Mafundisho na Maagano 2021
Februari 22–28. Mafundisho na Maagano 18–19: “Thamani ya Nafsi ni Kuu”


“Februari 22–28. Mafundisho na Maagano 18–19: ‘Thamani ya Nafsi ni Kuu,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Mafundisho na Maagano 2021 (2020)

“Februari 22–28. Mafundisho na Maagano 18–19,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2021

Picha
Shamba la Martin Harris

Shamba la Martin Harris, na Al Rounds

Februari 22–28

Mafundisho na Maagano 18–19

“Thamani ya nafsi ni kuu”

Funuo katika Mafundisho na Maagano zilitolewa kujibu hali maalumu karibia miaka 200 iliyopita, bali kanuni inazofundisha ni za milele. Tafuta kanuni hizi unaposoma, na fikiria jinsi zinavyotumika kwako.

Andika Misukumo Yako

Martin na Lucy Harris walikuwa na mojawapo ya mashamba mazuri katika Palmyra, New York. Ilikua imewachukua miaka kulipata, lilikuwa limewawezesha kulea familia, na lilikuwa limewapa sifa nzuri katika jamii. Lakini mnamo mwaka 1829 ilikuwa wazi kwamba Kitabu cha Mormoni kingeweza kuchapishwa tu kama Martin angeweka rehani shamba lake kumlipa mchapishaji. Martin alikuwa na ushuhuda wa Kitabu cha Mormoni, lakini Lucy hakuwa nao. Kama Martin angeendelea na kuweka rehani na Kitabu cha Mormoni hakikuuzika vizuri, angepoteza shamba lake na kuhatarisha ndoa yake. Kwa wakati mmoja au mwingine, sisi sote tunakabiliana na maswali sawa na hayo ambayo Martin alikuwa anayakabili: Ni nini thamani ya injili ya Yesu Kristo kwangu? Ni nini niko tayari kutoa dhabihu kusaidia kujenga ufalme wa Mungu? Inaweza kutusaidia kukumbuka kwamba hakuna mtu aliyewahi kulipa gharama ya juu kubariki watoto wa Mungu zaidi ya Yesu Kristo, “Mkuu zaidi ya wote” (Mafundisho na maagano 19:18).

Martin alifanya uamuzi wa kuweka rehani shamba lake. Dhabihu yake ililipia uchapishaji wa nakala 5,000 za mwanzo za Kitabu cha Mormoni. Na sasa, zaidi ya nakala milioni 190 baadaye, mamilioni ya nafsi ulimwenguni kote zimebarikiwa.

Kwa maelezo zaidi kuhusu uchapishwaji wa Kitabu cha Mormoni, ona Watakatifu, 1:76–84.

Picha
ikoni ya kujifunza kibinafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kibinafsi

Mafundisho na Maagano 18:10–16

Bwana anafurahi wakati tunapotubu.

Tilia maanani ni mara nyingi kiasi gani maneno tubu na toba yanavyotumika kote katika Mafundisho na Maagano 18 na 19, na tafakari kile unachojifunza kutokana na maneno haya kila wakati yanapotumika. Fikiria hususani Mafundisho na Maagano 18:10–16; ni kwa jinsi gani mistari hii inaathiri jinsi unavyohisi kuhusu toba—toba yako mwenyewe na wajibu wa kuwaalika wengine kutubu?

Ona pia Alma 36:18–21; Dale G.Renlund, “Toba: Uchaguzi wa Furaha,” Ensign au Liahona, Nov. 2016, 121–24.

Mafundisho na Maagano 18:34–36

Ninaweza kusikia sauti ya Bwana katika Mafundisho na Maagano.

Kama mtu angekuuliza sauti ya Bwana ikoje, ungesema nini? Fikiria kuhusu swali hili unaposoma Mafundisho na Maagano 18:34–36. Umejifunza nini kuhusu sauti ya Bwana kutokana na kusoma Mafundisho na Maagano? Unaweza kufanya nini kusikia sauti Yake dhahiri zaidi?

Mafundisho na Maagano 19:15–20.

Yesu Kristo aliteseka ili kwamba niweze kutubu na kuja Kwake.

