umesamehewa dhambi zako, unaweza kupambana kuhifadhi hisia hiyo na kubaki katika njia ya haki. Mfalme Benjamini aliwafundisha watu wake jinsi ya kupokea na kuhifadhi msamaha wa dhambi. Unapojifunza mlango wa 4 wa Mosia, fikiria kuuliza maswali kama haya:

Mistari 1–8.Je, ni masharti yapi ambayo kupitia hayo Mungu hutoa msamaha wa dhambi zako? Je, unajifunza kipi kuhusu Yeye kwenye mistari hii ambacho kinakupa ushawishi wa kutubu? Unawezaje kujua kwamba umetubu?

Mistari 11–16.Kulingana na mistari hii, nini kinafanyika maishani mwetu kama tutafanya mambo ambayo yameelezwa katika mstari wa 11? Je, ni jinsi gani wewe au mtu unayempenda, mmewahi kupata mabadiliko haya? Linganisha mabadiliko haya na yale yaliyoelezwa katika Mosia 3:19?

Mistari 16–30.Je, ni kwa jinsi gani kushiriki na wengine kile ambacho unacho hukusaidia uhifadhi msamaha wa dhambi zako? Ni kwa jinsi gani unaweza kutumia mstari wa 27 kwenye juhudi zako za kuwa kama Kristo?

Ni katika hali zipi sisi sote ni waombaji? Kulingana na mistari hii, ni jinsi gani tunapaswa kuwatendea watoto wote wa Mungu? (ona Mosia 4:26). Je, ni nani anahitaji msaada wako?

Ona pia Becky Craven, “Hifadhi Badiliko,” Liahona, Nov. 2020, 58–60.

Picha
ikoni ya seminari

Mosia 4:5–10

Ninaamini na kutumaini katika Mungu.

Mwaliko wa Mfalme Benjamini wa kuamini na kumtumainia Mungu ni wa muhimu hivi leo kama ilivyokuwa katika nyakati za kale. Unaposoma Mosia 4:5–10, tafuta kweli kuhusu Mungu ambazo zinakupa sababu ya kumuamini. Zingatia mwaliko ambao Mfalme Benjamini anautoa kwenye mstari wa 10. Kwa nini kumtumainia Mungu hufanya iwe rahisi kufanya kile ambacho Mfalme Benjamini anaalika?

Fikiria kutumia baadhi ya maandiko haya ya ziada ili kutengeneza orodha ya sifa za Mungu: Yeremia 32:17; 1 Yohana 4:8; 2 Nefi 9:17; Alma 32:22; Mormoni 9:9; Etheri 3:12; Mafundisho na Maagano 19:1–3; 88:41 (ona pia video ya “Christlike Attributes,” Gospel Library). Ungeweza kutumia orodha yako ili upate njia tofauti tofauti za kukamilisha sentensi kama hii: “Kwa sababu ninamjua Mungu ni , ninaweza kumwamini ku .”

Tumaini letu kwa Mungu huongezeka wakati tunapopata uzoefu wa kuwa Naye. Katika Mosia 4:1–3, ni kitu gani kiliwasaidia watu wa Mfalme Benjamini “kuja kwenye ufahamu wa wema wa Mungu”?(mstari wa 6). Fikiria kuhusu uzoefu uliowahi kuwa nao na Mungu. Je, uzoefu huu umekufundisha nini kumhusu Yeye? Je ni hatua zipi unazichukua (au ambazo ungeweza kuchukua) kuimarisha imani yako na tumaini lako kwa Mungu?

Ona pia Jeffrey R. Holland, “The Grandeur of God,” Liahona, Nov. 2003, 70–73; Mada za Injili “Mungu Baba,” Gospel Library; “Baba Anaishi,” Nyimbo za Dini, na. 182.

Kushiriki uzoefu mtakatifu. Baadhi ya uzoefu ni mtakatifu sana au binafsi zaidi kusimuliwa. Wakati unawaalika wengine washiriki uzoefu, usiwalazimishe kama hawataki kufanya hivyo.

Mosia 4:29–30

Lazima nichunge mawazo, maneno na matendo yangu.

Mungu hatupatii orodha ya kila kinachoweza kuwa dhambi. Kulingana na Mosia 4:29–30, Yeye anafanya nini badala yake? Fikiria jinsi gani mawazo, maneno na matendo yako vinakuathiri wewe na wengine. Je vinaathiri vipi uhusiano wako na Mungu? Je, “[unajichungaje]”?

Mosia 5:1–5

Roho wa Bwana anaweza kusababisha badiliko kuu moyoni mwangu.

