Mkutano Mkuu
Sivyo kama Ulimwengu Utoavyo
Mkutano mkuu wa Aprili 2021


Sivyo kama Ulimwengu Utoavyo

Vyombo tunavyohitaji kutengeneza siku angavu na kukuza uchumi halisi wa wema vinapatikana kwa wingi katika injili ya Yesu Kristo.

Kabla ya ile Pasaka ya kwanza, wakati Yesu alipohitimisha ibada mpya ya sakramenti aliyowafanyia wale Kumi na Wawili, alianza mahubiri Yake makuu ya kwaheri na akaondoka kwenda Gethsemane, kusalitiwa, na kusulubiwa. Hata hivyo, akihisi wasiwasi na pengine hata hofu kubwa ambayo baadhi ya wanaume hao lazima walionyesha, Yeye alisema hili kwao (na kwetu):

“Msifadhaike mioyoni mwenu: mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. …

“Sitawaacha ninyi yatima: Naja kwenu. …

“Amani nawaachieni, amani yangu nawapa: niwapavyo mimi, sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga.”1

Nyakati za changamoto huja katika ulimwengu huu, ikiwa ni pamoja na kwa waaminifu, lakini ujumbe wa kuondoa shaka wa Kristo ni kwamba japokuwa Yeye, mwanakondoo wa pasaka, angeenda kama “mwanakondoo apelekwaye machinjoni”2 hata hivyo angeinuka, kama mtunzi wa zaburi asemavyo, kuwa “kimbilio letu na nguvu, msaada (wetu) hasa utakaoonekana tele [nyakati za] mateso.”3

Tukitambua masaa magumu yaliyokuwa mbele kwa ajili ya Kristo pale alipokuwa akisonga kwenye msalaba na kwa wafuasi Wake kadiri ambavyo wangepeleka injili Yake ulimwenguni katika wakati wa meridia, nenda pamoja nami sasa kwenye ujumbe husika kwa waumini wa Kanisa la Mwokozi katika Siku za Mwisho. Unajikita katika mistari kadhaa tofauti katika Kitabu cha Mormoni iliyotolewa kwenye mgogoro wa aina moja au nyingine, kutoka mfano wa kuudhi milele wa Lamani na Lemueli mpaka vita vya mwisho vinavyohusisha mamia ya maelfu ya askari. Mojawapo ya sababu za wazi za msisitizo huu ni kwamba kadiri Kitabu cha Mormoni kilivyoandikwa kwa ajili ya hadhara ya siku za mwisho, waandishi hawa (ambao wao wenyewe walishuhudia vita vingi) kinabii wanatuonya kwamba vurugu na migogoro vitakuwa ishara bainifu ya mahusiano katika siku za mwisho.

Bila shaka, nadharia yangu kuhusu mabishano ya siku za mwisho si ya asili sana. Miaka elfu mbili iliyopita, Mwokozi alionya kwamba katika siku za mwisho kungekuwa na “vita, na uvumi wa vita,”4 baadaye akisema kwamba “amani [ingeondolewa] duniani.”5 Kwa hakika Mfalme huyu wa Amani, ambaye alifundisha waziwazi kwamba ubishi ni wa shetani,6 ni lazima analia, pamoja na Baba Yake Mtukufu, juu ya wale katika familia ya binadamu katika siku yetu ambao “hawana upendo” maandiko yanasema na ambao hawawezi kuelewa jinsi ya kuishi pamoja kwa upendo.7

Akina kaka na akina dada, tunaona migogoro mingi sana, hasira, na kwa ujumla ukosefu wa ustarabu kati yetu. Kwa bahati nzuri, kizazi cha sasa hakijapata Vita ya Tatu ya Dunia ya kupigana, au kupata uzoefu wa mdororo wa uchumi ulimwenguni kama ule wa mwaka 1929 ulioongoza kwenye Anguko la Uchumi wa Dunia. Sisi, hata hivyo, tunakabiliana na aina ya Vita ya Tatu ya Dunia ambayo siyo vita kuwapiga maadui zetu bali upangaji wa uandikishaji wa watoto wa Mungu kuwa wenye kujaliana zaidi na kusaidia kuponya vidonda tunavyoviona katika ulimwengu ulio na migogoro. Anguko Kuu tunalokabiliana nalo linahusu kidogo sana upotevu wa nje wa akiba zetu na linahusu zaidi upotevu wa ndani wa kujiamini, kwa kufifia kwa imani na tumaini, na hisani kote karibu nasi. Lakini vyombo tunavohitaji kutengeneza siku angavu na kukuza uchumi halisi wa wema katika jamii vinapatikana kwa wingi katika injili ya Yesu Kristo. Hatuwezi kukubali—na ulimwengu huu hauwezi kukubali—kushindwa kwetu kutumia dhana hizi za injili na kuyaimarisha maagano kwenye matumizi kamili kwa mtu binafsi na hadharani.

