Njoo, Unifuate 2024
Novemba 11–17: “Pasua Hilo Pazia la Kutoamini.” Etheri 1–5


Novemba 11–17: “Pasua Hilo Pazia la Kutoamini” Etheri 1–5,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Nyumbani na Kanisani: Kitabu cha Mormoni 2024 (2023)

“Novemba 11–17. Etheri 1–5,” Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Nyumbani na Kanisani: 2024 (2023)

Picha
Wayaredi wakisafiri kupitia nyikani

Wayaredi Wakiondoka Babeli, na Albin Veselka

Novemba 11–17: “Pasua Hilo Pazia la Kutoamini”

Etheri 1–5

Wakati ni kweli kwamba njia za Mungu ni za juu kuliko zetu na daima tunapaswa tukubali mapenzi Yake, Yeye pia anatutia moyo tuweze kufikiri na kutenda kwa ajili yetu wenyewe. Hilo ni somo moja ambalo Yaredi na kaka yake walijifunza. Kwa mfano, wazo la kusafiri kwenda katika nchi mpya iliyokuwa “chaguo juu ya zote duniani ” lilionekana kuanzia kwa Yaredi, na Bwana akakubali ombi lile akisema kwa kaka wa Yaredi, “Na hii nitakufanyia kwa sababu ya muda huu mrefu ambao umeomba kwangu” (ona Etheri 1:38–43). Na wakati kaka wa Yaredi alipohitaji mwanga ndani ya mashua ambazo zingewabeba hadi nchi yao ya ahadi, Bwana alimuuliza swali ambalo sisi kwa kawaida humuuliza Yeye: “Ungetaka nifanye nini?” (Etheri 2:23). Yeye anataka kusikia mawazo yetu na nia zetu, na Yeye atasikiliza na kutupatia uthibitisho au kutushauri vinginevyo. Wakati mwingine kitu ambacho kinatutenganisha sisi na baraka tunazotafuta ni “pazia letu la kutoamini,” na kama tunaweza “kupasua pazia hilo” (Etheri 4:15), tunaweza kushangazwa na kile ambacho Bwana yuko tayari kutufanyia.

Ona pia “The Lord Appears to the Brother of Jared” (video), Maktaba ya Injili.

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Nyumbani na Kanisani

Etheri 1:33–43

Ninapomlilia Bwana, Yeye atakuwa na huruma kwangu.

Etheri 1:33–43 inasimulia maombi matatu ya kaka wa Yaredi. Je, unajifunza nini kutokana na majibu ya Bwana kwa kila sala? Fikiria wakati ambapo ulihisi huruma ya Bwana wakati ulipomlilia Yeye katika sala. Unaweza kutaka kuandika uzoefu huu na kuushiriki na mtu ambaye anaweza kuhitaji kusikia ushuhuda wako.

Ona pia “Sala ya Faragha,” Nyimbo za Dini, na. 76.

Etheri 2; 3:1–6; 4:7–15

Picha
ikoni ya seminari
Ninaweza kupokea ufunuo kwa ajili ya maisha yangu.

Rais Russell M. Nelson alisema: “Ninawasihi muongeze uwezo wenu wa kiroho wa kupokea ufunuo. … Chagua kufanya kazi ya kiroho inayotakiwa ili kufurahia karama ya Roho Mtakatifu na kuisikia sauti ya Roho mara nyingi zaidi na kwa uwazi zaidi” (“Ufunuo kwa Ajili ya Kanisa, Ufunuo kwa Ajili ya Maisha Yetu,” Liahona, Mei 2018, 96).

Unaposoma Etheri 2; 3:1–6; 4:7–15, unajifunza nini kuhusu “kazi ya kiroho” Rais Nelson aliyoizungumzia? Unaweza kuwekea alama kwa rangi moja maswali au wasiwasi kaka ya Yaredi aliokuwa nao na kile alichofanya kuhusu maswali na wasiwasi huo, na ukitumia rangi nyingine unaweza kuwekea alama jinsi Bwana alivyomsaidia na kufanya mapenzi Yake yajulikane.

Hapa kuna baadhi ya maswali ya kutafakari wakati unaposoma:

  • Ni kipi kinachokuvutia sana kuhusu namna ambavyo Mwokozi alimjibu kaka wa Yaredi katika Etheri 2:18–25?

  • Ni kwa jinsi gani ungeweza kutumia Etheri 3:1–5 kumsaidia mtu ambaye anajifunza jinsi ya kusali?

  • Je, ni kipi kingeweza kukuzuia kupokea ufunuo kutoka kwa Bwana? (ona Etheri 4:8–10). Ni kwa jinsi gani unaweza kupokea ufunuo zaidi kutoka Kwake kila mara? (ona Etheri 4: 7, 11–15).

  • Unadhani inamaanisha nini “kupasua pazia la kutoamini” katika maisha yako” (Etheri 4:15).

Ni kipi kingine unajifunza kutoka kwa kaka wa Yaredi kuhusu ufunuo binafsi?

Mzee Dale G. Renlund alifundisha kuhusu “Mfumo kwa ajili ya Ufunuo Binafsi” (Liahona, Nov. 2022, 16–19). Fikiria kuchora fremu ya picha na kuandika vipengele vinne vya mfumo kila upande. Ni kwa jinsi gani mfumo huu unaweza kukusaidia “uongeze uwezo wako wa kupokea ufunuo binafsi?

Ona pia Mada za Injili, “Ufunuo Binafsi,” Maktaba ya Injili.

Etheri 2:14–15; 3:1–20

Kupitia kunirudi Kwake, Bwana ananialika nitubu na nije Kwake.

