Miito ya Misheni
Sura ya 2: Pekua Maandiko na Vaa Silaha za Mungu


“Sura ya 2: Pekua Maandiko na Vaa Silaha za Mungu,” Hubiri Injili Yangu: Mwongozo wa Kushiriki Injili ya Yesu Kristo (2023)

“Pekua Maandiko na Vaa Silaha za Mungu,” Hubiri Injili Yangu

Picha
Joseph Smith Anatafuta Hekima katika Bibilia, na Dale Kilbourn

Sura ya 2

Pekua Maandiko na Vaa Silaha za Mungu

Zingatia Hili

  • Kwa nini ni muhimu kujifunza neno la Mungu katika maandiko kwa uendelevu?

  • Ni kwa jinsi gani ninaweza kufanya kujifunza kwangu maandiko kuwe na tija zaidi?

  • Ni kwa jinsi gani ninaweza kutumia teknolojia kwa uadilifu ili inisaidie nitimize dhumuni langu?

  • Je, inamaanisha nini kuvaa silaha za Mungu?

Pekua Maandiko

Yesu Kristo “ndiye uzima na nuru ya ulimwengu. Tazama, yeye ni neno la ukweli na haki” (Alma 38:9); ona pia Yohana 1. Kujifunza neno la Mungu katika maandiko matakatifu kutaleta neema katika maisha yako (ona Yohana 10:10). Maneno Yake yatakujaza wewe—pamoja na wale unaowafundisha—kwa nuru na ukweli. Yatakusaidia wewe—pamoja na wale unaowafundisha—kuishi kwa haki na kupokea ulinzi na nguvu za kiungu. Yatakusaidia uje kumjua Yeye na kuonja upendo Wake, ambao ni mtamu zaidi ya yote yaliyo matamu. Maneno Yake yatajaza nafsi yako kwa shangwe (1 Nefi 8:11–12; ona mstari wa 1–34).

Maandiko ni zawadi kutoka mbinguni. Mojawapo ya baraka kuu ya misheni yako ni kuwa na muda ulioratibiwa wa kujifunza maandiko kila siku.

Kujifunza Injili ni mojawapo ya aina ya kazi ya kiroho yenye kuridhisha sana unayoweza kuifanya. Inaleta nguvu mpya kwenye vyote kiakili na kiroho. Kama Alma alivyofundisha, wakati “unapopanda” neno la Mungu katika moyo wako, linaanza “kuangaza kuelewa kwako” na kuwa la kupendeza sana kwako.(Alma 32:28; ona pia Alma 32:28). Unapoendelea kujifunza na kutumia neno la Mungu, litaanza “kumea mizizi, na… kuwa mti utakaochipukia kwenye uzima wa milele” (Alma 32:41; ona pia mstari wa 42–43). Ufahamu wako na ushuhuda wako wa injili utaongezeka. Hamu yako na uwezo wako wa kushiriki injili pia utaongezeka.

Kujifunza kutoka kwa mwalimu mzuri ni muhimu, lakini pia ni muhimu kwako kuwa na uzoefu wa maana kutokana na kujifunza kwako maandiko wewe mwenyewe. Hii pia ni kweli kwa wale unaowafundisha.

Kuelewa maandiko kunaweza kuwa changamoto hapo mwanzoni. Hata hivyo, kwa subira unapojitahidi kujifunza neno la Mungu, uelewa wako utakua. Utakuja kuthamini muda wako kwenye maandiko. Utatarajia kwa shauku kile utakachojifunza na pia uzoefu.

Kuyajua na kuyapenda maandiko kunaweza kuwa baraka ya maisha yote ya huduma yako ya umisionari. Unapopata uzoefu wa baraka za kujifunza maandiko wakati wa misheni yako, utataka kuendelea maisha yako yote.

Picha
Mzee D. Todd Christofferson

“Lengo muhimu la maandiko yote ni kujaza nafsi zetu kwa imani katika Mungu Baba na katika Mwana, Yesu Kristo—imani kwamba Wao wapo; imani katika mpango wa Baba kwa ajili ya maisha yetu ya kutokufa na uzima wa milele; imani katika Upatanisho na Ufufuko wa Yesu Kristo, ambayo inaonesha mpango huu wa furaha; imani ya kufanya injili ya Yesu Kristo kuwa njia yetu ya maisha; na imani ya kumjua ‘Mungu pekee wa kweli, na Yesu Kristo, ambaye (Yeye) alimtuma’ (Yohana 17:3)” (D. Todd Christofferson, “Baraka za Maandiko,” Liahona, Mei 2010, 34).

