2018
Kujisikia Nyumbani Tena
April 2018


Kujisikia Nyumbani Tena

Judy Rascher, Colorado, Marekani

Sikua nimejiandaa kupokea simu ya kaka yangu. “Mama amefariki sasa hivi,” alisema. “Alianguka na kugonga kichwa chake.”

Nilishtuka. Mama yangu alikuwa amefariki, na nilikuwa nimeongea naye usiku wa jana tu. Niliendelea kujiuliza mwenyewe kwa nini hili lilikuwa limetokea. Sikuweza kuelewa kwa nini alikuwa ameniacha. Nilikuwa na hasira! Nilikaa katika hasira yangu kwa wiki kadhaa.

Hatimaye, niliamua nani wa kumlaumu. Ilikuwa ni kosa la Mungu. Alimchukua kutoka kwangu mapema sana. Mama yangu alikosa matukio mengi katika maisha yangu, na nilihisi ni kwa sababu ya Mungu. Sikuwa muumini wa kanisa kwa kipindi kile, lakini nilikuwa Mkristo mwenye kumcha Mungu. Badala ya kumtegemea Mungu kwa ajili ya kupata nguvu, niligeuka mbali Naye na kumfukuza katika maisha yangu.

Nilimkosa sana mama yangu. Nilipokuwa nikikua, nyumba yetu ikiwa na wazazi wangu palikuwa ni mahali salama. Bila kujali wapi nilipokuwa au nini nilichokuwa nikifanya, kila mara nilipozungumza na mama yangu au kutumia muda naye, nilijisikia kuwa nyumbani. Sasa hisia ya “nyumbani” niliyoipenda ilikuwa imetoweka.

Miaka ilipita, na nilipoteza imani yangu karibu yote. Nilijaribu kuelewa kwa nini mama yangu alipaswa kufariki, lakini hakuna kilichonipa amani. Kisha, yapata kama wiki moja, wazo lifuatalo lilikuja kwa kujirudia akilini mwangu: ninahitaji kutazama kuelekea mbinguni kupata uelewa. Nilimwambia rafiki yangu mpendwa hilo ambaye alikuwa muumini wa Kanisa. Aliuliza kama ningependa kujifunza zaidi kuhusu imani yake.

Sikuweza kugundua mara moja, lakini Roho aliamsha nafsi yangu kutoka kwenye usingizi mzito. Kadiri nilivyojifunza kuhusu injili, ndivyo nilivyojisikia zaidi kuwa nimepata sehemu salama tena. Hisia za kuwa ‘nyumbani” zilirudi.

Nilibatizwa mnamo Mei 2013. Ninashukuru kwamba imani yangu imerudi. Simgeuzii Mungu mgongo tena. Badala yake, namkumbatia. Bado ninahuzunishwa na kifo cha ghafla cha mama yangu, lakini kwa sababu ya imani yangu katika Mungu, Ninajua kwamba siku moja Nitakuwa “nyumbani” pamoja na mama yangu na familia yangu milele.

Chapisha