Agano la Kale 2022
Novemba 21–27. Yona; Mika: “Yeye Hufurahia Rehema”


“Novemba 21–27. Yona; Mika: ‘Yeye Hufurahia Rehema’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: Agano la Kale 2022 (2021)

“Novemba 21–27. Yona; Mika,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Msingi: 2022

Picha
mtu akitambaa ufukoni na nyangumi baharini akiwa nyuma yake

Yona ufukoni huko Ninawi, na DanielA. Lewis

Novemba 21–27

Yona; Mika

“Yeye Hufurahia Rehema”

Chunguza kanuni muhimu katika Yona na Mika ambazo zitawabariki watoto unaowafundisha. Tafakari jinsi utakavyowasaidia watoto wajifunze kanuni hizi. Mawazo yaliyoko katika muhtasari huu yanaweza kusaidia.

Andika Misukumo Yako

Picha
ikoni ya kushiriki

Alika Kushiriki

Ili kuwasaidia watoto wakumbuke hadithi ya Yona au ukweli mwingine ambao yawezakuwa wamejifunza nyumbani, imbeni wimbo pamoja, kama vile mstari wa 7 wa “Follow the Prophet” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 110–11).

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wadogo

Yona 1:4–17; 3:3–5

Bwana hunibariki ninapomtii Yeye.

Wakati Bwana alipomtaka Yona kuhubiri kwa watu wa Ninawi, Yona hakutii. Wasaidie watoto waelewe kwamba tunabarikiwa tunapomtii Bwana.

Shughuli Yamkini

  • Onesha picha za hadithi ya Yona na waalike watoto wasimulie kile wanachofahamu kuhusu hadithi hii (ona “Yona Nabii” katika Hadithi za Agano la Kale; ukurasa wa shughuli ya wiki hii; au muhtasari wa wiki hii katika Njoo Unifuate—Kwa ajili ya Watu Binafsi na Familia). Uliza maswali kama haya: Nini kilitokea wakati ambapo Yona hakumtii Bwana? (ona Yona 1:4–17). Nini kilitokea wakati alipotii? (ona Yona 3:3–5). Shiriki ushuhuda wako kwamba Bwana atatubariki tunapomtii Yeye.

  • Imbeni pamoja wimbo kuhusu kumtii Bwana, kama vile “Quickly I’ll Obey” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto,197). Zungumza kuhusu vile ambavyo ingekuwa vyema kwa Yona kutii mara ya kwanza. Wasaidie watoto wafikirie mambo ambayo Mungu anawataka wafanye na kisha waigize jinsi wanavyoweza kutii kwa haraka.

Picha
wamisionari wakimfundisha mwanamume

Baba wa Mbinguni anataka kila mtu aisikie injili.

Yona3

Injili ni kwa ajili ya kila mtu.

Watu wa Ninawi walitubu wakati Yona aliposhiriki nao ujumbe wa Bwana. Ni fursa zipi watoto wanazo za kushiriki injili?

Shughuli Yamkini

  • Igiza sehemu za Yona 3:3–8 pamoja na watoto, kama vile kwenda mji wa Ninawi, kushiriki ujumbe wa Bwana na kuandika amri kutoka kwa mfalme kwenda kwa watu wake. Onesha picha ya wamisionari (ona Kitabu cha Sanaa ya Injili, na. 109, 110). Wamisionari wanafanya kazi gani? Ni kwa jinsi gani Yona alikuwa mmisionari? Wasaidie watoto wafikirie njia wanazoweza kushiriki injili na wengine, kama vile kushiriki makala ya imani au kutoa shuhuda zao juu ya Yesu Kristo.

  • Simulia uzoefu wakati uliposhiriki injili ya Yesu Kristo. Au, Siku chache kabla ya darasa, mwalike mtu kuzuru darasa lako na awasimulie watoto kuhusu wakati ambapo alishiriki injili au wakati mtu alipomfundisha yeye injili. Muhimize mtu huyo kuonesha picha, kama inawezekana. Wasaidie watoto wafikirie njia wanazoweza kuwa wamisionari sasa.

Mika 5:2

Yesu Kristo alizaliwa Bethlehemu.

Mika alitoa unabii kwamba “mtawala katika Israeli” wa siku zijazo angezaliwa Bethlehemu. Unaweza kuwasaidia watoto wafahamu kwamba kuzaliwa kwa Yesu Kristo kulitimiza unabii huu.

Shughuli Yamkini

  • Onesha picha za matukio yaliyozunguka kuzaliwa kwa Yesu Kristo (ona Kitabu cha Sanaa ya Injili, na. 28, 29, 30, 31). Waombe watoto wazungumzie nini kinatendeka katika kila picha. Soma Mika 5:2, na waalike watoto wasimame pale wanaposikia neno “Bethlehemu.” Shuhudia kwamba kuzaliwa kwa Yesu kulikuwa muhimu kiasi kwamba manabii walifahamu hilo kabla Yeye hajazaliwa.

