Agano la Kale 2022
Januari 17–23. Mwanzo 5; Musa 6: “Yafundisheni Mambo Haya kwa Uhuru kwa Watoto Wenu”


“Januari 17–23. Mwanzo 5; Musa 6: ‘Yafundisheni Mambo Haya kwa Uhuru kwa Watoto Wenu,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano la Kale 2022 (2021)

“Januari 17–23. Mwanzo 5; Musa 6,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2022

Picha
Adamu na Hawa nje ya Bustani ya Edeni

Bora kuliko Paradiso, na Kendal Ray Johnson

Januari 17–23

Mwanzo 5; Musa 6

“Yafundisheni Mambo Haya kwa Uhuru kwa Watoto Wenu”

Unaposoma na kutafakari Mwanzo 5 na Musa 6, andika misukumo ya kiroho unayoipokea. Je, ni ujumbe gani unapata ambao una thamani kubwa kwako na kwa familia yako?

Andika Misukumo Yako

Sehemu kubwa ya Mwanzo 5 ni orodha ya vizazi kati ya Adamu na Hawa na Nuhu. Tunasoma majina mengi, lakini hatujifunzi mengi kuhusu watu hao. Halafu tunasoma kuhusu Henoko, vizazi sita kutoka kwa Adamu, ambaye anaelezewa kwa mstari huu wa kuvutia sana lakini usiofafanuliwa: “Na Henoko akaenda pamoja na Mungu: naye akatoweka; maana Mungu alimtwaa” (Mwanzo 5:24). Hakika pana hadithi nyuma ya hilo. Lakini bila ufafanuzi wa ziada, orodha ya vizazi inaendelea.

Kwa shukrani, Musa 6 inafunua maelezo ya kina ya hadithi ya Henoko—na ni hadithi nzuri. Tunajifunza juu ya unyenyekevu wa Henoko, kukosekana kwa usalama wake, uwezo ambao Mungu aliouona ndani yake, na kazi kubwa aliyoifanya kama nabii wa Mungu. Pia tunapata picha ya wazi juu ya familia ya Adamu na Hawa ikiendelea kupitia vizazi vingi. Tunasoma juu ya “miliki kuu” ya Shetani lakini pia juu ya wazazi ambao waliwafundisha watoto “njia za Mungu” na juu ya “wahubiri wa haki” ambao “walinena na kutoa unabii” (Musa 6:15, 21, 23). Mahususi cha thamani ni kile tunachojifunza kuhusu mafundisho ambayo wazazi hawa na wahubiri walifundisha: imani, toba, ubatizo, na kumpokea Roho Mtakatifu (ona Musa 6:50–52). Mafundisho haya, kama ukuhani unaoambatana nayo, “yalikuwepo hapo mwanzo [na] yatakuwepo hadi mwisho wa ulimwengu pia” (Musa 6:7).

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

Musa 6:26–36

Nabii ni mwonaji.

Unaposoma Musa 6:26–36, unajifunza nini kuhusu macho, giza, na kuona? Katika wakati wa Henoko, ni nani hakuweza “kuona mbali zaidi”? Kwa nini watu hawa hawakuweza kuona ukweli? Je, Henoko aliweza kuona nini? Je, ni kitu gani kimejenga imani yako kwamba manabii wa kisasa ni waonaji? (ona mstari wa 36; Mwongozo wa Maandiko, “Mwonaji,” scriptures.ChurchofJesusChrist.org).

Musa 6:26–47

Mungu anatuita sisi kufanya kazi yake licha ya mapungufu yetu.

Siyo jambo lisilo la kawaida mtu kujisikia kuzidiwa na kile Bwana alichokuita kukifanya. Hata Henoko alijisikia hivyo wakati Bwana alipomwita yeye kuwa nabii. Unaposoma Musa 6:26-36, angalia ni kwa nini Henoko alijisikia kuzidiwa na kitu ambacho Bwana alichosema ili kumpa ujasiri. Katika mistari ya 37–47, tafuta njia ambazo Bwana alimsaidia Henoko na zilimpa nguvu ya kutimiza kazi Yake (ona pia Musa 7:13). Unaweza kulinganisha matukio ya Henoko na yale ya manabii wengine ambao walijiona wana mapungufu, kama vile Musa (ona Kutoka 4:10–16), Yeremia (ona Yeremia 1:4–10), Nefi (ona 2 Nefi 33:1–4), na Moroni (ona Etheri 12:23–29). Je, unahisi Mungu anataka wewe ujifunze nini kutoka katika maandiko haya kuhusu kazi ambayo amekupa kufanya?

Ona pia Yakobo 4:6–8.

Musa 6:48–68

Mafundisho ya Kristo ndio kitovu cha mpango wa Mungu wa wokovu.