Hata nabii mkuu kama kaka wa Yaredi alihitaji kurudiwa na Bwana. Unajifunza nini kutoka Etheri 2:14–15 kuhusu kurudiwa na Bwana? Fikiria kuhusu jinsi kurudiwa na Bwana na mwitikio wa kaka wa Yaredi vilivyoweza kusaidia kumwandaa kwa uzoefu alioupata katika Etheri 3:1–20.

Etheri 2:16–25

Bwana ataniandaa niweze kuvuka “bahari yangu kuu.”

Nyakati zingine, kuvuka “bahari kuu” ndiyo njia pekee ya kutimiza mapenzi ya Mungu kwetu. Je, unaona mifanano kwenye maisha yako katika Etheri 2:16–25? Je, ni kwa jinsi gani Bwana amekuandaa kwa ajili ya changamoto zako? Yeye anakuomba ufanye nini hivi sasa ili ujiandae kwa kile Yeye anachokuhitaji ufanye katika siku za usoni?

Ona pia L. Todd Budge, “Uaminifu Endelevu na Thabiti,” Liahona,, Nov. 2019, 47–49.

Tumia kile ulichojifunza. Kujifunza injili kunapaswa kutuongoza kwenye kubadili maisha yetu. Baada ya kusoma Etheri 4:11–12, ungeweza kuorodhesha baadhi ya ushawishi katika maisha yako na kuzingatia ikiwa umekusukuma kufanya mema. Ni mabadiliko yapi unahisi kuongozwa kuyafanya?

Etheri 5

Mashahidi hushuhudia juu ya ukweli wa Kitabu cha Mormoni.

Unaposoma unabii wa Moroni katika Etheri 5, tafakari kusudi la Bwana katika kuwaandaa mashahidi wengi wa Kitabu cha Mormoni. Je, mashahidi gani wamekuongoza kuamini kwamba Kitabu cha Mormoni ni neno la Mungu? Je, ni kwa jinsi gani Kitabu cha Mormoni kimekuonesha “nguvu za Mungu na pia neno Lake? (Etheri 5:4).

Mawazo kwa ajili ya Kuwafundisha Watoto

Etheri 1:33–37; 2:16–25; 3:1–6

Baba wa Mbinguni husikia na kujibu sala zangu.

  • Ikiwa unajua lugha ambayo watoto wako hawaifahamu, wape maelekezo kadhaa katika lugha hiyo (au wasikilizishe sauti iliyorekodiwa kwa lugha nyingine). Unaweza kutumia hii kueleza kwa nini kaka wa Yaredi alisali kwa ajili ya msaada katika Etheri 1:33–37. Sisitiza jinsi Bwana alivyohisi kuhusu sala hii na jinsi Yeye alivyojibu (ona pia “Mlango wa 50: Wayaredi Wakiondoka BabeliHadithi za Kitabu cha Mormoni, 143–44).

  • Watoto wako wangeweza kujifanya wanajenga mashua wakati unaposoma Etheri 2:16–17. Kisha wewe na watoto wako mngeweza kusoma kuhusu shida ambazo Wayaredi walikuwa nazo katika mashua zao (ona Etheri 2:19) na njia tofauti ambazo Bwana alijibu sala za kaka wa Yaredi (ona 3 2:19–25; 3:1–6). Picha na ukurasa wa shughuli mwishoni mwa muhtasari huu vingeweza kukusaidia wewe na watoto wako msimulie hadithi hii. Je, tunajifunza nini kutoka katika sala ya kaka wa Yaredi? Fikiria kushiriki uzoefu ambapo wewe ulisali kuomba msaada na Baba wa Mbinguni akakusaidia.

Etheri 3:6–16

Niliumbwa kwa mfano wa Mungu.

  • Kadiri wanavyokua, watoto wako watakumbana na jumbe nyingi za uongo kuhusu Mungu, wao wenyewe, na miili yao. Ungeweza kuwaomba wakusaidie kutafuta kweli kuhusu mada hizi katika Etheri 3:6–16. Ili kusisitiza ukweli uliofundishwa katika Etheri 3:13, 15, mngeweza kutazama picha ya Mwokozi pamoja na uwaalike watoto wako waoneshe sehemu mbalimbali za mwili Wake. Wangeweza kisha kuonesha kwa kidole sehemu za miili yao wenyewe. Mngeweza pia kuimba pamoja wimbo kuhusu miili yetu, kama vile “The Lord Gave Me a Temple” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 153). Wewe na watoto wako mngeweza kuzungumza kuhusu kwa nini mnashukuru kwa ajili ya miili yenu.

Picha
mtoto akikimbia uwanjani

Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu

Etheri 5

Mashahidi watatu walishuhudia juu ya Kitabu cha Mormoni.

  • Moroni alitoa unabii kwamba Mashahidi Watatu wangesaidia kudhihirisha ukweli juu ya Kitabu cha Mormoni. Ili kufundisha shahidi ni nani,ungeweza kuwaomba watoto wako waelezee kitu fulani walichokiona au kupitia ambacho wengine hawakukipitia. Kisha mnaposoma Etheri 5 pamoja, mngeweza kuzungumza kuhusu kwa nini Mungu huwatumia mashahidi katika kazi Yake. Mngeweza pia kuelezana ninyi kwa ninyi jinsi mnavyoweza kujua kuwa Kitabu cha Mormoni ni cha kweli na jinsi mnavyoweza kutoa ushahidi wenu kwa wengine.

Kwa ajili ya mawazo zaidi, ona toleo la mwezi huu la gazeti la Rafiki.

Picha
Yesu akigusa mawe 16 katika uwepo wa kaka wa Yaredi.

Je, Uliona Zaidi ya Hili?, na Marcus Alan Vincent

Chapisha