Njoo, Unifuate 2024
Januari 1–7: Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo. Kurasa za Utangulizi za Kitabu cha Mormoni


“Januari 1–7: Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo. Kurasa za Utangulizi za Kitabu cha Mormoni” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Nyumbani na Kanisani: Kitabu cha Mormoni 2024 (2024)

“Januari 1–7. Kurasa za Utangulizi za Kitabu cha Mormoni,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2024 (2024)

Picha
Mormoni akiandika kwenye mabamba ya dhahabu

Januari 1–7: Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo

Kurasa za Utangulizi za Kitabu cha Mormoni

Kabla hata hujafikia 1 Nefi mlango wa 1, utatambua kwamba Kitabu cha Mormoni si kitabu cha kawaida. Kurasa zake za utangulizi zinaelezea historia ya nyuma kuliko kitabu kingine chochote—ikijumuisha matembezi ya malaika, maandishi ya kale yaliyozikwa kwa karne nyingi pembeni ya kilima na kijana mdogo akitafsiri kumbukumbu hiyo kwa uwezo wa Mungu. Kitabu cha Mormoni siyo tu historia ya mataifa ya Amerika. Kinatafuta kuwashawishi wote kwamba “Yesu ni Kristo” (Ukurasa wa jina wa Kitabu cha Mormoni), na Mungu Mwenyewe alielekeza namna kilivyoandikwa, kutunzwa na kuweza kupatikana kwetu. Mwaka huu, unaposoma Kitabu cha Mormoni, kusali kuhusu kitabu hicho na kutumia mafundisho yake, utaalika nguvu ya Mwokozi katika maisha yako. Na utahisi msukumo wa kusema, kama wale Mashahidi Watatu walivyofanya katika ushuhuda wao, “Ni ya kustaajabisha machoni [mwangu].”

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Nyumbani na Kanisani

Ukurasa wa Jina wa Kitabu cha Mormoni

Kitabu cha Mormoni kinaweza kuimarisha imani yangu katika Yesu Kristo.

Ukurasa wa jina wa Kitabu cha Mormoni unatoa zaidi ya jina tu. Pamoja na mambo mengine, unaorodhesha madhumuni kadhaa ya kumbukumbu hii takatifu. Tafuta madhumuni hayo kwenye ukurasa wa jina. Maswali kama haya yanaweza kukusaidia wakati ukitafakari: Ni kwa nini tuna Kitabu cha Mormoni? Ni kwa namna gani Kitabu cha Mormoni kiko tofauti na vitabu vingine?

Sasa ingeweza kuwa wakati sahihi wa kutengeneza mpango binafsi au wa kifamilia kwa ajili ya kusoma Kitabu cha Mormoni mwaka huu. Lini na wapi utasoma? Unawezaje kumwalika Roho katika kujifunza kwako? Je, kuna kitu chochote maalumu utakuwa ukikitafuta wakati unapojifunza? Kwa mfano, ungeweza kuangalia vifungu vya maneno ambavyo vinatimiza madhumuni uliyoyapata katika ukurasa wa jina. Ungeweza kuandika orodha ya mistari ambayo inajenga imani yako kwa Yesu Kristo.

Ona pia 2 Nefi 25:26; Mosia 3:5–8; Alma 5:48; 7:10–13; Helamani 5:12; 3 Nefi 9:13–18; 11:6–14; Moroni 10:32–33.

Ahadi ya kinabii. Rais Russell M. Nelson alisema, “Ninaahidi kwamba unapotafakari kile unachojifunza [katika Kitabu cha Mormoni], madirisha ya mbinguni yatafunguka na utapokea majibu ya maswali yako na mwongozo katika maisha yako” (“Kitabu cha Mormoni: Maisha Yako Yangekuwaje Bila Hicho?,” Liahona, Nov. 2017,62–63).

Picha
ikoni ya seminari

Dibaji ya Kitabu cha Mormoni; “Ushuhuda wa Mashahidi Watatu”; “Ushuhuda wa Mashahidi Wanane

Ninaweza kuwa shahidi wa Kitabu cha Mormoni.

Roho Mtakatifu anaweza kukushuhudia kwamba Kitabu cha Mormoni ni cha kweli, hata kama hukuyaona mabamba ya dhahabu kama vile wale Mashahidi Watatu na Mashahidi Wanane walivyoyaona. Unaposoma maneno yao, fikiria jinsi gani shuhuda zao zinaimarisha ushuhuda wako.

Je, ni kitu gani kinakuvutia kuhusu jinsi mashahidi hawa walivyoshiriki shuhuda zao juu ya Kitabu cha Mormoni? Tafakari jinsi unavyoweza kushiriki ushuhuda wako juu ya Kitabu cha Mormoni—hasa ushuhuda wa kitabu juu ya Yesu Kristo. Kwa mfano, vuta taswira kwamba unazungumza na rafiki ambaye hapo kabla hakuwahi kusikia kuhusu Kitabu cha Mormoni. Utamwambia nini kuhusu Kitabu hicho? Je, ungewezaje kumshawishi rafiki yako akisome? Fikiria kupitia upya Dibaji ya Kitabu cha Mormoni. Ungeweza kupata maelezo ambayo yangekusaidia katika kushiriki na rafiki yako. Video zifuatazo pia zingeweza kukupa mawazo.