Kujifunza Binafsi

Tazama picha ya Joseph Smith mwanzoni mwa sura hii. Soma Joseph Smith—Historia ya 1:11—13. Jibu maswali yafuatayo katika shajara yako ya kujifunzia.

  • Ni kwa jinsi gani kusoma na kutafakari kwa Joseph Smith kwenye Yakobo 1:5 kulimwongoza yeye kupokea ufunuo?

  • Je, kujifunza kwake kumekuwa na ushawishi gani kwa vizazi vijavyo?

  • Ni athari ipi uamuzi wake wa kujifunza na kutafuta umeleta ndani ya maisha yako?

  • Ni kwa jinsi gani kujifunza kwako injili kumeshawishi maisha yako na maisha ya wengine?

Kujifunza Maandiko

Je, unaweza kujifunza nini kutoka kwenye maandiko yafuatayo kuhusu jinsi ya kuyaendea mafunzo ya injili?

Mtafute Roho

Kujifunza injili ni zaidi ya kupata taarifa. Pia ni mchakato wa kiroho wa kutumia ukweli wa milele chini ya mwongozo wa Roho Mtakatifu (ona Yakobo 4:8; Mafundisho na Maagano 50:19–25). Mtafute na mtumainie Roho akufundishe unapojifunza maandiko. Hii itatendeka kwa kiwango ambacho unalinganisha maandiko na wewe mwenyewe kwa kusudi halisi la kutenda juu ya kile unachojifunza (ona 1 Nefi 19:23; Moroni 10:4; Joseph Smith—Historia ya 1:18).

Kujifunza maandiko kwa sala kutafungua dirisha la ufunuo kwa ajili ya Roho kuzungumza kwenye akili na moyo wako. Yeye atakubariki kwa mwongozo, ushawishi, na majibu ya maswali yako. Kupitia kujifunza kwako maandiko, Roho Mtakatifu atakuimarisha na kukufariji. Atakupatia maarifa na uthibitisho ambavyo vitabariki maisha yako na kukuwezesha kuwabariki wengine milele.

Kujifunza Maandiko

Ni nini wajibu wa Roho Mtakatifu katika kumsaidia mtu ajifunze injili?

Tafuta Majibu ya Maswali

Kama mmisionari, utasikia maswali mengi. Wewe pia utakuwa na maswali yako mwenyewe. Kupekua maandiko na nyenzo zingine zilizoidhinishwa kwa ajili ya maswali haya ni njia nzuri sana ya kujifunza. Andika maswali na kile unachojifunza na kuhisi katika shajara yako ya kujifunzia.

Tumia nyenzo sahihi na za kutegemewa katika kujifunza kwako—kimsingi maandiko, maneno ya manabii walio hai, na Hubiri Injili Yangu. Tumia nyenzo katika Maktaba ya Injili, kama vile Mwongozo wa Maandiko, Kamusi ya Biblia, Kielezo cha Muungano wa Maandiko, Mada za Injili, na Insha za Mada za Injili. Jifunze ni nyenzo zipi zinapatikana katika lugha za watu unaowafundisha.

Picha
Rais M. Russell Ballard

“Kitu kimoja ambacho nimejifunza katika maisha ni jinsi ambavyo Bwana kila mara hujibu maswali yetu na kutupatia ushauri kupitia maandiko. … Acha basi twende kwa Bwana katika sala, tukisihi kwa ajili ya kupata msaada au majibu; na yale majibu yatakuja unapofungua maandiko na kuanza kujifunza. Wakati mwingine ni kama vile maandiko yenye umri takribani mamia au maelfu ya miaka yalitolewa ili kujibu swali letu” (M. Russell Ballard,”Be Strong in the Lord, and in the Power of His Might” [Brigham Young University fireside, Mar. 3, 2002], 5, speeches.byu.edu).