Agano Jipya linaelezea mateso ya Mwokozi katika Gethsemane katika mtazamo wa wale walioyaona. Katika Mafundisho na Maagano 19: 15–20, Yesu Kristo alisema kuhusu mateso yake kwa maneno yake mwenyewe. Unaposoma maelezo haya binafsi, matakatifu, tafuta maneno na virai ambavyo vinaelezea mateso ya Mwokozi. Fikiria nini kila neno au kirai vinakufundisha. Kwa nini Mwokozi alikuwa tayari kuteseka? Fikiria kuandika hisia zako kuhusu Yesu Kristo na dhabihu Yake kwa ajili yako.

Ona Yohana 15:13; Mosia 3:7; Alma 7:11–12; Mafundisho na Magano 18:10–13.

Picha
Yesu akiwa amembeba mvulana mdogo

Thamani ya Nafsi, na Liz Lemon Swindle

Mafundisho na Maagano 19–27, 34–41

Baraka za Mungu ni kubwa mno kuliko hazina za dunia.

Kitabu cha Mormoni hakikuuzika vizuri sana huko Palmyra, na matokeo yake, Martin Harris aliishia kuuza sehemu kubwa ya shamba lake ili kulipa deni (ona “Michango ya Martin Harris,” Funuo katika Muktadha, 7–8). Tafakari dhabihu ile—na baraka ulizopokea kwa sababu yake—unaposoma mistari hii. Ungeweza pia kufikiria kuhusu nini Bwana amekutaka utoe dhabihu. Unapata nini katika mistari hii ambacho kinakuvutia kufanya dhabihu hizi kwa “shangwe na furaha”? (Ona pia mstari wa 15–20).

Mafundisho na Maagano 19:23

Amani inakuja kutokana na kujifunza juu ya Yesu Kristo na kumfuata.

Fikiria mwaliko wa Mwokozi “jifunze Kwangu.” Unajifunza nini kuhusu Yesu Kristo katika Mafundisho na Maagano 19? Andika mawazo yako, na tafakari jinsi kweli hizi kuhusu Mwokozi zinavyokusaidia kupata amani. Inamaanisha nini kwako “kuenenda katika unyenyekevu wa Roho [Yake]”?

Picha
ikoni ya kujifunza kifamilia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko Kifamilia na Jioni ya Familia Nyumbani

Mafundisho na Maagano 18:1–5.Pengine wanafamilia wangeweza kushiriki baadhi ya “mara nyingi” (mstari wa 2) ambazo Roho ameonesha kwao kwamba maandiko ni ya kweli, kama Alivyofanya kwa Oliver Cowdery. Ni kwa jinsi gani familia yako “inategemea mambo ambayo yameandikwa” (mstari wa 3) katika maandiko? Je, ni kwa jinsi gani unaweza kujenga msingi wa familia yako juu ya “mwamba” (mstari wa 4) wa injili?

Mafundisho na Maagano 18:10–13; 19:16–19.Kila mwanafamilia angeweza kusoma Mafundisho na Maagano 18:10–13 na kubadili jina lake katika sehemu yenye maneno “nafsi,” na “watu wote.” Kisha mngeweza kujadili jinsi mistari hii inavyotusaidia kuelewa thamani yetu kwa Baba na Mwana (ona Mafundisho na Maagano 19:16–19).

Mafundisho na Maagano 18:21–25.Je, majina ya wanafamilia wako yana maana maalumu? Labda mngeweza kuzungumza kuhusu kwa nini majina ni muhimu na inamaanisha nini kujichukulia juu yetu jina la Yesu Kristo (ona Mosia 5:7). Hii ingeweza kuwa fursa nzuri kuwasaidia wanafamilia kujiandaa kujichukulia jina la Kristo juu yao wakati wanapobatizwa.

Mafundisho na Maagano 19:15–20.Ili kuisaidia familia yako kuwa na uzoefu wenye maana kwenye mistari hii, pengine ungeweza kuisoma wakati ukionesha picha ya Yesu Kristo (moja inayoambatana na muhtasari huu). Wanafamilia kisha wangeshiriki hisia zao kuhusu Mwokozi. Wimbo unaopendwa kuhusu Mwokozi ungeweza pia kumwalika Roho.

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “I Stand All Amazed,” Nyimbo za Kanisa, na.193

Kuboresha Kujifunza Kibinafsi

Uliza maswali. Mafundisho na Maagano ni ushahidi kwamba maswali yanaongoza kwenye ufunuo. Unapojifunza maandiko, weka kumbukumbu ya maswali ambayo yanakutokea. Kisha tafakari na sali kutafuta majibu.

Picha
Yesu akisali katika Bustani ya Gethsemane

Kristo Anasali katika Bustani ya Gethsemane, na Hermann Clementz

Chapisha