2023
Uwezo wa Kuinua
Machi 2023


“Uwezo wa Kuinua,” Liahona, Machi 2023.

Miujiza ya Yesu

Marko 5:22–24, 35–42

Uwezo wa Kuinua

Tunaweza kusaidia kuwainua wale wanaongojea ukombozi wa Mwokozi.

Picha
watu wakigusana mikono

Tumeshindwa. Tena. Nilijibamiza kwenye kiti changu kichwa changu kikiwa kimeinamishwa. Nilikuwa mtazamaji tu, lakini bado sikuwa na nguvu ya kusimama. Timu yetu ilikuwa imejaribu sana. Baadhi walikuwa na michubuko. Baadhi walikuwa wakichechemea wakati wakitoka nje ya uwanja. Baada ya kupoteza kulikofuatana kwa timu yetu ya soka ya shule ya upili ya juu, si tu tulikuwa tumefungwa—mioyo yetu ilikuwa imevunjika.

Katika njia sawa na ile kukata kwangu tamaa kulivyoonekana kunizidia, mmoja wa wasichana mdogo kabisa kwenye timu alipiga hatua mbele yangu. Nilivutwa ghafla kwenye mtazamo wa lengo niliouona kwenye uso wake.

Nilitazama wakati kila hatua chache alizopiga alinyosha mkono kwa kila msichana, lakini si kwa utambuzi wa kushindwa. Badala yake, alikuwa akitoa sifa, faraja na huruma kwa kila mtu mmoja mmoja. “Sijawahi kukuona ukikimbia vile ili kufikia kila pasi ya mpira. Huo ulikuwa mchezo wako bora kabisa.” Na kwa mwingine, “Wao!, mchezo mzuri sana. Hakika, leo umecheza kweli!”

Kwa kila pongezi ya kugonga mikono, mkono wake mmoja ulikaa kwa muda mrefu kwenye mikono yao, wakati mkono wake mwingine ukiwa begani au taratibu ukigusa mguu uliochubuka na uliochafuliwa kwa nyasi. Niliweza kuhisi kwamba alibeba kitu ndani yake, uwezo ambao kwa kiasi fulani ulihamishwa kutoka kwake kwenda kwenye moyo wa kila mshiriki wa timu. Tabasamu zilianza kupenya kupitia hisia za maumivu na kukata tamaa. Taratibu, mmoja mmoja, kila mchezaji alisimama akiwa na hisia mpya ikijidhihirisha mahala pale.

Nani alijali kuhusu michubuko na maumivu? Nani alijali kuhusu hasira na kukatishwa tamaa? Hakuna hata mmoja. Lakini ni kwa jinsi gani mkono tu umwinue mtu kutoka mahali pa mateso hadi mahali penye lengo na nguvu?

Niruhusu nishiriki baadhi ya mambo niliyojifunza kuhusu uwezo wa Mwokozi wa kuinua na jinsi tunavyoweza kusaidia, kama vile rafiki yangu kwenye timu ya soka.

Katika Agano Jipya, tunasoma maelezo yafuatayo kuhusu binti wa Yairo.

“Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona [Yesu], akaanguka miguuni pake,

“Akimsihi sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona, na kuishi.

“Akaenda pamoja naye” (Marko 5:22–24).

“Akaenda pamoja naye”

Ninapenda mstari “Akaenda pamoja naye” (Marko 5:24). Muujiza ulikuwa haujatendeka bado. Hakika, kungekuwepo na uchelewaji mkubwa kabla familia haijapokea ukombozi ambao waliuomba. Lakini Kristo tayari alikuwa safarini pamoja nao.

Wakati tunapohitaji kile ambacho hatuwezi kujifanyia wenyewe, tunaweza kutumaini kwamba Yesu anakuja. Na tunaweza kutumaini kwamba tunapongojea muujiza Wake kwa imani katika maisha yetu au maisha ya wapendwa wetu, Yeye atatembea nasi. Atatembea nasi safari yote kupita wasiwasi na hofu na huzuni ambayo yaweza kuwa inatungojea kwenye njia inayoongoza kwenye ukombozi.

“Uweke mkono wako juu yake”

Uponyaji si juu yetu kuutoa, lakini kama vile Yairo, tunaweza kumleta Yesu Kristo, Mponyaji Mkuu, kwa wale tunaowapenda. Yairo alijua kwamba mikono ya Mwokozi ingeweza kumwinua mtu kutoka mahala pa mateso hadi mahala penye lengo na nguvu.

Nililiona hilo kwenye mcheza soka wetu mleta nuru. Alikuwa akishiriki nuru ya Kristo kwenye uwanja wa soka na akimruhusu alete uponyaji Wake. Kwa kuinua juu nuru Yake, alikuwa akisaidia kuikusanya Israeli.

Kila mmoja wetu atahitaji uwokozi kutoka kwa mtu tofauti na sisi. Licha ya hilo kuonekana kutuacha wahanga, tunaweza kutumaini kwamba Baba wa Mbinguni alimtoa Mwokozi ambaye anaweza kusaidia kutuinua kutoka kwenye kukata tamaa. Na tunaweza kushiriki pamoja Naye, kama vile alivyofanya shujaa wangu wa soka.

Lakini vipi ikiwa mambo yanakuwa mabaya tu wakati unangojea baraka Zake zije?

“Kwani kuzidi kumsumbua Mwalimu?”

Wakati Kristo akitembea kuelekea kwenye nyumba ya Yairo, alikawizwa njiani. Mtaa ulikuwa umejaa watu na alipojaribu kupenya, mwanamke mwenye imani kuu, ambaye naye pia alingojea mkono Wake wa uponyaji, aligusa mavazi yake.

“Maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona.

“Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule” (Marko 5:28–29).

Ni hofu kiasi gani alikuwa nayo Yairo? Ni jinsi gani alikasirishwa na kukawia kule? Wakati alipoondoka nyumbani kwake, binti yake alikuwa tayari katika hali ya kufa. Kisha, wakati Mwokozi alipokuwa akimtafuta mwanamke aliyeponywa na kuzungumza naye, mtu kutoka nyumbani kwa Yairo aliwasili akiwa na habari mbaya: “Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua Mwalimu?” (Marko 5:35).

Ni baraka iliyoje kwa mwanamke aliyesubiri kwa muda mrefu! Lakini ni msiba ulioje kwa Yairo na familia yake, ambao hawakuwa na muda wa kusubiri! Nyakati zingine wakati tupo katika kusubiri, inaweza kuwa vigumu kuendeleza tumaini Kwamba Yeye anakuja. Lakini kwa Yairo na familia yake, ilionekana walikuwa wamechelewa kuendeleza tumaini kwamba Yeye anakuja. Binti yake alikuwa amekufa. Kwani kuzidi kumsumbua Mwalimu?

Kwa nini? Kwa sababu ukomo ambao wakati mwingine tunauweka kwenye miujiza ya Mwokozi hauna maana yoyote. Yeye hafungwi na ukomo wa muda, wala uwezo Wake hauzuiliwi kwa uelewa wetu wa kile kinachowezekana.

Ikiwa tutatazama kwa macho ya imani wakati tukisubiri, tutaona hakikisho kwamba ukombozi Wake unakuja (ona Alma 58:11). Hakikisho hili linaweza kuibadili mioyo yetu na kuthibitisha imani yetu Kwake. Hata ikiwa inaonekana kana kwamba fursa imepita, Yeye bado anakuja; wakati wako utafika.

Picha
Yesu anamfufua binti wa Yairo

Kumfufua Binti wa Yairo, na Gabriel Max / Peter Horree / Alamy Stock Photo

“Usiogope, amini tu”

Punde pale Mwokozi aliposikia habari mbaya, alimwambia Yairo, “Usiogope, amini tu” (Marko 5:36). Maneno ya Mwokozi kwa Yairo yalionesha jinsi Mwokozi anavyotamani kutupatia hakikisho katika kusubiri. Huduma Yake haipumziki, hata kama sisi tunapumzika. Yeye kwa haraka alimhimiza Yairo kusonga mbele katika imani.

“Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. …

“Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka.” (Marko 5:39, 41).

Umesikia hilo? Yesu alimshika msichana kwa mkono.” Uwezo upo mwikononi mwake. Rais Howard W. Hunter (1907–95) aliwahi kusema, “Chochote ambacho Yesu anakigusa kinaishi.”1 Ni kipi tunaweza kufanya vizuri zaidi ili tupokee mkono Wake wa uponyaji? Na tunawezaje kuwa mikono Yake ili kusaidia kuwainua wengine katika wakati wao wa maumivu na kukata tamaa?

“Mara akasimama yule kijana, akaenda”

Papo hapo maisha yalirejea kwa binti wa Yairo: “Mara akasimama yule kijana, akaenda” (Marko 5:42). Maisha ya duniani yataleta vitanda ambavyo lazima tuamke kutoka kwenye vitanda hivyo. Kwa kila mmoja wetu, vitanda hivyo vitaonekana tofauti kidogo—kuanzia kukata tamaa baada ya kupoteza uwanjani hadi kumpoteza mpendwa wetu. Mateso bila shaka yatakuja. Lakini kamwe Yeye hawezi kutuacha, licha ya hali kuwa mbaya au kufika kikomo. Nyakati zingine, Yeye huturuhusu tutembee kupita sehemu zisizo na uhai ama zenye ukiwa ili aweze kuunyosha mkono Wake na kuzijaza kwa uhai.

Kwa ishara ya Upatanisho Wake—alama za misumari katika kila mkono—Yeye anatuonesha kwamba sisi ndiyo huduma Yake: “Tazama, nimekuchora viganjani mwa mikono yangu” (1 Nefi 21:16). Huduma ya Kristo ilikuwa, ni, na daima itakuwa kutuinua kutoka kifo ambacho hatuwezi kukiepuka kimwili na kiroho na yote yanafanywa yawezekane kupitia dhabihu Yake ya upatanisho.

Wakati maumivu na changamoto kama hizo zinapotokea, tunaweza kuvuta taswira ya mikono iliyo na alama kwenye kila kiganja ikileta si tu ukarimu na upendo bali uwezo wa kushinda. Kwa kuonesha imani Kwake, urejesho kamili wa Mkombozi wa ulimwengu utashinda juu ya chochote tunachokabiliana nacho.

Na tunaweza kufanya kile ambacho angefanya kwa wengine wanaohitaji mguso Wake.

Ninashuhudia kwamba kila mmoja wetu atainuliwa kutoka kwenye udhaifu wetu na hatimaye kutoka kaburini. Kumbuka, hata kama yote yanaonekana kupotea, Yeye yupo na huinyosha mikono Yake yenye uwezo wa kuokoa. Fikiria shangwe itakayokuja wakati anaponyosha mikono Yake kwako na kutangaza, “nakuambia, Inuka.” Na hakika tutainuka.

Muhtasari

  1. Teachings of Presidents of the Church: Howard W. Hunter (2015), 150.

Chapisha