Ishi Kile Unachojifunza

Unapohisi shangwe ambayo inakuja kutokana na kukua katika uelewa wa injili, utataka kutumia kile unachojifunza. Jitahidi kuishi katika uwiano na kile unachojifunza. Kufanya hivyo kutaimarisha imani yako, ufahamu, na ushuhuda wako. Kutenda juu ya kile unachojifunza kutaleta uelewa zaidi na wa kudumu. (Ona Yohana 7:17.)

Picha
Rais Boyd K. Packer

“Mafundisho ya kweli, yakieleweka, hubadilisha mtazamo na tabia. Kujifunza [mafundisho] ya injili kutaboresha tabia haraka zaidi kuliko kujifunza tabia kutakavyoboresha tabia” (Boyd K. Packer, “Little Children,” Ensign, Nov. 1986, 17).

Kujifunza Binafsi

Ni kipi maandiko yafuatayo yanakifundisha kuhusu kujifunza injili?

Tumia Maktaba ya Injili

Maktaba ya Injili ni nyenzo ya mtandaoni ambayo inaweza kuboresha sana kujifunza kwako na kufundisha kwako. Elewa vipengele vyake vingi. Baadhi ya manufaa ya kutumia Maktaba ya Injili kama sehemu ya kujifunza kwako na kufundisha yameorodheshwa hapo chini.

  • Inakupa ufikiaji kwenye maandiko, maneno ya manabii walio hai, na maudhui mengine ya Kanisa katika lugha nyingi katika muundo wa matini, sauti, na video.

  • Kama ukiandika katika Maktaba ya Injili kile unachojifunza na misukumo uliyoipokea, unaweza kuendelea kuifikia na kuimarishwa na taarifa hiyo baada ya misheni yako.

  • Inakuruhusu kushiriki kwa urahisi maandiko, dondoo kutoka kwa manabii walio hai, na video kwa wale unaowafundisha.

  • Wengi wa watu unaowafundisha na kuwabatiza watatumia Maktaba ya Injili ili kupata nyenzo za Kanisa. Elewa vipengele vya Maktaba ya Injili ili uweze kuwasaidia wao wajifunze kuitumia.

Kujifunza Binafsi

Rejelea “Mwongozo wa Mtumiaji wa Maktaba ya Injili.” Chagua kipengele katika Maktaba ya Injili ili kukijaribu katika kikao kijacho cha mafunzo pamoja na mmisionari mwenza wako. Ni kwa jinsi gani kipengele hiki kilisaidia kujifunza kwako? Je, utajaribu kipi wakati ujao? Wafundishe wamisionari wengine kile unachojifunza.

Tumia Teknolojia kwa Uadilifu

Bwana na manabii Wake wamekuamini wewe kutumia teknolojia ili ikusaidie kutimiza kazi Yake. Teknolojia inaweza kuboresha kujifunza kwako maandiko na Hubiri Injili Yangu. Nyenzo za kidijitali zinaweza pia kukusaidia wewe uweke mipango. Zinaweza kukusaidia katika kufundisha kwako na katika juhudi zako za kupata watu wa kuwafundisha.

Matumizi ya teknolojia kwa hekima na uadilifu yanaweza kukusaidia utimize dhumuni lako la umisionari na utumie muda kwa tija. Inaweza pia kukusaidia uepukane na nyenzo zisizofaa.

Mfuate Roho kuhusu ni wakati gani na jinsi gani ya kutumia teknolojia katika njia ambazo zitakusaidia uimarishe imani yako katika Yesu Kristo na imani ya wale unaowatumikia na kuwafundisha.

Fuata Ulinzi kwa ajili ya Matumizi ya Teknolojia

Aina nne za ulinzi zilizoainishwa hapo chini zitakusaidia utumie teknolojia kwa usahihi. Kufuata ulinzi huu ni njia muhimu kwa ajili yako “kuvaa silaha zote za Mungu, ili uweze kuzipinga hila za Shetani” (Waefeso 6:11).

Kuwa kwenye Uwiano na Ushawishi wa Kiroho

Nefi aliahadi, “kama mtaingia kwa njia hiyo, na kupokea Roho Mtakatifu, atawaonyesha vitu vyote ambavyo mnastahili kutenda” (2 Nefi 32:5). Baba yako wa Mbinguni amekupatia vipawa viwili vyenye nguvu ambavyo vitakusaidia: haki ya kujiamulia na kipawa cha Roho Mtakatifu. Una uwezo wa kuchagua kufuata mwongozo wa Roho Mtakatifu. Mwongozo Wake ni muhimu katika kukusaidia utende wema akitumia teknolojia. Pia husaidia kukulinda kutokana na uovu.