Kwa sababu tunacho kitabu cha Musa, tunajua kuwa Mungu amekuwa akifundisha watoto Wake jinsi ya kupata msamaha na ukombozi tangu hapo mwanzo. Katika maandiko, mafundisho haya nyakati zingine yanaitwa mafundisho ya Kristo (ona 2 Nefi 31:13–21). Unaposoma Musa 6:48–68, pekua kwa ajili ya kitu ambacho ni lazima tukijue na kukifanya ili tukombolewe. Unaweza kuona ni vyema kuandika muhtasari wako mwenyewe juu ya mambo Henoko aliyofundisha. Je, kwa nini ni muhimu kujua kwamba ukweli huu umekuwa ukifundishwa tangu siku za Adamu na Hawa? Je, unahisi kushawishiwa kufanya nini kama matokeo ya kujifunza mafundisho haya?

Musa 6:51–62

“Yafundisheni mambo haya kwa uhuru kwa watoto wenu.”

Adamu na Hawa walifundishwa ukweli wa thamani wa injili ya Yesu Kristo. Lakini maneno ya Bwana katika Musa 6:27–28 yanaweka wazi kwamba katika vizazi kabla ya Henoko, watu wengi hawakuwa wakiishi ukweli huo tena. Bwana alimtaka Henoko kurejesha ukweli ambao ulikuwa umepotea—pamoja na amri ambazo mwanzoni zilitolewa kwa Adamu: “Yafundisheni mambo haya kwa uhuru kwa watoto wenu” (Musa 6:58). Unaposoma Musa 6:51–62, unajifunza nini kuhusu Yesu Kristo? Je, unapata nini ambacho kingekuwa cha thamani mahususi kwa ajili ya kizazi chipukizi? Unaweza kufanya nini ili kusaidia kupitisha ukweli huu kwa vizazi vya siku za baadaye?

Picha
familia ikisoma maandiko

Wazazi wanapaswa kuwafundisha watoto wao injili.

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

Mwanzo 5; Musa 6:5–25, 46.Kusoma kuhusu “kitabu cha kumbukumbu” ambacho familia ya Adamu na Hawa walikitunza kunaweza kuihamasiha familia yako kutengeneza kitabu chenu cha kumbukumbu. Jadilianeni kama familia kitu ambacho mngetaka kukijumuisha. Pengine mnazo picha, hadithi, au nyaraka kutoka katika historia ya familia yenu. Mnaweza kuchagua kujumuisha mambo ambayo yanatokea katika familia sasa. Je, vizazi vya siku zijazo watapata nini kilicho cha thamani? Mngeweza pia kujadili jinsi vifungu hivi vya maneno “kwa roho wa mwongozo” (Musa 6:5) na “utaratibu uliotolewa kwa kidole cha Mungu” (Musa 6:46) vingeweza kuongoza jitihada zako. Zingatia kuweka taarifa kutoka katika kitabu chenu cha kumbukumbu katika FamilySearch.org.

Musa 6:53–62.Je, tungewezaje kujibu swali la Adamu linalopatikana katika Musa 6:53? Je, ni majibu gani tunayapata katika mistari ya 57–62?

Musa 6:59.Je, inamaanisha nini “kuzaliwa tena katika ufalme wa mbinguni”? Je, tunaweza kufanya nini ili kuendelea kuzaliwa tena katika maisha yetu yote? Kwa msaada, ona Alma 5:7–14, 26; Mwongozo wa Maandiko, “Born Again, Born of Godscriptures.ChurchofJesusChrist.org; David A. Bednar, “Daima Linda Msamaha wa Dhambi Zako” (Liahona, Mei 2016, 59–62).

Musa 6:61.Je, tunajifunza nini kuhusu Roho Mtakatifu kutoka kwenye mstari huu?

Musa 6:63.Je, ni baadhi ya vitu gani ambavyo “vinathibitisha juu ya [Kristo]”? (ona pia 2 Nefi 11:4). Fikiria kuwaalika washiriki wa familia kuelezea kitu ambacho wanakiona “mbinguni juu” au “juu ya nchi” ambacho kinawasaidia wao kujifunza kuhusu Yesu Kristo. Kwa mfano, ni kwa jinsi gani miti, mawe, au jua huwakumbusha juu ya Mwokozi? Je, majina haya “maji ya uzima” na “mkate wa uzima” yanatufundisha nini kuhusu Yeye? (Yohana 4:10–14; 6:35).

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “I’ll Go Where You Want Me to Go,” Nyimbo za Kanisa, na. 270.

Kuboresha Kujifunza Binafsi

Tafuta ishara. Katika maandiko, vitu au matukio vinaweza mara nyingi kuwakilisha au kuwa ishara ya ukweli wa kiroho. Ishara hizi zinaweza kustawisha uelewa wako wa mafundisho. Kwa mfano, je, unajifunza nini kutokana na ishara ya macho na udongo wa mfinyanzi katika Musa 6:35?

Picha
Adamu na Hawa pamoja na watoto

Adamu na Hawa Wakiwafundisha Watoto Wao, na Del Parson

Chapisha