Njoo, Unifuate
Machi 2–8. 2 Nefi 31–33: “Hii Ndiyo Njia”


“Machi 2–8. 2 Nefi 31–33: ‘Hii Ndiyo Njia,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Kitabu cha Mormoni (2020)

“Machi 2–8. 2 Nefi 31–33,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2020

Picha
Yesu akiwafundisha wanafunzi wake

Kristo Akiwafundisha Wanafunzi Wake, na Justin Kunz

Machi 2–8

2 Nefi 31–33

“Hii Ndiyo Njia.

Muhtasari huu unapendekeza kanuni unazoweza kuona ni muhimu katika 2 Nefi 31–33. Lakini vitu muhimu zaidi utakavyojifunza katika kujifunza kwako vitatokana na minong’ono ya Roho. Tafuta mwongozo huu, na uandike misukumo ambayo inakuja.

Andika Misukumo Yako

Miongoni mwa maneno ya mwisho ya Nefi ambayo yaliandikwa, tunapata tangazo hili: “Bwana ameniamuru hivi, na ni lazima nitii” (2 Nefi 33:15). Huu unaonekana kama ufupisho unaofaa wa Maisha ya Nefi. Alitafuta nia ya Bwana na kwa ujasiri akajitahidi kuitii—hata kama ilimaanisha kuhatarisha maisha yake ili apate bamba za shaba kutoka kwa Labani, kujenga merikebu na kusafirini baharini, au kufundisha kwa uaminifu mafundisho ya Kristo kwa uwazi na nguvu. Nefi aliweza kuzungumza kwa ushawishi mkubwa kuhusu umuhimu wa “kusonga mbele mkiwa na imani katika Kristo,” wa kufuata “njia hii nyembamba iliyosonga ambayo inaelekea uzima wa milele” (2 Nefi 31:20, 18), kwa sababu hiyo ndiyo njia aliyofuata. Alijua kupitia uzoefu kwamba njia hii, ingawaje ni ngumu wakati mwingine, pia ina shangwe, na kwamba, “hakuna njia nyingine wala jina lililotolewa chini ya Mbingu ambalo mwanadamu anaweza kuokolewa katika ufalme wa Mungu” (2 Nefi 31:21).

Picha
ikoni ya kujifunza kibinafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kibinafsi

2 Nefi 31–32

Yesu Kristo na mafundisho Yake ndio njia pekee kwenye uzima wa milele.

Kama ungehitajika kufanya muhtasari wa njia ya uzima wa milele kwa maneno machache tu, ungesema nini? Nefi, katika uwazi na urahisi wake wa kawaida, alisema hivi: imani katika Kristo, toba, ubatizo, kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu, na kuvumilia hadi mwisho. Baada ya kujifunza mafundisho ya Nefi katika 2 Nefi 31–32, zingatia jinsi ambavyo unaweza kumuelezea mtu kwa maneno yako mwenyewe. Fikiria kuhusu jinsi kuishi mafundisho haya kulivyokubariki. Unaweza kuzingatia mafunzo ya Nefi katika 2 Nefi 31:18–20 na kutathmini juhudi zako mwenyewe za “kusonga mbele” katika njia ya injili.

Ona pia 3 Nefi 11:32–39; 27:13–22; D. Todd Christofferson, “Mafundisho ya Kristo,” Ensign au Liahona, Mei 2012, 86–90; Brian K. Ashton, “Mafundisho ya Kristo,” Ensign au Liahona, Nov. 2016, 106–9.

Picha
familia ikisali kwa pamoja

Kufuata mafundisho ya Yesu Kristo kunatuongoza hadi kwenye uzima wa milele.

2 Nefi 31:4–13

Yesu Kristo aliweka mfano kamili wa utiifu wakati alipobatizwa.

Hata kama ubatizo wako ulifanyika jana au miaka 80 iliyopita, lilikuwa tukio la maana sana—ulifanya agano la maisha yote la kumfuta Yesu Kristo. Fikiria kuhusu ubatizo wako unaposoma kuhusu ubatizo wa Mwokozi katika 2 Nefi 31:4–13. Kwa nini Mwokozi alibatizwa? Ni jinsi gani sababu zilizompelekea kubatizwa zinafanana na sababu zako za kubatizwa? Unafanya nini leo ili kuendelea kuiga mfano wa Mwokozi wa utiifu?

Ibada ya sakramenti ni nafasi kila wiki ya kujitolea tena kumfuata Yesu Kristo. Wakati mwingine utakaposhiriki sakramenti, zingatia kusoma 2 Nefi 31:13 na kutafakari uamuzi wako wa “kumtii Mwana, kwa moyo wa lengo moja” na utayari wako wa “kujivika juu yako jina la Kristo.”

2 Nefi 31:17–2032

Roho Mtakatifu atanionyesha kile ninachopaswa kufanya.