Fokasi kwenye Dhumuni Lako la Umisionari

Bwana alisema, “Na kama macho yenu yatakuwa katika utukufu wangu pekee, miili yenu yote itajazwa na nuru, na hakutakuwa na giza ndani yenu; na mwili ule uliojazwa na nuru hufahamu mambo yote” (Mafundisho na Maagano 88:67). Kuwa na macho yako katika utukufu wa Mungu pekee humaanisha kufokasi kikamilifu kwenye dhumuni la Mungu, ambalo pia ni dhumuni lako kama mmisionari.

Matumizi yako ya teknolojia yanapaswa kuwa na kiini kwenye dhumuni lako. Washa kifaa chako baada tu ya wewe kutambua dhumuni la umisionari ambalo kwa hilo utakitumia. Kisha zima wakati dhumuni hilo linapokuwa limekamilika.

Kuna uwezekano wa kukabiliana na maudhui yasiyofaa kwenye intaneti wakati ukivinjari kwenye tovuti bila dhumuni mahuhusi akilini.

Picha
wamisionari wakitazama simu

Kuwa Mwenye Nidhamu

Mormoni aliandika: “Mimi ni mfuasi wa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. Nimeitwa na yeye kutangaza neno lake miongoni mwa watu wake, ili wawe na uzima usio na mwisho” (3 Nefi 5:13). Kama vile Mormoni, wewe ni mfuasi wa Kristo. Kutumikia kama mmisionari wa muda wote ni fursa maalum ya kuongeza ufuasi wako.

Maneno mfuasi na nidhamu yanatokana na mzizi wa neno ambalo humaanisha “anayejifunza.” au “mwanafunzi.” Kuwa mfuasi wa Kristo humaanisha kwamba wewe unamfuata Yeye na kutii amri Zake. Humaanisha kwamba kwa uthabiti unajifunza na kufundisha juu ya Kristo.

Kuwa na nidhamu na fanya chaguzi zenye uadilifu katika jinsi unavyotumia teknolojia. Chagua kufuata maelekezo ya ulinzi. Unapozungumza ana kwa ana na watu, usiangalie ujumbe wa simu wala usijibu simu. Dhibiti jinsi ya kutumia vifaa hivi. Usiache vikudhibiti wewe.

Bwana alitamka, “Yeye ambaye huipokea sheria yangu na kuitenda, huyo ndiye mwanafunzi wangu; na yule asemaye ameipokea na haitendi, huyo siyo mwanafunzi wangu” (Mafundisho na Maagano 41:5). Wakati hakuna mtu aliye mkamilifu, Bwana anatarajia juhudi thabiti, endelevu za kumfuata Yeye.

Uzuri wa injili ni kwamba tunaweza kusamehewa pale tunapotubu—na Bwana anatutaka tutubu bila kuchelewa (ona Mafundisho na Maagano 109:21). Kama ukifanya makosa, ikijumuisha matumizi yasiyofaa ya teknolojia, tubu wakati huo huo na endelea kujaribu kuishi sheria Yake. Hii ni sehemu ya kuwa mfuasi wa Kristo.

Muwe na Umoja

Bwana alisema, “Muwe na umoja; na kama hamna umoja ninyi siyo wangu” (Mafundisho na Maagano 38:27). Saidia misheni yako ikuze desturi ya umoja, kuaminika, kuwajibika, na huruma ili muweze kuimarishana na kusaidiana.

Wamisionari wote wanapaswa kuhisi vizuri kuomba msaada wakati unapohitajika. Mmisionari ambaye ni imara katika Roho anaweza kumsaidia yule ambaye anahisi kuwa ni mdhaifu (ona Mafundisho na Maagano 84:106). Kama unahisi kujaribiwa, muombe mwenza wako au kiongozi wa misheni msaada.

Karibu changamoto zote zinazohusishwa na intaneti au ponografia hutokea sirini. Tumia vifaa pale tu unapoweza kuona skrini za wengine. Kuwa na ujasiri na uwe mwajibikaji kwa wengine.

