2023
Kubadili Mtazamo Wangu Uwe kwenye Kupokea Ushuhuda
Julai 2023


“Kubadili Mtazamo Wangu Uwe kwenye Kupokea Ushuhuda,” Liahona, Julai 2023.

Vijana Wakubwa

Kubadili Mtazamo Wangu Uwe kwenye Kupokea Ushuhuda

Kwa mara ya kwanza nilikuwa na mbegu ya kawaida ya imani ambayo ilikuwa halisi.

Picha
vifaa mbalimbali vya bustanini, ikijumuisha mmea wa kwenye kopo ulioshikiliwa kwa mikono miwili

Nimekulia ndani ya Kanisa—nilihudhuria shughuli, na nilishiriki katika maombi ya familia na kujifunza maandiko. Lakini kiukweli sikuwa na ushuhuda. Sikujua kama nilikuwa naamini katika Mungu au Mwana Wake. Sikujua kama Kitabu cha Mormoni ni cha kweli.

Nilihitaji ushuhuda, lakini nilihisi kuchanganyikiwa baada ya kusali mara nyingi bila kuhisi kama nilipokea jibu. Nilianza kujiuliza, “Kama Mungu ni halisi, kwa nini Yeye hanionyeshi? Kwa nini Yeye anaruhusu nikae hapa nikijiuliza?”

Nikiangalia nyuma, inaweza kuona vyema kwa nini nilikuwa sipati jibu: sikuwa naweka jitihada za dhati. Ningesoma maandiko yangu kwa dakika tano mara moja kwa wiki na kutegemea uzoefu wa ufunuo kisa tu niliuomba.

Sikuelewa kwamba imani ni kanuni ya tendo.

Mbegu ya Imani

Kila mtu aliyenitazama kwa nje angeniita “hai” ndani ya Kanisa, lakini bado sikujua kama Kanisa ni la kweli. Lakini nilitaka kujua.

Hivyo niliamua kutumikia misheni. Nilidhania kimakosa kwamba kama mmisionari, ningepokea majibu tu kutoka kwa Mungu. Bado sikuweka jitihada kubwa kwenye kusali au kujifunza, lakini muda sio mrefu nilikuwa na kazi yangu ya kufanya.

Mwanzoni mwa misheni yangu, nilipambana kumhisi Roho wakati nikipata mafunzo mtandaoni wakati wa janga la Uviko kwa sababu ya juhudi zangu nusu. Lakini baadaye nilienda kituo cha mafunzo cha umisionari mimi mwenyewe. Na muda wangu hapo ulikuwa ni uzoefu mkubwa wa kiroho wa maisha yangu. Ilikuwa ni mara ya kwanza kuwa na mbegu ya kawaida ya imani ambayo ilikuwa halisi.

Kuleta Badiliko

Hatimaye kuanza kazi ya misheni ilikuwa vigumu. Nilihisi kama ushuhuda mdogo nlioupata umepotea.

Siku moja nilikua nalia na kisha kumbukumbu ikaja kichwani mwangu. Baba yangu alizoea kuniuliza siku yangu shuleni ilikuwaje, na daima nilisema ilikuwa mbaya. Na angesema, “Hiyo ni kwa sababu umeifanya iwe mbaya. Kama unataka shule kuwa ya furaha, tengeneza furaha hiyo mwenyewe.” Nilitambua kwamba ningeweza kuutumia muda wangu mwingi wa misheni yangu kujifunza na kukua au wa kuwa wa taabu.

Hivyo nilisali kwa dhati zaidi kuliko awali ili kumwambia Baba wa Mbinguni kwamba nitajaribu na kubadili mtazamo wangu. Baada ya hilo, nilihamasika kuweka jitihada mpya. Nilianza kujifunza na kusali kwa dhati na kutafakari, na baada ya muda ule ushuhuda mdogo ulirejea— na ulizidi kukua. Sikuchanganyikiwa sana, na nilianza kupata shangwe katika injili.

Kile Tunachotoa Ndicho Tunachopata

Unapokuwa umekanganyikiwa na hisia kama imani yako haikui, unaweza kujiuliza kama Mungu yupo na kama Yeye anajali. Lakini nimejifunza kwamba daima yupo pamoja nasi na atatusaidia kuimarisha imani yetu na ushuhuda kama tutabeba jukumu na kuweka jitihada (ona Moroni 10:4).

Mzee Robert D. Hales (1932–2017) wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili alisema, “Japo inaonekana kutokuwepo kwa kanuni muafaka ambayo kwayo kila mmoja wetu hupokea ushuhuda, inaonekana kuna mfumo tunaoutambua.”1 Mfumo huo huhusisha kuwa na hamu ya dhati ya kujua ukweli, kuomba, kuwa radhi kutumikia popote tuitwapo, kujitahidi kuwa watiifu, kujifunza maandiko na kuyatumia katika maisha yetu na kuwa na mtazamo wa unyenyekevu.

Kamwe nisingeimarisha imani yangu bila kubadili mtazamo wangu, kufuata mfumo huu, na kuweka moyo wangu wote katika kuunganika na Baba wa mbinguni na Yesu Kristo. Nilipofanya mabadilio hayo, nilianza kupokea majibu na kuamini kweli.

Dada Rebecca L. Craven, Mshauri wa Pili katika Urais Mkuu wa Wasichana, hivi karibuni alisema: “Kuwa mfuasi wa Yesu Kristo hujumuisha zaidi ya kutumaini au kuamini. … Inahitaji kwamba tufanye kitu.”2 Nimejifunza mimi mwenyewe kuwa hili ni kweli: kile ninachoweka kwenye injili ndicho ninachovuna.

Kwa watazamaji, kiwango cha uhai wangu ndani ya Kanisa huenda kikaonekana kuwa sawa kama kilivyokuwa awali. Lakini nimebadili dhamira yangu kwenye injili ndani ya moyo wangu. Na hilo limeleta tofauti yote.

Mwandishi anaishi Washington, Marekani.

Mihutasari

  1. Robert D. Hales, “The Importance of Receiving a Personal Testimony,” Ensign, Nov. 1994, 21–22.

  2. Rebecca L. Craven, “Fanya Chenye Umuhimu Zaidi,” Liahona, Mei 2022, 62.

Chapisha