2021
Julia Mavimbela
Mei/Juni 2021


Waanzilishi katika Kila Nchi

Julia Mavimbela

Kiongozi wa Jumuiya huko Afrika Kusini

“Upendo huja tu kwa kuwasamehe wengine.”

Picha
woman standing in garden

Julia alipangusa paji la uso wake. Kisha akaokota koleo lake na akaanza kuchimba. Sasa hivi, ardhi kumzunguka yeye ilikuwa ni rundo la mavumbi. Lakini baada ya muda mfupi itakuwa bustani nzuri sana.

Nyakati zilikuwa ngumu kwa watu Weusi huko Afrika ya Kusini. Sheria huko ziliwaweka Weusi na Weupe kuwa tofauti. Watu wengi Weusi walilazimika kuziacha nyumba zao na kuishi maeneo fulani mbali na watu Weupe, na hawakuweza kupiga kura. Kumekuwa na vurugu huko katika mji ambao Julia aliishi, na shule zilifungwa kwa sababu ya hiyo. Nyakati zingine ilikuwa hatari kukaa nje.

Lakini hilo halikuweza kumzuia Julia. Alitaka kufanya kitu kitakacholeta uzuri katika jumuiya yake. Hii ndiyo sababu alianzisha bustani.

Baadhi ya watoto walimwona Julia akifanya kazi. “Je, tunaweza kusaidia?” waliuliza.

“Ndiyo,” alisema Julia. Akampa kila mmoja koleo. Aliwaonyesha jinsi ya kulegeza udongo na kuyaondoa magugu.

“Tulimeni udongo huu wa chuki, tupande mbegu ya upendo, na tuone ni matunda gani utatupatia,” alisema. “Upendo huja tu kwa kuwasamehe wengine.”

Wiki zilipita, na mimea zaidi ilikua. Watu wengine walikuja kufanya kazi katika ile bustani. Waling’oa magugu marefu. Walipanda mbegu zaidi. Waliimwagilia maji ile mimea. Ilimfanya Julia kuwa na furaha kuona watu wengi sana wakisaidia.

Siku moja Julia alikutana na vijana wawili wa kiume. Julia alishangazwa kwa sababu watu Weupe huja kwa nadra sana katika mitaa yao. Wao walisema walikuwa wamisionari. Aliwaalika kushiriki ujumbe wao nyumbani mwake.

Mwana wa Julia aliposikia kuwa walikuwa wanakuja, alishtuka. “Kwa nini uliwaalika?” alisema. “Wao ni Weupe. Sio salama.”

Lakini Julia aliwaamini wamisionari. “Wanaume hawa wako tofauti,” Julia alisema. “Wao wanahubiri amani.”

Wamisionari walipokuja, Julia aliwakaribisha ndani. Mmoja wao aliitambua picha kwenye joho. Ilikuwa kutoka kwenye harusi ya Julia.

“Huyu ni nani?” mmisionari aliuliza, akionyesha kwenye ile picha.

“Mume wangu, John.” Julia akaangalia chini. “Alifariki dunia katika ajali ya gari.”

Mmisionari alitikisa kichwa “Tunaamini familia zinaweza kuwa pamoja milele, hata baada ya kufariki dunia.”

Hisia ya amani ikamtiririkia Julia. Alijisikia furaha kujifunza kuhusu mpango wa Mungu na aliendelea kukutana na wamisionari hao. Upendo wa injili ulikua katika moyo wa Julia, kama vile tu mimea katika bustani yake. Baada ya muda mfupi aliamua kubatizwa.

Kanisani, Julia alikutana na watu wengi wapya. Wengine walikuwa Weusi. Wengine walikuwa Weupe. Lakini wote walihudumu na kujifunza pamoja.

Julia aliwaonyesha watoto kanisani jinsi ya kusaidia katika bustani yake. “Lazima tuwe laini katika mioyo yetu, kama udongo huu,” alisema. “Lazima tutengeneze nafasi kwa ajili ya injili ndani yetu. Lazima tutengeneze nafasi kwa ajili ya upendo.”

Miaka kumi na mitatu baada ya ubatizo wa Julia, sheria zilizowatenganisha watu Weusi na watu Weupe katika Afika Kusini zilikoma.

Kuna takribani waumini wa Kanisa 70,000 katika Afrika Kusini leo.

Afika Kusini inazo lugha rasmi 11.

Julia alisaidia kuanzisha Women for Peace, kikundi kinachohamasisha umoja na amani katika Afrika Kusini.

Yeye alikuwa mmoja wa wafanyakazi wa hekaluni wa kwanza katika Hekalu la Johannesburg, Afrika ya Kusini.

Julia alikuwa mwalimu. Aliwafundisha watoto kusoma walipokuwa wakifanya kazi katika bustani yake.

Picha
May 2021 Friend
Picha
May 2021 Friend

Chapisha