Bwana anamwamini kila mmisionari ambaye Yeye amemwita, ikiwa ni pamoja na wewe. Ametoa wenza na viongozi ili kusaidia kukulinda na kukuunga mkono. Kama vile Alma alivyomsaidia mwenza wake Amuleki, tafuta kuimarishana (ona Alma 15:18).

Unapaswa Kufanya Nini Kama Unahisi Kuwa Dhaifu au Kuathirika?

Kujifunza kufuata njia hizi nne za ulinzi kunahitaji juhudi, nidhamu, na mazoezi. Hata baada ya ulinzi kuwa sehemu ya kawaida ya jinsi unavyofikiri na kutenda, utakuwa na nyakati ambapo unahisi kuwa mdhaifu au mwathirika. Pengine ulikuwa na kiasi cha tabia mbaya za matumizi ya teknolojia kabla ya misheni yako ambazo zinakuwa ngumu kuzishinda. Baadhi ya wamisionari walihangaika na ponografia kabla ya wito wao na wanaweza kujaribiwa kuanguka tena katika mipangilio ya tabia za awali.

Kanuni zilizo hapa chini zitakusaidia uishi kwa ulinzi na kujikinga mwenyewe dhidi ya majaribu.

  • Kuwa makini na mawazo yako, hisia, na tabia. Elewa jinsi zinavyoweza kukufanya uwe muhanga zaidi kwa matumizi mabaya ya teknolojia.

  • Chagua Kutenda. Jibu kwa njia za haki, njia nzuri kwenye kile unachohisi.

  • Jifunze, tubu na jiboreshe. Tumia uzoefu wako kuendelea kujifunza na kujiboresha.

Hauhitaji kushinda changamoto peke yako. Tegemea nguvu ambazo huja kupitia Upatanisho wa Mwokozi na maagano uliyofanya Naye. Bwana anajua changamoto unazokabiliana nazo, na Yeye atakusaidia katika kazi hii kuu.

Daima ukikumbuka kwamba Mwokozi anaweza kukusaidia utumie teknolojia kwa uadilifu. Kuwa mkweli kwa uaminifu ambao Yeye amekupatia wewe. Amua “kutembea wima mbele yake” (Mafundisho na Maagano 53:21; ona pia mstari wa 20). Kuhisi shukrani kwa ajili ya yote ambayo Yeye na Baba wameyafanya kwa ajili yako itakusaidia wewe ufanye chaguzi nzuri kuhusu jinsi ya kutumia nyenzo za kijiditali.

Misheni yako ni fursa kubwa ya kujifunza kutumia teknolojia kwa busara. Msimamo na tabia nzuri unazokuza wakati wa misheni yako zitakuwa na manufaa katika maisha yako yote.

Vaa Silaha za Mungu

Uwezo wako wa kupinga majaribu utaongezeka pale unapojifunza na kutumia maandiko, maneno ya manabii walio hai, Hubiri Injili Yangu; Viwango vya Umisionari kwa ajili ya Wafuasi wa Yesu Kristo, na ulinzi ulioainishwa katika sura hii.

Picha
wamisionari wakisalimiana na mwanamume

Kwa kuvaa “silaha zote za Mungu,” utaweza kutambua kati ya ukweli na kosa. Miguu yako itavishwa “injili ya imani.” Kuvaa deraya ya haki” kutakulinda. Kwa “ngao ya imani,” utaweza kuizima mishale yote yenye moto ya adui; Utachukua “upanga wa Roho [Yake]” kufundisha ukweli kwa uwezo na mamlaka. Utaimarishwa dhidi ya ushawishi wa dunia ambao ungeweza vinginevyo kukuongoza kuyoyoma, kutengwa, na hata kufarakishwa. (Ona Waefeso 6:10–18; ona pia 1 Nefi 8:20, 30; 15:24–25; Helamani 3:29–30; Mafundisho na Maagano 27:15–18; Joseph Smith—Mathayo 1:37; 2 Timotheo 3:15–17.)

Kujifunza Binafsi

Kwa sala tambua mojawapo ya ulinzi ili kufokasi juu yake wiki hii. Tafuta Msaada wa Bwana. Andika hisia zako na kile unachojifunza.


