Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana
Kwa nini mimi Namhitaji Yesu Kristo
Machi 2024


“Kwa nini mimi Namhitaji Yesu kristo,” Kwa Ajili ya Nguvu Kwa Vijana, Machi 2024.

Nguvu katika Uhusiano Wako pamoja Naye

Kwa nini mimi Namhitaji Yesu Kristo

Kuelewa uhusiano wetu na Mwokozi ni muhimu.

Picha
Yesu Kristo akimponya mtu

Mguso wa Bwana, na Kelsy na Jesse Lightweave

“Kwa nini mimi namhitaji Yesu Kristo?” Ni swali muhimu la kujiuliza wewe mwenyewe—sio la “wote” au la familia yako ni “wote.” Lakini, kwa kweli, “mimi.” Ni lipi jibu langu kwa swali hilo?

Jibu nililojipatia mwenyewe lilikuja kupitia matendo ya kibinafsi ya imani; kila siku nikijitahidi kuishi maagano yangu, ikijumuisha agano langu la ubatizo; na kujifunza kusikiliza sauti ya Bwana kupitia Roho Wake. Na muhimu zaidi, ilizingatia uhusiano wangu na Mwokozi wangu.

Mahusiano na Mwokozi

Ninaweza kuorodhesha kwa ujasiri sababu ninazohitaji wazazi wangu au marafiki zangu wa karibu zaidi. Nimeyarutubisha mahusiano hayo mara kwa mara. Thamani yao katika maisha yangu inaonekana na imara kama vile wakati na jitihada ninazoweka ili kuwa karibu nao kupitia mambo rahisi kama vile mazungumzo ya kawaida, kuwafahamu, na kuruhusu hekima yao ya haki kushawishi maisha yangu.

Uhusiano wetu na Yesu Kristo unaweza kufuata mpangilio kama huo. Maombi ya kila siku kwa Baba wa Mbinguni katika jina la Yesu Kristo ni muhimu. Na ndivyo ilivyo kwennye kumjua Mwokozi kwa kupekua maandiko, kusoma maneno ya manabii na mitume na kumsikiliza Roho. Ninaimarisha uhusiano huo wakati ninaporuhusu yote ninayojifunza yaathiri maisha yangu na tabia yangu.

Pia, fikiria mpango wa wokovu. Kichwa hicho, “mpango wa wokovu,” kinadokeza kwamba wewe na mimi—watu wote—tunahitaji kuokolewa na kwamba wokovu ulikuwa sehemu ya mpango wa maisha haya. Tulihitaji msaada na hatungeweza kujiokoa wenyewe.

Lakini Mungu alitutuma duniani na ahadi ya milele kwamba angetoa Mwokozi, Yesu Kristo, ambaye angeshinda vizuizi vinavyotutenganisha na uwepo wa Mungu.1 Na tunapoweka maagano na Mungu, Anatuahidi kufanya kila Anachoweza, bila kuondoa uwezo wetu wa kuchagua, kutusaidia kutunza ahadi zetu takatifu Kwake.2

Picha
Tracy Y. Browning kwenye ubatizo wake

Picha kwa hisani ya Tracy Y. Browning

Nilihitaji Kujua kwamba Alielewa

Nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 16 na nikiwa naishi New York City. Mwanzoni nilihisi kama nilikuwa natumia muda mwingi kujitafuta kati ya imani yangu mpya, pamoja na uhusiano wake wa agano na Mungu, na uhusiano wangu na marafiki.

Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kutokuwa na marafiki shuleni ambao ningeweza kuungana nao. Lakini marafiki zangu walikuwa wamezoea kufanya mambo ambayo nilikuja kugundua yalikuwa na madhara kwa roho yangu na hayakuwa yakiendana na kujichukulia juu yangu jina la Yesu Kristo. Nilijua kwamba Yesu Kristo alitaka nifanye maamuzi bora zaidi.

Kile ambacho sikujua ni iwapo Mwokozi alielewa jinsi nilivyokuwa nimekanganyikiwa. Kila siku ilikuwa ngumu zaidi pale nilipoalikwa kufanya mambo ambayo nilijua si mazuri. Nyakati fulani nilizihalalisha kuwa hazina madhara, lakini nilijua nilikuwa nakubaliana na mambo ambayo sikupaswa kufanya.

Nilihitaji kujua kwamba Mwokozi alielewa jinsi nilivyohisi mpweke na mwenye hatia wakati nafikiria hata kupunguza viwango vya injili ili niweze kuhisi hali ya kuwa mmoja wa marafiki zangu Nilihisi kama ninazama. Nilihitaji kuokolewa. Nilimhitaji Yesu Kristo.