Kwa hiyo, katika ulimwengu “uliorushwa na tufani, na usio na faraja,” kama Yehova alivyosema ungekuwa, tunawezaje kupata kile Yeye alichokiita “agano la … amani”? Tunaweza kulipata kwa kumgeukia Yeye ambaye angekuwa na rehema kwetu na “kwa fadhili za milele” angewapa amani watoto wetu.“8 Licha ya unabii wa kuogofya na maandiko ya kutia wasiwasi yakitangaza kwamba amani itaondolewa kutoka duniani kote, manabii, ikijumuisha nabii wetu mpendwa Russell M. Nelson, wamefundisha kwamba haipaswi kuondolewa kwetu mtu mmoja mmoja!9 Kwa hiyo, Pasaka hii acha tujaribu kudumisha amani katika njia ya binafsi, tukitumia mafuta ya neema na uponyaji ya Upatanisho wa Bwana Yesu Kristo kwetu sisi na familia zetu pamoja na wale wote walio karibu yetu tunaoweza kuwafikia. Kwa bahati nzuri, hata ya kushangaza, marhamu haya yenye kupoza yanapatikana kwetu “bila pesa na bila bei.”10

Msaada na tumaini kama hili vinahitajika sana kwa sababu katika kusanyiko hili la ulimweguni kote leo kuna wengi ambao wanataabika na changamoto nyingi za—kimwili au kihisia, kijamii au kifedha, au jozi za kila aina ya shida. Lakini nyingi za shida hizi sisi si wenye nguvu vya kutosha kuzishughulikia sisi wenyewe, kwani msaada na amani tunayoihitaji siyo aina ile “ulimwengu utoavyo.”11 Hapana, kwa shida ngumu tunahitaji kile maandiko yanachokiita “nguvu za mbinguni,” na ili kupata nguvu hizi ni lazima tuishi kwa kile maandiko hayo hayo yanachokiita “kanuni za haki.”12 Sasa, kuelewa muunganiko huo kati ya kanuni na nguvu ndiyo somo moja ambalo familia ya binadamu kamwe haionekani kujifunza, hivyo ndivyo asemavyo Mungu wa mbinguni na duniani!13

Na kanuni hizo ni zipi? Vema, zimeorodheshwa tena na tena katika maandiko, zimefundishwa tena na tena katika mikutano kama huu, na katika kipindi chetu, Nabii Joseph Smith alifunzwa katika kujibu toleo lake mwenyewe la kilio chake “Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha?”14 Katika baridi, kizuizi kisichojali cha Jela ya Liberty, alifundishwa kwamba kanuni za haki zilijumuisha sifa kama vile, uvumilivu, upole, unyenyekevu na upendo usio unafiki.15 Bila kanuni hizo, ilikuwa wazi kabisa tungeweza kuishi kwa mifarakano na uadui.

Kuhusu swala hilo, acha nizungumze kwa muda kuhusu upungufu katika baadhi ya sehemu za kanuni hizi za haki katika wakati wetu. Kama sheria, mimi ni aina ya mtu mwenye tumaini, mwenye furaha na kuna mengi mema na mazuri katika ulimwengu wetu. Kwa hakika tuna baraka za kimwili nyingi sana kuliko kizazi chochote katika historia, lakini katika desturi ya karne ya 21 kwa kawaida na mara nyingi katika Kanisa, bado tunaona maisha yaliyo katika shida, yenye mwafaka unaoongoza kwenye maagano mengi yaliyovunjwa na mioyo mingi iliyovunjika. Fikiria lugha chafu ambayo ni sambamba na uvunjaji wa sheria ya kujamiiana, vyote ambavyo vimekithiri katika sinema au kwenye runinga, au tazama dhuluma za ngono na aina zingine za utovu wa nidhamu katika maeneo ya kazi ambao tunausoma sana siku za leo. Katika masuala ya usafi wa kimaagano, utakatifu mara nyingi hufanywa kuwa wa kawaida na utukufu mara nyingi hufanywa kuwa unajisi. Kwa yeyote anayejaribiwa kutembea au kuzungumza au kutenda katika njia hizi—“kama ulimwengu utoavyo,” nikisema hivyo—asitarajie hayo kumwongoza kwenye uzoefu wa amani; ninawaahidi katika jina la Bwana haitawezekana. “uovu haujapata kuwa furaha,”16 nabii wa kale wakati mmoja alisema. Wakati densi inapokwisha, mpiga zumari daima sharti alipwe na mara nyingi ni katika fedha ya machozi na majuto.17