Mawazo kwa ajili ya Kujifunza na Matumizi

Kujifunza Binafsi

  • Fikiria baadhi ya mapendekezo yafuatayo ili kuboresha kujifunza kwako:

    • Soma maandiko ukiwa na maswali na mashaka akilini.

    • Shiriki kile ulichojifunza pamoja na wamisionari wengine na pamoja na wale unaowafundisha. Kuelezea mafundisho au kanuni kutakusaidia uzikumbuke na upate ufafanuzi.

    • Jifunze kwa Mada. Fokasi kwenye mada ambazo zitakusaidia wewe na watu unaowafundisha.

    • Jiulize mwenyewe, “Mwandishi anasema nini? Ujumbe muhimu ni upi? Ni kwa jinsi gani ujumbe huu unatumika kwangu? Ni kwa jinsi gani hii inamsaidia mtu tunayemfundisha?”

    • Vuta taswira au chora kile unachojifunza. Kwa mfano, fikiria ilikuwaje kwa Amoni kusimama mbele ya mfalme Mlamani.

    • Andika wazo kuu la kifungu katika sentensi moja au aya fupi.

    • Kariri maandiko ambayo yanaelezea na kuunga mkono kanuni unazozifundisha.

  • Jitathmini mwenyewe kwa njia ifuatayo (1=hapana 3=wakati mwingine, na 5=karibu kila mara).

    • Ninakua katika imani yangu na kuja kuwajua vyema Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo.

    • Ninafikiri kuhusu watu ninaowafundisha wakati ninapojifunza.

    • Siku nzima, ninafikiria kuhusu kile nilichojifunza asubuhi.

    • Ninapojifunza, mawazo yanakuja akili mwangu ambayo hayakunijia hapo awali.

    • Ninaandika misukumo ya kiroho na mawazo katika mahali sahihi.

    • Ninakaa macho ninapojifunza.

    • Ninatazamia muda wa kujifunza binafsi.

    • Ninatazamia muda wa kujifunza na mmisionari mwenza.

    Rejelea majibu yako. Ni kitu gani unafanya vyema? Je, ni kwa namna gani ungeweza kuboresha? Weka lengo moja au mawili ili kuboresha kiwango cha kujifunza kwako.

Kujifunza na Mmisionari Mwenza na Kubadilishana Mmisionari Mwenza

Baraza la Wilaya, Mikutano ya Kanda na Baraza la Uongozi la Misheni

  • Waombe wamisionari waandike swali moja au mawili kuhusu injili kutoka kwenye somo katika sura ya 3. Maswali haya yangeweza kuwa ya binafsi au kutoka kwa watu unaowafundisha. Waalike wamisionari washiriki maswali yao na kundi. Kwa kila swali, jadili yafuatayo:

    • Ni kwa jinsi gani kujibu swali hili kungebariki maisha ya mmisionari?

    • Ni kwa jinsi gani kungebariki maisha ya watu ambao yeye anawafundisha?

    • Ni kwa jinsi gani mmisionari angeweza kupata jibu?

  • Wagawe wamisionari katika makundi, na lipangie kila kundi kujifunza mojawapo ya aina nne za ulinzi na maandiko yaliyoambatishwa. Waalike wamisionari washiriki kile walichojifunza na jinsi ulinzi ulivyowasaidia.

Viongozi wa Misheni na Washauri wa Misheni

  • Mara moja moja jiunge na wamisionari wengine na wenza wao katika kujifunza.

  • Wakati wa mahojiano au mazungumzo, waulize baadhi ya maswali yafuatayo:

    • Ni misukumo ipi umeipata hivi karibuni katika kujifunza kwako maandiko?

    • Ni sura ipi au sehemu ipi ya Hubiri Injili Yangu imekusaidia sana katika wiki mbili zilizopita? Ni kwa jinsi gani imekusaidia?

    • Unafanya kipi katika kujifunza kwako binafsi ambacho hukusaidia ujifunze?

  • Katika mahojiano, fikiria kurejelea ulinzi katika kutumia teknolojia na waulize wamisionari kile wanachojifunza wakati wanapotumia ulinzi huo.

  • Shiriki umaizi unaotokana na kujifunza kwako binafsi. Shiriki maingizo kutoka katika shajara yako ya kujifunzia na ushuhuda wako juu ya umuhimu wa kujifunza injili.

Chapisha