Fikiria kutengeneza orodha ya vitu ambavyo ungeshiriki na rafiki kuhusu Kitabu cha Mormoni. Jaribu kushiriki Kitabu cha Mormoni kwa kutumia aplikesheni ya Kitabu cha Mormoni

Ona pia Ronald A. Rasband, “Hivi Leo,” Liahona, Nov. 2022, 25–28; Mada za Injili, “Kitabu cha Mormoni,” Gospel Library; “Lo! Mlimani Kumora,” Nyimbo za Dini, no. 9.

Picha
Joseph Smith na Mashahidi Watatu wakisali pamoja

Mashahidi Watatu wakitoa ushuhuda juu ya Kitabu cha Mormoni.

Ushuhuda wa Nabii Joseph Smith

Ujio wa Kitabu cha Mormoni ulikuwa muujiza.

Kama mtu angekuuliza Kitabu cha Mormoni kilitoka wapi, ungesema nini? Ni kwa jinsi gani ungeeleza uhusika wa Mungu katika kutupatia Kitabu cha Mormoni? Unaposoma ushuhuda wa Joseph Smith, kuwa makini kwenye jinsi anavyouelezea. Kulingana na ulichosoma, je, unadhani Mungu anahisi nini kuhusu umuhimu wa Kitabu cha Mormoni?

Ona pia Ulisses Soares, “Ujio wa Kitabu cha Mormoni,” Liahona, Mei 2020, 32–35; Watakatifu, juzuu ya. 1, Bendera ya Ukweli, 21–30; Gospel Topics Essays, “Book of Mormon Translation,” Gospel Library.

Kwa mawazo zaidi, ona toleo la mwezi huu la Liahona na magazeti ya Kwa ajili ya Nguvu kwa Vijana.

Mawazo kwa ajili ya Kuwafundisha Watoto

Ukurasa wa Jina wa Kitabu cha Mormoni

Kusoma Kitabu cha Mormoni kunanisaidia niwe na imani katika Yesu Kristo.

  • Waruhusu watoto wako waangalie na kushika nakala ya Kitabu cha Mormoni. Wasaidie waoneshe kichwa kidogo cha habari Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo. Ungeweza pia kuwasaidia wapate, kwenye ukurasa wa jina, kirai “Yesu ndiye Kristo, Mungu wa Milele, akijidhirihisha mwenyewe kwa mataifa yote.” Wasaidie waelewe kwamba Kitabu cha Mormoni hufundisha kuhusu Yesu Kristo. Kwa ufupi waambie jinsi gani Kitabu cha Mormoni kimeimarisha imani yako katika Yesu Kristo. Pia ungeweza kuwauliza kuhusu hadithi zao pendwa za Kitabu cha Mormoni. Kuimba “Book of Mormon Stories” (Kitabu cha Nyimbo za Watoto, 118–19) kungeweza kuwakumbusha baadhi ya hadithi hizo.

Dibaji ya Kitabu cha Mormoni

Kitabu cha Mormoni ni jiwe la katikati la tao la dini yetu.

  • Ukurasa wa shughuli ya wiki hii pamoja na picha vinaweza kuwasaidia watoto wako waelewe maneno haya ya Joseph Smith kwenye dibaji ya Kitabu cha Mormoni: “Kitabu cha Mormoni [ni] jiwe la katikati la tao la dini yetu.” Ingeweza pia kuwa ya kufurahisha kutengeneza au kuchora tao likiwa na jiwe la katikati kwa juu. Je, nini kinaweza kutokea iwapo jiwe la katikati la tao litatolewa? Nini kingetokea kama tusingekuwa na Kitabu cha Mormoni? Mngeweza kusoma kwa pamoja aya ya mwisho ya dibaji ili kupata kitu kingine tunachoweza kujifunza wakati tunapoukubali ukweli wa Kitabu cha Mormoni. Tunawezaje kufanya Kitabu cha Mormoni kiwe jiwe la katikati la tao la imani yetu kwa Yesu Kristo?

Picha
tao la mawe likiwa limeshikiliwa na jiwe la katikati mahala pake

Kitabu cha Mormoni ni jiwe la katikati la tao la dini yetu.

Ushuhuda wa Mashahidi Watatu”; “Ushuhuda wa Mashahidi Wanane

Ninaweza kuwa shahidi wa Kitabu cha Mormoni.

  • Ili kuwasaidia watoto wako waelewe kinachomanishwa kuwa shahidi, ungeweza kuwaeleza kitu ambacho umewahi kukiona ambacho wao hawajawahi. Kisha waruhusu na wao wafanye vivyo hivyo kwako. Hii ingeweza kuwapeleka kwenye mazungumzo kuhusu watu 11 walioyaona mabamba ya dhahabu ambayo kwayo Kitabu cha Mormoni kilitafsiriwa. Mnaposoma shuhuda kwa pamoja, ungeweza kuzungumza kuhusu kwa nini mashahidi hawa walitaka watu wengine wajue kuhusu shuhuda zao. Nani tunataka kumwambia kuhusu Kitabu cha Mormoni?

Ushuhuda wa Nabii Joseph Smith

Kitabu cha Mormoni kilitolewa kwetu kwa nguvu ya Mungu.

Kwa ajili ya mawazo zaidi, ona toleo la mwezi huu la gazeti la Rafiki.

Picha
Joseph akipokea mabamba ya dhahabu kutoka kwa Moroni

Moroni Anakabidhi Mabamba ya Dhahabu, na Gary L. Kapp

Chapisha