Au pengine tunaona mifumo mingine ya unyanyasaji na ukosefu wa heshima. Tunapaswa kuwa makini maradufu kiasi gani kama wanafunzi wa Bwana Yesu Kristo kutoshiriki katika tabia yoyote kama hiyo. Kwa namna yoyote ile hatupaswi kamwe kuwa na hatia ya aina yoyote ya unyanyasaji au utawala usio haki au ukandamizaji wa kimaadili—si kimwili au kihisia au kikanisa au wa aina yoyote ile. Nakumbuka kuhisi ari ya Rais Gordon B. Hinckley miaka michache iliyopita alipokuwa akizungumza na wanaume wa Kanisa kuhusu wale ambao aliwaita “wanyanyasaji katika nyumba zao wenyewe”:18

“Ni janga na jambo la kuchukiza kiasi gani kumnyanyasa mke,” alisema. “Mtu yeyote katika Kanisa hili ambaye anamnyanyasa mke wake, ambaye humdharau, kumtusi, ambaye hutumia utawala usio haki hastahili kushikilia ukuhani. … [Yeye] hastahili kuwa na kibali cha Hekaluni.”19 Kinachochukiza sawa na hicho, alisema, ilikuwa aina yoyote ya unyanyasaji wa mtoto—au aina nyingine yoyote ya unyanyasaji.20

Katika matukio mengi, vinginevyo wanaume, wanawake na hata watoto waaminifu wanaweza kuwa na hatia ya kuzungumza bila ukarimu, hata kwa kuangamiza, kwa wale ambao kwao wanaweza kuunganishwa vyema na ibada takatifu katika hekalu la Bwana. Kila mmoja ana haki ya kupendwa, kuhisi amani, na kupata amani nyumbani. Tafadhali, acha tujaribu kudumisha mazingira hayo nyumbani. Ahadi ya kuwa mpatanishi ni kwamba utakuwa na Roho Mtakatifu kama mwenzi wako daima na baraka zitatiririka kwako “bila kulazimisha” milele na milele.21 Hakuna yeyote anayeweza kutumia ulimi mkali au maneno yasiyo ya ukarimu na bado “akaimba wimbo wa upendo wa ukombozi.”

Acha nimalize na kile nilichoanza nacho. Kesho ni Pasaka, wakati wa kanuni za haki za injili ya Yesu Kristo na Upatanisho Wake “kutuepusha”—kutuepusha na migogoro na ubishi, kutuepusha na dhiki na uvunjaji wa sheria, na hatimaye kushinda kifo. Ni wakati wa kuahidi uaminifu kamili katika maneno na matendo kwa Mwanakondoo wa Mungu, ambaye “ameyachukua masikitiko yetu na amejitwika huzuni zetu,”23 katika azimio Lake la kukamilisha kazi ya wokovu kwa niaba yetu.

Licha ya kusalitiwa na uchungu, kutendewa vibaya na ukatili na huku akibeba mrundikano wote wa dhambi za familia yote ya binadamu, Mwana wa Mungu Aliye Hai alitazama chini kwenye njia ya maisha ya duniani, akatuona wikiendi hii na kusema: “Amani nawaachieni, amani yangu nawapa: niwapavyo mimi, sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga.”24 Muwe na Pasaka yenye baraka, furaha na amani. Uwezakano wake usioweza kuelezeka tayari umelipiwa na Mfalme wa Amani, ambaye ninampenda kwa moyo wangu wote, ambaye hili ni Kanisa Lake na ambaye juu yake ninatoa ushahidi usio na mashaka, hata Bwana Yesu Kristo, amina.

Chapisha