Agano la Kale 2022
Agosti 15–21. Zaburi 49–51; 61–66; 69–72; 77–78; 85–86: “Nami Nitayatangaza Aliyonitendea Roho Yangu”


“Agosti 15–21. Zaburi 49–51; 61–66; 69–72; 77–78; 85–86: ‘Nami Nitayatangaza Aliyonitendea Roho Yangu,’” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: Agano la Kale 2022 (2021)

“Agosti 15–21. Zaburi 49–51; 61–66; 69–72; 77–78; 85–86,” Njoo, Unifuate—Kwa Ajili ya Watu Binafsi na Familia: 2022

Picha
Yesu akiwa ameshikilia kandili

Kuokoa Kile Ambacho Kilipotea, na Michael T. Malm

Agosti 15–21

Zaburi 49–51; 61–66; 69–72; 77–78; 85–86

“Nami Nitayatangaza Aliyonitendea Roho Yangu”

Muhtasari huu unafafanua baadhi ya mada za kimafundisho zilizoelezewa katika zaburi. Unaposoma, baadhi ya maneno, picha, au mawazo yanaweza kujitokeza kwako. Je, unahisi Bwana anajaribu kukufundisha nini?

Andika Misukumo Yako

Waandishi wa Zaburi walishiriki hisia binafsi za ndani katika mashairi yao. Waliandika kuhusu hisia za kukata tamaa, hofu, na majuto. Kwa wakati fulani, walionekana hata kuhisi wametelekezwa na Mungu, na baadhi ya zaburi zinabeba sauti ya kuvunjika moyo au kukatishwa tamaa. Kama uliwahi kuwa na hisia kama hizi, kusoma Zaburi kunaweza kukusaidia kujua kwamba sio wewe pekee. Lakini pia utaona zaburi ambazo zinaweza kukutia moyo unapokuwa na hisia kama hizo, kwa sababu watunga zaburi pia walimtukuza Bwana kwa wema Wake, walishangazwa na nguvu Zake, na kufurahi kwa huruma Yake. Walijua kwamba dunia imekithiri kwa maovu na dhambi ila kwamba Bwana ni “mwema, na amekuwa tayari kusamehe” (Zaburi 86:5). Walielewa kwamba kuwa na imani katika Bwana haina maana kwamba kamwe hutapambana na mahangailo, dhambi, au woga. Inamaanisha kwamba unajua nani wa kumwendea unapokuwa katika nyakati hizo.

Picha
ikoni ya kujifunza binafsi

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Binafsi Maandiko

Zaburi 49; 62:5–12

Ukombozi huja kwa njia ya Yesu Kristo pekee.

Zaburi 49 ina ujumbe kwa ajili ya “wote wakuu na wadogo, tajiri na maskini” (mstari wa 2). Ungeweza kusema ujumbe huu ni nini? Unahisi ni nini Zaburi 62:5–12 inaongeza katika ujumbe huo?

Kusoma zaburi hizi kunaweza kukushawishi kutafakari jinsi ambavyo baadhi ya watu huweka imani yao katika kitu kingine badala ya Mungu kwa ajili ya ukombozi (ona Zaburi 49:6–7). Ni kwa jinsi gani maisha yako yameshawishiwa na ushuhuda wako kwamba “Mungu atakomboa nafsi [yako], Ataitoa mkononi mwa kuzimu”? (mstari wa 15).

Ona pia Mithali 28:6; Alma 34:8–17.

Zaburi 51; 85–86

Kwa sababu ya huruma ya Mwokozi, ninaweza kusamehewa dhambi zangu.

Maombi ya huruma katika Zaburi 51 ni sifa za Mfalme Daudi, ambaye alikuwa na hatia ya uzinzi na mauaji (ona 2 Samweli 11). Hata kama dhambi zetu sio nzito sana, tunaweza kujihusisha na huruma iliyoelezewa katika zaburi hii. Tunaweza kujifunza pia kuhusu kile inachomaanisha kutubu. Kwa mfano, ni maneno gani au virai gani katika Zaburi 51 vinakufundisha wewe kuhusu tabia tunayohitaji ili kutubu? Unajifunza nini kuhusu matokeo ambayo Upatanisho wa Mwokozi unaweza kuleta katika maisha yako?

Unaweza kujiuliza swali hilohilo unaposoma Zaburi 85–86. Ungeweza pia kutafuta virai ambavyo vinamwelezea Bwana. Ni kwa jinsi gani virai hivi vinaimarisha imani yako kwamba Yeye atakusamehe? (ona, kwa mfano, Zaburi 86:5, 13, 15).

Ona pia Alma 36; Russell M. Nelson, “Tunaweza Kufanya Vyema na Kuwa Bora,” Liahona, Mei 2019, 67–69; Carole M. Stephens, “Bwana Mponyaji,” Liahona, Nov. 2016, 9–12.

Zaburi 51:13–15; 66:16–17; 71:15–24

Ushuhuda wangu wa Yesu Kristo unaweza kuwasaidia wengine kuja Kwake.