  • Waalike watoto wachore picha ya kuzaliwa kwa Yesu. Wanapoonesha picha zao, waombe kushiriki kwa nini wao wana shukrani kwa ajili ya Yesu Kristo.

Picha
ikoni ya kufundisha

Fundisha Mafundisho: Watoto Wakubwa

Yona 1:10–12; 2:1–4,9; 3:1–5

Toba hujumuisha kutambua dhambi zangu na kuomba msamaha.

Mfano wa Yona unaweza kuwashawishi watoto wamgeukie Bwana wakati wanapokuwa wametenda dhambi.

Shughuli Yamkini

  • Wasaidie watoto kutengeneza orodha ubaoni ya baadhi ya vipengele muhimu vya toba (ona Mwongozo wa Maandiko, “Repent, Repentance,” scriptures.ChurchofJesusChrist.org). Rejeleeni kwa pamoja hadithi ya Yona na waalike watoto wabainishe ushahidi kwamba Yona alikuwa akitubu (ona, kwa mfano, Yona 1:10–12; 2:1–4,9; 3:1–5). Ni jinsi gani tunaweza kumwonesha Bwana kwamba toba yetu ni ya dhati?

  • Imbeni wimbo kuhusu toba, kama vile “Repentance” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto,98). Waulize watoto ni maneno gani au vifungu vya maneno kutoka kwenye wimbo ambavyo wangeweza kushiriki na Yona ili kumsaidia atubu.

Yona 2:7–10; 3:10; 4:2; Mika 7:18–19

Bwana ni mwenye rehema kwa wale wote wanaomgeukia Yeye.

Watoto wanapoelewa kwamba Bwana ni mwenye rehema na ukarimu, watamgeukia Yeye wakati wanapohitaji neema.

Shughuli Yamkini

  • Waalike watoto kutafuta maana ya neno rehema katika kamusi au katika Mwongozo wa Maandiko (scriptures.ChurchofJesusChrist.org). Kwa nini Yona alihitaji rehema? Kwa nini watu wa Ninawi walihitaji rehema? (ona Yona 1:1–3). Waombe watoto wavute taswira kwamba wanamfanyia Yona mahojiano. Ni ushahidi gani Yona angeweza kutoa ili kuonesha kwamba Bwana ni mwenye rehema? (Ona, kwa mfano, Yona 2:7–10; 3:10; 4:2). Ni jinsi gani Bwana ametuonesha sisi rehema?

  • Waombe watoto watengeneze orodha ubaoni ya mambo ambayo wanaweza “kuyafurahia”, kama vile mambo ya kufanya katika muda wa ziada, baraka kutoka kwa Bwana na kadhalika. Waalike wasome Mika 7:18–19 ili kugundua jambo moja Bwana analolifurahia. Ni ukweli gani katika mistari hii ungemsaidia mtu anayeogopa kutubu?

  • Wasaidie watoto wafikirie mifano wakati Mwokozi alipoonesha rehema kwa wengine, kama vile Marko 2:3–12; Luka 23:33–34; na Yohana 8:1–11. Onesha picha za matukio haya, kama inawezekana. Wasaidie watoto wafikirie fursa walizonazo za kuwa wenye rehema na wakarimu kwa wengine.

Mika 6:8

Bwana ananitaka mimi kutenda kwa haki, kupenda rehema na kutembea na Yeye kwa unyenyekevu.

Mika 6:8 inatoa mpangilio wa kuishi kwa haki. Ni jinsi gani unaweza kuwasaidia watoto wagundue na kuishi mafundisho katika mstari huu?

Shughuli Yamkini

  • Someni kwa pamoja Mika 6:8, na wasaidie watoto waelewe vifungu hivi vya maneno vinamaanisha nini: “tenda kwa haki,” “penda rehema,” na “kutembea kwa unyenyekevu na Mungu wako.” Waalike watoto wachore picha zao wenyewe wakifanya jambo linalohusiana na moja ya vifungu hivi.

  • Andika ubaoni “Bwana anahitaji nini kwako?” Waalike watafute majibu katika Mika 6:8. Ni jinsi gani kutii amri za Bwana hutusaidia kutimiza kile Bwana anachohitaji kutoka kwetu katika mstari huu?

Picha
ikoni ya kujifunza

Himiza Kujifunza Nyumbani

Andika kwenye kipande cha karatasi kwa ajili ya kila mtoto kifungu muhimu kutoka kwenye moja ya maandiko mliyojadili kama darasa. Waalike watoto wajaribu kukariri kifungu hicho na wamuombe mwanafamilia kutoa mawazo yake kuhusu kifungu hicho.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Kuwa na usikivu kwa watoto. Ni jinsi gani watoto katika darasa lako wanaitikia shughuli za kujifunza? Kama hawaoneshi kushiriki, inaweza kuwa wakati muafaka wa kujaribu shughuli nyingine. Kwa upande mwingine, kama unagundua kwamba watoto wanashiriki katika shughuli, usijisikie kushinikizwa kuendelea mbele kwa sababu hujamaliza nyenzo zote za somo.

Chapisha