2023
Kuhudumu kwa Maarifa Makubwa Zaidi
Januari 2023


“Kuhudumu kwa Maarifa Makubwa Zaidi,” Liahona, Jan. 2023.

Kanuni za Kuhudumu

Kuhudumu kwa Maarifa Makubwa Zaidi

Huna haja ya kuwa na majibu yote, lakini kuja kumjua Yeye vyema zaidi kutatusaidia kuhudumu kama Mwokozi alivyohudumu.

Picha
kijana Yesu hekaluni

Maelezo ya kina kutoka Kristo akiwa Hekaluni, na Heinrich Hofmann

Yesu Alituonyesha Mpangilio wa Kujifunza

Mwokozi alipokuwa akikua, “aliongezeka nguvu, akajaa hekima: na neema ya Mungu ilikuwa juu yake” (Luka 2:40). Neno kuongezeka linamaanisha kukua pole pole, kama mwezi unavyokua na kukamilika baada ya mwendo wa mwezi. Luka anaongeza kwamba “Yesu aliongezeka katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu” (Luka 2:52). Yesu hakuweza ghafla tu kuwa na utimilifu wa maarifa—Aliyapata hatua kwa hatua (ona Mafundisho na Maagano 93:12–14).

Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, wazazi wake walimkuta ndani ya hekalu—sehemu muhimu ya kuabudu huko Yerusalemu—”akiwa amekaa katikati ya wasomi, wakimsikiliza na kumwuliza maswali” (Tafsiri ya Joseph Smith, Luka 2:46 [katika Luka 2:46, tanbihi c]). Kwa sababu kujifunza kumekuwa sehemu muhimu ya kukua Kwake, wakati fursa ilipokuja kuwafundisha wale waliokuwa ndani ya hekalu, Alikuwa amejiandaa. Mafundisho yake pale yalikuwa na matokeo ya kushangaza kwao na kwa wazazi Wake.

Kutumia Maarifa katika Kuhudumu

Hapa kuna njia tatu ambazo kukuza sifa kama ya Kristo ya maarifa kunaweza kutusaidia katika kuhudumu kwetu.

  1. Tunapokuja kumjua Mwokozi na kujifunzaa kuhusu sifa Zake, tutajua vizuri zaidi nini Yeye angefanya kuhudumu katika sehemu zetu.

  2. Tunapoongezeka katika maarifa na uelewa wa injili, tutakuwa katika nafasi nzuri kwa ajili ya Roho Mtakatifu kuleta kwenye kumbukumbu yetu kile tunachohitaji wakati tunapokihitaji (ona Yohana 14:26). Hii inaweza kutusaidia kuelewa mahitaji ya wale tunaowahudumia na kujibu maswali au mashaka yao.

  3. Tunapoongeza uwezo wetu wa kujifunza, tutakuwa wazuri zaidi kwenye kuweza kuungana na, au kuwahudumia wengine. Tunaweza kujifunza zaidi kuhusu somo la kutuunganisha na rafiki ambaye analipenda somo hilo pia. Au tunaweza kujifunza mbinu fulani ambazo zingeweza kusaidia kutatua shida.

Kupata maarifa kunaweza kutusaidia kuhudumu katika njia nyingi. Kwa nyongeza, “kanuni yoyote ya akili tunayoipata katika maisha haya, itafufuka pamoja nasi katika ufufuko” (Mafundisho na Maagano 130:18).

Picha
vijana wakubwa wakijifunza maandiko

Kukuza Maarifa

Tunawezaje kukuza sifa kama ya Kristo ya maarifa? Hapa kuna baadhi ya mawazo:

  1. Kumbuka kwamba hata Yesu alijifunza pole pole kwa muda. Kuwa mwenye bidii, lakini kuwa na subira kwako mwenyewe. Kujifunza kunatokea “msitari juu ya msitari, amri juu ya amri” (2 Nefi 28:30).

  2. Jifunze kutambua vyanzo vinavyoaminika vya taarifa. (Ona “Kutafuta ukweli katika Zama za Upotoshwaji” katika Liahona) ya kidigitali ya Oktoba 2022.

  3. Kuwa mdadisi. Jifunze kutokana na kile kinachotokea kwenye mazingira yako kila siku. Uliza maswali. Soma vitabu vizuri na uwe mwenye taarifa. (Ona Mafundisho na Maagano 88:79, 118; 90:15.)

  4. Jifunze kwa kujisomea na kwa imani (ona Mafundisho na Maagano 88:118). Uwezo wako wa kuelewa ukweli katika mada yoyote utaboreshwa kwa kuleta pamoja juhudi zako nzuri za kiakili na juhudi zako nzuri mno za kiroho. Ishi vyema ili uweze kuwa na msaada wa Roho Mtakatifu.

Chapisha