Ni kawaida kwa watu kusema ya kwamba, “Siwezi kubadilika. Hivyo ndivyo nilivyo.” Kinyume na hayo, uzoefu wa watu wa Mfalme Benjamini unatuonesha sisi jinsi gani Roho wa Bwana anavyoweza kwa hakika kuibadilisha mioyo yetu. Unaposoma katika Mosia 5:1–5, fikiria kuhusu jinsi gani “badiliko kuu” linaloongoza kwenye uongofu wa kweli lilivyotokea—au linavyoweza kutokea—katika maisha yako. Fikiria kuhusu badiliko la taratibu, na la kidogo kidogo na pia badiliko “kuu.” Je uzoefu huu unakusaidiaje wakati unapokumbana na majaribu?

Ona pia Ezekieli 36:26–27; Alma 5:14; “A Change of Heart,” “The People of King Benjamin Make a Covenant” (video), Gospel Library.

Picha
Kristo akimponya mwanamke mgonjwa

Mikono ya Uponyaji, na Adam Abram

Mosia 5:5–15

Ninajichukulia juu yangu jina la Kristo wakati ninapofanya Naye maagano.

Unajifunza kipi kutoka Mosia 5:7–9 kuhusu kile inachomaanisha kuhusu kujichukulia juu yako jina la Kristo? Je, sala za sakramenti (ona Moroni 4–5) zinafundisha nini kuhusu hili? Je, unawezaje kuonesha kwamba “wewe u wa” Mwokozi?

Ona pia D. Todd Christofferson, “Kwa Nini Njia ya Agano,” Liahona, Mei 2021, 116–19.

Mawazo kwa ajili ya Kuwafundisha Watoto

Mosia 4:1–3, 10

Toba huleta shangwe.

  • Kuwafundisha watoto wako kuhusu shangwe iletwayo na toba, pengine ungeweza kuwaacha watoto wako wachafue mikono yao na kuona jinsi gani wanavyohisi baada ya kuiosha. Kisha ungeweza kulinganisha hilo na jinsi watu katika Mosia 4:1–3 walivyohisi kabla na baada ya dhambi zao kuwa zimesamehewa. Shiriki ushuhuda wako juu ya nguvu ya Mwokozi ya kutusafisha kiroho.

  • Je, watoto wako wanajua jinsi ya kutubu kikamilifu na kwa dhati? Wasaidie wapate kile ambacho watu wa Mfalme Benjamini walikipata katika Mosia 4:1–3, 10. Wangeweza pia kurejelea “Tubu, Toba” katika Mwongozo wa Maandiko. Je, ni kwa jinsi gani Yesu Kristo anafanya toba iwezekane?

Mosia 4:12–26

Injili ya Yesu Kristo inanishawishi niwatendee wengine kwa upendo na ukarimu.

  • Kuwahudumia wengine hutufanya tuhisi vizuri. Pengine watoto wako wangeweza kuzungumza kuhusu nyakati ambapo walimpenda au kumhudumia mtu fulani na jinsi uzoefu huo ulivyowafanya wahisi. Je, ni zipi baadhi ya sababu ambazo watu wanaweza kutotaka kuwatumikia wengine? Je, tungeweza kusema nini kwa mtu fulani ili kuwaalika wawasaidie wenye shida? Tazama mawazo katika Mosia 4:16–26.

  • Mfalme Benjamini alifundisha kwamba tunapokuja kwa Kristo na kupokea ondoleo la dhambi zetu, “tunajazwa na upendo wa Mungu” (Mosia 4:12). Hii hutufanya sisi tupende na tuwe wakarimu kwa wengine. Wewe na watoto wako mngeweza kuchunguza katika Mosia 4:13–16, 26 (au wimbo kama “I’ll Walk with You,” Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 140–41) na kutafuta vifungu vya maneno ambavyo vinaeleza jinsi tuavyoweza kuwatumikia wengine. Wangeweza kuigiza mambo haya au kuchora picha zao wenyewe na kukisia vifungu vya maneno vya kila mmoja. Ni kwa jinsi gani tunaweza kuonesha upendo na ukarimu nyumbani, shuleni au kanisani?

Picha
msichana akicheza na mtoto

Yesu Kristo alitufundisha tuwe wakarimu kwa wengine.

Mosia 5:5–15

Ninapofanya maagano na Mungu, ninajichukulia juu yangu jina la Kristo.

  • Watoto wako wangeweza kufurahia kutengeneza beji zikionesha jina “Yesu Kristo” na kuzivaa kwenye vifua vyao (ona ukurasa wa shughuli ya wiki hii). Wakati wakifanya hivyo, ungeweza kuwasomea Mosia 5:12 na kuzungumza kuhusu jinsi gani kufanya maagano, au ahadi na Mungu ni kama kuwa na jina la Kristo “mara zote likiwa limeandikwa katika mioyo [yetu].”

Kwa ajili ya mawazo zaidi, ona toleo la mwezi huu la gazeti la Rafiki.

Picha
Kristo akiwalisha ndege

Daima Katika Utunzaji Wake, na Greg K. Olsen

Chapisha