Tafakari jinsi ulivyopata ushuhuda wako wa Yesu Kristo na nguvu zake za upatanisho. Kisha, unapojifunza, Zaburi 51:13–15; 66:16–17; 71:15–24, fikiria namna unavyoweza kuwaalika wengine “kuja na kuyatazama matendo ya Mungu” (Zaburi 66:5). Inamaanisha nini kwako “kusimulia haki [Yake] mchana kutwa.”? (Zaburi 71:24). Utawaambiaje wengine yale “aliyoitendea roho [yako]”? (Zaburi 66:16).

Ona pia Mosia 28:1–4; Alma 26.

Picha
wavulana wawili wakizungumza

Tunaweza kushiriki na wengine shuhuda zetu za kile ambacho Bwana amekifanya kwa ajili yetu.

Zaburi 63; 69; 77–78

Bwana atanisaidia katika uhitaji wangu wa haraka.

Zaburi nyingi zinaeleza, katika lugha ya wazi, vile ilivyo kuhisi kuwa mbali na Mungu na kuhitaji msaada Wake kwa kiasi kikubwa. Unaweza kufikiria kuangalia maelezo kama haya katika Zaburi 63:1, 8; 69:1–8, 18–21; 77:1–9. Unapata nini katika Zaburi 63; 69; 77–78 ambacho kiliwapa hawa watunga zaburi uhakika?

Unapokuwa na dhiki, ni kwa jinsi gani “kukumbuka matendo ya Bwana” na “maajabu Yake ya kale” kunakusaidia? (Zaburi 77:11). Baadhi ya maajabu haya yanaelezwa katika Zaburi 78. Wakati unapoyasoma, tafakari kile kinachokusaidia “umwekee Mungu tumaini [lako]” (mstari wa 7). Ni uzoefu gani kutoka kwenye historia ya familia yako unakupa msukumo?

Picha
ikoni ya kujifunza kama familia

Mawazo kwa ajili ya Kujifunza Maandiko kama Familia na Jioni ya Nyumbani

Zaburi 51:17.Fikiria ni kwa jinsi gani unaweza kuifundisha familia yako kile inachomaanisha kuwa na moyo uliovunjika. Kwa mfano, wanafamilia wangeweza kufanya zamu kuvunja kitu ambacho kina ganda gumu, kama yai au nazi. Ni kwa jinsi gani wakati mwingine mioyo yetu ni kama hilo ganda? Ni kwa jinsi gani tunaweza kufungua mioyo yetu kwa Bwana? Kusoma Zaburi 51 kwa pamoja kunaweza kutoa baadhi ya mawazo.

Zaburi 61:2–3.Wanafamilia wanaweza kufurahia kuchora picha za ishara katika mistari hii na kujadili jinsi gani Yesu Kristo ni kama “mwamba,” mrefu “kimbilio [letu],” na ngome yenye nguvu.”

Zaburi 71:17; 78:5–7.Bwana anakutaka wewe … uwajulishe nini wana [wako]”? (Zaburi 78:5). Labda kila mwanafamilia angeweza kushiriki mfano wa “matendo ya ajabu ya Bwana,” kama vile hadithi za maandiko, uzoefu, au ushuhuda binafsi, unaowasaidia “wamwekee Mungu tumaini lao” (Zaburi 71:17; 78:7).

Zaburi 72.Zaburi 72 iliandikwa na Daudi kuhusu mwanae Sulemani, ila mengi yake pia yanaweza kumhusu Yesu Kristo. Familia yako inaposoma zaburi hii, wangeweza kuinua picha ya Mwokozi wanapopata mistari ambayo inawakumbusha juu ya Yesu Kristo. Ni kwa jinsi gani tunaweza kusaidia kutimiza matamanio kwamba “dunia yote na ijae utukufu wake”? (Zaburi 72:19; ona pia Mafundisho na Maagano 65:2).

Zaburi 85:11.Mstari huu ungeweza kuleta msukumo wa mjadala kuhusu matukio ya Urejesho wa injili—jinsi gani Kitabu cha Mormoni ni ukweli ambao “[ulienezwa] kutoka duniani” na jinsi wajumbe wa mbinguni “walivyoshuka kutoka mbinguni” (ona pia Musa 7:62). Video ya “Preparation of Joseph Smith: Tutored by Heaven” (ChurchofJesusChrist.org) inaonyesha baadhi ya matukio haya.

Kwa mawazo zaidi kwa ajili ya kuwafundisha watoto, ona muhtasari wa wiki hii katika Njoo, Unifuate—Kwa ajili ya Msingi.

Wimbo uliopendekezwa: “I Need Thee Every Hour,” Nyimbo za Kanisa, na. 98.

Kuboresha Ufundishaji Wetu

Tumia utofauti. “Tafuta jinsi unavyoweza kuongeza utofauti katika juhudi zako za kufundisha injili. Kufanya hivyo kutaongeza utajiri na uzuri kwenye uzoefu. … Zingatia jinsi matumizi ya muziki, hadithi, picha na aina nyingine za sanaa kunavyoweza kumwalika Roho” (Kufundisha katika Njia ya Mwokozi, 22).

Picha
mtu akiwa amepiga magoti mbele ya Yesu

Usitie Shaka, Tomaso, na J. Kirk Richards

Chapisha