Kama ubatizo na kuthibitishwa ni “lango ambalo [sisi] tutaingilia” njia nyembamba na iliyosonga (2 Nephi 31:17), tunapaswa kufanya nini wakati sasa tupo kwenye njia? Hivyo ndivyo watu wa Nefi walivyojiuliza (ona 2 Nefi 32:1). Ni majibu gani Nefi alitoa katika 2 Nefi 31:19–20 na sura ya 32? Unapata majibu gani kwa ajili yako?

Ona pia David A. Bednar, “Pokea Roho Mtakatifu,” Ensign au Liahona, Nov. 2010, 94–97; “Roho Mtakatifu,” Mada za Injili, topics.ChurchofJesusChrist.org.

2 Nefi 33

Kitabu cha Mormoni kinawashawishi watu wote wamwamini Kristo.

Katika 2 Nefi 33, wakati Nefi akihitimisha maandishi yake, alitoa sababu za yeye kuandika. Ni sababu zipi unapata katika sura hii? Tafakari juu ya yale ambayo umesoma kufikia hapa katika 1 Nefi na 2 Nefi na maelezo ambayo unaweza kuwa umeandika. Ni jinsi gani hadithi na mafundisho vimetimiza lengo la Nefi kwako wewe? Kwa mfano, ni jinsi gani vimekushawishi wewe “kumwamini [Kristo], na kuvumilia hadi mwisho”? (mstari wa 4). Zingatia kuandika uzoefu huu au kuushiriki pamoja na mwanafamilia au rafiki.

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia.

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani

Unaposoma maandiko na familia yako, Roho anaweza kukusaidia kujua kanuni zipi zisisitizwe na kujadiliwa ili kukidhi mahitaji ya familia yako. Haya ni baadhi ya mawazo.

2 Nefi 31:5–13

Kuna mwanafamilia yeyote ambaye anajitayarisha kwa ajili ya ubatizo, au ambaye amebatizwa hivi karibuni? Pengine wanaweza kushiriki ni kwa nini waliamua kubatizwa. Kulingana na mafundisho ya Nefi, ni nini baadhi ya sababu za kubatizwa kwetu? Ni zipi baadhi ya baraka tunazopokea wakati tunapobatizwa?

2 Nefi 31:17–21

Ni jinsi gani unaweza kuisaidia familia yako kuelewa analojia ya Nefi kuhusu “njia nyembamba na iliyosonga”? (2 Nefi 31:18). Kwa mfano, mnaweza kushirikiana kuchora picha ya njia ambayo Nefi alielezea katika 2 Nefi 31:17–21, mkiitambulisha kwa vitu ambavyo hatuna budi kufanya ili kuingia kwenye njia na kusonga mbele. Ni jinsi gani Mwokozi anatusaidia kuendelea katika njia hiyo?

2 Nefi 31:20

Kama unataka kuisaidia familia yako kuelewa vizuri zaidi jinsi ya kuvumilia hadi mwisho, ukurasa wa 6 wa Hubiri Injili Yangu una ufafanuzi unaoweza kukusaidia; na pia ujumbe wa Mzee Dale G. Renlund “Watakatifu wa Siku za Mwisho Huendelea Kujaribu” (Ensign au Liahona, Mei 2015, 56–58).

2 Nefi 32:8–9

Ili kuwasaidia wanafamilia kuelewa kwamba tunaweza “kusali kila wakati,” unaweza kutengeneza orodha ya hali ambapo tunaweza tukasali (au kuchora picha kuziwakilisha). Kisha familia yako yaweza kuimba wimbo ambao unafundisha kuhusu sala, kama vile “Je, Uliomba?” (Nyimbo za Dini, na. 140), wakibadili baadhi ya maneno katika wimbo kwa maneno kutoka kwenye orodha zao. Ni namna gani Bwana anatubariki wakati tunaposali kila wakati?

2 Nefi 33:1–2

Nini kinaweza kusababisha watu “kushupaza mioyo yao dhidi ya Roho Mtakatifu”? Ni jinsi gani tunaweza kuhakikisha kuwa Roho Mtakatifu ana “nafasi ndani [yetu]”?

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kufundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika katika Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Kumuiga Mwokozi. Inasaidia kujifunza njia ambazo Mwokozi alifundisha—mbinu alizotumia na mambo aliyosema. Lakini nguvu za Yesu za kufundisha na kuwainua wengine kimsingi zilikuja kutokana na aina ya mtu Aliyekuwa na jinsi Alivyoishi. Kadiri unavyojitahidi kwa bidii kuishi kama Yesu Kristo na kutegemea nguvu Zake za Upatanisho, ndivyo utakavyoweza zaidi kwa kawaida kufundisha katika njia Yake.

Picha
Yohana Mbatizaji Anambatiza Yesu

Ili Kutimiza Haki Yote, na Liz Lemon Swindle

Chapisha