Wakati Uhusiano Wangu pamoja Naye Ulipoimarika

Uhusiano wangu na Yesu Kristo uliimarika nilipogundua kwa nini mimi nilimhitaji Yeye. Ilikuwa ni wakati nilipoanza kusonga kutoka kujua tu kwamba nilipaswa kuishi injili hadi kuelewa kwa nini nilitaka kuishi injili na kuomba msaada wa kufanya. Nilipiga magoti tu na kumimina moyo wangu kwa Mungu, nikiwa na matumaini kwamba ananijali mimi na shida yangu, kwamba mpango wa wokovu ulipangwa kunisaidia mimi, kwamba hata furaha yangu ilikuwa ni sehemu ya mpango huo.

Rais Russell M. Nelson alifundisha, “Mara tu mimi na wewe tukiwa tayari tumefanya agano na Mungu, uhusiano wetu na Yeye unakuwa wa karibu sana kuliko kabla ya agano letu. … Kwa sababu ya agano letu na Mungu, Yeye kamwe hatachoka katika juhudi Zake za kutusaidia sisi, na kamwe sisi hatuwezi kumaliza subira Yake ya rehema kwetu.”3

Nilizungumza na Baba wa Mbinguni kuhusu jinsi nilivyohisi hatia, jinsi ambavyo sikujua la kufanya ili kutunza viwango vyangu na marafiki zangu. Nilimwambia nilikuwa nahisi kutokuwa na furaha na ningeweza kutumia msaada Wake.

Nikiwa nimepiga magoti ndipo nilianza kupata amani. Hisia hii ya amani ilinisaidia kuelewa kwamba Mwokozi alijua jinsi nilivyokuwa nikihisi na kwamba Yeye kweli anajali—kwa hakika.

Ninapoendelea kuwa mtu mzima na kupata mtazamo zaidi, ninatambua kwamba kila wakati ninapokuja kwa Mungu nikiomba msaada au msamaha, ninaonekana kama nikisafirishwa kwa njia ya kisitiari hadi kwenye bustani ya Gethsemane, ambapo Mwokozi wetu alitetemeka kwa maumivu na kuanza kuteseka katika mwili na roho kwa makosa na dhambi zinazotutenganisha na Mungu.4 Ni ukumbusho kwamba anaelewa kile ninachopitia—vyema kuliko mtu mwingine yeyote angeweza.

Picha
Yesu Kristo

Kwa Unyenyekevu, Mwokozi Wetu, na Jay Bryant Ward

Hauko Peke Yako

Nilipotoka kupiga magoti, Roho alinisaidia kutambua baadhi ya mambo na kunitia moyo kufanya mambo mengine. Kwanza, nilikumbuka kwamba rafiki yangu mmoja alikuwa Muislamu na hakuombwa kamwe kuachana na viwango vyake kwa sababu tuliheshimu imani yake na tulielewa kuwa kuna mambo fulani ambayo hangefanya. Nilitiwa moyo kushiriki imani yangu mpya kwa marafiki zangu ili wao pia waweze kuelewa zaidi kuhusu mimi na kwa nini viwango vyangu vipya vilikuwa muhimu kwangu.

Nilianza kidogo kidogo. Nilimwambia rafiki mmoja jinsi nilivyokuwa nikihangaika. Alikuwa mkarimu na mwenye heshima. Alinisaidia nilipokuwa nikizungumza na marafiki zangu wengine. Sio kila mtu alielewa, lakini baada ya muda, niliona kwamba walipanga mipango ambayo ningeweza kushiriki ambayo haikukiuka ahadi zangu kwa Mungu.

Ninajua kwamba sote tunaweza kutumia nguvu zaidi kuhimili ushawishi wa kila mara wa ulimwengu. Kuweka maagano huleta hilo, na Yesu Kristo yuko katikati ya maagano yetu.5 Hili ndilo nililojionea mwenyewe—kwa nini nilimhitaji Yesu Kristo.

Kufika nyumbani kwa Mungu si jambo ninaloweza kufanya peke yangu. Na kuna hatua nyingi ndogo za kila siku na uzoefu wa kila siku ambao mimi—na sisi sote—tutafanya katika safari hiyo ya kurudi nyumbani. Lakini jinsi gani tumebarikiwa kama wafanya maagano na washika maagano kwamba Mungu “hatachoka kamwe katika juhudi Zake za kutusaidia” hadi tufike huko.

Chapisha